Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 4/22 kur. 8-11
  • Kuwalinda Watoto Wetu na Magenge

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuwalinda Watoto Wetu na Magenge
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kutahadhari Ni Muhimu
  • Jihusishe na Watoto Wako
  • Kile Ambacho kwa Kweli Watoto Wetu Wanahitaji
  • Kuwaandalia Wanachohitaji
  • Mambo Tupaswayo Kujua Kuhusu Magenge
    Amkeni!—1998
  • Je! Nijiunge na Genge?
    Amkeni!—1992
  • Tatizo Laenea
    Amkeni!—1998
  • “Nilikuwa Nikijichimbia Kaburi”
    Biblia Inabadili Maisha
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 4/22 kur. 8-11

Kuwalinda Watoto Wetu na Magenge

“Watoto huhitaji watu wanaowajali.”—Not My Kid—Gang Prevention for Parents.

BAADA ya uhusiano wetu pamoja na Mungu, watoto wetu ni miongoni mwa mali zetu zenye thamani ya juu zaidi. Twapaswa kuongea nao, kuwasikiliza, kuwakumbatia, na kuhakikisha kwamba wanajua kuwa wao ni wa maana sana kwetu. Lazima tuwafundishe mambo mazuri—kuwa wenye kufuatia haki na wenye nia ya kusaidia, jinsi ya kuwa na maisha mema, na jinsi ya kuwa wenye fadhili kuelekea wengine.

Msimamizi wa kituo cha kizuizi cha watoto alitambulisha tatizo kubwa leo, akisema: “Maadili hayafunzwi katika familia.” Kwa hakika twahitaji kutoa uangalifu katika kufanya jambo hili. Lazima tuishi katika njia ambayo twawataka watoto wetu waishi na kuacha waone shangwe ambayo jambo hili huongezea maishani mwetu. Ikiwa hatuwafundishi thamani zinazofaa, twawezaje kuwatarajia wafuate kanuni kama hizo?

Gazeti Today, linalochapishwa kwa ajili ya walimu wa shule wa Marekani, lilisema kwamba mara nyingi magenge huvutia vijana ambao “hujiona kuwa wasiofaulu maishani” na ambao “hutafuta usalama, uhusiano wa karibu, na kukubaliwa na jamii.” Ikiwa kwa kweli tunawapa watoto wetu mambo hayo nyumbani—usalama na hisi thabiti ya kufanikiwa katika familia na katika maisha yao wenyewe—wataelekea kuvutiwa kidogo sana na ahadi zisizo za kweli zinazotolewa na genge fulani.

Kiongozi wa kikosi cha polisi cha kupambana na magenge cha California asema juu ya ishara ambazo yeye huona nyusoni mwa wazazi wakati polisi wanapobisha mlangoni pao kusema kwamba mtoto wao yuko taabani. Hawaamini kwamba yule waliyefikiri kuwa walimjua vema sana angeweza kufanya jambo lililo baya. Lakini mtoto wao alipata marafiki wapya na alikuwa amebadilika. Wazazi hawakutambua tu.

Kutahadhari Ni Muhimu

Watu wanaoishi katika maeneo ambapo magenge hutenda husema kwamba vijana na watu wazima wanapaswa kutumia uamuzi mzuri na si kutoa sai au tisho kwa genge. Jiepushe na vikundi vikubwa vya washiriki wa genge, na usiige namna wanavyoonekana au kutenda, kutia ndani mtindo na rangi ya mavazi wanayovalia. Kuwaiga kungeweza kukufanya uwe shabaha ya genge la upinzani.

Pia, ikiwa mtu avalia au atenda kana kwamba anataka kuwa sehemu ya genge, washiriki wake wanaweza kumsonga awe mmoja wao. Umaana wa kujua mtazamo wa washiriki wa genge la mahali penu ulitolewa kielezi na baba mwenye watoto watatu katika Chicago. Alisema: ‘Ikiwa ninavalia kofia yangu ikiwa imetazama upande wa kulia, wao hufikiri ninawadharau.’ Na jambo hilo lingeweza kuongoza kwenye jeuri!

Jihusishe na Watoto Wako

Mama mmoja alisema: “Ni lazima tuwajue watoto wetu—kile wanachohisi na kile wanachofanya. Hatutaweza kuwasaidia watoto wetu ikiwa hatuonyeshi upendezi wa kibinafsi katika maisha zao.” Mwingine alisema kwamba tatizo la magenge halitaisha mpaka wazazi walimalize. Aliongezea: “Acheni tuwape upendo. Ikiwa wataharibika, tutakuwa tumepotea.”

