Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g94 9/8 kur. 16-20
  • Nilizoezwa Kuua, Sasa Natolea Watu Uhai

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nilizoezwa Kuua, Sasa Natolea Watu Uhai
  • Amkeni!—1994
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu ya Mimi Kuondoka Israeli
  • Kuipata Kweli Juu ya Mesiya
  • Kulisikia Jina Yehova
  • Kuipata Kweli
  • Kulinganisha Biblia na Waamini
  • Twakuta Ndugu Wapalestina
  • Wazazi Wangu Waikabili Kweli
  • Sababu kwa Nini Watu wa Namna Zote Wanakuwa Mashahidi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1974
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • “Umtazame Mtu Mnyofu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1994
g94 9/8 kur. 16-20

Nilizoezwa Kuua, Sasa Natolea Watu Uhai

“Wavamizi-haramu wanawazuia watekwa-nyara katika nyumba moja kaskazini mwa Israeli.”

NILIKUWA katika pumziko la mwisho-juma kutoka jeshi la Israeli nikipiga kambi kando ya Bahari ya Galilaya nilipoisikia habari hiyo redioni. Nilijua vema maana ya maneno hayo. Mimi nilikuwa ofisa-jeshi katika kikosi maalumu kilichozoezwa kitaalamu kushughulika na uvamizi-haramu. Pia nilijua kwamba ningekuwa miongoni mwa wale ambao wangejitupa ndani, wawaue wavamizi-haramu, na kuwafungulia watekwa-nyara. Niliingia ndani ya gari langu bila kusita nikatimka niwezavyo hadi mahali hapo.

Kwa kuwa sikuzote maofisa katika jeshi la Israeli waliingia kwanza, nilijua ningekuwa miongoni mwa walio wa kwanza kukabiliana na wavamizi-haramu, lakini wazo la kuuawa au kujeruhiwa halikunizuia. Niliwasili mahali hapo dakika chache tu baada ya rafiki zangu katika kikosi chetu kuifanya kazi, wakiua wavamizi-haramu watano na kuwafungulia watekwa-nyara. Nilitamauka sana kwa kukosa patashika hiyo.

Kwa nini nikahisi hivyo? Kwa sababu nilikuwa mtaifa sana, nami nilitaka kuthibitisha uzalendo wangu. Lakini niliingiaje katika kikosi hiki maalumu cha kupambana na wavamizi-haramu?

Nilizaliwa Tiberiasi, katika Israeli, katika 1958 nikalelewa katika makao yenye utukuzo mwingi wa taifa. Niliamini nchi yangu ilikuwa ya haki sikuzote. Hivyo nilipojiunga na jeshi katika 1977, nilijitolea kutumikia katika kikosi chenye utaalamu mwingi zaidi wa kupigana katika jeshi la Israeli. Ni asilimia ndogo sana ya wale waombao kazi hukubaliwa kuanza ule mtaala mgumu sana wa mazoezi. Si wote wamalizao, na kati ya hawa, ni wachache tu huchaguliwa kuwa maofisa. Nilikuwa mmoja wao.

Mafanikio yangu kwa kweli yalionyesha uzalendo wangu. Nilikuwa na sababu njema ya kujionea fahari. Kwani, mimi nilikuwa ofisa aliye katika kikosi maalumu cha kupigana chenye kufanya mambo yasiyoonwa vyepesi na mtu wa kawaida barabarani, hata katika sinema. Hata hivyo, yale mafanikio, umaarufu, na usiri yaliandamana na utupu wa kiroho ulioongezeka hadi nikang’amua kwamba maisha yana kusudi la maana kuliko hili. Hivyo baada ya miaka minne yenye magumu sana, niliondoka jeshini nisafiri kujionea ulimwengu.

Sababu ya Mimi Kuondoka Israeli

Safari zangu kuzunguka ulimwengu zilikoma wakati, nikiwa katika Thailand, nilipokutana na Kunlaya, aliyekuja kuwa mke wangu, aliyekuwa akijifunza sanaa wakati huo katika Chuo Kikuu cha Bangkok. Yeyote kati yetu hakuwa na mipango ya kufunga ndoa, lakini upendo wetu ulikuwa na nguvu kuliko tulivyong’amua. Hivyo Kunlaya aliacha mafunzo yake, mimi nikakomesha safari zangu, nasi tukaamua kushirikiana maisha zetu. Wapi? Israeli, bila shaka. “Lazima nisaidie kulinda nchi yangu,” nikamwambia.

