Maoni ya Biblia
Je, Viwango vya Mungu Ni Vigumu Mno Kufikia?
“MUNGU HAKADIRII WANADAMU KULINGANA NA KIPIMO CHA INCHI.” —METHALI YA KALE YA KISKOTI.
MITIHANI ya shule, mahoji ya kuajiriwa kazi, na majaribio ya kitiba ni baadhi tu ya mabadiliko yenye umaana ambayo mtu hukadiriwa kwayo. Lakini inapohusu kuishi kila siku kulingana na viwango vya Mungu, watu wengi huhisi kwamba huenda wakashindwa kwa namna moja au nyingine kuvifikia. Je, wewe unaamini hivyo pia? Je, waweza kufikia viwango vya Mungu?
Ili kujibu, ebu kwanza tutazame viwango ambavyo Mungu amewekea waabudu wake. Biblia huweka wazi namna tupaswayo kutembea katika maisha. (Zaburi 119:105) Mwandikaji wa Biblia Mfalme Sulemani mwenye hekima alifikia mkataa kwamba “wajibu wote” wa mwanadamu ni “kumhofu Mungu wa kweli na kuzishika amri zake.” (Mhubiri 12:13, NW) Nabii Mika alionelea hivi: “BWANA anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako?”—Mika 6:8.
Yesu Kristo, mwana wa Mungu mwenyewe, alitangaza kwamba hakuna amri zilizo kubwa kuliko ‘kumpenda BWANA Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote’ na ‘kumpenda jirani yako kama nafsi yako.’ (Marko 12:30, 31) Kwa kuongezea, sisi huonyesha kwamba tunampenda Mungu kwa kutii amri zake zote.—1 Yohana 5:3.
Ikiwekwa kwa usahili, binadamu wanapaswa kumpenda Mungu, kutii amri zake, kutenda kwa haki, kuwa wenye fadhili kuelekea wote, na kuepuka kiburi. Je, si twaweza kufikia viwango hivyo?
Mungu Huachilia Mapungukio
Mungu kwa haki hutarajia binadamu wafikie viwango vyake. Lakini, kwa weupe wote wa moyo, je, kuna binadamu yeyote anayefuata kikamilifu viwango hivi wakati wote? Bila shaka la, kwa kuwa tumerithi kutokamilika kutoka kwa babu yetu wa kale Adamu. (Warumi 5:12) Hivyo, sisi huelekea kukosea. Hata hivyo hili halitufanyi tukose kustahili kumtumikia Mungu kwa kukubalika.
Ili kutoa kielezi, fikiria matatizo ya kujifunza kuendesha gari. Huchukua uangalifu wa daima na wakati ili kuendesha vizuri vya kutosha kupita mtihani wa uendeshaji gari. Bila shaka, bado twahitaji kufanyia kazi kuendesha vizuri hata baada ya kupata leseni. Kadiri tupatavyo uzoefu, tunanoa stadi zetu. Lakini hakuna madereva wakamilifu!
Kwa kufurahisha, Mungu huachilia mapungukio yetu. Yeye si mwenye kutokubali sababu, akidai tusichoweza kutoa, wala hafulizi kutafuta kosa. Yeye hufahamu mapungukio na udhaifu wetu. Mfalme Daudi, aliyetenda dhambi nzito aliungama hivi: “Hakututenda sawasawa na hatia zetu; wala hakutulipa kwa kadiri ya maovu yetu.” Kwa sababu gani? “Maana mbingu zilivyoinuka juu ya nchi, kadiri ile ile rehema zake [Mungu] ni kuu kwa wamchao.” Hata ingawa Yehova ajua tunatenda dhambi, yeye yuko tayari kuweka makosa yetu “kama vile mashariki ilivyo mbali na magharibi.”—Zaburi 103:10-14.
Usikate Tamaa
“Ninaposhuka moyo,” aeleza mwabudu mnyofu wa Mungu, “nyakati fulani mimi hufikia mkataa kwamba sitafanikiwa katika kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Lakini nisitawishapo mtazamo chanya zaidi, nahisi kwamba naweza kufaulu kuishi katika njia ambayo Mungu anataka niishi. Lakini si rahisi hivyo!” Usivunjike moyo ukihisi hivyo. Wewe si wa kwanza, wala hutakuwa wa mwisho, kuwa na maoni kama hayo.
Mtume Mkristo Paulo alikiri waziwazi hivi: ‘Nitakapo kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi. Ole wangu maskini mimi!’ Hata hivyo, yeye hakuamua kwamba kile alichotarajia Mungu kilikuwa kigumu mno, kwa kuwa yeye aliongeza hivi: “Ni nani atakayeniokoa na mwili huu wangu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.” (Warumi 7:21-25) Hivyo yeye alihisi akiweza kumpendeza Mungu ingawa bado alikuwa mtenda-dhambi.
Yehova, Muumba wetu mwenye upendo, husamehe makosa na mapungukio yetu kupitia faida ya fidia ya ukombozi ya Mwana wake mpendwa, Yesu. “Kama mtu akitenda dhambi,” akaandika mtume Yohana, “tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki. Naye ndiye kipatanisho [kifuniko] kwa dhambi zetu.” (1 Yohana 2:1, 2) Kizuizi ambacho dhambi huweka na kinachotuzuia kufikia viwango vya Mungu ili kupata urafiki kinaondolewa au kuvunjwa na nguvu ya dhabihu ya Kristo. Kwa hiyo uhusiano na Mungu unarudishwa.
Kukubali kwa unyenyekevu mpango huu wenye upendo huleta msamaha, kwa kuwa Mungu hukaa “pamoja na yeye aliye na roho iliyotubu na kunyenyekea.” (Isaya 57:15) Twaweza kumtegemea ili ahuishe roho zetu. Yeye aahidi ‘kumwinua mnyonge kutoka mavumbini.’ Hatuhitaji kuendelea tena kubaki tukiwa tumeshuka moyo wakati tukosapo kumtii Mungu kikamilifu. Badala yake, twaweza kuwa na hakika kwamba Mungu hapuuzi kamwe jitihada tunazofanya ili kuishi kulingana na viwango vyake.—Zaburi 113:7; Waebrania 6:10-12.
Ingawa ni jambo la kujikakamua, utaona kwamba una furaha zaidi katika kufanya yale yampendezayo Mungu. Ujitoaji kwa Mungu hufanya maisha yaweze kuvumilika kwako na kwa wale walio karibu nawe. Fikiria pia juu ya wakati ujao. Kujikaza kuishi kwa kupatana na viwango vya Mungu sasa huleta taraja la uhai udumuo milele chini ya hali za kiparadiso.—Isaya 48:17; Warumi 6:23; 1 Timotheo 4:8.
Wapanda milima wenye uzoefu hutambua kwamba mara wafikapo kwenye kilele, bado wako nusu ya safari tu. Ni lazima bado washuke salama. Vivyo hivyo, wale wamhofuo Mungu wanahitaji kufikia viwango vya Mungu kisha kuendelea kuishi kupatana navyo.—Luka 21:19; Yakobo 1:4.
Pata faraja kutokana na ujuzi wa kwamba viwango vya Mungu si vigumu mno kufikia. Ukosapo kuvifikia kikamilifu mara kwa mara, tafuta msamaha. Tegemea utegemezo wake wenye upendo. (Zaburi 86:5) Kwa hiyo, ukiwa na Yehova na Mwana wake wakiwa Wasaidiaji wako, waweza kufikia viwango vya Mungu na kupata ukubali wake.—Mithali 12:2.