Je! Wakati Umeenda Sana Kuliko Unavyofikiri?
SIKU tatu kabla ya kifo chake, Yesu alikuwa na siku yenye shughuli sana katika Yerusalemu, siku ambayo ikawa ndiyo yenye umaana kabisa kwa Wakristo wanaoishi sasa. Alifundisha katika hekalu, akigeuza maswali mengi ya kumtega yawarudie viongozi wa kidini Wayahudi waliojaribu kumnasa. Mwishowe, aliwatupia waandishi na Mafarisayo shutumu kali lililowabandika sifa ya kuwa wanafiki na nyoka-vipiri wenye kuelekea Gehena.—Mathayo, sura 22, 23.
Alipokuwa akiondoka kwenye eneo la hekalu, mmoja wa wanafunzi wake alimwambia hivi: “Mwalimu, tazama, yalivyo mawe na majengo haya!” Yesu, bila kuvutiwa, akamwambia hivi: “Wayaona majengo haya makubwa? Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomolewa.” (Marko 13:1, 2) Ndipo Yesu akaondoka kwenye hekalu kwa mara ya mwisho, akashuka kuingia Bonde la Kidroni, akavuka ng’ambo nyingine, na kuipanda miinuko ya Mlima wa Mizeituni.
Akiwa ameketi katika jua la kumalizia alasiri hapo juu ya mlima, huku hekalu likionekana juu ya Mlima Moria ng’ambo ya bonde hilo, Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea walimjia kwa faragha. Maneno aliyokuwa ametamka juu ya kubomolewa kwa hekalu yalikuwa mazito juu ya akili zao. Walimwuliza hivi: “Tuambie, Mambo hayo yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3; Marko 13:3, 4, NW) Jibu alilotolea swali lao alasiri hiyo juu ya Mlima wa Mizeituni ni la muhimu sana kwetu. Laweza kutuzuia tusingoje mno kabla ya kufikiria “umalizio wa mfumo wa mambo.”
Swali lao lilikuwa la sehemu mbili. Sehemu moja ilikuwa juu ya mwisho wa hekalu na mfumo wa Kiyahudi; ile nyingine ilihusu kuwapo kwa Yesu akiwa Mfalme na umalizio wa mfumo huu uliopo wa mambo. Maswali yote mawili haya yalihusishwa katika jibu la Yesu, kama lilivyotolewa katika Mathayo 24 na 25, Marko 13, na Luka 21. (Ona pia Ufunuo 6:1-8.) Kuhusu umalizio wa ulimwengu huu uliopo, au mfumo wa mambo, Yesu alieleza mambo ka-dhaa ambayo, yakichukuliwa pamoja, yangekuwa ishara ya ujumlisho yenye kutambulisha siku za mwisho. Je! hiyo ishara ya ujumlisho inatimizwa? Je! yatuweka sisi katika siku za mwisho zilizotajwa katika Biblia? Je! utimizo wayo watuonya kwamba huenda ikawa wakati umeenda sana kuliko tunavyofikiri?
Jambo moja la ishara ya ujumlisho ya Yesu ni hili: “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme.” (Mathayo 24:7, NW) Katika 1914, Vita ya Ulimwengu ya 1 ilianza. Mashahidi wa Yehova wa mwongo huo wakawa chonjo mara hiyo. Na kwa nini? Katika Desemba 1879, kama miaka 35 mapema, gazeti Mnara wa Mlinzi (kwa Kiingereza) lilikuwa limesema, kwa msingi wa orodha ya matukio ya Biblia, kwamba 1914 ungekuwa mwaka wenye umaana mkuu katika historia ya kibinadamu. Je! vita hii, vita ya kwanza kwa kadiri ya ulimwenguni pote kweli kweli, ambamo mataifa 28 yalihusika hatimaye na watu milioni 14 wakauawa, ingeweza kuwa ndiyo mwanzo wa matukio yenye kutimiza ishara ya Yesu ya ujumlisho juu ya ule mwisho? Je! mambo yale mengine ya ishara yangefuata?
Katika “ufunuo kwa Yesu Kristo,” mwosho-damu uu huu watabiriwa. Hapa farasi mwenye rangi kama ya moto na mpandaji wake ‘waondolea mbali amani kutoka dunia.’ (Ufunuo 1:1; 6:4, NW) Hakika hilo lilitendeka kuanzia 1914 hadi 1918. Na Vita ya Ulimwengu ya 1 ilikuwa mwanzo tu. Katika 1939, Vita ya Ulimwengu ya 2 ilifuata. Mataifa 59 yalifyonzwa kuingia katika pigano hilo, na watu kama milioni 50 wakauawa. Katika ile miaka 45 iliyofuata Vita ya Ulimwengu 2, vita zaidi ya 125 vimepiganwa, vikiua watu zaidi ya milioni 20.
Jambo jingine la ile ishara ni hili: “Kutakuwako upungufu wa chakula.” (Mathayo 24:7, NW) Kulikuwako njaa kuu yenye kuenea kotekote wakati na baada ya Vita ya Ulimwengu ya 1. Habari moja yaorodhesha njaa kubwa zaidi ya 60 tangu 1914, zikiua uhai wa mamilioni wengi. Zaidi ya hilo, hata sasa, watoto 40,000 hufa kila siku kutokana na ukosefu wa chakula chenye kufaa mwili na magonjwa yawezayo kuzuiliwa.
“Kutakuwako matetemeko ya dunia makubwa.” (Luka 21:11, NW) Hayo yalitikisa dunia baada ya Vita ya Ulimwengu ya 1 kuanza. Katika 1915 tetemeko la dunia lilichukua uhai wa watu 32,610 katika Italia; katika 1920 jingine likaua 200,000 katika China; katika 1923 katika Japani, 99,300 walikufa; katika 1935 katika ile ambayo sasa ni Pakistan, 25,000 walipoteza uhai wao; katika 1939 katika Uturuki, 32,700 walitokomea; katika 1970 katika Peru, 66,800 waliuawa; katika 1976 katika China, 240,000 (wengine husema ni 800,000) walikufa; katika 1988 katika Armenia, 25,000 walipoteza uhai wao. Kwa uhakika, kumekuwako matetemeko ya dunia makubwa tangu 1914!
“Katika mahali pamoja baada ya pengine magonjwa ya kipuku.” (Luka 21:11, NW) Katika 1918 na 1919, watu kama 1,000,000,000 walikuwa wagonjwa kwa homa ya Kihispania, na zaidi ya 20,000,000 walikufa. Lakini huo ulikuwa mwanzo tu. Katika ule ulimwengu unaositawi, maleria, homa ya konokono, upofu wa mtoni, ugonjwa wa kuhara vikali, na maradhi mengine yaendelea kulemaza na kuua mamia ya mamilioni. Kwa kuongezea, ugonjwa wa moyo na kansa huchukua uhai wa mamilioni wengine zaidi. Magonjwa yenye kuambukizwa kingono yanakumba ainabinadamu kwa wingi. Lenye kutia hofu kubwa katika mioyo ya watu leo ni lile pigo lenye kifo la UKIMWI, linalokadiriwa kuambukiza mhanga mpya kila dakika, kukiwa hakuna maponyo yenye kuonekana mbele.
“Kuongezeka kwa kutokutii sheria.” (Mathayo 24:12, NW) Kutokutii sheria kumeongezeka kwa fujo tangu 1914, na leo kunalipuka. Mauaji, visa vya kunajisi wanawake, unyang’anyi, vita vya magenge—huwa ndivyo vichwa vikubwa vya magazeti na habari za redio na televisheni. Jeuri ya bure tu yaendelea kuwaka bila kuzuiliwa. Katika United States, mtumia-bunduki anyunyiza marisau mia moja kutoka bunduki ya ushambulizi yenye kumimina risasi kwa kuzifyatusha kati ya umati wa watoto wa shule—5 wafa, 29 wajeruhiwa. Katika Uingereza mwanamume kichaa aua ovyo watu 16 kwa bunduki ya ushambulizi ya muundo wa AK-47. Katika Kanada mwanamume mmoja achukiaye wanawake aenda Chuo Kikuu cha Montreal na kuua 14 kati yao. Watu wa jinsi hiyo ni kama majibwa ya mwituni, simba, hayawani-mwitu, wanyama wasiosababu ambao wamezaliwa kushikwa na kuharibiwa.—Linganisha Ezekieli 22:27; Sefania 3:3; 2 Petro 2:12, NW.
