Wamishonari Mawakili wa Nuru au wa Giza?—Sehemu 2
Kuhama Magharibi Kuingia Ulaya
IKIWA utume wa Yesu wa kimishonari ungetekelezwa, ingekuwa lazima watu ulimwenguni pote wafikiwe kwa ujumbe wa Ukristo. (Mathayo 28:19; Matendo 1:8) Uhakika huu ulikaziwa wakati ambapo mtume katika safari ya pili kati ya zile tatu za kimishonari, mtume Paulo aliona njozi ambamo alisihiwa hivi: “Vuka, uje Makedonia utusaidie.”—Matendo 16:9, 10.
Paulo alikubali mwaliko huo, na karibu 50 W.K., alivuka kuhubiri katika Filipi jiji la Ulaya. Lidia na nyumba yake wakawa waamini, na kutaniko likaanzishwa. Hicho kilikuwa kituo cha kwanza tu cha msongo wenye ushindi wa Ukristo kuvuka Ulaya yote. Paulo mwenyewe alihubiri baadaye katika Italia, yawezekana hata katika Hispania.—Matendo 16:9-15; Warumi 15:23, 24.
Hata hivyo Paulo hakuwa mishonari pekee wa Ukristo. Mtungaji J. Herbert Kane aandika hivi: “Lazima iwe kulikuwa na wengine wengi, ambao majina yao yameachwa yapotee katika historia. . . . Matendo ya Mitume hakisimulii hadithi yote.”—A Global View of Christian Missions From Pentecost to the Present.
Hata hivyo, hatujui ni kwa kadiri gani wafuasi wengine wa Yesu walitumikia wakiwa wamishonari katika mabara ya kigeni. Imani za mapokeo ya kwamba Thomas alienda India na Marko mweneza-evanjeli akaenda Misri haziwezi kuhakikishwa. Jambo tujualo ni kwamba wanafunzi wote wa kweli wa Kristo walikuwa na roho ya kimishonari na kwamba wote walifanya kazi ya mishonari angalau katika bara la kwao. Kama vile Kane aandikavyo: “Tukio hili la kihistoria [Pentekoste] lilikuwa alama ya mwanzo wa kanisa la Kikristo na mzinduo wa harakati ya kimishonari, kwa maana katika siku hizo kanisa lilikuwa misheni.”
Kwenye Pembe za Mbali za Ulaya
Wayahudi waliamini katika ibada ya Mungu mmoja wa kweli. Waliweka matumaini yao juu ya Mesiya aliyeahidiwa. Waliyakubali Maandiko ya Kiebrania kuwa Neno la Mungu la kweli. Hivyo, raia za nchi ambazo Wayahudi walikuwa wametawanywa ndani yazo yaelekea walifahamiana kidogo na imani hizi. Kwa kuwa hizi zilikuwa pande za ibada ambazo Wakristo na Wayahudi walifuata kwa hali moja, ujumbe wa Ukristo haukuwa mgeni kabisa ulipotokea. Kulingana na Kane, “mambo haya yalikuwa ya msaada mkubwa kwa wamishonari Wakristo walipokuwa wakisafiri kotekote katika ulimwengu wa Kiroma wakiihubiri gospeli na kuanzisha makanisa.”
Hivyo utawanyo wa Wayahudi uliutayarishia Ukristo njia. Ukristo ulienea kwa haraka kwa sababu Wakristo walikuwa na roho ya umishonari. “Gospeli ilihubiriwa na watu wa kawaida,” asema Kane, akiandika hivi: “Kokote walikoenda waliishiriki kwa furaha imani yao mpya pamoja na marafiki, majirani, na watu wasiowajua.” Mwanahistoria Will Durant aeleza hivi: “Karibu kila mwongofu, akiwa na juhudi ya mtaka-mapinduzi, alijitwika daraka la usambazaji.”
Kufikia 300 W.K., namna iliyofisidiwa ya Ukristo ilikuwa imeenea kwa mapana kotekote katika Milki ya Kiroma. Ufisadi huo, kuanguka kutoka ibada safi, ulikuwa umetabiriwa. (2 Wathesalonike 2:3-10) Uasi-imani kwa hakika ulitukia. Durant aeleza hivi: “Ukristo haukuangamiza upagani; ulikubali kuupokea.”
