Sababu kwa Nini Makanisa Yalikaa Kimya
DESEMBA 8, 1993, Dakt. Franklin Littell wa Chuo Kikuu cha Baylor alizungumza kwenye Jumba la Kuhifadhi Vitu vya Kale la Ukumbusho wa Teketezo la Umati katika Marekani kuhusu “kweli halisi” yenye kusumbua. Hiyo ilikuwa nini?
Hiyo kweli, Littell alisema, ilikuwa kwamba “Wayahudi milioni sita walilengwa shabaha na kwa mfululizo kuuliwa kimakusudi katika vituo vya Jumuiya ya Wakristo, na Wakatoliki wa Kiroma, Waprotestanti, na Waothodoksi wa Mashariki waliobatizwa ambao hawakukemewa kamwe, bila kutaja kuondolewa katika ushirika.” Hata hivyo, sauti moja kwa udumifu ilisema kwa ujasiri kuhusu kujihusisha kwa makasisi na utawala wa Hitler. Na sauti hiyo, kama tulivyoona, ilikuwa ile ya Mashahidi wa Yehova.
Hitler alibatizwa akiwa Mkatoliki wa Kiroma, kama ilivyokuwa na wengi wa viongozi katika serikali yake. Kwa nini hawakuondolewa katika ushirika? Kwa nini Kanisa Katoliki halikushutumu yale maafa ambayo watu hawa walikuwa wakitenda? Kwa nini makanisa ya Protestanti pia yalikaa kimya?
Je, kwa kweli makanisa yalikaa kimya? Je, kuna uthibitisho kwamba waliunga mkono jitihada za vita ya Hitler?
Fungu la Kanisa Katoliki
Mwanahistoria Mkatoliki E. I. Watkin aliandika hivi: “Ingawa inasononesha kukubali, sisi hatuwezi kwa sababu ya ufundishaji-maadili wa kibandia ama ukosefu wa haki ya uaminifu-mshikamanifu kukana ama kupuuza ule uhakika wa kihistoria kwamba Maaskofu kwa udumifu wameunga mkono vita vyote ambavyo vimepigwa na serikali ya nchi yao. . . . Mahali ambapo uzalendo wa kijeshi unahusika makasisi wamesema kama wawakilishi wa Kaisari.”
Watkin aliposema kwamba maaskofu wa Kanisa Katoliki “waliunga mkono vita vyote ambavyo vimepigwa na serikali ya nchi yao,” yeye alitia ndani vita vya kikatili vilivyopigwa na Hitler. Kama vile profesa wa historia wa Katoliki ya Kiroma kwenye Chuo Kikuu cha Vienna, Friedrich Heer, alivyokiri: “Ni kweli zilizo wazi kabisa katika historia ya Ujerumani, Msalaba na swastika zilikuja kuwa karibu sana, mpaka utawala wa swastika ukapiga mbiu ya ushindi kutoka kwenye vinara vya makathedro ya Ujerumani, bendera za swastika zilitokea kwenye altare, na wanatheolojia Wakatoliki na Waprotestanti, mapasta, wanakanisa na wanasiasa walikaribisha muungamano huo na Hitler.”
Viongozi wa Kanisa Katoliki waliunga mkono vita vya Hitler kabisa hivi kwamba profesa wa Katoliki ya Kiroma Gordon Zahn aliandika hivi: “Mkatoliki Mjerumani yeyote aliyetafuta mwongozo na mwelekezo wa kiroho kutoka kwa viongozi wake wa kidini kuhusu utumishi wa kijeshi katika vita vya Hitler alipata majibu yaleyale ambayo angepata kutoka kwa mtawala huyo wa Nazi mwenyewe.”
Ule uhakika wa kwamba kwa kutii Wakatoliki walifuata mwelekezo wa viongozi wao wa kanisa uliandikwa na Profesa Heer. Yeye aliandika hivi: “Kati ya yapata milioni thelathini na mbili ya Wakatoliki Wajerumani—milioni kumi na tano unusu ambao walikuwa wanaume—ni saba [mtu mmoja-mmoja] ambao kwa wazi walikataa utumishi wa kijeshi. Sita kati ya hawa walikuwa Waaustria.” Uthibitisho wa hivi majuzi zaidi waonyesha kwamba Wakatoliki wengine wachache, pamoja na Waprotestanti kadhaa, walipinga kwa ujasiri Serikali ya Nazi kwa sababu ya itikadi za kidini. Wengine hata walipoteza maisha zao, huku wakati uleule viongozi wao wa kiroho wakiwasaliti washiriki wao ili kupata upendeleo wa Utawala wa Nazi.
