Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Familia Yakaidi Wanazi Nina umri wa miaka 90 na ninajifunza pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilisoma ile makala “Ee, Yehova, Msaidie Msichana Wangu Mchanga Aendelee Kuwa Mwaminifu!” (Septemba 22, 1993) Ilizungumza juu ya wazazi Mashahidi na binti yao ambaye, ingawa alidhulumiwa sana kwa sababu ya Hitler, alijitahidi kishujaa ashikilie mafundisho ya Yehova. Nililia machozi nilipokuwa nikisoma makala hiyo. Nimeazimia kujifunza mafundisho ya Yehova kwa mtazamo mzito hata zaidi.
S. T., Japani
Ono hilo lilinigusa moyo sana. Simone Arnold Liebster alikuwa msichana mdogo tu, akiwa bila wazazi na kufungwa katika mahali pa kurekebisha tabia kwa sababu tu ya utii wake kwa Yehova. Hicho ni kielelezo kizuri kama nini cha imani!
M. C. L. S., Brazili
Ule utegemezo kwa Yehova na ule upendo, staha, na nguvu ambazo yeye na wazazi wake waliishi nao zilinifanya nichunguze upya uhusiano wangu na Yehova. Nilihisi nimenyenyekezwa, na ilinisaidia nithamini sifa nzuri za kiroho za uvumilivu na imani.
V. B., Australia
Upweke Nilisoma zile makala juu ya upweke (Septemba 22, 1993) mara tatu au nne hivi. Mnadokeza kwamba mtu anaweza kucheza dansi, kuimba, na kujifanya kuwa na furaha. Lakini hamkutaja juu ya ukosefu wa usawaziko uwezao kufanya mtu awe na hisia za kutaka kujiua.
P. C., United States
Makala hizo hazikuelekezwa kwa watu walioshuka moyo sana au wenye hisia za kutaka kujiua, ambazo kwa kawaida huhitaji uangalifu wa kipekee. Badala ya hivyo, zilielekezwa kwa wale wanaopatwa na upweke wa muda kwa sababu ya hali zenye kuhuzunisha, kama vifo vya wapendwa. Habari kuhusu kushuka moyo zilichapishwa katika toleo letu la Oktoba 8, 1988, na pia katika makala ya “Vijana Huuliza . . .” katika toleo hili.—Mhariri.
Nuru za Kaskazini Nilifurahia makala yenu “Vipandaji vya Kifumbo vya Pepo za Kimbingu” (Septemba 22, 1993) juu ya aurora borealis. Lakini hamkutaja kwamba nuru hizo zaweza kuonwa pia kutoka sehemu za kaskazini na mashariki za Skotland. Hata kuna wimbo juu ya ‘nuru za kaskazini za Aberdeen ya kale’!
G. S., Skotland
Asante kwa habari hiyo ya ziada.—Mhariri.
Kulinda Wanyama wa Pori Mimi ni msimamizi wa shirika fulani la hapa la kimazingira. Nafurahi kuona mfululizo wa makala juu ya mazingira. (“Ni Nani Atakayelinda Wanyama Wetu wa Pori?,” Novemba 8, 1993) Nimekuwa nikisema kwa miaka mingi kwamba kama si Mungu, tayari sisi tungekuwa tumeangamia.
M. S., United States
Bila shaka Mungu ameifanya dunia iwe na uwezo kujirekebisha, jambo ambalo bila shaka limefanya ivumilie jitihada za binadamu kuiangamiza. Hata hivyo, hatimaye suluhisho Lake ni ‘kuwaharibu hao waiharibuo nchi.’ (Ufunuo 11:18)—Mhariri.
UKIMWI Nilifurahia sana zile makala za UKIMWI katika mfululizo wa “Vijana Huuliza . . .” (Agosti 22, 1993, Septemba 8, 1993) Nina miaka 20 na nilikuwa nikipatwa na haya kwamba nilikuwa bikira. Lakini baada ya kusoma makala hizo, nimekuja kuona kwamba ubikira ni zawadi kutoka kwa Yehova.
L. K., United States
Si sahihi kudokeza kwamba ngono ya kawaida ina hatari inayotoshana na ya ugoni jinsia-moja. Utafiti wote umeonyesha kwamba wagoni jinsia-moja waelekea zaidi kupatwa na virusi HIV.
J. S., United States
Utafiti waonyesha kwamba kwa kweli wagoni jinsia-moja waelekea zaidi kuambukizwa virusi HIV. Hata hivyo, wastadi wasema kwamba ambukizo kutokana na ngono ya kawaida laongezeka kwa kasi sana. Na kulingana na msemaji mmoja wa Usimamizi wa Chakula na Dawa wa U.S., wanawake “ndio sehemu inayokuwa haraka zaidi ya watu wenye ambukizo la virusi HIV katika nchi [hiyo].” Si kwamba nyakati zote ni wanawake wenye makosa; wengi wao wanaambukizwa na waume zao wenye kuzurura-zurura.[1]—Mhariri.