Je, twawajua marafiki wa watoto wetu, mahali watoto wetu huenda baada ya shule, na mahali wanapokuwa jioni baada ya giza? Bila shaka, si kila mama awezaye kuwa nyumbani wakati watoto wake wawasilipo nyumbani kutoka shule. Lakini akina mama wa wasio na wenzi ambao hung’ang’ana kwa ujasiri kulipia kodi na kuwalisha watoto wao huenda wakaweza kufanya mipango na mama wengine au mtu mwingine wanayemwitibari aandae usimamizi wakati wa mchana kwa watoto wao.

Mwanamume mmoja anayeishi katika eneo kuu la magenge aliulizwa jinsi angewalinda watoto wake na magenge. Alisema angemchukua mwana wake kuzunguka ujirani ili kumwonyesha matokeo ya utendaji wa genge. Angeelekeza kwenye michoro iliyo ukutani na majengo yaliyobomoka ili kumwonyesha “kwamba eneo hilo si salama na kwamba washiriki wa genge wanarandaranda tu karibu na hapo, bila jambo la kufanya maishani.” Aliongezea: “Kisha ningemweleza kwamba kuishi kwa kupatana na kanuni za Biblia kungemzuia asipatwe na tokeo la namna hiyo.”

Jambo la namna hiyo lililo sahili kama vile upendezi wa kweli kwa kazi ya shule ya watoto wetu laweza kuwa ulinzi. Ikiwa shule yao ina usiku uliotengwa kwa ajili ya wazazi au wakati mwingine ambao wazazi hualikwa wazuru madarasa na kuzungumza na walimu, hakikisha kuwa umeenda. Wajue walimu wa watoto wako, na acha wajue hangaiko lako kwa mtoto wako na upendezi wako katika kisomo chake. Ikiwa shule haina programu ya kutembelewa, jaribu kutafuta pindi za kuzungumza na walimu juu ya maendeleo ya mtoto wako katika shule na jinsi uwezavyo kusaidia.

Ukaguzi katika jiji moja kubwa la Marekani ulipata kwamba miongoni mwa wanafunzi ambao familia zao ziliwasaidia au kuwatia moyo katika mgawo wao wa masomo ya nyumbani, asilimia 9 walijiunga na genge. Lakini katika familia ambazo uangalifu wa namna hiyo haukutolewa, idadi maradufu ya wanafunzi—asilimia 18—walijiunga na genge. Ikiwa familia yetu ni yenye upendo na iliyoshikamana kwa ukaribu na ikiwa twafanya mambo yajengayo, hili litapunguza uwezekano wa kwamba watoto wetu watavutiwa na ahadi zisizo za kweli za magenge.

Kile Ambacho kwa Kweli Watoto Wetu Wanahitaji

Watoto wetu wanahitaji mambo yaleyale tuhitajiyo—upendo, fadhili, na shauku. Watoto wengi hawajawahi kamwe kuguswa kwa njia yenye shauku, yenye upendo au kuambiwa kwamba kwa kweli yeye ni wa maana. Jambo hili lisitukie kwa watoto wetu kamwe! Na tuwakumbatie, tuwaambie kwamba twawapenda, na tujaribu kuona kwamba wanaishi maisha ya adili ambayo tumewafunza kuishi. Wao ni wenye thamani sana kwetu kuwatendea kwa njia yoyote nyingine.

Gerald, mshiriki wa genge wa hapo zamani, alieleza: “Sikuwa na baba wa kumtegemea, kwa hiyo nilienda kwenye magenge ili kujazia pengo hilo katika maisha yangu.” Alianza kutumia dawa za kulevya alipofikisha umri wa miaka 12. Lakini alipofikisha umri wa miaka 17, mama yake alianza funzo la Biblia nyumbani la kawaida pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alitumia kanuni bora za Biblia maishani mwake. Anasema: “Niliona badiliko kwa upande wake, na nikafikiri, ‘Lazima kuwe na jambo fulani lililo la kweli na linalofaa.’” Kielelezo kizuri cha mama yake kilimchochea abadili maisha yake.

Watoto wetu wapaswa kuona kielelezo chetu kizuri—kwamba tunaishi kulingana na yale tunayowafunza. Wanapaswa kuwa na hisi nzuri kuelekea familia yao, si kwa kile ilicho nacho, bali kwa kile ifanyacho. Na watoto wanapaswa wasaidiwe kwa njia ambayo wataonea fahari tabia yao ya kiadili. Mwanasheria wa hapo zamani wa Mkoa wa Los Angeles, Ira Reiner, alieleza hivi: “Lazima tuwaonyeshe watoto hangaiko lenye upendo kabla hawajaishia kwenye magenge.”

