Sehemu ya 5
Sayansi—Jitihada Inayoendelea ya Ainabinadamu ya Kutafuta Kweli
Kufanya “Miujiza” Katika Karne ya 20
MAMBO yaliyoonekana katika karne ya 19 kuwa “miujiza” isiyowezekana yamekuwa halisi katika karne ya 20. Katika kizazi kimoja tu, watu walianza kuendesha magari yao aina ya Model T Ford hadi kusisimuka juu ya kuona kwenye TV yenye rangi watu wakitembea mwezini. Badala ya kuonwa kuwa matimizo yasiyo ya kawaida, kwa ujumla “miujiza” ya sayansi huonwa kuwa mambo ya kawaida tu.
“Matimizo ya kisayansi ya miaka ya mwanzo-mwanzo ya karne ya 20,” yasema The New Encyclopædia Britannica, “ni mengi sana kuweza kuorodheshwa.” Hata hivyo, inarejezea “mwendo fulani wa maendeleo,” ikisema kwamba “katika kila uwanja mkuu, maendeleo yalitegemea kazi ya ufafanuzi yenye mafanikio ya karne ya 19.” Hiyo inakazia uhakika kwamba sayansi ni jitihada inayoendelea ya kutafuta kweli.
Watu Mmoja-Mmoja Wabadilishwa na Vikundi
Sosaiti za kisayansi, yaani vikundi vya wanasayansi vilivyokuwa vikikutana ili kushauriana juu ya mawazo na habari za kisayansi, vilifanyizwa katika Ulaya mapema kama karne ya 17. Ili zijulishe magunduzi ya karibuni zaidi, sosaiti hizo hata zilianza kuchapisha majarida yazo zenyewe. Hiyo ilifanya kuwe na kushauriana kwingi kulikosaidia kuwekea msingi imara maendeleo zaidi ya kisayansi.
Kufikia karne ya 19, vyuo vikuu vilikuwa vimejihusisha sana na utafiti wa kisayansi, na katika miaka iliyofuata maabara za vyuo hivyo zilifanya magunduzi makubwa.a Kufikia mwanzo wa karne ya 20, makampuni ya kibiashara yalikuwa yakianzisha pia maabara za utafiti, ambazo baada ya muda zilitengeneza dawa mpya za tiba, vitu visivyo asili (kutia ndani plastiki), na vitu vingine. Umma umenufaika na vitu hivyo, na makampuni ya utafiti yamechuma faida ya mamilioni ya dola.
Kusimamishwa kwa maabara hizo na vikundi vya utafiti kulidokeza mwelekeo wa kufanya utafiti uliopangwa kwa utaratibu ambao ni tofauti na jitihada ya watu mmoja mmoja. Wanasayansi wengine walijiuliza kama hiyo ilikuwa ndiyo njia bora zaidi. Katika 1939, John D. Bernal, mwanafizikia na mfuwelografia wa eksirei wa Ailandi aliuliza swali hili: “Je! sayansi ifanye maendeleo kwa upatano usio na utaratibu wa kazi ya watu mmoja mmoja wenye vipawa, kila mmoja akifuata uelewevu wake mwenyewe, au kwa vikundi au magenge ya wafanyakazi wakisaidiana na kupatanisha kazi yao kulingana na mpango uliofikiriwa kimbele lakini unaoweza kubadilishwa?”
Kwa sababu ya ugumu na gharama ya juu ya utafiti, Bernal aliunga mkono kufanya kazi kwa vikundi, akisema kwamba tatizo lilikuwa tu kupanga utendaji ifaavyo. Yeye alitabiri hivi: “Kufanya kazi pamoja kutaendelea zaidi na zaidi kuwa njia ya kufanya utafiti wa kisayansi.” Sasa, zaidi ya nusu karne baadaye, ni wazi kwamba Bernal alisema kweli. Njia hiyo imeendelea, ikiharakisha mwendo wa kufanya “miujiza” ya kisayansi ya karne ya 20.
“Ni Mambo Gani Aliyoyatenda Mungu!”