Wenye kudai kuwa Wakristo walipokuwa wakizidi kupeperuka mbali zaidi na Ukristo wa kweli, walio wengi kati yao waliipoteza roho ya kimishonari. Hata hivyo, mmoja aliyekuwa na roho ya kimishonari alikuwa mtoto aliyezaliwa kwa wazazi Wakatoliki katika Uingereza karibu na mwisho wa karne ya nne. Jina lake lilikuwa Patrick, naye ajulikana kwa kuwa alipeleka ujumbe wa Kristo kwenye ukingo wa magharibi ya Ulaya—Ireland—ambako ngano husema kwamba aliongoa maelfu ya watu na kuanzisha mamia ya makanisa.
Upesi Ireland ikawa ikiongoza katika kazi ya mishonari. Kulingana na Kane, “mishonari wayo walijitosa kwa bidii kali katika pambano dhidi ya upagani.” Mmojapo wamishonari hawa alikuwa Columba, ambaye ni wazi alitimiza sehemu kubwa katika kuongoa Scotland. Katika karibu 563 W.K., yeye na waandamani wake 12 walianzisha makao ya watawa-waume katika Iona, kisiwa kilicho mbali kidogo na pwani ya magharibi ya Scotland, nacho kikawa kitovu cha utendaji wa kimishonari. Columba alikufa muda mfupi kabla ya 600 W.K., lakini kwa miaka 200 iliyofuata, wamishonari waliendelea kutumwa kutoka Iona hadi sehemu zote za Visiwa vya Uingereza na Ulaya.
Baada ya ule wenye kujiita Ukristo kuenea Uingereza, waongofu fulani Waingereza waliiga roho ya kimishonari ya watu wa Ireland na wao wenyewe wakawa wamishonari. Kwa kielelezo, katika 692 W.K., Willibrord kutoka Northumbria, ufalme mmoja wa kale wa Waingereza-Wasaksoni kaskazini mwa Uingereza, na waandamani 11 wakawa wamishonari wa kwanza Waingereza kwenda zile Nchi za Vibonde—Uholanzi, Ubelgiji, na Luxembourg.
Mapema katika karne ya nane, Boniface, mtawa-mume Mwingereza wa Benedict, aligeuza uangalifu wake kuelekea Ujerumani. Kane asema “kazi-maisha maarufu ya umishonari [ya Boniface] iliyoendelea muda wa miaka arobaini ilimpatia kile cheo cha Mtume kwa Ujerumani” na kusaidia kumfanya awe “mishonari mashuhuri zaidi wa zile Enzi za Giza.” Boniface alipokuwa na miaka zaidi ya 70, yeye na waandamani wapatao 50 waliuawa na Wafrisia wasio waamini.
The Encyclopedia of Religion yaeleza njia aliyotumia Boniface kwa mafanikio kuongoa watu wafuate Ukatoliki: “Kule Geismar [karibu na Göttingen, Ujerumani] yeye alithubutu kuangusha mti mtakatifu wa oki wa Thor . . . [Ilipokuwa kwamba hakupatwa] na kisasi chochote kutoka kwa yule mungu mkaaji wa hapo wa Kijerumani, ilikuwa wazi kwamba Mungu ambaye yeye alimhubiri ndiye aliyekuwa Mungu wa kweli apaswaye kuabudiwa na kustahiwa sana yeye peke yake.”
Wamishonari fulani walitumia njia nyinginezo, yaonekana wakifikiri kwamba si vibaya kutumia njia ya udhalimu wowote ule mradi tu matokeo yawe mazuri. Kane akiri kwamba uongofu wa Wasaksoni Wajerumani “ulitekelezwa na ushinde wa kijeshi wala si usadikishi wa kiadili au wa kidini.” Aongezea hivi: “Ule muungano usiofaa kati ya kanisa na serikali . . . ulichochea kanisa litumie njia za kimwili kutimiza shabaha za kiroho. Hakuna mahali sera hii ilipoleta matokeo mabaya sana kama vile ilivyoyaleta katika misheni za Kikristo, hasa miongoni mwa Wasaksoni. . . . Matendo ya kinyama yalifanywa.” Nasi twaambiwa kwamba wamishonari walipohama kuingia Scandinavia, “badiliko hilo lilikuwa sana-sana lenye amani; nguvu zilitumiwa Norway tu.”
Eti nguvu zikatumiwa? Eti matendo ya kinyama yakafanywa? Eti njia za kimwili zikatumiwa kutimiza shabaha za kiroho? Je, hili ndilo twapaswa kutarajia kwa wamishonari wanaotumikia wakiwa mawakili wa nuru?