“Watu wakizirai kwa sababu ya woga na taraja la vitu vinavyokuja juu ya dunia inayokaliwa.” (Luka 21:26, NW) Muda mfupi baada ya mlipuko wa lile kombora la atomi la kwanza, mwanasayansi wa atomi Harold C. Urey alisema hivi juu ya wakati ujao: “Sisi tutakula hofu, tutalalia hofu, tutaishi katika hofu na kufa katika hofu.” Kwenye hofu ya vita ya nyukilia imeongezewa hofu ya uhalifu, njaa kuu, ukosefu wa uthabiti katika uchumi, mzoroto wa maadili, kuchakaa kwa familia, uchafuzi wa dunia. Kwa uhakika, nyakati mbaya ambazo huonyeshwa mfululizo mbele yetu na magazeti ya kila siku na habari za televisheni hueneza hofu kila mahali.
Mtume Paulo pia aliandika juu ya hali ambazo zingekuwa nyingi katika siku za mwisho za mfumo huu wa mambo. Kusoma maneno yake ni kama kusoma habari za siku. “Lakini jua hili,” yeye akaandika, “kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wajipenda wenyewe, wapenda fedha, wenye kimbelembele, wenye kujigamba, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na shauku ya asili, wasiotaka mwafaka wo wote, wachongezi, bila kujiweza, wakali, bila upendo wa wema, wasaliti, wenye kichwa kigumu, wenye kuvimbishwa kwa kiburi, wapenda raha kuliko kuwa wapenda Mungu, wenye umbile la ujitoaji kimungu lakini wakithibitika kuwa mabandia kwa nguvu zao; na kutoka hao geuka mbali.”—2 Timotheo 3:1-5, NW.
Mambo Yote Yanaendelea “Hali Iyo Hiyo, Tangu Mwanzo wa Kuumbwa”?
Mtume Petro alitabiri jambo jingine la siku za mwisho: “Katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe, na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.”—2 Petro 3:3, 4.
Leo, wakati habari ya siku za mwisho itokeapo, watu wengi hutimiza maneno ya kiunabii ya Petro kwa kudhihaki na kusema hivi: ‘Ah, mambo yote hayo yametendeka kabla. Ni historia tu inayojirudia yenyewe.’ Hivyo basi wao hupuuza maonyo na kuendelea ‘kufuata tamaa zao wenyewe.’ Ni kwa ‘kufuata tamaa yao wenyewe’ kwamba wao hupuuza utimizo wa unabii mbalimbali ambao hutambulisha wazi sana siku za mwisho.—2 Petro 3:5, NW.
Hata hivyo, yale mambo tofauti ya ishara ya ujumlisho iliyotabiriwa na Yesu hayajapata kamwe kutimizwa yote pamoja katika kipindi kifupi jinsi hii na kwa uzito mwingi jinsi hii na kwa matokeo yenye kufika mbali jinsi hii. (Kwa kielelezo, fanya pitio la Mathayo 24:3-12; Marko 13:3-8; Luka 21:10, 11, 25, 26.) Na sisi tungependa kuvuta uangalifu wako hasa kwenye jambo jingine bado lililotabiriwa la siku za mwisho, lielezwalo katika Ufunuo.
Acheni tugeukie Ufunuo 11:18, HNWW. Huo wasema kwamba Ufalme wa Kristo uanzapo kutawala na mataifa yakasirike na wakati wa hukumu ufike, ndipo Yehova ‘atakapowaangamiza wale wanaoangamiza dunia.’ Je! uchafuzi hauharibu mazingira leo? Ni kweli, sikuzote wanadamu wametumia mali za dunia kujitajirisha. Lakini katika kufanya hivyo, hawajawa kamwe katika hali ya kuiharibu iache kuwa sayari yenye kukalika. Sasa, kwa sababu ya ufundi wa kisayansi uliositawishwa tangu 1914, wanadamu wana uwezo huo, na kwa kujibidiisha mno kwa pupa ya utajiri, kwa kweli wanaiangamiza dunia, wakichafuza mazingira na kuhatarisha uwezo wa dunia kuendeleza uhai.
Jamii yenye kujaa uchoyo na ufuatiaji wa vitu vya kimwili sasa inafanya hivyo kwa kadiri ya kushtua. Haya ni baadhi ya matendo ya kinyama yanayotokea: mvua ya asidi, kupata joto kwa tufe lote, matundu katika tabaka ya hewa ozoni, mjazano wa takataka, marundo ya takataka zenye sumu, dawa hatari za kuua vijidudu katika mimea na za kuua wadudu, takataka za silaha za nyukilia, mimwago ya mafuta, kumwagwa ovyo-ovyo kwa kinyesi kibichi, kuhatarishwa kwa namna za wanyama, maziwa-maji yasiyo na uhai, maji-ardhi yaliyochafuzwa, misitu iliyoharibiwa, udongo uliochafuzwa, udongo wa juu uliopotezwa, na ukungu wa moshi unaosababisha hasara kwa miti na mazao na pia kwa afya ya kibinadamu.
Profesa Barry Commoner asema hivi: “Mimi naamini kwamba uchafuzi wenye kuendelea wa dunia, usipozuiwa, hatimaye utaharibu kufaa kwa sayari hii kuwa mahali pa uhai wa kibinadamu. . . . Tatizo halikuwamo katika kukosa maarifa ya kisayansi, bali katika pupa ya kimakusudi.” Kitabu State of the World 1987 chase-ma hivi katika ukurasa wa 5: “Kadiri ya utendaji wa kibinadamu imeanza kutisha kukalika kwa dunia yenyewe.” Mfululizo wa habari kubwa-kubwa za televisheni ya umma zenye kutangazwa hewani katika United States katika 1990 ulikuwa na kichwa “Harakati ya Kuiokoa Sayari.”
Binadamu hataacha kamwe ule uchafuzi; Mungu ataukomesha atakapoharibu wale wanaoiharibu dunia. Mungu na Jemadari Mkuu wake wa kimbingu, Kristo Yesu, atafanya hivyo kwa kufikiliza hukumu juu ya yale mataifa yenye kufuatia vitu vya kimwili kwenye vita ya mwisho ya Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16; 19:11-21.
Mwisho, angalia jambo la kutokeza linalofuata la unabii wa Yesu juu ya siku za mwisho: “Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia nzima yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14, NW) Habari njema hizi zasimulia kwamba Ufalme wa Mungu sasa unatawala katika mbingu na karibuni utachukua hatua kuharibu mfumo mbovu huu na kurudisha Paradiso duniani. Ile gospeli imepata kuhubiriwa kabla lakini si kufunika dunia nzima inayokaliwa. Hata hivyo, tangu 1914 Mashahidi wa Yehova wamefanya hivyo, kujapokuwa na mnyanyaso ambao Yesu alitabiri—marufuku za kiserikali, jeuri ya wenye ghasia, vifungo gerezani, kuteswa-teswa, na vifo vingi.
Katika 1919 kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 4,000 wakihubiri habari njema hizi. Idadi zao zimeendelea kuongezeka, hivi kwamba mwaka uliopita zaidi ya 4,000,000 walikuwa wakihubiri katika mabara 212, katika lugha kama 200, wakigawa mamia ya mamilioni ya Biblia, vitabu, na magazeti, wakiongoza mamilioni ya mafunzo ya Biblia katika nyumba za watu, na kufanya mikusanyiko katika viwanja vikubwa vya michezo katika sehemu zote za ulimwengu. Kadiri hii kubwa ajabu ya kuhubiri gospeli haingaliweza kufanywa kabla ya 1914. Kutimizwa kwayo kwa kadiri ambayo imefanyika kulitaka matbaa za uchapaji za ki-siku-hizi zenye mwendo wa kasi sana, vifaa vya usafirishaji, kompyuta, mashine za kufaksi habari upesi, na pia vifaa vya usafirishaji na mawasiliano ambavyo vyapatikana katika wakati wetu pekee.
Yerusalemu la siku ya Yeremia lilionywa juu ya uharibifu walo uliokuwa unakuja; wakaaji walo walidhihaki tu, lakini wakati ulikuwa umeenda sana kuliko walivyofikiri. Leo, onyo kubwa zaidi la uharibifu wa Har–Magedoni linavumishwa, likiwa na ushuhuda mwingi sana wa kulitegemeza. (Ufunuo 14:6, 7, 17-20) Mamilioni wajifanya viziwi. Lakini wakati unakwisha; wakati umeenda sana kuliko wanavyofikiri. Je! wakati umeenda sana kuliko unavyofikiri?
[Picha katika ukurasa wa 7]
Katika siku ya Yeremia wakati ulikuwa umeenda sana kuliko walivyofikiri