Ishara ya Jumla Yenye Sehemu Nyingi
Mwisho wa Ulimwengu—Ni karibu Kadiri Gani?
HEKAYA moja kutoka India husema juu ya wanaume sita vipofu kutoka Indostan walioenda kumwona ndovu. Yule wa kwanza aligusa sehemu ya upande wa ndovu na kusema: “Ala! ndovu anafanana sana na ukuta!” Wa pili aligusa pembe zayo na kusema: “Ndovu anafanana sana na mkuki!” Wa tatu aligusa mkonga wayo na kusema: “Ndovu anafanana sana na nyoka!” Wa nne alifikilia akagusa goti layo na kusema: “Ni wazi ndovu anafanana sana na mti!” Wa tano aligusa sikio layo na kusema: “Ndovu huyu wa kustaajabisha anafanana sana na upepeo!” Yule wa sita alishika mkia wayo na kusema: “Ninaona ndovu anafanana sana na kamba!” Wanaume hao sita vipofu waligombana kwa muda mrefu na kwa ukali kuhusu ndovu anafanana na nini, lakini hakuna yule aliyetoa maelezo sahihi. Habari isiyo kamili haikutoa picha kamili.
Tatizo hilohilo hutokea kwa habari ya kutambua ishara ya kurudi kwa Kristo. Kwa kuitikia swali la wanafunzi wake: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Yesu alijibu: “Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi; na njaa na tauni mahali mahali.” (Mathayo 24:3, NW; Luka 21:10, 11) Lakini wakati mambo hayo tu yanapotajwa kuwa ithibati kwamba Kristo alirudi mwaka 1914, watu hupinga: “Aa! sikuzote kumekuwa na vita, njaa, tauni, na matetemeko ya nchi!” Na hawakosei.
Mambo hayo machache—ingawa kufikia sasa yameleta taabu isiyopata kuonwa—kwa watu wengi hayatoshi kutia alama kurudi kwa Kristo; mengi yanahitajiwa ili kufanya ishara hiyo iwe kamili, iliyo dhahiri. Wakati mwisho wa ulimwengu unapopigiwa mbiu kwamba u karibu kwa kutegemea ithibati chache, juu ya ishara moja au sehemu chache za ishara zinazoonwa, maonyo bandia hutokea. Yale yanayohitajiwa ni sehemu zote ambazo Yesu alitoa kuhusu kurudi kwake, si moja tu au chache. Yale aliyotoa ili kutia alama kuwapo kwake yalikuwa ishara ya jumla, ishara iliyofanyizwa kwa sehemu za kutosha kufanya ishara iwe ya hakika, jumla ya sehemu kadhaa mbalimbali ambazo, zikiwa pamoja, zinaifanya iwe dhahiri.
Ukiwa mfano wa ishara ya jumla, fikiria ule uliotolewa katika Biblia ili kumtambulisha Yesu kuwa Mesiya wakati wa kuja kwake kwa kwanza. Ilitia ndani matukio mengi yaliyohusu Mesiya yaliyotolewa katika Maandiko ya Kiebrania. Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake kuhusu baadhi ya maandiko hayo, lakini hawakuwa wameelewa maana yayo. Kama Wayahudi kwa ujumla, wanafunzi walitaka mesiya ambaye angepindua Rumi na kutawala ulimwengu, wao wakiwa washiriki. Kwa hiyo alipokufa, walivurugika na kukatishwa tamaa. Baada ya kufufuliwa kwa Yesu, alikutana nao na kusema: “Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii, na Zaburi. Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko.”—Luka 24:44, 45.
Kulingana na tafsiri ya Kingdom Interlinear ya mstari wa 45, Yesu alifanya hivyo kwa “kuweka pamoja Maandiko” kutoka kwa sehemu ya Kiebrania ya Biblia iliyotabiri matukio na hali za maisha ya Mesiya aliyeahidiwa ambaye angekuja, na kuyaweka pamoja na matukio ya maisha ya Yesu ambayo yalikuwa yameyatimiza. Baadaye, mtume Paulo alitumia njia iyo hiyo alipokuwa “akieleza na kuthibitisha kwa marejezo” kwamba Yesu ndiye Mesiya. (Matendo 17:3, NW) Tena, ni Kingdom Interlinear inayodhihirisha utaratibu kwa kusema kwamba alifanya hivyo kwa “kufunua kabisa na kulinganisha” unabii mbalimbali wa Kimesiya katika Maandiko ya Kiebrania na matukio ya maisha ya Yesu ambayo yaliutimiza. Sanduku linaloandamana laonyesha baadhi ya unabii mwingi wa Kiebrania uliotimizwa na matukio ya maisha ya Yesu na yaliyothibitisha kwamba ndiye aliyekuwa Mesiya aliyetabiriwa. Inaonyesha yale yanayotiwa ndani katika ishara ya jumla.
