Vijana Wanauliza . . .
Je! Nijiunge na Genge?
“Nilipokuwa nimeketi kwenye bohari ya shule, wavulana hawa wakanijia na kuanza kunisumbua. Mmoja wao akanipiga ngumi ya kifua. Kufikia hapo mmoja wa wavulana niliyejua wa genge hili kutoka ujirani wetu akanisaidia. Nikafikiria, ‘Nikijiunga na genge, labda nitapata ulinzi kama huo.’”—Greg.
MAGENGE yanaendelea kuongezeka katika shule nyingi na ujirani mwingi. Katika 1989 polisi walikadiria kwamba katika Jimbo la Los Angeles, U.S.A., peke yake kulikuwako magenge 600 yakiwa na washiriki 70,000. Hata hivyo magenge hayapatikani tu katika United States. Kwa mfano, gazeti Macleans’s liliripoti kwamba katika mji wa Vancouver, Canada, kuna magenge 13 hivi, yakiwa na washiriki zaidi ya 600.
Kama vile Greg, wengi hujiunga na magenge ili kupata ulinzi kutokana na jeuri ya shule, na katika siku hizi zenye jeuri, si vigumu kuelewa ni kwa nini vijana wengine wanahisi uhitaji kama huo. Tunashuhudia “kuongezeka maasi” kwa ulimwenguni pote. (Mathayo 24:12) Hata hivyo, kuna sababu nyinginezo zinazofanya magenge ya mitaani yawe uvutio mkubwa kwa vijana wengine.
Utegemezo na Urafiki
“Nilitaka sana kuwa na marafiki, hisi ya kuwa wa mtu fulani au kikundi fulani, mtu fulani ambaye ungemjali,” aeleza Bernard, aliyekuwa mwanagenge hapo awali. Marianne, aliyejiunga na genge la wasichana, akubali kwamba alifanya hivyo “kwa ajili ya kutaka kudhibiti kitu fulani,” pamoja na “ile hali ya kifamilia” iliyotoa.
Ingawa ni kweli kwamba vijana wengine hujiunga na magenge ili kukabiliana na uchovu au kwa ajili ya msisimko ambao huenda yakatoa, inaonekana kwamba wengi zaidi hujiunga ili kuwa wa fulani, kupata utegemezo wa kihisia-moyo, kupata marafiki ambao watashirikiana mambo yanayofanana. Kwa kawaida hilo hufanywa kuwa badala ya hali ya familia isiyotamanika.
Bernard anasema juu yake mwenyewe na wanagenge wenzake: “Wengi wetu tulitoka kwa familia zilizovunjika. Wengi walilelewa na mzazi-mmoja, sanasana mama, katika familia kubwa. Kwa hiyo hakukuwa na mtu wa kuchukua wakati ili kuwazungumzia. Wengi walitoka kwenye nyumba ambapo waliumizwa kimwili na kwa maneno na ambapo hakuna aliyejali ikiwa walikuwa na hisia au sivyo. Kwa hiyo walihisi vizuri, kama mimi, kuwa na mtu unayeweza kuzungumzia na akusikilize.”
Jambo hili latajwa pia na mshauri wa vijana Mkanada Lew Golding. Alisema: “Watoto wenye matatizo nyumbani hujifunga katika genge kupata malezi ya kihisia-moyo.”
Katika United States, magenge mengi huundwa kulingana na kabila au tamaduni. Basi, magenge katika nchi hiyo, hutoa uvutio wa ziada wa ushirika pamoja na wale wanaoshiriki maoni yaleyale kuhusu chakula, muziki, lugha, na mambo mengine mengi. Kwa vijana na hata watu wazima pia, tamaa ya kuhisi kuhitajiwa na kukubaliwa ni ya kawaida. Lakini je, hisia hizi na mahitaji hayo kweli yaweza kutoshelezwa kwa kujiunga na genge?
