Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Askari-Vita Aliyegeuka Kuwa Mkristo Macho yangu yalijawa na machozi niliposoma ile makala “Nilizoezwa Kuua, Sasa Natolea Watu Uhai.” (Septemba 8, 1994) Mpalestina kuita Myahudi “ndugu”—ni katika tengenezo la Yehova tu ambapo umoja wa jinsi hiyo waweza kupatikana!
K. T. O., Malasia
Chapa Yako Asanteni kwa ile makala yenye kupendeza “Chapa Yako—Sahihi Yako.” (Mei 22, 1994) Mume wangu nami twajifunza Biblia pamoja na mtawa Mbuddha kutoka Taiwan. Yeye alieleza jinsi makala hiyo ilivyokuwa sahihi! Kisha akamwandikia mama yake Taiwan na kumwomba atupelekee chapa yenye jina letu likiwa limechongwa juu yayo. Tulifurahishwa mno!
K. J., Marekani
Ukimwa Nimetoka tu kusoma ule mfululizo “Je, Maisha Yako Ni Makimwa? Waweza Kuyabadili!” (Januari 22, 1995), na ni lazima niwaambie jinsi ilivyonisaidia. Sikupata kujiwazia kuwa mkimwa, lakini sikutosheka na maisha yangu kwa sababu ya kawaida yangu yenye kuchosha. Hiyo makala ilinifanya nione mambo kwa njia tofauti.
S. V., Marekani
Visiwa vya Canary Baada ya kusoma makala ya Novemba 22, 1994, “Visiwa vya Canary—Tabia-Anga Tulivu, Mandhari Yenye Ushawishi,” nataka kuonyesha uthamini wangu kwayo na kwa makala kama hizo katika Amkeni! Hizo huongeza utambuzi na uthamini wetu kwa dunia yetu yenye kuvutia na uumbaji mbalimbali wa Yehova. Asanteni kwa kutupeleka kwenye “safari” hizi zenye kusisimua.
D. G., Marekani
Wamishonari Nalithamini sana mfululizo wenu bora zaidi “Wamishonari—Mawakili wa Nuru au wa Giza?,” hasa sehemu ya sita, “Kufanya Wanafunzi wa Kweli Leo.” (Desemba 22, 1994) Kutaniko letu limenufaika sana kwa kufanya kazi na mume na mke wamishonari waliozoezwa katika shule ya Gileadi. Shauri lao lenye hekima na bidii yao vimenichochea kufanya huduma ya wakati wote kuwa kazi-maisha yangu.
J. K., Botswana
Kupinga Unazi Nilichochewa na ile makala “Hatukuunga Mkono Vita ya Hitler.” (Oktoba 22, 1994) Ilikuwa na picha ya “Julisho Zito” la maaskofu sita Waaustria la kuunga mkono Unazi. Mmoja wa hao maaskofu alikuwa yule yule ambaye alinitolea kipaimara katika 1928 nilipokuwa mwanafunzi Myesuiti. Nacheka “kipaimara” hicho kilichotoka kwa mtu ambaye mwenyewe hakujua namna ya kuwa imara katika imani ya Kikristo! Vita hiyo ilimaliza uhusiano wangu na Kanisa Katoliki. Pia niliondoka katika nchi nilikozaliwa. Ingawa nilijaribu kukinza hiyo vita kwa njia yangu mwenyewe, sikuwa na nguvu ya ujasiri wa washiriki wa familia ya Wohlfahrt. Bado nakumbuka Mashahidi wa Yehova wawili waliokataa kubeba bunduki. Waliuawa mara hiyo. Mimi natamani kuwa kama hao.
P. K., Chile
Vijana Huuliza Asanteni kwa makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuboreshaje Jumla ya Mavazi Yangu?” (Januari 22, 1995) Ilinifanya nisimame na kupanga kijumba changu cha kuwekea nguo chenye kufurika. Kila siku nilitaabika kupata kitu cha kuvaa, licha ya kuwa na kiasi kikubwa cha nguo. Lakini asanteni kwa madokezo yenu yenye msaada, kufanya hivyo ni rahisi zaidi sasa.
T. B., Hawaii
Asanteni kwa mawazo bora zaidi yaliyokuwa katika makala “Mitindo—Ina Uvutio Gani?” na “Mitindo—Je, Nifuate Halaiki?” (Novemba 22 na Desemba 8, 1994) Nikiwa mzee Mkristo, naungama kwamba si rahisi sikuzote kuepuka kulazimisha viwango vyangu kwa wengine. Lakini maneno yenu kama “kufikiria hisia na mitazamo ya wengine” na “kuepuka mitindo ya mavazi na mwenendo ambao wengine huona kuwa wa kupita kiasi” huchochea watu.
D. Č., Kroatia