Wamishonari Katika Nyumba Iliyogawanyika
Kampeni za kando za umishonari ziliendeshwa na yale matawi mawili ya ule wenye kudai kuwa Ukristo uliozoewa katika Roma na Constantinople. Majaribio yao ya “kutia Ukristo katika” Bulgaria yaliongoza kwenye vurugu iliyo kawaida ya nyumba iliyogawanyika kidini. Mtawala wa Bulgaria, Boris 1, aliongoka akafuata Uorthodoksi wa Kigiriki. Hata hivyo, alipoona kwamba Constantinople ilipunguza sana uhuru wa kanisa la Bulgaria, aligeukia Magharibi, akiruhusu wamishonari Wajerumani, wenye kuwakilisha Roma, walete namna yao ya Ukristo. Kufikia 870 W.K., ilikuwa wazi kwamba kanisa la Magharibi liliweka vizuizi vingi hata kuliko lile la Mashariki, kwa hiyo Wajerumani walifukuzwa, kisha Bulgaria ikarudi mikononi mwa Uorthodoksi wa Mashariki, ambapo ndipo imebaki kwa njia ya kidini tangu wakati huo.
Karibu na wakati huohuo, wamishonari wa Magharibi walikuwa wakianzisha “Ukristo” katika Hungaria. Kwa wakati huo, namna zote mbili za “Ukristo” zilikuwa zikiungwa mkono katika Poland. Kulingana na The Encyclopedia of Religion, “kanisa la Wapoland lilidhibitiwa kwa jumla na Magharibi, na wakati huohuo likaathiriwa sana na Mashariki.” Lithuania, Latvia, na Estonia ‘zilinaswa kati ya ushindani wa nguvu za Magharibi na Mashariki, pamoja na matokeo yote ya kikanisa yaliyotokana nao.’ Nayo Finland ilijikuta katika mkokotano huohuo wa Mashariki na Magharibi, baada ya kukubali kufuata “Ukristo” mwisho-mwisho wa karne ya 11 na ya 12.
Wakati wa karne ya tisa, ndugu wawili wa familia mashuhuri ya Kigiriki katika Thesalonike walileta “Ukristo” wa enzi ya Byzantium kwenye sehemu za Kislavu za Ulaya na Asia. Cyril, aitwaye Constantine pia, na Methodius walikuja kujulikana kuwa “mitume kwa Waslavu.”
Mojapo matimizo ya Cyril lilikuwa kukuza lugha ya kimaandishi kwa ajili ya Waslavu. Alfabeti yayo, iliyotegemea herufi za Kiebrania na za Kigiriki, yajulikana kuwa alfabeti ya Cyril na ingali hutumiwa katika lugha kama vile Kirusi, Kiukraine, Kibulgaria, na Kiserbia. Ndugu wawili hawa walitafsiri sehemu za Biblia katika lugha mpya iliyoandikwa na pia wakaanzisha liturjia katika Kislavu. Hii ilikuwa kinyume cha sera ya kanisa la Magharibi, lililotaka kufanya liturjia hiyo ibaki katika Kilatini, Kigiriki, na Kiebrania. Mtungaji Kane asema: “Utumizi wa lugha ya kienyeji katika ibada, ambalo ni zoea lililotiwa moyo na Constantinople lakini lililoshutumiwa na Roma, ulikuwa ukengeufu mpya na ulianzisha kawaida iliyovuvumuka kwa ukamili katika shughuli ya ki-siku-hizi ya umishonari wa karne za kumi na tisa na ishirini.”
Kufikia mwisho wa karne ya kumi, Ukristo wa jina ulikuwa umeingizwa pia katika maeneo ya ule ambao sasa ni Muungano wa Sovieti wa wakati uliopita. Mwana-mfalme Vladimiri wa Kiev, Ukraine, asemwa na mapokeo kuwa alibatizwa katika 988 W.K. Yasemwa kwamba alichagua ile namna ya Byzantium ya dini “ya Kikristo” badala ya Uyuda na Uislamu kwa sababu ya desturi yao ya kuvutia, wala si kwa sababu ya ujumbe wowote wa tumaini na kweli.
Kwa kweli, Keeping the Faiths—Religion and Ideology in the Soviet Union chasema kwamba “wakati uliopangiwa kuongoka kwa Vladimir wadokeza kwamba yeye alichagua kufuata dini mpya hiyo ili aendeleze masilahi yake ya kisiasa, hivyo akianza mapokeo ambayo yamefululiza bila kukatizwa karibu muda wote wa historia ya Kanisa Orthodoksi la Urusi.” Ndipo kitabu hicho chaongezea fikira hii ya kumakinisha: “Kwa jumla kanisa limekuwa na nia ya kuendeleza masilahi ya serikali, hata wakati ambapo serikali imeingilia masilahi ya kanisa.”