Mithali 17:17 husema: “Rafiki hupenda siku zote.” Je! wanagenge huona uaminifu na urafiki wa kweli kama huo? Kwa kinyume, kutoelewana na hata kupigana miongoni mwa wanagenge ni kwa kawaida sana. Naam, katika mazingira yenye misongo mingi ambamo magenge huendesha shughuli zayo, vinyongo hutokea upesi. Utofautiano wa maoni waweza kufikiriwa kuwa ukosefu wa uaminifu. Bernard aeleza: “Ikiwa tulikuwa na bishano, nilihitaji kuwa chonjo kwa sababu kwa ghafula, kisu au bunduki ingeweza kutolewa. Na hawa walipaswa kuwa rafiki zangu! Maisha ya genge yaliniacha nikiwa nimetamauka kwa sababu sikuwa na marafiki wa kweli.”
Kama vile anavyoongeza mwanagenge mmoja wa umri wa miaka 18: ‘Hauwi na marafiki wowote, hata katika genge lako mwenyewe. Uko peke yako.’
“Usiandamane na Mkutano”
“Usiandamane na mkutano kutenda uovu.” (Kutoka 23:2) Hilo lilisemwa kwa watu wa Mungu katika nyakati za kale, na kwa kanuni latumika vizuri kwa kijana yeyote anayenuia kujiunga na genge. Huenda ukafikiria genge kuwa njia ya kujilinda au chanzo cha urafiki. Lakini kwa kweli, mwanagenge atalazimika kufuatia “kutenda uovu.”
The Globe and Mail lasema hivi kuhusu hilo: ‘Genge lawa familia. Hilo pia lamaanisha kwamba genge laamua tabia inayokubalika. Katika ulimwengu wa matineja wasioangaliwa, unyang’anyi, mapigo, mashambulizi ya kingono yaweza kuwa “ndio” mambo ya kufanya.’
Katika 1989 peke yake, magenge katika Jimbo la Los Angeles yalihusika katika mauaji 570. Na karibu kila mahali ambapo kuna magenge, kuna jeuri. Jaribio lolote la kukataa kujiingiza ni wazi litaonekana kuwa ukosefu wa utegemezo kwa genge au, hata vibaya zaidi kuwa woga. Katika tukio lolote lile, unaweza kwa urahisi kujipata kuwa ndiyo shabaha ya shambulizi. Kama alivyosema mwanagenge mmoja: “Hauwezi kusema la kwa [genge] lako.” Je! hisia ya kuwa na uhusiano wa karibu au ya kupata ulinzi yastahili mbano wa aina hiyo?
Mwandikaji wa Mithali 1:10-15 anajibu: “Mwanangu, wenye dhambi wakikushawishi, wewe usikubali. Wakisema, Haya, njoo pamoja nasi, na tuvizie ili kumwaga damu; tumwotee asiye na hatia, bila sababu. . . . Wewe utashirikiana nasi. . . . Mwanangu, usiende njiani pamoja nao.”
Kuishi kwa Upanga
Fikiria, pia, mambo yanayoweza kutokea kwa afya na hali njema yako. Mwanagenge mmoja alisema kwamba ‘ni lazima uwe tayari kufa kwa ajili ya wanagenge wenzako.’ Na mara nyingi huwa hivyo.
Kinyume cha hilo, fikiria somo ambalo Yesu alifundisha wanafunzi wake usiku wa kukamatwa kwake. Yesu hakuwa na silaha na alikabili umati wenye jeuri. Je! Yesu alitaka wanafunzi wake wajikusanye na kumlinda kwa kutumia nguvu? Petro alifikiri hivyo. Aliutoa upanga wake na akamshambulia mmoja wa watu hao katika umati, akikata sikio lake. Ingawa hivyo, itikio la Yesu ni lazima liwe lilimshangaza Petro. Yesu kwa mwujiza aliponya sikio la yule mtu na kumwambia Petro: “Rudisha upanga wako mahali pake; maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.”—Mathayo 26:52.
