Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kusomea Nyumbani Nilithamini makala yenu “Kusomea Nyumbani—Je! Kunakufaa Wewe?” (Aprili 8, 1993) Mimi binafsi ninafundishwa nyumbani, na sikuwa natimiza mengi katika kazi yangu ya shule. Lakini niliposoma makala yenu, ilinichochea. Sasa ninarudia ratiba nzuri.
N. S., United States
Kupanga Uzazi Niliudhika sana na makala zenu kuu katika toleo la Februari 22, 1993, “Kupanga Uzazi—Suala la Ulimwenguni Pote.” Ni upuuzi kudokeza kwamba Wakristo wenye kuchukua madaraka wahitaji kupunguza ukubwa wa familia zao. Ni kwa msingi gani mnadokeza kwamba amri ya Mungu katika Mwanzo [ya ‘kuijaza nchi’] haitumiki kwa Wakristo?
A. D., United States
Amri ya Mungu kwa Adamu na Hawa ya ‘kuijaza nchi’ ilirudiwa kwa Noa na familia yake. Hata hivyo, hakuna mahali popote ambapo Biblia inawekea Wakristo sharti ya kuzaana. (Mwanzo 1:28; 9:1-5; Matendo 15:29) Kwa kweli, Biblia yapongeza Wakristo wanaoendelea kuwa waseja “kwa ajili ya ufalme.” (Mathayo 19:12; 1 Wakorintho 7:38) Ni lazima mume na mke wenyewe wafanye maamuzi yao katika suala la kulea watoto na kupanga uzazi. Na kwa kuwa Wakristo wanaamriwa watunze mahitaji ya kimwili, kihisia-moyo, na ya kiroho ya watoto wao, wazazi wenye kuchukua madaraka waweza kuona kuwa jambo la busara kuwa na familia ndogo ili utunzi kama huo uweze kutolewa. (1 Timotheo 5:8) Jambo hilo halipuuzi kamwe uhakika wa kwamba watoto ‘ni urithi kutoka kwa Yehova.’ (Zaburi 127:3, “NW”)—MHARIRI.
Ulevi Asanteni sana kwa makala bora kabisa za “Vijana Wanauliza . . .” katika matoleo ya Januari 8 na 22, 1993, yaani, “Je! Unywaji Waweza Kunifanya Niwe Mzoevu Kweli?” na “Naweza Kuachaje Kunywa Kileo?” Nina umri wa miaka 48 na mzoevu [anayeacha] kileo. Matokeo yenye uharibifu mwingi sana wa “ugonjwa” huo kwa mwili, akili, na roho yanavunja moyo sana. Nilipoanza kutambua kwamba nilikuwa nimekuwa mzoevu wa kileo, nilihisi kana kwamba Yehova hangeweza kunisamehe. Lakini nilienda kwa wazee, na wakanipa msaada wenye upendo. Baada ya kurudia tatizo langu, niliingia katika programu ya kutibu uzoevu wa kileo. Tamaa ya kunywa ikija sasa, mimi husali juu ya ulimwengu mpya wa Mungu. Mimi husoma pia makala nyingi za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zenye kushughulikia uzoevu wa kileo au zenye kusimulia maono yenye kutia moyo. Asanteni kwa kuelewa kwenu matatizo ambayo watu wa Yehova hupitia na kwa kutupatia makala zilizo nzuri.
C. D., United States
Vijana Huuliza . . . Nashukuru sana kutoka moyoni kwa ajili ya ile makala “Je! Niende Kwenye Dansi ya Uhitimu?” (Machi 8, 1993) Nimekuwa na msongo mwingi nihudhurie dansi ya kuhitimu “kwangu” shule ya sekondari. Lakini baada ya kusoma makala hiyo yenye thamani kubwa, shaka zangu zote zilimalizwa. Sitaenda, na sifikiri kwamba nitakosa mambo mengi.
J. L., United States
Asanteni sana kwa makala “Je! Nifanye Nini Kuhusu Kazi Nyingi ya Shule ya Kufanyia Nyumbani?” (Aprili 8, 1993) Nilitumia madokezo iliyokuwa nayo mara hiyo, na nimefaidika sana kutokana nayo. Sasa naweza kuokoa wakati zaidi kwa mambo ya kiroho. Asanteni sana!
M. M., Italia
Asanteni sana kwa kuchapisha makala “Naweza Kukabilianaje na Mapenzi Yaliyovunjika?” (Mei 8, 1993) Ninapitia wakati mgumu sana. Mara nyingi huwa inaonekana kwamba sitapata mume. Kwa hiyo nilipokuwa nikisoma gazeti hilo, sikuweza kuzuia machozi yangu. Hata hivyo, kuisoma makala hiyo kulinifanya nione nimeeleweka na kuthaminiwa. Ilinifanya nielewe hata zaidi kwamba Yehova hutupenda na huelewa yale tunayopitia.
R. Z., Italia