Mnamo Mei 24, 1844, maneno hayo matano yalipigwa telegrafu kwa mafanikio na Samuel Morse, mvumbuzi wa njia ya mawasiliano ya Morse, kwa umbali unaopita kilometa 50. Mizizi ya karne ya 19 ya “miujiza” ya mawasiliano ya simu ya karne ya 20 ilikuwa ikipandwa sasa.
Miaka 30 hivi baadaye, katika 1876, Alexander Graham Bell alikuwa akijitayarisha kujaribu transmita akiwa na msaidizi wake, Thomas Watson, Bell alipomwaga asidi ya aina fulani kwa makosa. Mlio wake, “Bwana Watson, njoo hapa. Nakutaka,” ukawa zaidi ya mlio tu wa kuomba msaada. Watson, aliyekuwa katika jumba tofauti, alisikia ujumbe huo, akautambua kuwa ujumbe wa kwanza ulio dhahiri kabisa uliopata kupitishwa kwa simu, naye akaja haraka. Milio ya simu imewaharakisha watu tokea wakati huo.
Wakati wa miaka 93 ambayo imepita, ujuzi wa kisayansi, ukiwa pamoja na maarifa ya kitekinolojia, yameandalia watu wengi zaidi na zaidi kiwango cha maisha ambacho hakijapata kufikiwa kamwe. Ulimwengu umekuwa mdogo. Mambo “yasiyowezekana” yamekuwa ya kawaida. Kwa kweli, simu, televisheni, magari, na ndege—na vitu vingine vya “miujiza” ya karne ya 20—vinatumika sana katika ulimwengu wetu hivi kwamba tunakuwa na mwelekeo wa kusahau kwamba ainabinadamu haikuvitumia kwa sehemu kubwa ya kuwapo kwayo.
Karne hii ilipoanza, yasema The New Encyclopædia Britannica, “ushindi wa sayansi ulionekana kama ungeleta ujuzi na uwezo mwingi zaidi.” Lakini maendeleo ya kitekinolojia yaliyofanywa wakati uo huo hayajafurahiwa kila mahali kwa kiwango kilekile, wala si maendeleo yote yanaweza kuonwa kuwa yenye kunufaisha kabisa. “Watu wachache,” inaongezea, “wangeweza kuona kimbele matatizo ambayo mafanikio ayo hayo yangeletea mazingira yao ya kijamii na ya asili.”
Ni Nini Kilichosababisha Matatizo Hayo?
Mambo hakika ya kisayansi yanayotusaidia kuelewa ulimwengu wote mzima kwa njia nzuri zaidi hayana makosa, wala hakuna makosa katika tekinolojia inayotumia mambo hakika ya sayansi kwa njia ifaayo kwa manufaa ya ainabinadamu.
Zote mbili—sayansi na tekinolojia—zimefurahia uhusiano wa karibu kwa muda mrefu. Lakini kulingana na kitabu Science and the Rise of Technology Since 1800, “uhusiano wazo wa karibu, ambao sasa unajulikana, haukufahamiwa kikamili mpaka hivi karibuni sana.” Inaonekana kwamba hata wakati wa kwanza wa mapinduzi makubwa ya viwanda, uhusiano wazo haukuwa wa karibu. Huku ujuzi wa kisayansi uliopatikana karibuni ukichangia kutokezwa kwa vitu vipya, mambo mengine kama ufundi, kazi ya mikono, na ustadi wa mitambo yakachangia vilevile kutokezwa huko.
Hata hivyo, baada ya mapinduzi makubwa ya viwanda kuanza, kurundikwa kwa ujuzi wa kisayansi kuliongeza mwendo, hivyo kukiweka msingi mpana zaidi ambao tekinolojia ingefanyia kazi. Ikiwa na ujuzi mpya, tekinolojia ikaanza kutafuta njia za kuondoa kazi ngumu, kufanya afya iwe bora zaidi, na kuleta ulimwengu bora, wenye furaha zaidi.