Ishara ya Jumla ya Kuwapo kwa Kristo
Ni ishara ya jumla kama hiyo tu ndiyo inayotia alama wakati wa kuja kwa pili kwa Yesu, au kwa usahihi zaidi, kuwapo kwake. Neno la Kigiriki pa·rou·si̇́a ambalo tafsiri nyingi hufasili “kuja” kwenye Mathayo 24:3 halimaanishi wakati fulani ambao angekuja au awasili bali lamaanisha kwamba tayari amekwisha wasili na yu karibu, yeye yupo. Katika kisa cha Yesu inamaanisha kwamba yeye yupo bila kuonekana akiwa Mfalme mwekwa wa Yehova na anatawala akiwa mbinguni. Hilo linapatana na maneno ya Yesu kwenye Yohana 14:19: “Bado kitambo kidogo na ulimwengu haunioni tena.” Kwa kuwa hangeonekana kimwili, alitoa ishara ambayo ingeonyesha kurudi kwake na kuwapo kwake kusikoonekana akiwa Mfalme wa Yehova anayetawala.
Ishara aliyotoa haikuwa na jambo moja tu au mambo machache tu. Ilikuwa na mengi ambayo yangechukuliwa pamoja kuwa ishara ya jumla, kama ilivyokuwa na ishara ya jumla wakati wa kuja kwake kwa kwanza akiwa Mesiya. Hivyo, kukiwa na mambo au matukio mengi, yeye aonyesha kwa dhahiri kuwapo kwake kusikoonekana wakati huu akiwa Mfalme wa Yehova anayetawala aliyetawazwa mbinguni lakini anayeeneza uwezo na uvutano wake juu ya mambo duniani. Maonyo bandia yaweza kutolewa wakati jambo moja au mawili tu yanapokaziwa, badala ya mambo mengi yanayofanyiza ishara ya jumla. Ni kama wale wanaume sita vipofu kutoka Indostan, ambao kila mmoja wao alifikia mkataa mbaya kwa sababu ya kuhisi sehemu moja tu ya mwili wa ndovu.
Kutimizwa kwa ishara hiyo ya jumla iliyotolewa na Yesu, hutia ndani hali za ziada zilizotolewa na mitume watatu, kulianza kwa njia yenye kutokeza kuanzia 1914 kuendelea. Muhtasari wa mambo hayo mbalimbali pamoja na utimizo wayo unafuata.
“Taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Vita ya Ulimwengu 1 ilianza mwaka 1914 huku mataifa 28 yakitiwa ndani, watu milioni 14 wauawa. Vita ya Ulimwengu 2 ikafuata huku mataifa 59 yakitiwa ndani, watu milioni 50 wauawa.
“Tauni mahali mahali.” (Luka 21:11) Vita ya Ulimwengu 1 ilipokwisha, watu wapatao milioni 21 waliuawa kwa homa ya Kihispania. Tangu wakati huo, ugonjwa wa moyo, kansa, UKIMWI, na tauni nyinginezo zimeua mamia ya mamilioni.
“Kutakuwa na njaa.” (Mathayo 24:7) Njaa kubwa zaidi ya yote katika historia ilianza baada ya Vita ya Ulimwengu 1. Nyingine yenye kuhofisha ilifuata Vita ya Ulimwengu 2, na sasa ukosefu wa lishe bora huathiri sehemu moja kwa tano ya idadi ya watu ulimwenguni. Kila mwaka, watoto wapatao milioni 14 hufa kutokana na ukosefu wa lishe bora.
“Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi.” (Luka 21:11) Matetemeko ya nchi baada ya 1914—fikiria machache makubwa. Katika 1915, nchini Italia, 32,610 wauawa; 1920, Uchina, 200,000 wauawa; 1923, Japan, 143,000 wauawa; 1939, Uturuki, 32,700 wauawa; 1970, Peru, 66,800 wauawa; 1976, Uchina 240,000 (wengine husema 800,000) wauawa; 1988, Armenia, 25,000 wauawa.
“Kuongezeka maasi.” (Mathayo 24:12) Maasi yameenea sana tangu 1914; leo yanaongezeka kwa kasi. Uuaji wa kukusudia, unajisi, wivi, vita vya magenge—hayo ndiyo hufanyiza vichwa vikuu na matangazo ya habari. Wanasiasa hupunja umma, matineja hubeba bunduki na kuua, watoto wa shule hushambuliana. Katika sehemu nyingi si salama kutembea barabarani hata wakati wa mchana.
“Dhiki ya mataifa [wasijue njia ya kutokea, NW] . . . Watu wakivunjika mioyo kwa hofu, na kwa kutazamia mambo yakatakayoupata ulimwengu.” (Luka 21:25, 26) Uhalifu, jeuri, uzoefu wa dawa za kulevya, kuvunjika kwa familia, uchumi uliozorota, ukosefu wa kazi—orodha ni ndefu na inazidi kuongezeka. Mwanasayansi mmoja mashuhuri alisema: “Tutakula woga, tulale kwa woga, tuishi kwa woga na tufe kwa woga.”
“Siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1) Mtume Paulo alisema juu ya watu ‘ambao wameisha kufa ganzi.’ (Waefeso 4:19) Hata hivyo, alifafanua juu ya kuvunjika kwa maadili alikotabiri kwa ajili ya “siku za mwisho.” Kunasikika kuwa kama matangazo ya habari ya leo: “Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.”—2 Timotheo 3:1-5.
“Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka.” (2 Petro 3:3) Nyusipepa, matangazo ya habari, magazeti, vitabu, na sinema hupuuza Biblia kwa dhihaka na kutumia propaganda yao wenyewe ya kufikiri kwa kujitegemea badala ya kutegemea Biblia, wakisema, kama vile Petro alivyotabiri: “Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.”—2 Petro 3:4.
“Watawakamata na kuwaudhi.” (Luka 21:12) Kuanzia mwaka 1914 na kwa muda wa miaka, Mashahidi wa Yehova wamekamatwa kikatili, wakashtakiwa kwa uwongo, wakapigwa na magenge, na kutupwa kwa maelfu katika kambi za mateso za Hitler, ambamo waliteswa, wengi wakauawa, wengine kikatili kwa kukatwa kichwa. Katika mabara mengine, ya kidikteta na kidemokrasia pia, kazi yao ya kutoa ushahidi kwa Yehova na Ufalme wake imepigwa marufuku na Mashahidi wakatupwa gerezani. Yote hayo kwa utimizo wa maneno ya Yesu kuhusu siku za mwisho.—Mathayo 5:11, 12; 24:9; Luka 21:12; 1 Petro 4:12, 13.
“Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote.” (Mathayo 24:14) Habari njema zipi? Habari njema za Ufalme wa Kristo ukitawala kutoka mbinguni, kwani hilo ndilo swali aliloulizwa Yesu lililotokeza unabii wake wa ishara ya jumla juu ya tukio hilo. Zimehubiriwa na Mashahidi wa Yehova tangu 1914. Elfu nne walikuwa wakifanya hivyo katika 1919, zaidi ya milioni nne kufikia 1990, na katika 1992 katika mwezi mmoja 4,472,787. Fasihi ya Biblia iligawanywa katika lugha zipatazo 200 katika nchi 229. Sehemu hii ya ishara ya jumla haijapata kamwe kutimizwa hapo mbeleni.
“Kuharibu hao waiharibuo nchi.” (Ufunuo 11:18) Sikuzote wanaume wenye pupa wametaka kuiharibu dunia kwa faida za kichoyo, lakini kabla ya karne hii hawakuwa wamepata kamwe kuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Sasa, tangu 1914, tekinolojia ya kisasa imewapa uwezo huo, na wanautumia vibaya. Wao wanaiharibu dunia.
