Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 12/8 kur. 4-10
  • Ulimwengu Mpya Unaoridhisha Wote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ulimwengu Mpya Unaoridhisha Wote
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matatuzi ya Wakati Uleule
  • Matatizo Mengine Yatatuliwa
  • Sio Ndoto ya Mataraja Yanayoahirishwa
  • Ulimwengu Mpya Utakuridhisha
  • Namna Mahitaji Yetu Yatakavyojazwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Kuwa Raia wa Serikali ya Mungu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Serikali ya Mungu ya Amani
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 12/8 kur. 4-10

Ulimwengu Mpya Unaoridhisha Wote

HATA iwe vigumu kuaminika jinsi gani, ulimwengu mpya kwa kweli u karibu. Utawasili kwa wakati ili kuokoa dunia yetu kabla ya uwezo wayo wa kuendeleza uhai haujaharibiwa kabisa. Na ulimwengu huo mpya utaondoa hatari zote zinazotisha kuwako kwa binadamu. Utafanyaje hivyo?

Baada ya kutaja kuhusu hali ya ulimwengu yenye hatari, mwanahistoria Arnold J. Toynbee aliuliza hivi miaka mingi iliyopita: “Tutafanya nini ili tuokolewe?” Akijibu swali lake mwenyewe, yeye alisema: “Katika siasa, anzisha mfumo wa ushirikiano wa kikatiba wa serikali ya ulimwengu.”

Hata hivyo, ingawa ulimwengu mpya unaokuja ni “mfumo wa ushirikiano,” huo hautakuwa “katika siasa.” Hautatia ndani demokrasia au mawazo yoyote mengine ya kisiasa yaliyofanyizwa na mwanadamu. Ulimwengu huo mpya utatimiza miradi yao kwa sababu serikali moja tu ndiyo itakayotawala juu yao. Katika mfululizo wa hatua zenye kushangaza, serikali hiyo ya tufe lote itaondoa upesi matatizo yote yanayokabili binadamu leo. Jinsi gani? Kwa kuondolea mbali visababishi vya matatizo hayo na vizuizi ambavyo mara nyingi huzuia jitihada za kuyatatua.

Kihalisi, hilo lingeweza kutimizwaje kamwe? Je! watu wasiokamilika wasingekuwa bado wanatawala, watu ambao wamethibitika kuwa wafisadi na wasioweza kutatua matatizo ya mwanadamu? Basi, ebu wazia ikiwa kungekuwako watawala wakamilifu katika serikali hiyo ya ulimwengu, wakiwa na masilahi ya raia zao moyoni bila ubinafsi. Basi fikiria jinsi matatizo yangeweza kutatuliwa.

Matatuzi ya Wakati Uleule

Kukiwa na serikali ya tufe lote ya watawala wakamilifu, kila taifa na aina yalo ya serikali hususa hazingekuwako tena. Watawala, mabalozi, na wanasiasa wengine wasingekuwa tena na uwezo juu ya mataifa, makabila na jamii mbalimbali za ainabinadamu. Miji mingi ya sehemu na ya kitaifa, kutia na majengo na makao yayo rasmi, isingehitajika. Hilo lingekomesha gharama kubwa za kudumisha majengo hayo, pamoja na gharama za usafiri za maofisa wanaohudhuria mabaraza, mikutano ya halmashauri, na mijadala ya kitaifa na ya kimataifa. Mashirika yote ya serikali yenye kutumia mali ovyoovyo yangekoma pia, kutia na wasaidizi, masekretari, na makarani wayo wengi, na utaratibu mwingi wa kiofisi ambao huzuia maendeleo.

Amani ingekuwa halisi kwa sababu utaifa wenye kugawanya ungekoma, mahali pao pakichukuliwa na mamlaka ya tufe lote yenye muungano. Majeshi, wanamaji, na wanahewa, pamoja na silaha zao zote, wafanyakazi wa makamanda wenye vyeo vikubwa, na maofisa wa vyeo vya chini, wasingehitajika tena ili kulinda enzi ya kila taifa. Wala kusingekuwako mifumo yoyote ya upelelezi. Chini ya serikali ya tufe lote yenye watawala wakamilifu, kusingekuwako masoko huru au yale ya magendo ambamo silaha zingeweza kununuliwa au kuuzwa; wala kusingekuwako maeneo yanayobishaniwa. Watu wote duniani wangekuwa udugu mmoja usioweza kugawanyika. Kwa hiyo, utaifa ungetokomea mbali.

Fikiria manufaa zaidi ambazo zingekuwa za watu walio chini ya serikali moja isiyogawanyika yenye watawala wakamilifu. Wafanya biashara wenye uwezo mkubwa, kama vile watengenezaji silaha, wasingekuwa na njia yoyote ya kuwavuta wanasiasa ili kwamba waendelee kutokeza na kuuza bidhaa zao zenye uharibifu. Kusingekuwako tena watu wajanja wenye kuwashawishi wabunge kuhusu sheria au miswada fulani inayoathiri faida zao tu; hakuna tena vurugu ya idara za serikali zinazofanya kazi maalumu zinazopingana katika makusudi yazo, zikitumia kiasi kikubwa cha fedha katika miradi isiyofaa kitu inayofaidi watu wachache tu; hakuna kupinga masuluhisho ya matatizo ya uchafuzi kwa ajili ya sababu za kibiashara zenye ubinafsi (ili kuendelea kupata faida nyingi); hakuna kupinga sheria ambazo zingelinda jamii ya wanyama wanaokaribia kumalizika kwa faida za kipekee zenye nguvu.

Matatizo Mengine Yatatuliwa

Serikali kamilifu kama hiyo isingevumilia ukosefu wa kufuata haki. Baada ya kutwaa uongozi, ingehakikisha kwamba matendo ya uhalifu yangeshughulikiwa katika njia ifaayo, yenye haki. Hivyo, raia wasingekuwa na hofu kwamba wauaji hatari zaidi wangeweza kuua wengi kimakusudi.

Na namna gani mashirika ya uhalifu na mashirika ya biashara ya dawa za kulevya yaliyopangwa kitengenezo yenye kuenea na yenye uwezo mkubwa ulimwenguni pote? Serikali kamilifu ya ulimwengu ingeweza kukomesha kabisa yote hayo. Sheria za kitaifa zinazozuia wahalifu wasirudishwe nchi nyingine ili wahukumiwe zisingekuwa tena maficho ya wahalifu wa kimataifa. Kutumiwa kwa ujanja kwa upungufu wa sheria za nchi ili kuzikiuka na kutumiwa kwa mahusiano ya kisiasa yenye nguvu na hao wavunja sheria kutakuwa jambo la zamani. Tendo hilo moja la kufutilia mbali uhalifu pia lingeiondolea dunia matatizo mengine mengi ya kijamii, kama vile kucheza kamari, vita vya magenge, pornografia, umalaya na magendo. Ni utatuzi wenye matokeo na usiogharimu kama nini!

Naam, matatizo yote yaliyo tata, magumu, na yanayofumba yanayotatiza watu wenye akili zaidi kati ya ainabinadamu leo yangetatuliwa kabisa katika ulimwengu mpya kama huo. Na kila mojawapo lingetatuliwa kwa muda wote—kikamili. Vizazi vijavyo visingelazimika kuteseka hayo tena.

Sio Ndoto ya Mataraja Yanayoahirishwa

‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘watawala hao wakamilifu watatoka wapi ili kutawala ulimwengu huo mpya?’ Muumba wa mwanadamu atawaleta! Je! hilo laonekana kuwa gumu kuaminika? Basi, ebu fikiri: Ikiwa ungalikuwa na uwezo wa kufanya hivyo, je usingalikomesha hali zote duniani zinazoleta taabu nyingi? Bila shaka ungalizikomesha! Basi je! twapaswa kufikiri kwamba Muumba wetu hatafanya zaidi ya hiyo?

Jambo ni kwamba, Muumba wetu mwenye upendo anakusudia kuumba ulimwengu mpya, na njia ya kuuleta ni kupitia serikali ya ulimwengu yenye uadilifu. Hiyo ndiyo Mwanae, Yesu Kristo, aliwafundisha wanadamu kuomba kwa maneno haya: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Ufalme huo ni serikali halisi, serikali ya ulimwengu. Mfalme wayo, Yesu Kristo, ‘atakuwa na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia.’ (Zaburi 72:8) Na karibuni itachukua mahali pa serikali zote za wanadamu, kama vile Neno la Mungu linavyoahidi linaposema: “Na katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali inayotawalwa na Mfalme wa Mungu, Yesu Kristo] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote [za leo] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

Kwa kuwa serikali hiyo iliyosimamishwa na Mungu wa mbingu itasimamiwa na watawala wanaopita uwezo wa wanadamu, itatimiza mambo yote mazuri ambayo watawala wa kibinadamu wanashindwa kufanya. Biblia inaeleza serikali ya Mungu kuwa serikali ya mtawala mmoja wa kimbingu ambayo itakuwa na Mfalme, Yesu Kristo, akisaidiwa na wafanyakazi 144,000 watu wa roho. Watawala hao wote watakuwa watu wenye kuaminika walioonyesha uaminifu-maadili usio na hatia walipoishi duniani kabla ya kufufuliwa kwenye uhai mbinguni. Wote watakuwa katika hali nzuri kabisa ya kufanya kazi kwa ajili ya mema ya ainakibinadamu kwa sababu waliona mahitaji ya wanadamu walipoishi duniani.—Ufunuo 14:1-3.