Lakini tekinolojia haiwezi kushinda ujuzi wa kisayansi ambao ni msingi wayo. Ujuzi wa kisayansi ukiwa na kosa, basi maendeleo yoyote ya kitekinolojia yanayoutegemea yatakuwa na kosa vilevile. Mara nyingi, matokeo mabaya yataonekana waziwazi baada tu ya madhara makubwa kufanywa. Kwa mfano, ni nani angaliona kimbele kwamba kutokezwa kwa vinyunyizo vya erosoli zenye mchanganyiko wa klorini, florini na karboni au haidrokarboni vingalikuja kuhatarisha tabaka ya ozoni inayolinda dunia?
Jambo jingine lahusika—kusudi. Mwanasayansi aliyejitoa huenda akapenda ujuzi wenyewe na huenda akataka kutumia miongo mingi ya miaka akifanya utafiti. Lakini mfanya biashara, ambaye huenda anapenda zaidi kufuatilia faida, anatamani kutumia kwa haraka iwezekanavyo ujuzi huo. Na ni mwanasiasa gani ambaye atangojea kwa saburi kwa miongo ya miaka kabla ya kutumia tekinolojia ambayo anafikiri itampatia nguvu ya kisiasa ikitumiwa mara hiyo?
Mwanafizikia Albert Einstein alitambua tatizo hilo aliposema: “Uwezo wa atomu ambao umetokezwa umebadili kila kitu ijapokuwa tu njia zetu za kufikiri na hivyo twaelekea msiba mkuu usio na kifani.” (Italiki ni zetu.) Naam, mengi ya matatizo yanayosababishwa na “miujiza” ya karne ya 20 hayakutokezwa tu na kosa la ujuzi wa kisayansi bali pia kwa sababu ya tekinolojia inayoenda kwa kasi na inayochochewa na mapendezi yenye ubinafsi.
Mfano mmoja ni hii, sayansi iligundua kwamba sauti na mwono zaweza kupitishwa hadi sehemu za mbali—televisheni. Tekinolojia ilisitawisha ujuzi wa kufanya jambo hilo. Lakini ilikuwa ni njia isiyofaa ya kufikiri kwa upande wa biashara yenye pupa na watumiaji vitu wenye kudai mno iliyotumia ujuzi huo na tekinolojia hiyo ya ajabu kupitisha picha za pornografia na ujeuri wenye umwagaji mwingi wa damu katika makao ya watu yenye amani.
Vivyo hivyo, Sayansi iligundua kwamba mata (kitu halisi) ingeweza kufanyizwa kuwa nishati. Tekinolojia ikatokeza ujuzi unaotakikana wa jinsi ya kufanya hivyo. Lakini ilikuwa ni njia isiyofaa ya kufikiri kwa upande wa siasa ya utukuzo wa taifa iliyotumia ujuzi huo katika kutengeneza mabomu ya nyukilia ambayo bado yanatisha jumuiya ya ulimwengu.
Kuweka Sayansi Mahali Pafaapo
Vilevile inaonyesha kufikiri kwa njia isiyofaa watu wakiruhusu vyombo vya kazi vilivyotengenezwa kitekinolojia kuwa watumishi viwe mabwana-wakubwa. Gazeti Time lilitahadharisha juu ya hatari hiyo katika 1983 lilipoteua kompyuta kuwa “mashine bora ya mwaka” badala ya kawaida yalo ya kuteua mtu bora wa mwaka.
Time lilitoa sababu hii: “Watu wakitegemea kompyuta kuwafanyia kazi ambazo walikuwa wakifanya na akili zao, akili zao hupatwa na nini? . . . Ikiwa kamusi iliyowekwa ndani ya kumbukumbu la kompyuta inaweza kwa urahisi kusahihisha makosa yoyote ya maendelezo ya maneno, kuna haja gani ya kujifunza namna ya kuendeleza maneno? Na akili ikiacha kufuata mambo yanayohitaji akili nyingi, je, itafuatilia kwa bidii mawazo makubwa au itatumia wakati wayo kwa uvivu ikicheza michezo ya vidio? . . . Je! kweli kompyuta inachochea utendaji wa ubongo au, kwa kufanya kazi nyingi zaidi yenyewe, inafanya akili ilegee?”