Katika Israeli mwanamume Myahudi aweza kuoa Myahudi tu; hivyo nilijua vema kwamba Kunlaya, aliyekuwa Mbuddha wakati huo, angelazimika kuongolewa kwenye Uyuda, naye alifurahia hilo. Lakini Wayahudi wa kidini waliofanya uongofu huo hawakumtaka. Kokote tulikotafuta msaada, tulipata jibu lilelile lisilofaa: “Mtu kama wewe apaswa kutafuta msichana mzuri Myahudi wala si kuoa Mmataifa huyu.” Si kwamba tu Kunlaya alikuwa Mmataifa bali pia alikuwa wa jamii tofauti.

Baada ya miezi sita ya kujaribu, hatimaye tukaalikwa kwenye mahakama ya kidini tuhojiwe na marabi watatu ambao wangeamua kama Kunlaya angeongolewa au sivyo. Huko nikajikuta nikikaripiwa kwa kutaka kuoa Mmataifa. Waliniambia nimpeleke nyumbani kwao. “Mbona usimfanye mtumwa wako!” rabi mmoja akadokeza halafu. Walikataa ombi letu.

Nilikuwa nimeshiba hayo. Huku wakiwa bado wanasema, nilimshika Kunlaya mkononi tukaondoka chumba cha mahakamani, nikitangaza kwamba Kunlaya hangekuwa kamwe Myahudi hata akiruhusiwa na kwamba mimi sikutaka kubaki nikiwa mmoja wao. ‘Ingawaje, dini itendayo watu hivi haifai kitu!’ nikajiwazia. Sasa nikiwa nimefanya uamuzi wangu, jitihada za pekee zilifanywa kututenganisha. Hata wazazi wangu wapendwa walihusika katika hayo kwa kuchochewa na hisia kali za kidini na mbano uliowekwa juu yetu ili tuachane.

Kwa sasa vita katika Lebanoni kati ya majeshi ya Israeli na maharamia Wapalestina ilikuwa imeanza. Bila shaka, mimi niliitwa nijiunge piganoni, na nilipokuwa nimepenya sana eneo la adui nikihatarisha uhai ili kupigania nchi yangu, paspoti ya Kunlaya ilitwaliwa akaagizwa aondoke nchini. Yote haya yalikuwa sehemu ya jitihada ya kututenganisha. Palepale nilipojua lililokuwa limetendeka, uzalendo wangu ulikwisha. Kwa mara ya kwanza, nilianza kung’amua utaifa ni nini hasa. Nilikuwa nimekuwa na nia ya kujinyima mengi sana kwa ajili ya nchi yangu, na sasa hata sikuruhusiwa kuoa mwanamke niliyempenda! Nilihisi maumivu sana na kuwa nimesalitiwa. Kwangu mimi, kumwondolea mbali Kunlaya kulikuwa kuniondolea mbali mimi. Hivyo, kujitahidi kushinda kesi ile kwa kweli kulikuwa sawa na kujitahidi nijitafutie makao Israeli, nami sikutaka kufanya hivyo.

Hatukuwa na budi ila kuruka ng’ambo tukaoane kisha turudi Israeli kufanya mipango ya mwisho kabla ya kuondoka nchini. Tuliondoka Israeli Novemba 1983, lakini baada tu ya kufanya amani na wazazi wangu. Sikuzote nilikuwa nimeuona unafiki katika dini kuwa ndicho kisababishi kikuu cha matata yetu, lakini sikuwa nimepata kujitenga mbali sana na dini kama wakati huo.

Kuipata Kweli Juu ya Mesiya

Tulishangaa sana kujifunza kwamba sheria fulani hususa ya uhamiaji ilifanya isiwezekane tuishi katika nchi ya mke wangu. Tulilazimika kutafuta nchi ya tatu ili kuishi humo! Mwana wetu wa kwanza alizaliwa Australia, lakini hatungeweza kukaa hata huko. Tuliendelea kuhama nchi hadi nchi. Miaka miwili ilikuwa imepita, na polepole tukaanza kupoteza tumaini la kupata mahali ambapo tungeweza kuishi daima. Oktoba 1985, tulifika New Zealand. ‘Hii ni nchi nyingine tu ya kupitia,’ tukawaza tulipokuwa tukiomba lifti za magari kwenda kaskazini tukiwa na mvulana wetu wa miezi 11. Lakini tulikoseaje!

Jioni moja tulialikwa kwenye mlo na mume na mke wazuri. Baada ya kusikia kisa chetu, mke alijitolea kutusaidia kwa ombi letu la makao ya kudumu New Zealand. Kesho yake, kabla tu ya kuagana, alinipa kitabu kidogo chenye kichwa The New Testament (Maandiko ya Kigiriki). “Kisome,” akasema. “Waandikaji wacho wote walikuwa Wayahudi.” Nilikiingiza katika mkoba wangu na kuahidi kukitazama. Sikujua kamwe yaliyokuwa katika kitabu hicho—kwa kawaida Wayahudi hawasomi fasihi ya Kikristo. Baadaye tulinunua gari kuukuu kisha tukahamia kusini, tukifanya gari hilo liwe kao letu.

Kwenye kituo kimojapo, nilikumbuka ahadi yangu. Nilichomoa kile kitabu nikaanza kukisoma. Nilijikuta nikijifunza juu ya yule mwanamume ambaye imani ya Kiyahudi ilinifunza kutompenda, hata kuchukizwa naye. Nilishangaa kusoma kwamba Yesu alikuwa ametumia muda mwingi wa maisha yake mahali nilipokuwa nimeutumia wangu, kuzunguka Bahari ya Galilaya. Nilishangaa zaidi kuyaona aliyosema. Nilikuwa sijasikia kamwe yeyote akiongea kama yeye.

Nilijaribu kumtafuta makosa mwanamume huyo, lakini wapi. Badala ya hivyo, nilipenda sana aliyofundisha, na kadiri nilivyozidi kusoma juu yake, ndivyo nilivyozidi kujiuliza kwa nini Wayahudi walikuwa wameniambia uwongo juu yake. Nikaanza kuona kwamba ingawa sijawahi kuwa mtu wa kidini, nilikuwa nimehadaiwa na dini hali moja na nilivyokuwa nimefanywa na utaifa. Nilijiuliza, ‘Kwa nini Wayahudi humchukia sana hivyo?’

Swali langu lilijibiwa nusu niliposoma sura 23 katika Mathayo. Niliinuka ghafula kitini niliposoma kwamba Yesu alifichua kwa moyo mkuu unafiki na mwenendo mwovu wa viongozi Wayahudi wa kidini wa wakati wake. ‘Hakuna badiliko,’ nikawaza. ‘Maneno hayahaya ya Yesu yatumika kikamili kwa viongozi Wayahudi wa kidini leo. Nimejionea hilo na kupatwa nalo mwenyewe!’ Sikuwa na namna ila kustahi mwanamume huyu aliyeisema kweli bila hofu. Sikuwa nikitafuta dini nyingine, lakini singeweza kuipuuza nguvu ya fundisho la Yesu.

Kulisikia Jina Yehova

Nilikuwa nimemaliza kusoma karibu nusu ya Maandiko ya Kigiriki tulipowasili Milford Sound, katika Fiordland ya South Island ya New Zealand. Tuliegesha gari letu kando ya gari jingine ambapo mwanamke Mwasia aliketi karibu nalo. Mke wangu alianza kuongea naye. Mume wake Mwingereza alipowasili, tuliwasimulia kisa chetu kwa ufupi. Kisha mume akatuambia kwamba karibuni, Mungu ataharibu serikali zilizopo afanye serikali Yake itawale ulimwengu wenye uadilifu. Ingawa hilo lilisikika kuwa jema, niliwaza: ‘Mwanamume huyu anaota.’

Mwanamume huyo aliendelea, akatuambia juu ya unafiki wa kidini na mafundisho bandia ya makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Halafu mke wake akasema: “Sisi ni Mashahidi wa Yehova.” Nikawaza ghafula, ‘Wamataifa hawa wana nini na Mungu wa Wayahudi? Tena wahusikeje na jina hilo Yehova!’ Nilijua jina hilo, lakini ni mara ya kwanza nilipokuwa nimelisikia likisemwa. Wayahudi hawaruhusiwi kutamka jina hilo. Mume na mke hao wakatupa sisi anwani yao na fasihi fulani ya Biblia, nasi tukaondoka. Hatukujua kwamba kukutana na watu wawili hawa kungebadili maisha zetu.

Kuipata Kweli

Majuma mawili baadaye tukawa katika Christchurch. Tulipangiwa tukae na kusaidia katika shamba la kondoo lililomilikiwa na washiriki wa kanisa moja la Kipentekoste. Hapo shambani nilimalizia kusoma Maandiko ya Kigiriki na kuanza kuyasoma upya. Niliona jinsi Yesu alivyokuwa na maoni ya wazi sana kwamba Mungu yuko. Kwa mara ya kwanza maishani mwangu nikajiuliza, ‘Je, kweli Mungu yuko?’ Nikaanza kulitafuta jibu. Niliweza kupata nakala ya Biblia kamili kwa lugha yangu mwenyewe, Kiebrania, na kuanza kuisoma, ili nijue mengi zaidi juu ya Yehova, yule anayedai kuwa Mungu Mweza Yote.