Vladimir aliamuru kwamba raia zake wabatizwe kuwa Wakristo; hawakuwa na hiari katika jambo hilo. Alipokwisha ‘kuchagua Uorthodoksi kuwa dini ya serikali,’ asema Paul Steeves, “alianza programu ya kung’oa mazoea ya kimapokeo ya kidini ya makabila ya uenyeji wa Kislavu.” Kwa kielelezo, katika viwanja ambavyo hapo kwanza watu walikuwa wametoa dhabihu kwa sanamu za kipagani, yeye alijenga makanisa. Steeves aongezea hivi: “Hata hivyo mabaki ya upagani yaliendelea kuwapo muda wa karne kadhaa na hatimaye yakafyonzwa kuingizwa katika maisha ya dini ya Urusi badala ya kukomeshwa hasa.”
Kujapokuwa na msingi huu wa kuyumbayumba, Kanisa Orthodoksi la Urusi liliunga mkono kazi ya mishonari kwa bidii. Thomas Hopko wa Seminari ya Mtakatifu Vladimir ya Theolojia ya Orthodoksi asema hivi: “Maandiko na huduma za kanisa zilitafsiriwa katika lugha nyingi za Siberia na lahaja za Alaska kadiri mikoa ya Mashariki ya milki ilivyokaliwa na kuenezewa evanjeli.”
Utendaji wa Kimishonari Ulioongezeka
Yale Mageuzo ya Kidini ya karne ya 16 yaliwasha mioto ya kiroho kotekote Ulaya. Msingi wa kazi ya kimishonari “ya Kikristo” iliyoongezeka uliwekwa huku viongozi wa Kiprotestanti wakifufua upendezi wa umma katika dini, kila mmoja kwa njia yake mwenyewe. Tafsiri ya Luther ya Biblia katika Kijerumani ilikuwa jambo kubwa, na pia ile tafsiri ya Biblia ya William Tyndale na Miles Coverdale katika Kiingereza.
Halafu, katika karne ya 17, harakati moja ilitokea Ujerumani ikijulikana kuwa Kicho. Ilikazia kujifunza Biblia na kufuata dini kwa hiari ya mtu binafsi. The Encyclopedia of Religion chaeleza hivi kwa mapana: “Utambuzi wayo kwamba jamii ya kibinadamu ilihitaji gospeli ya Kristo ulifanya kuwe na uanzishi na upanuzi wa shughuli za umishonari katika nchi za kigeni na nyumbani.”
Leo, yaweza kuonwa kwamba wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo walishindwa kihoi kukazia katika waongofu wa Ulaya imani na tumaini la Kikristo lenye nguvu za kutosha kuzuia mawazo ya Ukomunisti usioamini kuwako kwa Mungu na mawazo mengine ya utawala wa kimabavu katika karne yetu ya 20. Tangu Ukomunisti ulipokufa katika nchi fulani-fulani, wamishonari wamefufua utendaji wao, lakini Wakatoliki wa Roma, Wakatoliki wa Orthodoksi, na Waprotestanti hawaungamanishwi katika ile imani ya Kikristo ambayo wao hudai kuishiriki pamoja.
Wakazi wa Kroatia walio Wakatoliki wa Roma na Waserbia walio Waorthodoksi ni sehemu ya matunda ya umishonari wa Jumuiya ya Wakristo. Ni nini kingine isipokuwa mazao ya Jumuiya ya Wakristo kionyeshacho wazi zaidi kwamba ina sifa mbaya ya kuwa nyumba iliyogawanyika? Ni “ndugu” Wakristo wa aina gani ambao huinua bunduki kwanza dhidi ya mmoja na mwenzake kisha wanajiunga pamoja kuzielekeza kwa majirani wasio Wakristo? Ni Wakristo wa bandia tu ambao wangeweza kuwa na hatia ya mwenendo huo usio wa Kikristo.—Mathayo 5:43-45; 1 Yohana 3:10-12.
Je, wamishonari wote wa Jumuiya ya Wakristo wameshindwa kufikia kiwango kifaacho? Acheni tuendelee na uchunguzi wetu kwa kuona waliyotimiza katika Asia. Soma katika toleo letu lifuatalo ile makala yenye kichwa “Wamishonari wa Jumuiya ya Wakristo Warudi Kule Ambako Yote Yalianzia.”
[Picha katika ukurasa wa 21]
Boniface asemwa kuwa alionyesha kwamba miungu ya kipagani ni hoi
[Hisani]
Picha kutoka kitabu Die Geschichte der deutschen Kirche und kirchlichen Kunst im Wandelder Jahrhundertey