Ni Nani Mwingine Alikuwa Kimya, Nani Hakuwa
Kama ilivyoonyeshwa hapo juu, Profesa Heer alitia ndani viongozi Waprotestanti miongoni mwa wale ambao “walikaribisha muungano huo na Hitler.” Hilo ni kweli?
Waprotestanti wengi wamejikunyata katika kujilaumu kwa ajili ya uhalifu wa kibinafsi kwa sababu ya kujinyamazia wakati wa vita vya Hitler vya kikatili. Kwa kielelezo, makasisi 11 wenye kuongoza walikutana katika Oktoba 1945 ili kurasimu ule eti ulioitwa kukiri kwa hatia ya Stuttgart. Wao walisema hivi: “Sisi twajishtaki wenyewe kwa kutokuwa wenye ujasiri zaidi katika kuungama itikadi zetu, kutokuwa waaminifu zaidi katika kusali, kutokuwa wenye shangwe zaidi katika kueleza imani yetu, na wenye msimamo thabiti zaidi katika kuonyesha upendo wetu.”
History of Christianity cha Paul Johnson kilisema hivi: “Kati ya mapasta wa Kievanjeli 17,000, hakukupata kamwe kuwa zaidi ya hamsini waliotumika vifungo vya muda mrefu [kwa kutounga mkono utawala wa Nazi] kwa wakati wowote ule.” Akionyesha tofauti kati ya mapasta hao na Mashahidi wa Yehova, Johnson aliandika hivi: “Waliokuwa wajasiri kupita wote walikuwa Mashahidi wa Yehova, ambao walipiga mbiu ya kimafundisho yenye kupinga moja kwa moja tangu mwanzoni nao wakateseka vilivyo. Wao walikataa ushirikiano wowote na serikali ya Nazi.”
Huko nyuma katika 1939, wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilianza, Consolation lilimnukuu T. Bruppacher, mhudumu mmoja Mprotestanti, akisema hivi: “Huku watu ambao hujiita Wakristo wakiwa wameshindwa kupita mtihani wa kuamua, hawa mashahidi wa Yehova wasiojulikana, wakiwa wafia-imani Wakristo, wanadumisha upinzani mkali dhidi ya kulazimishwa kwa dhamiri na ibada ya ulimwengu. Mwanahistoria wa wakati ujao lazima siku moja akubali kwamba si makanisa makubwa, bali watu hawa wanaochongewa na kudhihakiwa, ndio wanasimama imara dhidi ya hasira kali ya utawala wa Nazi . . . Wanakataa ibada ya Hitler na Swastika.”
Vivyo hivyo, Martin Niemoeller, kiongozi wa kanisa la Protestanti ambaye mwenyewe alikuwa katika kambi ya mateso ya Nazi, baadaye alikiri hivi: ‘Inaweza kukumbukwa kwa kweli kwamba makanisa ya Wakristo, katika mihula yote, sikuzote yamekubali kubariki vita, vikosi, na silaha na kwamba yamesali kwa njia isiyo ya Kikristo kwa ajili ya kuangamizwa kwa adui zao.’ Yeye alikubali hivi: “Yote haya ni kosa letu na kosa la baba zetu, lakini kwa wazi si kosa la Mungu.”
Niemoeller kisha akaongezea hivi: “Na kufikiri kwamba sisi Wakristo wa leo tunaonea haya kile kiitwacho eti kidhehebu cha wasomi wa Biblia wenye kuchukua mambo kwa uzito [Mashahidi wa Yehova], ambao kwa mamia na maelfu wameenda kwenye kambi za mateso na kufa kwa sababu walikataa kutumika katika vita na kupiga risasi binadamu.”
Susannah Heschel, profesa wa masomo ya Kiyahudi, alipata barua za kanisa zilizothibitisha kwamba makasisi wa Kilutheri walikuwa na hiari, naam wenye hamu, kumuunga mkono Hitler. Mwanamke huyo alisema waliomba pendeleo la kuweka bendera ya swastika katika makanisa yao. Wengi zaidi wa makasisi hawakuwa washiriki walioshurutishwa, utafiti wake ulionyesha kwamba walikuwa waunga-mkono wenye idili wa Hitler na maoni yake ya Kiarya.
Anapotoa mihadhara, mara nyingi Heschel huulizwa na washiriki wa kanisa, “Sisi tungelifanya nini?”
“Mngelikuwa kama Mashahidi wa Yehova,” yeye hujibu.
Sababu kwa Nini Walikuwa Kimya
Sababu iliyofanya makanisa kuwa kimya yawa dhahiri. Ni kwa sababu makasisi wa Jumuiya ya Wakristo na makundi yao walikuwa wameacha mafundisho ya Biblia wakipendelea kuunga mkono serikali ya kisiasa. Katika 1933 Kanisa Katoliki ya Kiroma lilifanya mkataba na Wanazi. Kadinali wa Katoliki ya Kiroma Faulhaber alimwandikia Hitler hivi: “Mapatano haya yaliyofanywa na Makao ya Papa . . . ni tendo la baraka zisizolinganika . . . Mungu na amhifadhi [Hitler] Kiongozi wa Serikali.”
