Vijana Wanauliza
Nimenaswa! Naweza Kuachaje Kucheza Kamari?
“NILIANZA kucheza na mashine za kamari nilipokuwa na umri wa miaka 13,” akiri David. “Nilifikia hatua ambayo singeweza kupita majumba ya michezo bila kuingia ili kucheza na mashine za kamari.” Mtu mwingine aliyekuwa mcheza kamari anayeitwa Thomas akiri hivi: “Hata nilikuwa nikiibia marafiki, familia, na wafanyakazi wenzangu ili niendeleze zoea langu. Nilicheza kamari kwa karibu kila kitu.”
Wote wawili David na Thomas walilelewa wakiwa Wakristo. Wote walinaswa na kucheza kamari—wakinaswa na jambo linaloshurutisha sana. Watafiti husema kwamba idadi kubwa za vijana wamenaswa na mbinu zenye hila za kisaikolojia zinazoshawishi vijana waingie katika mchezo wa kamari. Gazeti Time lasema: “Watafiti wa kamari husema kwamba kati ya watu wanaokadiriwa kuwa milioni 8 wenye kucheza kamari kupindukia katika Amerika, milioni 1 kamili ni vijana.” Watu fulani huamini kwamba katika United States, kutoka asilimia 4 hadi 6 wa vijana wote wana ugonjwa wa kucheza kamari.
Vijana hufuatia aina mbalimbali za kamari. Katika Japani, hata zijapokuwa sheria kali zinazokataza wachanga wasicheze mchezo wa kubahatisha, vijana “wameongezeka zaidi katika kucheza kamari kwenye [viwanja vya mashindano ya mbio] na kwenye sehemu za kucheza kamari, kwa njia ya kushtusha,” kulingana na Mainichi Daily News. Kucheza kamari, kubahatisha matokeo ya michezo, na kucheza karata kunapendwa sana vilevile miongoni mwa vijana na kuwafanya washindwe na tamaa ya kubahatisha.
Uzoelevu wa Kamari —Matokeo
Gordon Moody, wa Shirika la Kurekebisha Zoea la Kucheza Kamari, asema hivi: “Mara ya kwanza, [kucheza kamari] ni ono jipya linalofurahisha sana, ni kama kuvumbua kitu cha maana sana au kushikwa na mapenzi. . . . Kucheza nasibu kunafurahisha na kuvutia sana.” (Quit Compulsive Gambling) Naam, kwa watu wengi kuwa na ono la kushinda kwa mfululizo na kupata msisimko unaofuata ni jambo la kufurahisha sana. Lakini huwezi kushinda nyakati zote. Hatimaye, mcheza kamari hushindwa. Na deni na hasara ya kifedha huwa mwanzo tu wa matatizo yake.
Kipitisha-wakati chenye kuzoeleza, kama ilivyo na kitu chenye kuzoeleza, kinaweza kuleta madhara makubwa sana ya kiroho, kihisia-moyo, na kiadili. Kinaweza kusitawisha ndani yako jambo ambalo Gordon Moody aliita “udanganyifu ambao . . . hatimaye, utakufanya uwe mtumwa.” Tunakumbushwa maneno haya ya mtume Paulo: “Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake katika kumtii, mmekuwa watumwa wake yule mnayemtii.” (Warumi 6:16) Tafsiri ya J. B. Phillips inaufasiri hivi mstari huo: “Nyinyi ni mali ya uwezo ambao mnachagua kuutii.” Ebu wazia, kuwa chini ya utawala mkatili wa zoea ambalo huwezi kudhibiti!
Kwa sababu mara nyingi kijana huanza kusema uwongo, njia za vipengee, na wizi ili aendeleze zoea hilo, uhusiano wa familia yao pia huelekea kuharibika. Gazeti la Uingereza Young People Now laonelea hivi: “Unapong’amua kwamba umekuwa mwizi, mwongo, na mzigo kwa watu unaowapenda na wanaokupenda, kujistahi kwako huharibika kabisa.” Basi haishangazi kwamba The Harvard Mental Health Letter laripoti kwamba mara nyingi wacheza kamari wa kupindukia hupatwa na “mshuko mkubwa wa moyo, mahangaiko ya akili,” na magonjwa mengine mengi ya kimwili, kama vile “matatizo ya kuyeyusha chakula tumboni, ukosefu wa usingizi, kuumwa na kichwa, msongo wa juu wa damu, pumu, maumivu ya mgongo, na maumivu ya kifua.”
Hata hivyo, dhara kubwa zaidi la yote ni kuharibika kwa hali ya kiroho ya mtu. Biblia inashutumu pupa na kupenda fedha. (1 Wakorintho 5:10, 11; 1 Timotheo 6:10) Kama ilivyo na uzoelevu mwingine wowote, kucheza kamari kupindukia ni ‘uchafu wa mwili na roho.’ (2 Wakorintho 7:1) Kwa kadiri unavyocheza kamari, ndivyo unavyozidi kuharibu dhamiri yako na uhusiano wako pamoja na Mungu.—Linganisha 1 Timotheo 4:2.
Moyo wa Kuacha
Mtu anaweza kuachaje mshiko huo mkubwa wa zoea hilo? Kwanza kabisa, ni lazima uwe kwa kweli unataka kuacha. “Hakuna uzoelevu unaoweza wakati wowote kushindwa isipokuwa tu kama mzoelevu kwa kweli anataka kubadilika,” asema Liz Hodgkinson katika kitabu chake Addictions. Hilo lamaanisha kujifunza ‘kuchukia uovu,’ kukirihi kamari. (Zaburi 97:10) Kwa njia gani? Kwa kutofikiria anasa bali kufikiria matokeo ya kucheza kamari. Je! “kujifurahisha katika dhambi kwa kitambo”—ule msisimko wa kushinda mchezo fulani—kwafaa kupoteza uhai wa milele? (Waebrania 11:25) Kufikiria kwa njia hiyo kunaweza kukusaidia usitawishe azimio la kuacha zoea hilo.
Hata hivyo, mtafiti Liz Hodgkinson asema hivi: “Aina yoyote ya uzoelevu inaweza kukazika sana hivi kwamba kuiondoa ni kama kukata kiungo fulani cha mwili.” Lakini Yesu alisema: “Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe; kwa maana yakufaa kiungo chako kimoja kipotee wala mwili wako mzima usitupwe katika jehanum.” (Mathayo 5:29) Kitu chochote kinachohatarisha uhusiano wako na Mungu ni lazima kikatwe kutoka maishani mwako!
Jambo hilo lamaanisha kusitawisha kujidhibiti. Mtume Paulo alikuwa na tamaa zilizokuwa zikimrudia ambazo angaliweza kuziachilia tu zimshinde, lakini alikataa kuwa mtumwa wa tamaa zake. Alisema, “nautesa mwili wangu na kuutumikisha.” (1 Wakorintho 9:27) Ni lazima wewe pia ujifunze kuutesa mwili wako, bila kuacha tamaa zako zikudhibiti.
Kutafuta Chanzo cha Tatizo
Hata hivyo, ili kushinda pigano hili, itahitaji zaidi ya kuwa na moyo wa kuacha kamari. Uzoelevu mara nyingi huonyesha matatizo mengine makubwa. Mcheza kamari wa kupindukia anayeitwa Dick asema hivi: “Utoto wangu ulikuwa wa ajabu sana. Hakukuwa na upendo wowote katika familia yetu. . . . Nilikuwa nikiaibishwa sikuzote. Nilijidharau sana.” Tokeo la mkazo huo wa akili likawa kucheza kamari.