Mke wangu nami tuling’amua upesi kwamba mafundisho tuliyojifunza kwa wamiliki wa shamba hilo hayakupatana na tuliyosoma katika Biblia yetu. Wala mwenendo wao. Kwa kweli, hatua moja tuliudhiwa sana na jinsi tulivyotendwa shambani hata nikaandika barua juu ya hilo kwa bibi aliyekuwa ametupa yale Maandiko ya Kigiriki. “Kufikia sasa, nadhani, Mungu ametuonyesha ni ‘Ukristo’ upi bandia, na ikiwa kweli Mungu yuko, sasa atatuonyesha Ukristo wa kweli.” Nilimwandikia, bila kujua nilivyokuwa sahihi hasa. Hapo ndipo nikakumbuka waliyokuwa wametuambia wale Mashahidi wawili juu ya unafiki wa makanisa. Tukaamua kukutana tena na Mashahidi hao.

Siku chache baadaye, mume na mke hao walipanga Mashahidi wengine wawili wa Yehova, walioishi karibu, watutembelee. Walitualika kula mlomkuu. Tulizungumzia Biblia kwao, nasi tukapenda tuliyoyasikia. Kesho yake tulialikwa tena tukawa na mazungumzo mengine marefu. Waliyotuonyesha katika Biblia yalisikika kuwa ya kiakili sana hata sote wawili mke wangu nami tukahisi tumegundua ajabu fulani, naam, ile kweli!

Ilikuwa shida kwetu kulala usiku huo. Tulijua kwamba maisha yetu yangebadilika kabisa tangu hapo. Nilianza kukisoma kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, kilichochapishwa na Mashahidi, nami nilipokuwa nikikisoma, nilihisi kama kwamba nilikuwa nimekuwa kipofu lakini sasa ningeweza kuona! Niliweza kuelewa kusudi la uhai, kwa nini mwanadamu aliwekwa duniani, kwa nini sisi hufa, kwa nini Mungu huruhusu mateso mengi sana, na jinsi matukio ya ulimwengu yatimizavyo unabii mbalimbali wa Biblia. Niliazima kwa Mashahidi wa Yehova vitabu vingi kadiri nilivyoweza na kutumia saa nyingi nikivipitia. Ningeweza kuuona vyepesi ubandia wa mafundisho ya Utatu, moto wa mateso, na kutokufa kwa nafsi. Mimi niliipenda hoja ya kiakili na usababu thabiti wa Biblia uliotumiwa na vichapo hivyo.

Kulinganisha Biblia na Waamini

Wamiliki wa shamba lile walijaribu kutuvunja moyo tusijifunze na Mashahidi wa Yehova. “Wao wana Biblia tofauti, tafsiri bandia,” wakatuambia. “Eeh, lazima nihakikishe kama ni kweli,” nikasema. Niliazima tafsiri chache za Biblia kwa wamiliki wa shamba hilo nikapata pia nakala ya New World Translation of the Holy Scriptures nikalinganisha zote na nakala ya Biblia kwa lugha ya Kiebrania. Nilisisimuka kugundua kwamba New World Translation ndiyo tafsiri sahihi na ya kweli zaidi. Uhakika wangu katika vichapo vya Watch Tower Bible and Tract Society uliongezeka.

Mara ya kwanza tulipohudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme, hatukuelewa yote yaliyozungumzwa huko, lakini hatukutatizika kuuelewa upendo mzuri ajabu tulioonyeshwa na kutaniko. Tulivutiwa kwamba jina Yehova lilitajwa mara nyingi sana. “Yehova, Yehova,” nikasema tena na tena wakati wa kurejea kutoka mkutanoni. “Sasa si ‘Mungu’ tu, ni ‘Yehova Mungu’” nikamwambia mke wangu.

Hatimaye tulihamia Christchurch ili kushirikiana zaidi na Mashahidi wa Yehova na kuhudhuria mikutano yote. Kichapo Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? hakikuacha shaka yoyote akilini mwangu kwamba kweli Yehova Mungu yuko na kwamba ndiye Muumba.

Twakuta Ndugu Wapalestina

Baada ya kuwasiliana habari na ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Israeli, nilipokea barua kadhaa kutoka kwa Mashahidi huko. Barua mojapo ilikuwa kutoka kwa Mpalestina anayeishi West Bank, na maneno yake ya ufunguzi yalikuwa: “Ndugu Yangu Rami.” Niliona haiaminiki, kwa kuwa Wapalestina walikuwa adui zangu, halafu sasa ona mmoja wao ananiita “Ndugu Yangu.” Nikaanza kuuthamini upendo usio na kifani wa ulimwenguni pote ulio miongoni mwa Mashahidi wa Yehova. Nikasoma kwamba katika Vita ya Ulimwengu 2, Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani waliingizwa kambi za mateso, walitaabishwa, na waliuawa kwa sababu hawakutaka kupigana na ndugu zao wa kiroho katika mabara mengineyo. Naam, hili ndilo nililotarajia kwa wafuasi wa kweli wa Yesu.—Yohana 13:34, 35; 1 Yohana 3:16.

Tuliendelea kusonga mbele katika funzo letu. Kwa sasa ofisi ya uhamiaji New Zealand ilituruhusu kuishi huko daima, hiyo ikatuongezea shangwe. Sasa tungeweza kutulia na kumwabudu Yehova katika mojapo nchi za kupendeza zaidi ulimwenguni.

Wazazi Wangu Waikabili Kweli

Bila shaka, mara tulipojifunza kweli hizi nzuri ajabu za Biblia, nilianza kuwaandikia wazazi wangu juu yazo. Walikuwa tayari wameonyesha tamaa ya kuja kututembelea. “Nimepata kitu cha bei kuliko kiasi chochote cha fedha,” nikaandika, nikikuza tazamio lao. Walifika New Zealand mwishoni mwa 1987, nasi tukaanza kuongea juu ya kweli ya Biblia karibu mara hiyo. Baba yangu alifikiri nimeshikwa na kichaa kwa sababu ya imani yangu katika Yesu, akajaribu sana kunithibitisha mwenye makosa. Tulibishana karibu kila siku. Hata hivyo, baadaye mabishano hayo yakawa mazungumzo, na mazungumzo hayo yakawa funzo la Biblia. Kwa kuonyeshwa upendo wa kweli na Mashahidi, wazazi wangu waliona upendezi na hoja nzuri ya ile kweli.

Niliona shangwe kama nini kuona wazazi wangu wakifunguliwa kutoka utumwa wa dini bandia na baadaye kutoka utukuzo wa taifa pia! Baada ya ziara ya miezi minne, walirudi na ile kweli kwenye mji wa kwao kando ya Bahari ya Galilaya. Huko waliendelea kujifunza na Mashahidi wawili kutoka kutaniko la karibu zaidi, lililokuwa umbali wa kilometa 65. Upesi wakaanza kuambia wengine juu ya Yehova na Neno lake. Siku chache kabla ya kuanza kwa ile vita ya Ghuba la Uajemi, walionyesha wakfu wao kwa Yehova.

Kwa sasa mke wangu nami tulikuwa tumejiunga na familia ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova tulipoonyesha hadharani wakfu wetu kwa Yehova Mungu katika Juni 1988. Nilijua vema kwamba kwangu ilikuwako njia moja tu ya kumtumikia Yehova na hiyo ilikuwa nikiwa mhudumu wa wakati wote, hivyo nikabamba fursa ya kwanza kuingia utumishi wa wakati wote. Sitasahau kamwe nilivyokuwa sana na nia ya kujitahidi kwa niaba ya nchi yangu, hata kuhatarisha uhai wangu. Sembuse kuwa na nia zaidi kumfanyia hivyo Yehova Mungu, ambaye najua hataniaibisha kamwe!—Waebrania 6:10.

Twamshukuru Yehova kwa tumaini zuri ajabu atupalo, tumaini la kwamba karibuni sayari Dunia itakuwa kao la upendezi kwa wale wapendao uadilifu kwelikweli—kao lisilokuwa na utukuzo wa taifa na dini bandia na, kwa hiyo, lisilo na vita, kuteseka, na ukosefu wa haki. (Zaburi 46:8, 9)—Kama ilivyosimuliwa na Rami Oved.

[Ramani katika ukurasa wa 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

LEBANON

SYRIA

ISRAEL

Tiberias

Occupied Territories

Jericho

Jerusalem

Gaza Strip

JORDAN

[Picha katika ukurasa wa 18]

Rami Oved na familia yake leo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki