Wamishonari Mawakili wa Nuru au waGiza? Sehemu 5
Ujumbe Mpya kwa Ulimwengu Mpya
KIZIO cha Magharibi kiliitwa kwanza Ulimwengu Mpya katika 1516. Wakati Columbus ‘alipokigundua’ katika 1492, aligundua pia kwamba tayari watu walikuwa wakiishi humo na walikuwa wamekuwa wakifanya hivyo kwa mamia ya miaka. Lakini ndipo kwa mara ya kwanza, Waamerika Wenyeji walipata mwonjo wa Ukristo wa jina. Hii ingemaanisha nini kwa ule Ulimwengu Mpya?
Kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilikuwa limedhibiti maisha za Wanaulaya karibu kikamilifu. Liliweka viwango na kuamrisha sheria katika karibu kila uwanja wa shughuli ya kibinadamu, kutia na serikali. Ushirikiano huo wa Kanisa na Serikali, upatano uliokuwa umezidisha zile Krusedi, ulikuja kuutawala Ulimwengu Mpya pia.
Sidney H. Rooy wa Educación Teológica katika Buenos Aires aandika kwamba kufikia mwisho wa karne ya 15, wafalme Wahispania walisadiki kwamba “taji la Kihispania ndilo lililokuwa chombo kilichochaguliwa kimungu kwa wokovu wa Ulimwengu Mpya.” Ofisi ya papa iliweka mpaka wa kuwazia wa kaskazini-kusini katika Atlantiki ikizigawanya haki za ugunduzi kati ya Hispania na Ureno. Katika 1494 zile serikali mbili zilitia sahihi mkataba wa kusogeza mpaka huo mbali zaidi magharibi. Hivyo, Hispania ilipokuwa ikichukua hatua ya kukaa sehemu zilizo nyingi za Amerika ya Kati na ya Kusini, Ureno ilihamia Brazili, ambayo pwani yayo ya mashariki sasa ilikuwa mashariki mwa ule mpaka. Kulingana na Rooy, nchi zote mbili zilifasiri amri hiyo ya kipapa kumaanisha kwamba “haki ya mabara hayo iliambatana na wajibu wa kueneza evanjeli kwa vikundi vya wenyeji.”
Kuushinda Ulimwengu Mpya
Columbus aliandamwa katika uabiri wake wa pili katika 1493 na kikundi cha mandugu-watawa waliochaguliwa ili hasa wawageuze wenyeji. Tangu hapo na kuendelea, majemadari Wanaulaya washinda mabara na mapadri wamishonari walifanya kazi bega kwa bega kuushinda Ulimwengu Mpya.
Katika 1519, Hernán Cortés alifikia ile iitwayo Mexico sasa akiandamwa na kasisi wa kijeshi na mapadri wengine. Katika muda wa miaka 50, idadi ya wamishonari ilikuwa imeongezeka kufikia 800. Wengine 350 walikuwa katika Peru, ambayo Francisco Pizarro alikuwa ameifikia katika 1531.
Barua rasmi za papa zilizotolewa katika 1493 ziliwapa wenye mamlaka wa kilimwengu haki ya kuungwa mkono waliyoitaka kwa shughuli yao ya kushinda mabara. Walifikiri kwamba wangeweza kutegemea kuungwa mkono na Mungu kwa sababu walihisi kwamba ukoloni ulikuwa mapenzi yake. Maofisa wa Kanisa, wakiwa na hamu ya kujipendekeza, walijiingiza kuhalalisha mfumo huo wa kikoloni. Kwa kweli, Myesuiti wa karne ya 17 jina lake António Vieira, aliyezaliwa katika Ureno lakini akalelewa katika Brazili, alisifu ukolonishi, akisema kwamba bila huo isingaliwezekana kueneza evanjeli.
Wamishonari hawakuona dosari yoyote katika kutumia ukoloni kuwa chombo cha kuenezea dini yao. Hata hivyo, hii iliwafanya sehemu kamili ya ulimwengu ambao Yesu alisema wafuasi wake hawapaswi kuwa sehemu yao.—Yohana 17:16, linganisha NW.