Kwa kweli, Kanisa Katoliki na makanisa mengine vilevile yalikuja kuwa vijakazi vya serikali yenye uovu ya Hitler. Hata ingawa Yesu Kristo alisema wafuasi wake wa kweli ‘si sehemu ya ulimwengu,’ makanisa na wanaparokia walikuja kuwa sehemu kuu ya ulimwengu wa Hitler. (Yohana 17:16) Kama tokeo, walishindwa kusema kwa ujasiri kuhusu maafa dhidi ya ubinadamu yaliyofanywa na Wanazi katika kambi zao za kufishia.
Ni kweli, watu wachache mmoja-mmoja wenye ujasiri kutoka Katoliki, Protestanti, na dini nyingine mbalimbali walipinga Serikali ya Nazi. Lakini hata wengine walipolipia kwa uhai wao, viongozi wao wa kiroho, waliodai kumtumikia Mungu, walikuwa wakitumikia kama vibaraka vya Utawala wa Nazi.
Hata hivyo, kulikuwa na sauti moja ambayo kwa udumifu ilisema kwa ujasiri. Ingawa vyombo vya habari, kwa ujumla, vilipuuza makanisa kuwa na sehemu kubwa katika tamasha ya Nazi, Mashahidi wa Yehova walihisi kusukumwa kufunua ujanja na unafiki wa makasisi, wakiwa na habari za kindani kuhusu ushirikiano wao wa kichini-chini. Katika kurasa za mtangulizi wa gazeti hili pamoja na vichapo vingine kotekote katika miaka ya 1930 na 1940, walichapisha mashtaka makali kuhusu matengenezo ya kidini ambayo yalikuja kuwa vijakazi vya Unazi.
Kuwatambulisha Wafuasi wa Kweli wa Kristo
Mashahidi wa Yehova wako tofauti kabisa na dini za ulimwengu. Wakiwa si sehemu ya ulimwengu, wao hawashiriki katika vita vya mataifa. Kwa kutii maagizo ya Mungu, ‘wamefua panga zao kuwa majembe.’ (Isaya 2:4) Ndiyo, kwa kutii maagizo ya Kristo, wao wanapendana. (Yohana 13:35) Hili lamaanisha hawaendi kamwe vitani na kuumizana kwa kukusudia.
Inapowatambulisha waabudu wa kweli wa Mungu, Biblia iko wazi sana katika kusema: ‘Katika hili watoto wa Mungu ni dhahiri, na watoto wa Ibilisi nao. Mtu ye yote asiyetenda haki hatokani na Mungu, wala yeye asiyempenda ndugu yake. Maana, hii ndiyo habari mliyoisikia tangu mwanzo, kwamba tupendane sisi kwa sisi; si kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake.’—1 Yohana 3:10-12.
Ndiyo, historia imeonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova sikuzote wameonyesha upendo kwa wenzao, hata wanapokabili mkazo mkali. Hitler alipofanya vita kotekote katika Ulaya, Mashahidi walisimama imara walipokabili majaribio ya kinyama ya Wanazi ya kuwafanya wajiunge katika mauaji ya kupindukia. Profesa Christine King aliweka hiyo habari kwa muhtasari hivi: “Mashahidi wa Yehova walisema kwa ujasiri. Wao walisema tangu mwanzoni. Walisema kwa sauti moja. Nao walisema kwa ujasiri mkubwa, ule uhakika wa kwamba walisema kwa ujasiri hivyo una somo kwa sisi sote.”
Hadi ulimwengu huu utakapokuwa salama chini ya utawala wenye upendo wa serikali ya Yehova na isiyo na vita na uovu, Mashahidi wa Yehova wataendelea kusema kwa ujasiri. Mradi ni mapenzi ya Mwenye Enzi Kuu wa Ulimwengu Wote Mzima Bwana Yehova, gazeti hili litafunua maovu ya ulimwengu huu wa kishetani na kutangaza tumaini pekee kwa mwanadamu, Ufalme wa Mungu.—Mathayo 6:9, 10.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Matbaa ya Marekani ilihakikisha makanisa yaliunga mkono Unazi
New York Post, Agosti 27, 1940, Blue Final Edition, ukurasa 15
The New York Times, Desemba 7, 1941, Late City Edition, ukurasa 33
The New York Times, Septemba 25, 1939, Late City Edition, ukurasa 6
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kinyume na makanisa, Mashahidi wa Yehova walisema kwa ujasiri dhidi ya Unazi