Kuwaandalia Wanachohitaji

Si vitu vya kimwili ambavyo sisi huwaandalia watoto wetu vilivyo na umaana wa kwanza. Jambo lililo la maana ni kuwasaidia wakue wawe watu wazima wenye upendo na wenye kujali ambao wana viwango bora vya kiadili. Biblia husema kwamba Yakobo mwenye haki aliwaita wachanga wake ‘watoto Mungu alionipa kwa neema yake.’ (Mwanzo 33:5) Ikiwa tutawaona watoto wetu kwa njia hiyo—wakiwa zawadi ambazo Mungu ametupa sisi—tutakuwa tayari zaidi kuwatendea kwa upendo na kuwafundisha kuishi maisha ya kufuatia haki, manyoofu, na maisha yenye adili.

Hivyo tutafanya yote tuwezayo kuishi maisha kwa namna ya kwamba twaweka kielelezo kinachofaa kwa ajili ya watoto wetu. Tutawapatia fahari inayofaa na ijengayo kuelekea familia yao, si kwenye mali za kimwili za familia, bali kutuelekea kwa ajili ya utu wetu. Hivyo, hawataelekea kutafuta msaada kutoka kwa wale walioko mitaani.

Akitazama nyuma kwenye ujana wake, babu mmoja alisema: “Singefanya kamwe jambo la kuaibisha familia yangu.” Alikiri kwamba alihisi hivyo kwa sababu alitambua upendo ambao wazazi wake walikuwa nao kumwelekea. Kweli, kuonyesha upendo kwa watoto wao huenda kusiwe jambo rahisi kwa akina mama na baba fulani ambao hawakupokea kamwe upendo kutoka kwa wazazi wao. Hata hivyo, wazazi wanahitaji kufanya jitihada ya kuwapenda watoto wao.

Kwa nini jambo hili ni la maana sana? Kwa sababu kama vile gazeti “What’s Up,” linalochapishwa na Shirika la Upelelezi la Genge la Utah, lilivyosema, “wakati vijana wahisipo kuwa wanapendwa na wako salama—si kuwa salama kiuchumi, bali salama kihisia-moyo—mahitaji ambayo huwasukuma kujiunga na magenge hutoweka.”

Huenda wasomaji fulani wakafikiri kwamba familia zenye kuonyesha upendo kama hizo hazipatikani tena kamwe. Lakini zinapatikana. Unaweza kuzipata nyingi kati ya hizo miongoni mwa makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Kweli, familia hizi si kamilifu, lakini zinapata faida kubwa: Zinajifunza kile ambacho Biblia husema kuhusu kulea watoto na hujitahidi kutumia kanuni za Biblia za kimungu katika maisha zao. Zaidi ya hayo, hufundisha watoto wao kanuni hizi.

Mashahidi wa Yehova hukubaliana na taarifa iliyoandikwa katika The Journal of the American Medical Association: “Mtu hawezi kutumaini kuwa na . . . matineja ‘Wanaosema tu la’ bila kuwapatia jambo fulani la ‘Kusema ndiyo.’” Yaani, ikiwa twataka watoto wetu waseme ndiyo kwa mambo mazuri na yajengayo, lazima tuwaelekeze katika upande huo.

Hakuna hata mmoja wetu ambaye angependa kamwe kusema, kama alivyosema baba mmoja: ‘Katika genge lake mwana wangu alipata ushirika na staha ambayo hakuwahi kuhisi hapo awali.’ Wala hatungependa kusikia watoto wetu wakisema, kama mwanamume mmoja mchanga alivyosema: “Nilijiunga na genge kwa sababu nilihitaji familia.”

Sisi, wazazi, lazima tuwe familia hiyo. Na lazima tufanye yote tuwezayo ili kuona kwamba wachanga wetu wenye thamani wanabaki wakiwa sehemu yenye joto na upendo ya familia hiyo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Orodha ya Kupimia kwa Wazazi Wanaohangaika

✔ Tumia wakati nyumbani pamoja na watoto wako, na fanyeni mambo pamoja mkiwa familia

✔ Jua marafiki wa watoto wako na familia zao, na fuatia kujua waendako watoto wako na huenda pamoja na nani

✔ Acha watoto wako wajue kwamba wanaweza kukufikia wakati wowote wakiwa na tatizo lolote

✔ Wafundishe watoto kuwaheshimu watu wengine, haki zao, na maoni yao

✔ Wategemeze watoto wako kwa kufahamiana na walimu wao, na wajulishe walimu kwamba unawathamini na unaunga mkono jitihada zao

✔ Usitatue matatizo kwa kupiga kelele au kwa kutumia jeuri

Watoto wako wanahitaji shauku yako yenye joto

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kuwa na upendezi katika kazi ya shule ya mtoto wako kwaweza kuwa ulinzi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki