Tumaini Halisi kwa Watoto
“Kamwe tena hakutakuwa na . . . kitoto kichanga kiishicho siku chache tu . . . Hawatajitaabisha kwa jasho bure wala kuzaa watoto walioachiwa msiba tu; kwa maana wao watakuwa kikundi cha watu waliobarikiwa na BWANA.”—Isaya 65:20, 23, New International Version.
JAPO mwanadamu amefanya jitihada za kusifika kuleta nafuu ya mambo, mamilioni ya watoto wangali ‘wameachiwa msiba tu.’ Haitakuwa hivyo sikuzote. Unabii wa Isaya si kwamba tu watuhakikishia kwamba kila mtoto siku moja atakuwa na wakati ujao ulio salama bali pia chaeleza jinsi mradi huo waweza kutimizwa.
Kwenye Isaya 65:17, Zaire Swahili Bible, Mungu asema hivi: “Mimi ninaumba mbingu mpya na dunia mpya, na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” Ili kuwatunza ifaavyo watoto wa ulimwengu, kwahitajiwa “mbingu mpya” na “dunia mpya” pia.
“Dunia mpya” hiyo ni jamii mpya ya watu washikao kanuni ambazo Yesu Kristo alifundisha. Moja ya kanuni hizo, Yesu alieleleza, ni kwamba “mtu akimpokea mtoto mmoja wa namna hii kwa jina langu, anipokea mimi.” (Marko 9:37) Jamii ambayo ingetendea kila mtoto mdogo kama kwamba yeye ni Kristo mwenyewe kwa kweli ingekuwa “dunia mpya”! Tayari, mamilioni ya watu wanajitahidi kufanya lilohilo, nao wamefaulu kuwapa tumaini baadhi ya watoto wa ulimwengu.
Watoto Walio na Tumaini Sasa
Tshepo, pamoja na ndugu na dada zake wanne wakubwa, waliishi katika mji wa vitongojini katika Afrika Kusini. Wakati mvulana huyo alipokuwa na umri wa mwaka mmoja, tayari alikuwa na tumbo lililofura lililo kawaida ya mtoto mwenye utapiamlo. Wazazi wake waliponda sehemu kubwa ya mapato yao haba wakinywa pombe wakijaribu bure tu kujisahaulisha huzuni zao. Ni mara haba Tshepo alipokula mlo moto, na aliachwa acheze katika takataka na mikebe ya pombe iliyozagaa nyumbani.
Wakati ujao wa Tshepo ulionekana wenye giza mpaka jambo fulani lilipotendeka likabadili njia ya kufikiri ya wazazi wake. Jirani mmoja jina lake George aliwapa mtaala wa elimu ya Biblia bila malipo. Matokeo yakawa ya kuvutia—tatizo la kunywa lilitoweka, ile nyumba ikasafishwa, familia ikapata mlo moto kila siku, na Tshepo na ndugu na dada zake wakaanza kuonekana safi, wenye kuvalia vizuri, na wenye furaha.
George alisaidia familia ya Tshepo kwa sababu, akiwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, yeye ahisi kwamba ana daraka kuelekea watu wote, kutia na wale wasiofanikiwa sana kama wenzao. Bila shaka, wakati na saburi nyingi zilihitajiwa kusaidia familia hiyo kubadili mtindo-maisha wao, kuwafundisha kanuni mpya zenye msingi wa Neno la Mungu. Lakini George ahisi kwamba jitihada hiyo ilistahili, hasa wakati aonapo tofauti kubwa sana ambayo imewaletea watoto.[1]
Katika mji wa San Salvador Atenco wa Meksiko aliishi mkulima mdogo aitwaye José, baba wa watoto tisa. Alikuwa mnywaji wa kupindukia, na watoto wake walimwogopa kwa sababu alipolewa alikuwa mwenye jeuri. Nyumba yao ilikuwa chafu, na ua ulitumika kama zizi la punda na nguruwe za familia, nao walizurura ovyo tu ndani ya nyumba. Tokeo ni kwamba, watoto walipatwa na maambukizo ya matumbo, na nyakati fulani miili yao ilijawa na vidonda vyenye usaha.