Fikiria matatizo ambayo hilo linaondosha. Kwa sababu hawawezi kufa, watawala hao wa roho hawatachoka au kuzeeka. (1 Wakorintho 15:50, 53) Na hawawezi kufisidiwa na mashawishi ya kupunja haki au kuonyesha upendeleo kwa kupewa zawadi. Kwa vyovyote, mtu anaweza kutoa nini kisiri kiwe hongo kwa mtu wa roho asiyekufa? Fedha, sanduku la pombe ghali, safari kwenda kwenye kisiwa cha fahari, au tiketi ya maonyesho au maigizo? Vitu hivyo vya kimwili vyaweza kujaribu wanadamu lakini si viumbe-roho hao. Kwa hiyo watu watakaoongozwa na watawala hao hawatapatwa na ufisadi wa serikali ulio wa kawaida sana leo.

Ulimwengu Mpya Utakuridhisha

Je! wewe ni mzee-mzee? Fikiria maarifa yote, stadi, na ujuzi ambao umepata kwa muda wa miaka. Lakini je! umeona kwamba ingawa huenda akili yako au uwezo wako wa akili ukawa mzuri, uwezo wako wa kimwili unadhoofika polepole lakini kwa kuendelea? Mwili wako hauitikii tena maagizo yako ya akili kama ulivyofanya wakati mmoja. Naam, wepesi wako wa kufanya mambo unapungua, nguvu yako inapungua, na uvumilivu wako unapungua. Uwezo wako wa kuona na kusikia unazidi kufifia na misuli yako inazidi kudhoofika huku maumivu yakizidi kuwa ya mara kwa mara.

Lakini jaribu kuwazia hekima inayopatikana kwa muda wa miaka mingi ya kuishi iliyo katika mwili mchanga ulio bora hata kuliko ule uliokuwa nao ulipokuwa katika miaka yako ya 20—naam, uwezo wako wa kimwili ukiwa mzuri kama ule wa akili yako. Fikiria mambo mengi ambayo ungeweza kufanya ukiwa na mwili wako wenye afya! Kwani, ukiwa na mwili wenye afya hivyo unaopatana na akili yako komavu, ungepata kwamba kazi yoyote unayofanya ingekufurahisha sana. Ujuzi wako ungekuwezesha kufanya mambo kwa njia bora zaidi, jambo ambalo lingekuongezea sana uradhi. Na ikiwa wewe ni kijana, wazia furaha ya kudumisha ujana wako na nguvu zako huku ukiongeza hekima, maarifa, na ujuzi milele.

Sasa, piga hatua nyingine tena, na ufikirie washiriki wako na marafiki, waandamani na watu wa ukoo, wote wakiwa katika hali hiyohiyo. Wazia yale ambayo ninyi nyote mngeweza kutimiza kwa namna ya ujenzi, uundaji, au ufundi. Ah, hayo ni mataraja mazuri yaliyoje kwa watu wenye vipawa, kama vile wasanii, wanamuziki, warembeshi, watengeneza bustani, wapanda maua, na wastadi wa mimea! Mambo ambayo wangetimiza yangestaajabisha! Machache kati yayo ni michoro, makao, mashamba, bustani nzuri sana—naam, kutokezwa kwa ala nzuri za muziki na usanii wa kuwa stadi wazo.

Kusudi moja la serikali hiyo ya ulimwengu mpya ni kurudisha jamii ya kibinadamu kwenye ukamilifu wa kimwili. Uwezo wako wa kuona, kusikia, na hisia nyinginezo zingetenda kazi vizuri sana. Kwa muda gani? Ikiwa serikali ya kibinadamu ingekutolea tiba ambayo ingekuhakikishia kufanywa upya kwa asilimia 50 kwa viungo vyote vya mwili wako kwa muda wa mwaka mmoja kwa kiasi kidogo tu cha pesa, Je! usingekuwa wa kwanza kwenye mstari ili kuipata? Serikali hiyo ya ulimwengu mpya inahakikisha kurudishwa kamili kwa nguvu za ujana, kwa asilimia 100 bila malipo—si kwa muda wa mwaka mmoja, miaka 5, au miaka 50, bali kwa umilele wote.

Usidhani kwamba ni vigumu kuamini taraja hilo zuri ajabu ambalo kwa hakika litafurahiwa na wanadamu kwenye dunia ii hii. Angalia, kwenye ukurasa 7 hadi 10 baadhi ya baraka zitakazofurahiwa na wale wanaompenda Mungu.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7-10]

Yale Yatakayoletwa na Ulimwengu Mpya

Kukomeshwa kwa Uhalifu na Jeuri

“Bali waovu watatengwa [watakatiliwa mbali, New World Translation] na nchi.”—Mithali 2:22.

Kuondolewa Mbali kwa Vita

“Watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.

Vitu Vingi Vizuri vya Kuliwa na Wote

“Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.”—Zaburi 72:16.

Makao Mazuri na Kazi Yenye Kufurahisha kwa Kila Mtu

“Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.”—Isaya 65:21, 22.

Amani Kati ya Watu na Wanyama

“Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; . . . na mtoto mdogo atawaongoza.”—Isaya 11:6.

Hakuna Ugonjwa Tena, Uzee, au Kifo

“Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.

Ufufuo wa Wapendwa Waliokufa

“Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [maziara ya ukumbusho, NW] wataisikia sauti yake [Yesu]. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki