Wamishonari—Nani Apaswaye Kuweka Kigezo?
KABLA Yesu Kristo hajaamuru wafuasi wake wafanye wanafunzi, dini nyingine tayari zilikuwa zimekuwa zikiendesha utendaji wa umisheni wa namna zote. Nyingine zilifanya zaidi ya nyingine, kwa kuwa si dini zote zilizo na mfikio wa kijumla, yaani, si zote hufundisha ujumbe uhisiwao kuwa watumika kwa jamii zote za watu kwa usawa.
Kwa kielelezo, kulingana na The Encyclopedia of Religion, maoni hayo ya kufikia watu wote kwa jumla hayazingatiwi sana “katika imani za dini za kikabila na Shintō, na hayaonekani sana katika namna nyingi za Dini ya Confucius, Dini ya Kiyahudi, na Dini ya Zoroaster.” Dini hizi huenezwa “zaidi na mihamo ya jamii za watu au kwa kuingizwa pole kwa pole na majirani wa karibu na utendaji uliopangwa na wamishonari.”
“Dini ya Kihindu ni mfano wa pekee tena wa kutatanisha sana,” yaongezea ensaiklopedia hiyo. “Ingawa kwa njia nyingi yafanana na mapokeo yasiyo ya umisheni,” maana ilienea kwa kukubaliwa pole kwa pole na watu wasio Wahindu, kwa upande mwingine ‘imekuwa na vipindi vya utendaji wa juhudi ya kimishonari.’
“Dini zile zinazotenda kazi sasa zikidai kuwa na maoni ya kuhusisha watu wote kwa jumla na kuonyesha bidii ya kimishonari yenye kusambaa mahali pengi kuliko zilikoanzia,” asema Max L. Stackhouse wa Shule ya Theolojia ya Andover Newton, zatia ndani Uislamu na Dini ya Buddha. Hata hivyo, wamishonari wa Uislamu wasingaliweza kuwa vigezo vya wamishonari Wakristo kwa sababu enzi ya Kiislamu haikuanza mpaka miaka kama 590 baada ya Kristo kutoa amri ya kufanya wanafunzi. Kwa upande mwingine, Dini ya Buddha ilitangulia kuanzishwa kwa Ukristo kwa karibu muda uleule ambao Usilamu uliufuata.
Kigezo cha Kuruhusu Sana Mambo
Mapokeo hudai kwamba yule Buddha alichochea harakati ya kimishonari kwa kuwaambia wanafunzi wake: “Enendeni, watawa wa kiume, mkahubiri lile Fundisho bora, . . . wawili kati yenu wasiende upande uleule!” Harakati za umishonari wa kadiri kubwa hata hivyo zimekuwa chache, hata ingawa wamishonari Wabuddha walikuwa Ulaya mapema kufikia karne ya nne K.W.K. Katika visa vilivyo vingi dini hiyo ilisambazwa na wanabiashara, wahaji, au wanafunzi mmoja-mmoja wenye kusafiri. Ilifika China na sehemu mbalimbali za Asia ya Kusini-magharibi, kwa kielelezo, kupitia njia za biashara baharini na nchi kavu.
Erik Zürcher wa Chuo Kikuu cha Leiden katika Uholanzi ahesabia visababishi vitatu kusambaa kwa Dini ya Buddha. Kimoja ni “mtazamo [wa Dini ya Buddha] wa kuruhusu sana mambo ya dini zote.” Hii ilifanya iwezekane kukubali “itikadi zisizo za Kibuddha kuwa ndizo ukweli uliofunuliwa kwanza na kwa sehemu ndogo” na hata ikawezesha kuingiza “miungu isiyo ya Kibuddha katika jumla ya miungu ya dini hiyo.”
Kisababishi cha pili ni kwamba wamishonari Wabuddha waliingia katika ile iitwayo “hali ya kukosa makao,” maana yake walikanusha hali zote za kilimwengu za kutofautisha watu kitabaka. Wakiwa huru na mipaka yote ya mfumo wa tabaka za vyeo mbalimbali, ambao maana yao ya kidini ilikataliwa na yule Buddha, wangeweza kuchangamana na watu wa kigeni bila kuhofu kuchafuliwa kwa desturi zao.
Kisababishi cha tatu ni kwamba maandishi matakatifu ya Dini ya Buddha hayakushirikiana na lugha yoyote moja iliyo takatifu. Yangeweza kutafsiriwa kwa urahisi katika lugha yoyote. “Hasa katika China,” asema Zürcher, “wamishonari wote wa kigeni walio mashuhuri zaidi walikuwa watafsiri watendaji.” Kwa kweli, walitafsiri kwa kadiri ambayo Kichina kilipata kuwa lugha kubwa ya tatu kwa fasihi ya Kibuddha, ikajiunga na Pali na Sanskrit.
Katikati ya karne ya tatu K.W.K., mtawala wa milki ya Kihindi, Mfalme Aśoka, alifanya mengi kueneza Dini ya Buddha, akiimarisha umishonari wao pia. Ingawa hivyo, katika enzi hii iliyoutangulia Ukristo, Dini ya Buddha ilibaki sana-sana ikiwa na kitovu chao katika India na ile iitwayo Sri Lanka leo. Kwa njia nyingi, ni baada tu ya mwanzo wa enzi ya Kikristo kwamba Dini ya Buddha ilienea katika China, Indonesia, Iran, Japani, Korea, Malasia, Myanmar, Vietnam, na kwingineko.
Wamishonari Wabuddha walioenda China yaonekana hawakuona ubaya wowote wa kurekebisha dini yao ili ikubalike zaidi. The Encyclopedia of Religion yasema kwamba “maandiko makuu ya Kibuddha yalipewa fasiri mpya; fasihi za kukubali-kubali makosa, mashairi mapya, na sheria na virekebishi vipya vilitangazwa vikarekebisha, naam, hata vikabadili mambo ya ujumbe wa Kibuddha ili uweze kupachikwa, na kwa njia fulani-fulani utie nguvu mpya, katika mambo ya dini za wenyeji na zile za Confucius na Tao katika bara hilo.”
Nyakati fulani, kama vile makala za wakati ujao katika mfululizo huu zitakavyoonyesha, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wamefuata kigezo cha watangulizi wao wa umishonari wa Kibuddha. Ingawa wametafsiri miandiko yao mitakatifu katika lugha nyinginezo, mara nyingi wameruhusu, au hata wakaendeleza, “mfyonzo wa imani na desturi ya ibada ya kipagani,” kama vile mwanahistoria Will Durant auitavyo, katika mazoea yao ya kidini.
Kufuata “Mishonari Mkuu”
Judaism and Christian Beginnings chaeleza kwamba Uyuda haukuendeleza utendaji wa kimishonari katika maana ileile ambayo Ukristo ulifanya bali “kwa kulinganishwa haukufanya kazi ya kuongoa watu.” Hata hivyo, mtungaji wa kitabu hicho, Samuel Sandmel, asema kwamba “kulikuwa angalau na msukumo wenye kurudi-rudi, angalau wa mara kwa mara, wa kuelekea kuongoa watu.”
Sandmel aeleza kwamba “katika fasihi ya Kirabi Baba Abrahamu huonyeshwa mara nyingi kuwa ndiye mishonari mkuu.” Yeye awaza kwamba “hakika maoni [haya] ya kwamba Abrahamu ndiye mishonari yasingaliweza kutokea kama angalau sehemu fulani za jumuiya ya Kiyahudi zisingalikuwa na mwelekeo fulani wa kupendelea kutafuta waongofu au, angalau wa kupendelea kuwapokea katika imani wale ambao kwa hiari yao wenyewe walitafuta kuongolewa.”a[16]
Kwa wazi, katika karne mbili za kabla tu ya Wakati wa Kawaida, utendaji wa umishonari wa Kiyahudi ulizidishwa, hasa katika nchi zenye kusema Kigiriki, wakati dini za kipagani zilipoanza kupoteza uvutio wazo. Utendaji huu uliendelea hadi Wakati wa Kawaida, lakini ukaharamishwa katika karne ya nne W.K., ambapo Milki ya Kiroma ilichagua kufuata namna iliyotoholewa ya Ukristo uwe dini yayo rasmi.
Kuweka Kigezo
Hata hivyo, kigezo kilichowekwa na wamishonari Wayahudi hakikuwa kile wamishonari Wakristo walichoambiwa wafuate. Kwa kweli, kwa habari ya Mafarisayo Wayahudi wa siku yake, Yesu alisema: “Nyinyi huendea bahari na nchi kavu kukuru-kakara kufanya mwongofu mmoja tu, halafu nyinyi humfanya aive mara mbili kwa uharibifu kuliko nyinyi wenyewe.” (Mathayo 23:15, Phillips) Kwa hiyo hata ingawa wamishonari Wayahudi walimwona Abrahamu kuwa “ndiye mishonari mkuu,” kwa wazi hawakuongoa watu waifuate aina ya imani ambayo Abrahamu alikuwa nayo katika Yehova Mungu.
Kwa wamishonari Wakristo kigezo cha kufuata ni kile kielelezo kikamilifu kilichotolewa na mishonari mkuu aliye maarufu zaidi, Yesu Kristo. Muda mwingi kabla hajaitoa amri yake ya kufanya wanafunzi, alianza kuwazoeza wanafunzi wake wa mapema kuufanya utendaji wa umishonari wa kimataifa ambao amri hiyo ingehusisha. Kwa kuwa ungekuwa mradi wa karne nyingi, ilifaa kuuliza swali la kwamba, Je, wafuasi wa Kristo wangeshikamana na kigezo alichokuwa ametoa?
Karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida ilipokuwa ikikaribia kumalizika, bado jibu halikuwa wazi. Lakini sivyo ilivyo leo, wakati karne ya 20 ikaribiapo kumalizika. Miaka kama 1,900 iliyopita yatuonyesha wazi kabisa kwamba utendaji wa kimishonari umefanywa.
Kuanzia wakati Ukristo ulipozaliwa katika Palestina, ulipanuka kuingia katika ulimwengu mzima. Kusonga kwao kuingia Makedonia kulikuwa hatua moja. Soma juu ya hilo katika toleo letu linalokuja.
Kupata kielelezo cha yale ambayo wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo wamefanya, angalia yaliyotukia kwa karne kadhaa katika Mexico. Unaposoma usimulizi unaofuata, jiulize, ‘Je, wao wamekuwa mawakili wa nuru au mawakili wa giza?’
[Maelezo ya Chini]
a A Guide to Jewish Religious Practice chasema: “Abrahamu huonwa kuwa ndiye baba ya waongofu wote . . . Ni desturi kwa waongofu kuitwa mwana, au binti, ya baba yetu Abrahamu.”
[Picha katika ukurasa wa 7]
Yesu alianzisha kazi ya umishonari wa Kikristo, akizoeza wafuasi wake na kuweka kigezo walichopaswa kufuata