Kufanya Wageuzwa
Kulingana na Rooy, kwanza wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walianza “kung’oa desturi za zamani za kidini na madhihirisho yaliyo ya nje-nje zaidi ya dini ya Kihindi.” Aliongezea hivi: “Ingawa ushurutisho bado ulitumiwa ulipohitajika, Wahindi wengi waligeuzwa kwa njia zenye amani kwa kufikiwa moja kwa moja na mapadri.”
Bila shaka, wamishonari fulani waliamini kwamba kwa kweli ushurutisho haukupata kamwe kuwa wa haki. Kwa kielelezo, mishonari mmoja aliye padri wa Dominika ya Kihispania jina lake Bartolomé de Las Casas alikuja kutokubali njia hizo katili zilizotumiwa. Alisihi-sihi katika Hispania kwa ajili ya Wahindi, na kwa sababu hiyo serikali ikampa cheo cha “Mtetezi wa Wahindi.” Hata hivyo, jitihada zake zilipokewa kwa maitikio mchanganyiko. Wengine wamemwita mwanakrusedi, nabii, mtumishi wa Mungu, na mwona-maono; wengine wamemwita haini, mwenye kichaa cha kushuku-shuku, na mleta-machafuko, na mtangulia-Marx.
Ule mradi wa kung’oa desturi za zamani za kidini uliachishwa baadaye. Mara wenyeji walipokwisha kusongwa kulikubali jina la Ukristo, waliruhusiwa kudumisha imani na mazoea yao ya kipagani. Hivyo, “misherehekeo mingi ya Kikristo miongoni mwa Wahindi Wasierra wa Peru,” chasema Man, Myth & Magic, “zina mazoea yaliyo masalio ya imani za Inca zilizosahauliwa.” The Cambridge History of Latin America chaeleza kwamba Wahindi wa Mexico walichukua katika Ukristo “mambo yale yaliyofaana na mahitaji yao wenyewe ya kiroho na ya desturi za kidini kisha wakayachanganya na mambo ya imani yao ya mababu wa kale.”
Ni kweli, mamia ya maelfu wa Waamerika Wenyeji walibatizwa. Lakini ule “Ukristo” waliotwikwa ulikuwa wa kijuujuu tu. Ni wakati mchache uliotumiwa kuwafundisha misingi ya Ukristo ya kujengea imani yenye nguvu. The Cambridge History of Latin America chasema hivi: “Kulikuwako vionyeshi vya kuhangaisha kwamba Wahindi waliokuwa wamechagua kufuata ile imani mpya wakiwa na kile kilichoonekana kama idili bado walistahi sanamu zao za zamani kwa siri.” Kwa kweli, Wahindi fulani yaripotiwa waliweka sanamu zao za kipagani nyuma ya altare zao ‘za Kikristo’ iwapo yule “Mungu wa Kikristo” angeshindwa kuitikia. Pia walifanya polepole kuacha vigezo vyao vilivyoimarika zamani vya mwenendo kama vile ndoa ya wenzi wengi.
Washiriki wa jumuiya za Wakatoliki wa Kiroma hawakutenda sikuzote kwa njia ambayo mtu angaliwatarajia wamishonari “wa Kikristo” watende. Magombano kati ya jumuiya mbalimbali yalitokea-tokea. Wayeswiti hasa walichambuliwa mara nyingi kwa sera na matendo yao. Kwa kweli, katika 1759 wao walifukuzwa kutoka Brazili.
Kuwasili kwa wamishonari Waprotestanti hakukubadili mambo sana. Kadiri idadi za wamishonari zilivyoongezeka, ndivyo pia ulivyoongezeka ukosefu wa muungamano ulio kawaida ya Ukristo wa jina. Wakatoliki waliwashtaki Waprotestanti juu ya kukuza ubeberu; Waprotestanti waliwashtaki Wakatoliki juu ya kueneza imani za kipagani na daraka la kudumisha watu katika umaskini. Madai yote haya yalikuwa na kweli chungu nzima. Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo, Wakatoliki na Waprotestanti pia, walishindwa kufuata kielelezo cha Yesu.
Kulingana na The Encyclopedia of Religion, kotekote katika ule Ulimwengu Mpya “ugeuzaji ulisonga mbele ukiwa silaha ya majasirio ya serikali za Kihispania, Kifaransa, na Kiingereza za kutafuta koloni.” Ijapokuwa Hispania na Ureno zilikaza fikira juu ya Amerika ya Kilatini, Ufaransa na Uingereza zilihusika zaidi katika zile ambazo baadaye zilikuja kuwa Marekani na Kanada.a
Kama wale wamishonari katika Amerika ya Kilatini, wamishonari Wafaransa na Waingereza walitanguliza mambo yasiyopaswa na wakanaswa katika mambo ya kisiasa. Hivyo, chasema The Encyclopedia of Religion, “kufikia mwisho wa enzi ya Kifaransa katika Kanada, wamishonari walikuwa wamefanikiwa zaidi katika kufanya Wahindi wawe waaminifu washikamanifu kwa Ufaransa kuliko katika kuwageuza.”
Upande wa Mungu au wa Dhahabu?
Watu fulani huenda wakadai kwamba “mpanuko wa ufalme wa Mungu ulikuwa ndio mradi” uliofuatiwa na majemadari washinda mabara wa mapema. Lakini kwa uhalisi zaidi, The Cambridge History of Latin America chasema hivi: “Juu ya yote, walitaka dhahabu.” Ilifikiriwa kwamba Wahindi wakiisha kugeuzwa, ‘wangetoa wingi wa dhahabu kwa usikivu.’
Hivyo wengine wa wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walijiacha wawe vyombo vya hiari vya wale waliokuwa na makusudio manyonge. Mmojapo Wanaulaya wa kwanza kutambua hili alikuwa Bartolomé de Las Casas, aliyetajwa mapema kidogo. The New Encyclopædia Britannica chamnukuu akiandika hivi katika 1542: “Sababu ambayo imefanya Wakristo waue na kuangamiza idadi ile isiyohesabika ya nafsi ni kwamba wamesukumwa na kutaka kwao dhahabu na tamaa yao ya kujitajirisha kwa muda mfupi sana.”
Washindi Wanaulaya hawakuleta faida kubwa kwa njia ya mwangazio wa kiroho. Katika kitabu chake Mexico, James A. Michener asema kwamba watetezi wa Kikristo hudai kwamba wakati Cortés alipovamia Mexico, ‘aliikuta imekaliwa na washenzi aliowaletea ustaarabu na Ukristo pia.’ Hata hivyo, Michener asema kwamba Wahindi wa Mexico, hata katika 900 W.K., ‘hawakuwa washenzi, lakini walilegea sana katika kulinda ustaarabu wao mzuri sana hivi kwamba waliruhusu washenzi halisi wawatawale.’ “Washenzi halisi” hawa walikuwa baadhi ya wale waitwao eti Wakristo.
Kazi ya Matayarisho
Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo hawakutii maagizo ya Yesu ‘kufanya wanafunzi, kuwafundisha kushika mambo yote’ aliyokuwa ameamuru. (Mathayo 28:19, 20) Wageuzwa wapya hawakufundishwa kudhihirisha tunda la roho ya Mungu. Hawakuungamanishwa katika ile imani moja.
Hata wale kati ya wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo waliokuwa na moyo mweupe hawangeweza kufanya jambo lizidilo kueneza namna ya Ukristo wa uasi-imani. “Nuru” iliyoangazwa juu ya ule Ulimwengu Mpya ilikuwa hafifu kwelikweli. Hata hivyo, kwa kujulisha Biblia kwa kadiri fulani, wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walifanya kazi ya matayarisho kwa ajili ya ile kampeni muhimu ya kimishonari ambayo Yesu alitoa unabii kwamba ingetukia wakati wa mwisho. (Mathayo 24:14) Ingekuwa kampeni isiyo na kifani, iliyo na mafanikio zaidi ya zote zilizopata kuendeshwa katika historia ya Kikristo, ikinufaisha watu wa mataifa yote. Soma habari zayo katika toleo linalokuja katika ile makala “Kufanya Wanafunzi wa Kweli Leo.”
[Maelezo ya Chini]
a Bila shaka, uvutano wa Kihispania ulihisiwa katika Florida na sehemu ya kusini-magharibi na ya magharibi ya mbali ya ile iliyo Marekani sasa, hasa California.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Wamishonari walikuja kwenye zile kontinenti za Amerika wakiwa na majemadari washinda mabara Wanaulaya
[Hisani]
Kutoka kitabu Die Helden der christlichen Kirche