Dawa za Kulevya, Uwasiliani-Roho, na Biblia
Paulo aliwaonya Wakristo wa karne ya kwanza dhidi ya “zoea la uwasiliani-roho.” (Wagalatia 5:20, NW) Neno la Kigiriki alilotumia Paulo mahali hapo, phar·ma·kiʹa, lamaanisha kihalisi “matumizi ya dawa za kulevya.”[1] “Kwa sababu wachawi wa kike na walozi walikuwa wakitumia dawa za kulevya,” yaeleza The Interpreter’s Bible, “neno hilo lilikuja kumaanisha uchawi, uganga, ulozi, na mizungu.”[2]
Si ajabu kwamba dawa za kulevya hutimiza fungu kubwa katika uwasiliani-roho wa kisasa. Kwa kielelezo, yaripotiwa kwamba kileo na dawa za kulevya zimetumiwa katika kuingiza washiriki wapya katika madhehebu ya kishetani. Imesemekana pia kwamba dawa za kulevya zaweza kutumiwa kufanya mtu atende kwa urahisi zaidi mambo fulani wakati wa sherehe za kishetani.[3] Hali iwe gani, Petro aliandika kwamba Ibilisi ‘huzunguka-zunguka kama simba angurumaye, akitafuta mtu ammeze.’ (1 Petro 5:8) Neno la Kigiriki ka·ta·piʹno, lililotafsiriwa ‘kumeza,’ lamaanisha kimfano “angamiza,” au “shinda kabisa.”[4] Dawa za kulevya na uwasiliani-roho hufanya vivyo hivyo. Jambo hilo lawapa Wakristo sababu yenye nguvu ya kuepuka aina yoyote ya matumizi ya dawa za kulevya.—Linganisha 2 Wakorintho 4:4.