Mambo yalibadilika José alipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Aliacha kunywa kupindukia akawa baba halisi kwa watoto wake. “Sasa sisi twaweza hata kucheza na baba!” mmoja wa wale watoto wadogo zaidi asema kwa mshangao. Sasa nyumba yao ni moja ya zilizo safi zaidi—badala ya kuwa moja ya zilizo chafu zaidi—mjini. Wale punda na nguruwe huwekwa katika uwanja, na familia huchemsha maji ya kunywa. Maendeleo ya kufuata kanuni za afya yamefanya watoto wawe na afya zaidi na wenye furaha zaidi.[2]
Kama vielelezo viwili hivyo vionyeshavyo, mara nyingi ufunguo wa kuwasaidia watoto ni kuwasaidia wazazi. Azimio la Mkutano wa Viongozi wa Ulimwengu Kuhusu Watoto ulitambua kwamba “familia ndiyo yenye daraka la kwanza kuwalea na kuwalinda watoto.”[3] Na kama itakuwa au haitakuwa kwamba familia zitakuza na kulinda watoto wao huenda ikategemea sana elimu na vilevile mapato.
Kubadili Mtoto wa Barabarani
Katika Brazili, Domingos alikuwa na umri wa miaka tisa tu baba yake alipokufa. Mama yake alipoolewa tena, alipelekwa ghafula kuishi katika makao ya yatima. Ukatili aliotendwa katika makao ya yatima ulimfanya aamue kujiunga na kikundi kilichokuwa kikipanga kutoroka. Ingawa mama yake alimchukua tena aliposikia juu ya mipango yake, mapigo kadhaa kutoka kwa baba yake wa kambo yalimsadikisha kuondoka nyumbani daima. Akawa mmoja wa maelfu ya watoto wa barabara za São Paulo ambao hung’arisha viatu, kuuza pipi, au hata kupelekea watu dawa za kulevya ili kuendeleza uhai.
Domingos alipofika mara ya kwanza kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, hakuwa na imani na watu na alikosa adabu—jambo lisiloshangaza kamwe kwa kufikiria malezi yake. Hata hivyo, Mashahidi walio watu wazima waliuvutia uhakika wake, nao wakamsaidia apate viwango vipya kupitia funzo la Biblia la kibinafsi. Hatimaye alijifunza kwamba angeweza kumtumaini Yehova na wengine. Mashahidi walimsaidia kupata kazi, kwanza akiwa msaidizi wa mjenzi wa kuunga matufali kisha kama mvulana wa kutumwa na ofisi. Sasa, miaka kadhaa baadaye, yeye hutumikia akiwa mhudumu Mkristo wa wakati wote.[5]
Vielelezo hivyo vyaonyesha kwamba jamii ya watu wenye kujali yaweza kupunguza baadhi ya mateso ya watoto wa ulimwengu. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova wang’amua kwamba hali za kusononesha hazitaondolewa kabisa kamwe kwa jitihada za kibinadamu. Utatuzi kamili kwa matatizo ya watoto wa ulimwengu ungetaka uwezo uzidio ule wa kibinadamu, rasilmali zisizo na kikomo, na mamlaka ya tufeni pote.
“Mbingu Mpya” kwa Ajili ya Ulimwengu Mzuri Zaidi
Ni Mungu peke yake awezaye kuandaa utatuzi kamili. Kwa sababu hiyo, unabii wa Isaya waeleza kwamba “dunia mpya” itaandamana na “mbingu mpya.” Nyakati kadhaa Biblia huahidi kwamba “mbingu mpya” itaanzishwa au zitaanzishwa. (Isaya 65:17; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:1, New World Translation) Katika kila pindi kuanzishwa kwa “mbingu mpya” kwaonyeshwa kuwa hatua muhimu kuelekea kuondoa mateso na kuleta uadilifu duniani. “Mbingu mpya” hizo ni nini hasa?
Biblia hutumia mara nyingi neno “mbingu” kama neno-fanani la utawala, ama wenye kufanywa na Mungu ama na wanadamu. (Linganisha Danieli 4:25, 26.)[6] Serikali mpya hiyo ni Ufalme wa kimbingu, Ufalme wa Mungu—ule ambao Yesu alifundisha wafuasi wake kusali juu yao. (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu utakuwa na uwezo wa kuondoa hali yoyote ya kusononesha ambayo huenda ikatisha watoto wa ulimwengu, nao utaazimia kabisa kufanya hivyo.
Kwa nini twaweza kuwa na uhakika juu ya hilo? Kwa sababu serikali huonyesha utu wa watawala wayo. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu utasimamia mambo kupatana na viwango vya Mungu na vile vya Mwana wake, Yesu Kristo, Mfalme mwekwa wa Mungu. Wote wawili wameonyesha upendezi mchangamfu katika hali njema ya watoto.—Zaburi 10:14; 68:5; Marko 10:14.
Tuungojeapo kwa hamu nyingi Ufalme au “mbingu mpya” hizo zilizoahidiwa, twaweza kujitahidi kuleta nafuu ya watoto katika ujirani wetu. Kama vile Mkutano wa Viongozi wa Ulimwengu Kuhusu Watoto ulivyokata shauri kwa kufaa: “Hakuwezi kuwako jukumu lenye kuheshimika zaidi ya kumpa kila mtoto wakati ujao ulio bora.”[7]
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Programu Yenye Kutumika ya Kuwasaidia Watoto
KAZI ya kuelimisha ya Mashahidi wa Yehova huwapa watoto msaada wenye kutumika na wa kudumu. Pande fulani za programu hiyo ni hizi:
Elimu ya watu wazima. Hii yahusisha mtaala wa masomo kwa wazazi wasioweza kusoma au kuandika, pamoja na maagizo mengi ya Kibiblia yaliyopangwa kwa njia ya kukazia viwango vihitajiwavyo sana kwa utunzi ufaao wa watoto.
Uongozi wa kifamilia. Biblia huhimiza wazazi—hata wale walio maskini hoi—watunze watoto wao wote badala ya kupeleka baadhi yao wakaishi na watu wa ukoo. Kitabu Kufanya Maisha ya Jamaa Yako Yawe Yenye Furaha kimethibitika kuwa chenye mafaa katika kusaidia familia zilizo na matatizo maalumu.a
Kuhusisha watoto na kuwapa mwelekezo. Wakati watoto wenyewe wahusikapo katika elimu, utunzaji wa afya, na usafi wa kuondoa takataka katika mazingira, matokeo huwa mazuri zaidi. Mashahidi hujifunza mara nyingi Biblia pamoja na watoto, wakitumia vichapo vinavyolingana na mahitaji yao kama vile Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia na Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi ili kuwasaidia kushughulikia matatizo nyumbani na kufanyia maendeleo ufuataji wao binafsi wa kanuni za afya.*
Maagizo ya kufuata na kutunza kanuni za afya. Mashahidi wa Yehova huchapisha jarida Amkeni! katika lugha 74, na gazeti hili huwa na makala kuu kuhusu utunzaji wa afya.
Kazi ya kusaidia waliopatwa na maafa. Nyakati za dharura, Mashahidi wa Yehova hupanga kitengenezo shughuli za kusaidia upesi ambazo huandaa msaada moja kwa moja kwenye eneo la msiba.
[Maelezo ya Chini]
a Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Utatuzi kamili kwa matatizo ya watoto wa ulimwengu ungetaka uwezo uzidio ule wa kibinadamu. Ni Mungu tu awezaye kuandaa utatuzi huo