Hapa pana baadhi ya mabaya yanayotokea: mvua ya asidi, kuongezeka kwa joto la dunia, mashimo katika tabaka ya ozoni, dawa za wadudu zilizo hatari, takataka za sumu, msongamano wa takataka, takataka za nyukilia, kuvuja kwa mafuta, kutupwa kwa takataka chafu, maziwa ya maji yasiyo na kitu, misitu iliyoharibiwa, maji ya ardhi yaliyochafuliwa, jamii ya wanyama walio hatarini, afya ya binadamu iliyoharibiwa.
Mwanasayansi Barry Commoner asema: “Ninaamini kwamba ikiwa kuchafuliwa kwa dunia kunakoendelea hakutakomeshwa, hatimaye kutaharibu kufaa kwa sayari hii kuwa mahali pa uhai wa kibinadamu. . . . Tatizo si kutojali kwa sayansi, bali ni pupa ya kukusudia.” State of the World 1987 chasema: “Kiwango cha utendaji wa kibinadamu umeanza kutisha uwezo wa kukalika kwa dunia yenyewe.” Mfululizo wa televisheni ulioonyeshwa katika 1990 ulikuwa na kichwa cha kutokeza “Jitihada za Kuokoa Sayari Hii.”
Matukio hayo mengi yakijumlishwa kuwa ishara moja katika wakati wa kizazi kimoja hayawezi kupuuzwa kuwa tukio la ajali tu. Ukubwa wayo pia huongeza maana. Na baadhi ya matukio hayo, kama kuhubiriwa kwa ujumbe huu wa habari njema na kuharibiwa kwa dunia, ambako hakujapata kutukia tokea mwanzo wa uumbaji. Ishara ya jumla ya kuwapo kwa Kristo Yesu ni dhahiri sana.
”Mtu akiwa na masikio ya kusikilia, na asikie.”—Marko 4:23
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Ithibati ya Jumla ya Kuja kwa Kwanza kwa Yesu Akiwa Mesiya
ATAZALIWA katika kabila la Yuda (Mwanzo 49:10); achukiwe, asalitiwe na mmoja wa mitume wake; kura zapigwa kwa ajili ya vazi lake; apewa siki na nyongo; atukanwa akiwa kwenye mti; hakuna mifupa inayovunjika; hakuona uharibifu; afufuliwa (Zaburi 69:4; 41:9; 22:18; 69:21; 22:7, 8; 34:20; 16:10); azaliwa na bikira; familia ya Daudi; jiwe la kikwazo; akataliwa; akimya mbele ya washtaki; achukua magonjwa; ahesabiwa na wafanya dhambi; kifo cha kidhabihu; achomwa kwenye upande wake; azikwa pamoja na matajiri (Isaya 7:14; 11:10; 8:14, 15; 53:3; 53:7; 53:4; 53:12; 53:5; 53:9); aitwa kutoka Misri (Hosea 11:1); azaliwa katika Bethlehemu (Mika 5:2); atolewa kuwa mfalme; ampanda punda; asalitiwa kwa vipande 30 vya fedha; wafuasi watawanyika.—Zekaria 9:9; 11:12; 13:7.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Ishara ya Jumla ya Kuwapo kwa Kifalme kwa Yesu Kwenye Kuja kwa Pili
VITA ya ulimwengu; upungufu wa chakula; tauni; matetemeko ya nchi (Mathayo 24:7; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:1-8); uasi ulioongezeka; wasalitiana na kuchukiana; wasiotii wazazi wao; wasiowapenda wa kwao, wasiojizuia; wasiotaka kufanya suluhu, wenye kupenda fedha; wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; wenye mfano wa utauwa lakini wakikana nguvu zake; wakaidi; wakali; wanyanyasa wafuasi wa Kristo; waleta wafuasi mbele ya mahakama, na kuua wafuasi wa Kristo (Mathayo 24:9, 10, 12; Luka 21:12; 2 Timotheo 3:1-5); wadhihaki wa kuwapo kwa Yesu; wasema mambo yote yaendelea vilevile tangu mwanzo wa uumbaji (2 Petro 3:3, 4); waharabu wa mazingira ya dunia.—Ufunuo 11:18.