Somo ni nini? Si kwamba tu kujilinda mwenyewe na silaha ni jambo lisilo la kimaandiko bali pia ni upumbavu, usiofaa. Mithali husema hivi: “Atafutaye madhara, hayo yatamjia.”—Mithali 11:27.
Kupata Hisi Hakika ya Kuwa na Uhusiano wa Karibu na Wengine
Miaka kama 50 iliyopita, uchunguzi ulifanywa ambao ulionyesha mambo tofauti yenye kuchangia muundo wa magenge. Miongoni mwa matatizo yaliyoorodheshwa yalikuwa ukosefu wa maisha ya familia yenye kutosheleza, umaskini, majirani yenye kuharibika, na elimu ya hali ya chini. Utendaji wa magenge haujasaidia hali hiyo hata kidogo, wala haijasaidia vijana wenye upweke kupata marafiki wa kweli. Hata hivyo, kundi la Kikristo, hukutolea ushirika na watu ambao wana mapendezi yako moyoni mwao. Kwa nini usisitawishe urafiki hapo?
Lakini, unaweza kujilindaje ikiwa unaishi katika eneo ambapo magenge yameenea? Makala ya wakati ujao itazungumzia hilo.
[Sanduku katika ukurasa wa 27]
‘Nilijiunga na Genge la Mtaani’
“Nilikuwa na umri wa miaka 17. Rafiki zangu nami tulichukizwa kuona watu wakipigwa risasi, wakiviziwa, na kunajisiwa katika ujirani wetu. Tukafikiria kwamba ikiwa tungeanzisha genge letu wenyewe, labda tungekomesha hali hiyo. Kwa wakati ule ule nilitaka kuwa na ile hisi ya kuwa wa kikundi fulani. Kwa hiyo tukaanzisha genge.
“Tulianza kuuzunguka ujirani, na upesi magenge mengine yakatujaribu. Wawili wa wanagenge wetu walishambuliwa na genge la upinzani. Mmoja alipigwa usoni kwa kibao cha besiboli; mwingine alidungwa kisu. Tulilipiza kisasi kwa ukosefu huo wa haki na tukawa genge lililoogopewa sana mahali hapo.
“Hata hivyo, nilipata kwamba wanagenge si rafiki za kweli. Usingeweza kumtumaini yeyote. Wengine hawangekusaidia ikiwa ulikuwa na shida. Na wengine hawakushiriki mawazo yangu—walianza kuvizia na hata kuua watu bila sababu. Kwa hiyo nikaanza kuchukia maisha yangu. Nilihisi kwamba Mungu alikuwepo lakini nikajiuliza kwa nini aliruhusu ukosefu wa haki mwingi. Pia nilijifunza shuleni kwamba kanisa lilihusika katika Mabaraza ya Kuhukumu Wazushi wa Kidini na katika kuharibu staarabu nzima-nzima kwa jina la Mungu. Niliamini kwamba dini zilikuwepo ili kujitengenezea pesa.
“Siku moja nilimwomba Mungu anisaidie nipate tengenezo alilokuwa akitumia. Nilifungua Biblia ambayo mjomba wangu alikuwa amenipa na kusoma Matendo 20:20. Ilisema kuhusu kwenda nyumba kwa nyumba. Wale tu niliojua walifanya hivyo walikuwa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo nilipata mahali ambapo Jumba la Ufalme la mahali petu lilikuwa na nikaenda asubuhi iliyofuata. Nikiwa na machozi machoni pangu, nilimkaribia mmoja wa Mashahidi na kumnong’onezea, ‘Nataka kujifunza.’ Nilikuwa nimepata watu wa Mungu. Siku zangu nikiwa mwanagenge zilikuwa zimekwisha.”—Mwandikaji ambaye amechagua kutojulisha jina lake, sasa anatumikia akiwa mwangalizi-msimamizi wa kundi la Mashahidi wa Yehova.
[Picha katika ukurasa wa 17]
“Mbona usisitawishe urafiki na watu ambao wana mapendezi yako moyoni mwao?”