Mavuno ya Jumuiya ya Wakristo Katika Afrika
NDOTO ya Charles Lavigerie la kugeuza Algeria kuwa ‘taifa la Kikristo’ ilithibitika kuwa hivyo tu—ndoto. Leo asilimia 99 ya wakazi wa Algeria ni Waislamu, na Jumuiya ya Wakristo imedhoofika katika sehemu kubwa za Afrika Kaskazini. Lakini namna gani sehemu ile nyingine ya bara hilo?
“Ukristo,” adai Dakt. J. H. Kane, katika A Concise History of the Christian World Mission, “umefanya waongofu wengi zaidi katika Afrika ya Weusi kuliko nchi nyinginezo zote zinazositawi.” Hata hivyo, je, waongofu hao kwa kweli ni Wakristo? “Hatari moja kubwa katika kanisa la Afrika,” akiri Dakt. Kane, “ni ule mchanganyiko wa Ukristo na upagani.” Pia, maneno yake “kanisa la Afrika” yametumiwa vibaya. Kihalisi kuna maelfu ya makanisa ya Afrika, kila moja likiwa na njia ya ibada yalo lenyewe. Kwa nini?
Kupanda Mbegu za Farakano
Mbegu za farakano zilipandwa hata kabla ya wamishonari kuanza kuabiri kuelekea Afrika. Sosaiti ya Wamishonari ya London ilipata washiriki kutoka kwa makanisa tofauti-tofauti, na mabishano makali ya kimafundisho yalitukia kati ya wamishonari hao walipokuwa wakisafiri kwenda kwenye migawo yao. Pambano kwa hakika lingekuwa baya zaidi baada ya wao kuishi kwa muda fulani katika mahali pa misheni zao.
“Wamishonari,” aandika Profesa Robert Rotberg katika kitabu chake Christian Missionaries and the Creation of Northern Rhodesia 1880-1924, “walipigana vikali wao kwa wao na pia pamoja na wakurugenzi wao wa ng’ambo, mara nyingi kwa hasara ya makusudio yao ya kueneza evanjeli. . . . Ilionekana kana kwamba wamishonari walitumia kiasi kilekile cha wakati na nishati katika kuandika mabishano hayo kama walivyotumia katika kujaribu kupata waongofu.”
Nyakati nyingine, mabishano ya wamishonari yalitokeza kufanyizwa kwa misheni za ushindani. Misheni za Katoliki na Protestanti zilishindana kwa bidii nyingi ili kupata waongofu. Ukosefu huohuo wa umoja bila shaka ungeonyeshwa miongoni mwa waongofu wao. Baadaye mamilioni ya Waafrika waliyaacha makanisa ya misheni wakafanyiza makanisa yao wenyewe.
“African Independent Churches,” aandika mwanahistoria wa umishonari Dakt. Kane, “hupatikana kotekote Afrika . . . Kwa ujumla kuna vikundi elfu saba hivi katika harakati hiyo.” Si ushindani pekee miongoni mwa wamishonari wenye imani zenye kupingana uliosababisha hilo. Katika kitabu chake The Missionaries, Geoffrey Moorhouse aeleza kwamba sababu nyingine ya “kujitenga kwa makanisa hayo ya Waafrika” ilikuwa “kuchukia kwayo ubwana mkubwa wa watu weupe.”
Wakristo au Wabaguzi Rangi wa Ulaya?
“Wamishonari,” akiri Dakt. Kane, “walijiona kuwa mabwana wakubwa.” “Waliamini kwamba ni lazima dini ya Kikristo iandamane na utamaduni wa Ulaya na uongozi wa Ulaya,” asema Adrian Hastings katika kitabu chake African Christianity.
Charles Lavigerie alikuwa kiongozi mmoja mishonari aliyekuwa na maoni hayo. Mwingine alikuwa John Philip, kiongozi wa misheni za Sosaiti ya Wamishonari ya London katika kusini mwa Afrika. “Wamishonari wetu,” akajigamba katika 1828, “wanapanua . . . masilahi ya Uingereza, uvutano wa Uingereza, na milki ya Uingereza. Popote ambapo mishonari aanza kutafuta waongofu miongoni mwa kabila lisiloerevuka, chuki zao zisizo na sababu dhidi ya serikali ya kikoloni hukoma; kutegemea kwao koloni kunaongezeka kwa kuundwa kwa tamaa zisizo halisi; . . . viwanda, biashara na ukulima husitawika kwa ghafula; na mwongofu yeyote wa kweli kutoka miongoni mwao . . . huwa msaidizi na rafiki wa serikali ya kikoloni.”
