Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Mikao Hospitalini Asanteni sana kwa habari fupi, yenye kujaa maana katika makala “Hospitali—Wewe Waweza Kukabilianaje?” (Septemba 8, 1991) Ningependa kuongeza kwamba katika hali isiyo ya dharura, baada ya kutambulisha ugonjwa kwa usahihi, unapaswa kujifunza sana juu ya ugonjwa wako na matibabu yao kwa kadiri uwezavyo. Ni baada tu ya kuwa na ufahamu mwema ndipo unapoweza kufanya maamuzi mazuri. Maktaba ya mahali penu au maktaba ya hospitali mara nyingi huwa na habari nyingi zenye msaada.
E. D., United States
Binadamu na Mnyama ingependa kuonyesha uthamini wangu wa kutoka moyoni kwa habari “Wakati Binadamu na Mnyama Waishipo kwa Amani.” (Septemba 8, 1991) Nimekuwa nikijifunza Biblia kwa mwaka mmoja sasa, na nimejifunza kuhusu makusudi ya Yehova ya kufanya dunia iwe paradiso ya milele. Makala hiyo iliongezea sana upendo wangu kwa Yehova na tamaa yangu ya kuishi kwa amani na wanyama katika ulimwengu wake mpya.
A. S., Brazili
Mimi hupenda wanyama. Hata nilitaka kujiunga na chuo kikuu katika programu ya kujifunzia wanyama. Hata hivyo, ningelipata faida ipi, kutumia maisha yangu kujifunza aina chache tu za wanyama? Katika ulimwengu mpya wa Yehova, nitaweza kujifunza juu ya wanyama wote—milele! Kusoma makala hiyo kulinifanya nitokwe machozi ya shangwe, nikijua kuwa siku moja matamanio hayo yatakuwa hakika.
L. M., United States
Watoto wa Talaka Shukrani za moyoni kwa makala “Msaada kwa Watoto wa Talaka.” (Oktoba 8, 1991) Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, baba alitaliki mama yangu. Mama alifanya kazi nzuri ya kutulea na dada yangu mchanga tumpende Yehova. Lakini wakati wa miaka ya utineja, ilikuwa sawa na vile mlivyoeleza. Nilihisi kwamba “mahusiano yote hayategemeki, yakielekea kufunuka siku fulani katika usaliti na ukosefu wa uaminifu.” Niliogopa kuwapenda wengine na kupendwa, na hata miongoni mwa Wakristo wenzangu, niliweka mahusiano yote yakiwa ya kijuu juu tu. Kwa kujifunza kufanyia mambo watu wengine na kutumikia nikiwa mwevanjeli wa wakati wote kulinisaidia kushinda mielekeo hiyo kwa kiwango fulani. Hata hivyo, makala yenu iliniwezesha kuelewa baadhi ya hisi zangu za ndani sana kwa mara ya kwanza.
M. H., Japani
Makala hizo zilifanya mimi na mume wangu tuhisi tumekosea. Mume wangu wa kwanza alitengwa na kundi la Kikristo kwa sababu ya kukosa uaminifu. Ndipo mimi na wavulana wangu tulipohamia kwa wazazi wangu, umbali wa kilometa 3,200 hivi. Wavulana hao walikuwa na uwasiliano mdogo sana na baba yao. Baada ya mimi kuolewa tena, tuliendelea kukatiza uwasiliano wowote, tukihisi kuwa baba alikuwa uvutano mbaya. Je! tulifanya uamuzi unaofaa?
C. W., United States
Talaka au kutengwa na kundi la Kikristo hakukatizi uhusiano wa mzazi na mtoto; watoto huendelea kuhitaji wazazi wote wawili. Hata hivyo, hali zinatofautiana. Umbali au kutojali kwa aliyekuwa mwenzi kwaweza kupunguza sana uwasiliano wa mzazi na mtoto. Kwa upande mwingine, mahakama yaweza kuweka mipango ya ziara, na huenda Mkristo asiwe na la kufanya ila tu kushirikiana. Mahali ambapo hakuna mipango ya kuzuru ambayo imeamuriwa na mahakama, ni juu ya mzazi mwenye utunzi wa watoto kuamua kama ushirikiano na aliyekuwa mwenzi wa ndoa ungekuwa hatari sana kimwili au kiroho.
—MHARIRI.
Asanteni kwa kweli tupu iliyo katika makala zenu juu ya talaka. Wazazi wangu walitaliki nilipokaribia umri wa miaka 20, na nikapitia kipindi ambamo nilichukia mpango wenyewe wa ndoa. Niliuona kama mtego au gereza! Kwa msaada wa vitabu na magazeti yenu yenye kuongozwa na Biblia, ninatazamia kuoa siku fulani, nikitarajia kufanya hivyo hivi karibuni.
L. T., United States