Watu wengi wanaohusika na afya ya kiakili sasa huhusianisha aina mbalimbali za uzoelevu na tamauko la kihisia-moyo linalotokana na kutendwa vibaya au kuachwa wakati wa utotoni. Hata iwe ni hali gani, kutafuta chanzo cha tatizo lako kwaweza kukusaidia ulishinde. Mtunga Zaburi alisali hivi: “Ee Mungu, unichunguze, uujue moyo wangu, unijaribu, uyajue mawazo yangu; uone kama iko njia iletayo majuto ndani yangu, ukaniongoze katika njia ya milele.” (Zaburi 139:23, 24) Kuyazungumza mawazo yako ya moyoni na Mkristo mkomavu, labda mzee wa kutaniko, laweza kukusaidia sana ujue ni kwa nini unacheza kamari na jambo unalohitaji kufanya ili ubadili njia zako za kufikiri na za mwenendo.a
“Kitu Kizuri Zaidi cha Kufanya”
Kulingana na kitabu Quit Compulsive Gambling, kuacha “ni [hatua] ya kwanza tu ya kupigana na tatizo hilo.” Ni lazima mabadiliko makubwa yatafanywa pia katika mtindo wa maisha yako. Ili usirudie tatizo hilo, ni lazima uepuke wenzi wako wa zamani wa kucheza kamari na kuepuka sehemu za zamani za kuchezea kamari, kama vile vyumba vya kuchezea kamari, vyumba vya umma vya mchezo wa biliadi ambapo watu hubahatisha, na sehemu nyinginezo kama hizo. (Mithali 13:20) Hilo halimaanishi kwamba ujitenge. (Mithali 18:1) Jaribu kusitawisha urafiki unaofaa, wenye kukutegemeza katika kutaniko la Kikristo. Jishughulishe na kazi yenye matokeo, utendaji wa kiroho, na vitumbuizo vinavyofaa.
Hata hivyo, Hodgkinson atukumbusha kwamba mzoelevu atashinda vita yake wakati tu “aonapo kwamba kuna kitu kizuri zaidi cha kufanya huko nje—kwamba maisha yana mambo mengi zaidi kuliko kujaribu kuridhisha uzoelevu.” Naam, kuna kitu gani kizuri kushinda lile tumaini ambalo Biblia hutoa?
Mtu mmoja anayeitwa Roddy aliona jambo hilo kuwa kweli. Anajieleza kuwa alikuwa “mcheza kamari mshupavu” kwa miaka 25, kuanzia alipokuwa kijana. Roddy alijaribu karibu kila aina ya kamari—mashindano ya mbio za farasi, mashindano ya mbio za mbwa, kubahatisha matokeo ya kandanda, katika vyumba vya kuchezea kamari. Kisha akaanza kutumia maishani zile kweli zilizo katika Neno la Mungu ambazo alijifunza kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. “Kwa miezi mitatu tu,” asema Roddy, “badiliko kubwa sana likatokea.” Aliacha kucheza kamari, na leo hii anatumikia akiwa mzee katika kutaniko la Kikristo.
Lakini, labda tayari una ujuzi fulani wa mafundisho ya Biblia. Kama David na Thomas, waliotajwa awali, huenda bado umeshindwa kuzitumia kibinafsi kweli za Biblia. Kama ni hivyo, mbona ‘usipate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu’ kwa kuwa na funzo la Biblia lenye bidii? (Warumi 12:2) Mara David na Thomas walipoanza kutumia maishani mambo ambayo walikuwa wamejifunza na kusitawisha imani na usadikisho thabiti, waliweza kushinda uzoelevu wa kamari. Wewe pia unaweza kushinda!
Kufanya bidii katika kujifunza Biblia kutafanya tumaini la Biblia la wakati ujao—kitu kizuri zaidi ya kucheza kamari—liwe halisi zaidi kwako. Kwa wakati uo huo, kutakusaidia kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Hivyo utahisi kuwa huru ‘kumwomba msaada bila kukoma,’ ukiwa na hakika kwamba aelewa hisia zako. (1 Wathesalonike 5:17; Zaburi 103:14) Atathawabisha jitihada zako zenye bidii kwa kukupa nguvu zinazohitajika ili kushinda vita dhidi ya kucheza kamari kupindukia.—Wagalatia 6:9; Wafilipi 4:13.
[Maelezo ya Chini]
a Wengi wa watu ambao wanashughulika na afya ya kiakili huamini kwamba mashauri ya wastadi yanahitajiwa ili mtu aache mwenendo wa kuwa mzoelevu kwa kitu fulani. Kama Mkristo anachagua tiba isiyohitilafiana na kanuni za Biblia, huo unakuwa uamuzi wa kibinafsi kabisa.
[Picha katika ukurasa wa 16]
Mara nyingi wacheza kamari hutumia uwongo na wizi ili kuendeleza zoea lao la kucheza kamari