Je! inashangaza kwa vyovyote kwamba serikali za Ulaya ziliwaona wamishonari hao kuwa mawakili wenye kusaidia sana upanuzi wa kikoloni? Kwa upande wao, wamishonari walikaribisha ushindi wa kikoloni wa Afrika. Kama walivyotangaza rasmi kwenye Mkutano wa Wamishonari wa Ulimwengu wa 1910 katika Edinburgh: “Isingewezekana . . . sikuzote kutenganisha lengo la umishonari na lengo la Serikali.”
Walitawala Wakiwa Wafalme Katika Afrika
Ili kuthibitisha mamlaka yao, baadhi ya wamishonari walitegemea nguvu za kijeshi za koloni. Miji ya pwani nyakati nyingine iliharibiwa na meli za kivita za Uingereza kwa sababu wakaa-vijijini walikuwa wamekataa kukubali mamlaka ya wamishonari. Katika 1898, Dennis Kemp, mishonari wa dini ya Wesley, alionyesha “usadikisho wake thabiti kwamba Jeshi na Kikosi cha Wanamaji cha Uingereza hutumiwa na Mungu leo ili kutimiza kusudi Lake.”
Baada ya kujiimarisha wenyewe, wamishonari nyakati nyingine walijitwalia mamlaka ya kilimwengu ya machifu wa kikabila. “Wamishonari wa Sosaiti ya Wamishonari ya London,” aandika Profesa Rotberg, “mara nyingi walitumia nguvu ili kudumisha sheria yao ya kitheokrasi. Chombo walichopenda sana ambacho kwacho walijulisha kutopendezwa kwao kilikuwa kile kikoti, mjeledi mrefu uliofanyizwa kwa ngozi ya kiboko iliyokaushwa. Kwao, Waafrika walichapwachapwa bila kusita kwa karibu kisababu chochote.” “Mwongofu mmoja Mwafrika,” asema David Lamb katika kitabu chake The Africans, “akumbuka mishonari mmoja Mwanglikana katika Uganda aliyeitwa Bwana Botri aliyekuwa mara nyingi akishuka kutoka mimbara yake wakati wa mahubiri ili kuwachapa kwa henzirani Waafrika waliochelewa.”
Akishtushwa na vitendo vya jinsi hiyo, mishonari mmoja, James Mackay, aliwasilisha lalamiko lake kwa wakurugenzi wa Sosaiti ya Wamishonari ya London. “Badala ya kuonwa kuwa watu weupe wanaowaletea habari njema za upendo wa Mungu,” alionya, “twajulikana na kuogopwa.”
Vita vya Ulimwengu
“Kwa karne moja na zaidi,” chataarifu kitabu The Missionaries, “[Waafrika] walikuwa wameambiwa daima na kwa dhati kwamba kupigana, hata tabia zote za kikatili ambazo hutokezwa na kupigana huko, zilikuwa za bure na zenye uovu.” Kisha, katika 1914, Vita ya Ulimwengu 1 ilitokea kati ya nchi za Ulaya zilizoitwa eti nchi za Kikristo.
“Wamishonari wa karibu kila taifa walivutwa wahusike katika Vita hiyo Kubwa,” aeleza Moorhouse. Kwa aibu yao, wamishonari waliwasihi waongofu wao Waafrika waunge mkono upande mmoja. Baadhi ya wamishonari hata waliongoza vikosi vya Waafrika vitani. Tokeo la vita hiyo huelezwa vizuri na Profesa Stephen Neill katika kitabu chake History of Christian Missions: “Bila kufikiri kwanza na bila akili timamu, mataifa ya Ulaya, yakiwa na madai yao yenye juhudi kuhusu kuwa na mamlaka yote ya Ukristo na mwerevuko, yalikuwa yameingia vita ya wenyewe kwa wenyewe ambayo ingeyaacha yakiwa yamefukarika kiuchumi na bila wema hata kidogo.” “Vita ya Ulimwengu ya Pili,” aendelea Neill, “ilimaliza tu lile ambalo ile ya kwanza ilikuwa imetimiza tayari. Visingizio vya kiadili vya Magharibi vilionyeshwa kuwa vya uwongo; ‘Jumuiya ya Wakristo’ ilifunuliwa kuwa ngano tu. Haikuwezekana tena kusema juu ya ‘Magharibi ya Kikristo.’”
Kwa kueleweka, kujitenga kwa makanisa ya Waafrika baada ya Vita ya Ulimwengu 1 kuliongeza mwendo. Lakini namna gani Waafrika walioshikamana na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo? Je! baada ya hapo walifundishwa kweli kutoka Biblia?