Hata hivyo, watu wengine wamevutiwa sana na matimizo ya kisayansi hivi kwamba wanaona sayansi kuwa karibu kama mungu. Mwanasayansi Anthony Standen alizungumzia hilo katika kitabu chake cha 1950 Science Is a Sacred Cow. Hata kama alitia chumvi kidogo, Standen alitaja jambo la maana: “Mwanasayansi mwenye vazi lake jeupe . . . akitangaza kitu fulani kwa umma, huenda umma usimwelewe, lakini ana uhakika wa kuaminiwa. . . . Wakuu wa maserikali, wafanya biashara, wahudumu wa dini, viongozi wa mitaa, wanafalsafa, wote huulizwa maswali na kuchambuliwa, lakini wanasayansi—hawafanywi hivyo kamwe. Wanasayansi ni watu wanaotukuzwa wanaosimamia upeo wa umashuhuri, kwa sababu ni wao wenyewe walio na neno hili ‘Imethibitishwa kisayansi . . . ’ jambo ambalo huonekana kuondoa uwezekano wote wa kubisha.”
Kwa sababu ya njia isiyofaa ya kufikiri, watu wengine hurukia mambo yanayoonekana kupingana kati ya sayansi na Biblia kuwa uthibitisho wa “hekima” ya kisayansi kwa kutofautisha na “ushirikina” wa kidini. Wengi hata huona mambo hayo yanayoonekana kuwa yanapingana kuwa uthibitisho wa kutokuwapo kwa Mungu. Hata hivyo, kwa kweli Mungu yuko lakini yale mambo yanayochukuliwa kuwa yanapingana ambayo makasisi wametokeza kwa kufasili vibaya Neno lake ndiyo hayako. Kwa kufanya hivyo, wanamtukana Mungu ambaye ni Mtungaji wa Biblia na wakati uo huo kupinga jitihada inayoendelea ya ainabinadamu ya kutafuta kweli ya kisayansi.
Kwa kuongezea, kwa kushindwa kuwafundisha waumini wao kusitawisha matunda ya roho ya Mungu, viongozi hao wa kidini huendeleza hali ya ubinafsi inayowafanya watu wafikirie tamaa zao tu ili wenyewe binafsi wapate ustarehe na hali njema. Mara nyingi hiyo hufanywa kwa hasara ya wengine, hata kufikia hatua ya kutumia vibaya ujuzi wa kisayansi kuua wanadamu wenzao.—Wagalatia 5:19-23.
Dini bandia, siasa ya kibinadamu ambayo haijakamilika, na biashara yenye pupa zimefanya watu wawe jinsi walivyo sasa, “wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na shukrani, . . . wasiojizuia,” wenye ubinafsi wanaoongozwa na njia isiyofaa ya kufikiri.—2 Timotheo 3:1-3.
Hao ndio watu na mashirika ambao wametokeza magumu ya karne ya 21 ambayo sasa sayansi inaombwa ikabili. Je! sayansi itafaulu? Soma jibu katika sehemu ya mwisho ya mfululizo huu katika toleo litakalofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mfano, utafiti mwingi wa Mradi wa Manhattan, ile programu ya U.S. yenye bidii nyingi iliyotokeza bomu la atomu, ulifanywa katika maabara za utafiti za Chuo Kikuu cha Chicago na Chuo Kikuu cha Kalifornia katika Berkeley.
[Blabu katika ukurasa wa 20]
Ujuzi wa kisayansi ukiwa na kosa, basi maendeleo yanayoutegemea yatakuwa na kosa vilevile
[Blabu katika ukurasa wa 22]
Si matimizo yote ya kisayansi yanayonufaishay
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]
Kutoka kwa Mkusanyo wa Henry Ford Museum & Greenfield Village
Picha ya NASAyyy