Imani za Afrika za Wazazi wa Kale
Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walilaumu mazoea ya kidini ya Waafrika, kama vile kuomba shauri kwa waaguzi ili kutuliza wazazi wao wa kale waliokufa. Wakati uo huo, wamishonari walisisitiza kwamba wanadamu wote wana nafsi isiyoweza kufa. Waliendeleza pia kuheshimiwa kwa Mariamu na “watakatifu.” Mafundisho hayo yalithibitisha imani ya Waafrika kwamba wazazi wao wa kale walikuwa hai. Pia, kwa kuheshimu mifano ya kidini, kama vile msalaba, wamishonari walithibitisha utumizi wa Mwafrika wa hirizi kuwa njia ya kujilinda na roho waovu.
Profesa C. G. Baëta aeleza katika kitabu chake Christianity in Tropical Africa: “Inawezekana kwa Mwafrika kuimba kwa idili Kanisani, ‘Sina kimbilio jingine ila Mungu’, huku angali akibeba hirizi mahali fulani mwilini mwake, au aweze kutoka Kanisani na kwenda moja kwa moja kwa mwaguzi wake, bila kuhisi kwamba anavunja kanuni yoyote.”—Linganisha Kumbukumbu la Torati 18:10-12 na 1 Yohana 5:21.
Wamishonari wengi waliwaambia Waafrika kwamba babu zao wapagani walikuwa wakiteswa katika helo yenye moto na kwamba wangepatwa na jambo ilo hilo ikiwa wangekataa kukubali mafundisho ya umishonari. Lakini fundisho la mateso ya milele hupingana na taarifa za wazi katika Biblia ileile ambayo wamishonari walijitahidi sana kutafsiri katika lugha za Afrika.—Mwanzo 3:19; Yeremia 19:5; Warumi 6:23.
Kwa kweli, Biblia hutaarifu kwamba nafsi za kibinadamu zenye dhambi hufa na kwamba “wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, 10; Ezekieli 18:4) Kwa habari ya Waafrika ambao hawakupata nafasi ya kusikia kweli ya Biblia, wana taraja la kutiwa ndani katika ule “ufufuo [unaokuja] wa wafu, wenye haki na wasio haki.” (Matendo 24:15) Hao waliofufuliwa watafundishwa kuhusu uandalizi wa Mungu wa wokovu. Kisha, wakiitikia upendo wa Mungu kwa kuthamini, watathawabishwa na uhai wa milele kwenye dunia-paradiso.—Zaburi 37:29; Luka 23:43; Yohana 3:16.
Badala ya kufundisha kweli hizo nzuri ajabu za Biblia, Jumuiya ya Wakristo imewaongoza Waafrika vibaya kwa mafundisho bandia na unafiki wa kidini. Kwa hakika, kujihusisha kwa wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo katika ushindi wa kikoloni wa Afrika hakuungwi mkono popote katika Biblia. Tofauti na hilo, Yesu alisema kwamba Ufalme wake “si sehemu ya ulimwengu huu” na kwamba wafuasi wake vilevile ‘wasingekuwa sehemu ya ulimwengu.’ (Yohana 15:19; 18:36, New World Translation) Wakristo wa mapema walikuwa mabalozi wa Yesu Kristo, si wa serikali za kilimwengu.—2 Wakorintho 5:20.
Kwa hiyo, mavuno ya Jumuiya ya Wakristo katika Afrika kwa ujumla ni ya kuhuzunisha, yakionyeshwa na mafarakano yenye kushtua, ukosefu wa uaminifu, na “mchanganyiko wa Ukristo na upagani.” Jeuri ambayo imeonekana katika sehemu nyingi za “Kikristo” za Afrika kwa hakika haipatani na mafundisho ya yule “Mwana-Mfalme wa Amani.” (Isaya 9:6, NW) Mazao ya kazi ya Jumuiya ya Wakristo katika Afrika yanatofautiana kabisa na maneno ya Yesu kuhusu wafuasi wake wa kweli. Katika sala kwa Baba yake wa kimbingu, Yesu aliomba kwamba “wawe wamekamilika katika umoja; ili ulimwengu ujue ya kuwa ndiwe uliyenituma.”—Yohana 17:20, 23; 1 Wakorintho 1:10.
Je! hilo lamaanisha kwamba kazi yote ya mishonari katika Afrika imekosa kufaulu? Hasha. Mazao mema ya kazi ya kweli ya Kikristo ya mishonari katika Afrika na kotekote ulimwenguni itazungumziwa katika makala zifuatazo.
[Picha katika ukurasa wa 6]
Viongozi wamishonari wa karne iliyopita, kama vile John Philip, waliamini kwamba mwerevuko wa Ulaya na Ukristo vilikuwa kitu kimoja
[Hisani]
Cape Archives M450
[Picha katika ukurasa wa 7]
amishonari wa Jumuiya ya Wakristo walitia moyo imani za Afrika za wazazi wa zamani kwa kueneza mafundisho yasiyo ya kibiblia, kama vile kutokufa kwa nafsi
[Hisani]
Kwa hisani ya Africana Museum, Johannesburg