Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w78 4/15 kur. 8-12
  • Huzitii Habari Njema ni Njia ya Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Huzitii Habari Njema ni Njia ya Maisha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JE! MWANADAMU HAWEZI KUWA MKRISTO?
  • BIBLIA INA UBORA GANI KATIKA KUONGOZA MAISHA?
  • JE! MAISHA YA MKRISTO NI YA KUJINYIMA MAMBO KUPITA KIASI?
  • JINSI KUSEMA KWELI KUNAVYOHUSIKA KATIKA MAISHA YA MKRISTO
  • Msingi wa Maisha Yenye Kusudi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Je, Viwango vya Mungu Ni Vigumu Mno Kufikia?
    Amkeni!—1995
  • Dhambi
    Ufahamu wa Kina wa Maandiko
  • “Uvumilivu na uwe na Kazi yake Kamilifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
w78 4/15 kur. 8-12

Huzitii Habari Njema ni Njia ya Maisha

‘‘[Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!” ​—⁠Mik. 6:8.

1. Mara nyingi leo watu wanakuwa na maoni gani juu ya dini yao?

LEO ni jambo la kawaida kuona watu wanaosema wanaamini mafundisho ya dini, lakini hawayafuati mafundisho hayo katika maisha yao ya kila siku. Mara nyingi wanajichukua kuwa “watu wa dini” fulani, lakini hawaioni dini hiyo kama inapasa kuongoza matendo yao nyumbani, kazini, na katika shughuli zao na wengine.

2. Katika karne ya kwanza, kwa sababu gani Ukristo uliitwa “ile Njia”?

2 Walakini, Ukristo wa kweli si jambo la kuonyesha kijuujuu tu. Kwa kweli, siku za mwanzoni Ukristo uliitwa “ile Njia,” kwa sababu haukuwa desturi ya ibada tu. (Matendo 19:9, 23) Ni NJIA YA MAISHA iliyojawa na kumwabudu Mungu, kwa kuongozwa na roho yake. (Yohana 4:23, 24; 1 Kor. 2:11-13) Mahali pote katika Maandiko ya Kikristo tunaona maneno yanayotukataza kumtumikia Mungu kwa moyo nusunusu. Mtu anayetaka kuwa Mkristo halisi anaambiwa hivi: ‘Ugeuzwe kwa kufanywa upya nia yako,’ ‘upate kufanywa mpya katika nguvu yenye kuendesha akili zako’ na “kuuvaa utu mpya.” (Rum. 12:2; Efe. 4:22-24, NW) Zaidi ya kutoa ushuhuda kwa juhudi, mkazo unatiwa nyakati zote tuwe na mwenendo mwema.​—⁠1 Pet. 1:15; 2:12; 3:16; 5:12.

3. Ni kwa kadiri gani Ukristo wa kweli unaongoza maisha ya mtu?

3 Kwa hiyo, Ukristo wa kweli unahusu kila upande wa maisha, ya mtu mwenyewe na ya jamaa. Lazima Mkristo ampende Mungu na kumtumikia ‘kwa moyo wake wote na kwa nafsi yake yote na kwa akili zake zote na kwa nguvu zake zote.’ (Marko 12:30, NW) Hiyo haiachi nje sehemu yo yote ya mwili wake, maisha yake wala utu wake.​—⁠Mt. 22:37-39.

JE! MWANADAMU HAWEZI KUWA MKRISTO?

4, 5. (a) Je! Mungu anamtaka Mkristo afanye mambo magumu sana au ya kupita kiasi? (b) Je! ugumu kuwa Mkristo unazipita faida zinazopatikana Katika ulimwengu huu kwa sababu ya kufuata Ukristo?

4 Basi, je! ni vigumu zaidi sana kuwa Mkristo? Je! Mungu anataka wanadamu wafanye jambo la kupita kiasi, jambo kubwa sana wasiloliweza? Hapana. Yeye aliwaambia Waisraeli watu wake wa kale hivi: “Ee mwanadamu, yeye amekuonyesha yaliyo mema; na [Yehova] anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”​—⁠Mik. 6:8.

5 Sasa kuna ugumu gani kuhusu takwa hilo? Mungu anapendezwa watu wakiishi kama walivyoumbwa waishi​—⁠kama inavyowapasa kuishi​—⁠na bas! Ni kweli kwamba kufuata mwendo huo katika ulimwengu ambao umeziacha kanuni za Mungu kutafanya mtu apingwe na kupatwa na magumu. (Yohana 16:33; 2 Tim. 3:12) Lakini ni hakika kwamba mtu anayeishi kupatana na kanuni za Mungu yu huru zaidi katika dhamiri, ana amani nyingi zaidi ya akili, tena ana kusudi la kuishi na tumaini la wakati ujao.-​—⁠1 Tim. 4:8; 6:6-8.

6. Mungu amefanya mpango gani tupate kufaulu katika Ukristo, ingawa sisi si wakamilifu?

6 Kwa sababu ya kutokamilika, huenda tukadhani ni vigumu mtu kufuata kanuni za Biblia na kuzaa matunda yake mema. Ni kweli kwamba watu wasio wakamilifu wanafanya makosa mengi, na mengine yanakuwa makubwa, lakini sababu hiyo hiyo ndiyo iliyofanya dhabihu ya Kristo ya upatanisho itolewe. Inawezesha Mkristo mwenye kutubu amfikie Mungu apate msamaha, nayo roho ya Mungu inamsaidia abadili utu wake​—⁠abadili njia zake zizidi kupatana na njia za Mungu. (Ebr. 4:15, 16; 2 Kor. 3:17, 18) Mtume Yohana aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Watoto wangu wadogo, nawaandikia haya ili kwamba msitende dhambi. Na kama mtu akitenda dhambi tunaye Mwombezi kwa Baba, Yesu Kristo mwenye haki, naye ndiye kipatanisho kwa dhambi zetu; wala si kwa dhambi zetu [Wakristo waliotiwa mafuta] tu, bali na kwa dhambi za ulimwengu wote [dhambi za wanadamu wengine wote].”​—⁠1 Yohana 2:1, 2.

BIBLIA INA UBORA GANI KATIKA KUONGOZA MAISHA?

7. Sisi Wakristo wa kweli tunaionaje na kuitumiaje Biblia?

7 “Wakristo wakifahamu kwamba wanahitaji uongozi wa Mungu ili kufuata kanuni zake zenye haki, watakuwa na kawaida ya kujifunza Biblia maishani mwao. Watashikamana sana na maneno yaliyosemwa na mtume Paulo kwamba “kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya watu juu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa mafundisho katika haki; ili mutu wa Mungu awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.” ​—⁠2 Tim. 3:16, 17, ZSB.

8. Tukikubali kwamba Biblia iliongozwa na Mungu, je! maana yake ni kwamba tuyachukue maneno yake yote kwa njia halisi? Toa mifano.

8 Kwa hiyo, Biblia nzima, yaani, Maandiko ya Kiebrania, au “Agano la Kale,” na Maandiko ya Kigiriki, au “Agano Jipya,” ndiyo Neno la Mungu kamili, lililo kweli kila sehemu na lenye kuongozwa na Mungu ili limwelekeze Mkristo katika njia zake zote. Lakini, hiyo si kusema kwamba maneno yote yachukuliwe kwa njia halisi kabisa, kama wengine wanavyodhani. Ni kweli kwamba kuna amri fulani zenye maana halisi. Lakini kuna historia na maneno mengi pia ya mfano na yenye kufananisha vitu fulani. Kwa mfano, serikali za ulimwengu zinafananishwa nyakati nyingine na wanyama. (Dan. 8:1-8, 20-22; Ufu. 17:3, 9-12) Nayo “siku” inaweza kuwa siku ya saa 24 au inaweza kuendelea kipindi cha miaka mingi. (Mwa. 2:4; Yohana 8:56) Habari zinazouzunguka mstari, na maneno mengine ya Biblia yanayohusiana nao, zinamsaidia mwanafunzi atofautishe kati ya maandiko yenye maana halisi na yaliyo ya mfano na ya unabii.

9. Kwa sababu gani Biblia nzima ni yenye ubora mwingi kwa Mkristo?

9 Kwa kuiona Biblia kwa njia hiyo, Wakristo wanajifunza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yenye amri na sheria nyingi za wazi, na vilevile Maandiko ya Kiebrania, yenye kuonyesha kanuni nyingi, mifano, unabii mbalimbali na kumbukumbu la matukio ya kweli yanayofunua nia na maoni ya Mungu juu ya mambo ya maisha. (1 Kor. 10:11) Katika Biblia yote mna visa vingi na matukio yanayoonyesha njia ya Mungu ya kushughulika na hali mbalimbali. Mambo yote hayo yanafahamisha mtu jinsi utu wa Mungu ulivyo na kumsaidia Mkristo awe na “nia ya Kristo,” ambaye ndiye anayemjua Mungu kuliko mtu mwingine ye yote.​—⁠1 Kor. 2:16; Mt. 11:27.

JE! MAISHA YA MKRISTO NI YA KUJINYIMA MAMBO KUPITA KIASI?

10. Maisha ya Yesu duniani yalionyeshaje kwamba hakujinyima mambo kupita kiasi wala hakufuata desturi tu?

10 Basi, maisha ya Mkristo si ya kufuata orodha yenye sheria nyingi wala si ya kufuata desturi tu. Maisha ya Mkristo yanaionyesha roho na upendo ambao lazima Mkristo ajitahidi kusitawisha. (Mt. 5:44; 1 Yohana 5:3) Yesu ni mwanadamu aliyempendeza Mungu katika kila jambo. (Yohana 8:29) Yeye hakutenda jambo lo lote lisilo haki. Lakini ingawa alikuwa mkamilifu hakujinyima mambo kupita kiasi. Alihudhuria arusi na karamu, akavifurahia vitu vilivyo vizuri maishani. (Yohana 2:1-10; Luka 5:29; Mt. 11:18, 19) Alikuwa na kiasi katika mambo yote wala hakutaka yeye mwenyewe wala wengine wafanye mambo ya kupita kiasi. (Marko 6:31; Yohana 4:6) Yesu alifurahia maisha na kazi aliyofanya kusaidia wengine wajue habari za Mungu. (Yohana 4:34) Yeye hakujilinganisha na wengine nyakati zote akionyesha jinsi alivyokuwa mwenye haki na jinsi walivyokuwa wenye makosa. Alihurumia watu na kuwarehemu. (Mt. 9:36; Marko 1:41) Lakini, alilaumu makosa na kuonyesha wazi unafiki wa watu.​—⁠Mt. 15:1-9; 23:23-32.

11. (a) Je! Mashahidi wa Yehova watumie hali yao ya kutokamilika kama kisababu cha kutenda dhambi, au wajitukuze kuhusu haki waliyo nayo? (b) Ni tamaa gani zenye kupingana zinazompata kila Mkristo, kama Mume Paulo anavyoeleza?

11 Katika mambo hayo Yesu aliwekea Wakristo kielelezo. Bila shaka, wanajua kwamba wao si kama Yesu, kwamba hawana ukamilifu, lakini wanajitahidi sana kufuata kielelezo chake. Wanajaribu kuepuka makosa lakini wanajua kwamba wameipata haki waliyo nayo kwa sababu ya rehema ya Mungu na kufuata Biblia. Hawawezi kujipatia sifa ya kuwa na haki hiyo. Kama mtunga zaburi, wao wanatambua kwamba: “Kama Wewe ungehesabu maovu, Ee Bwana, nani angesimama?” (Zab. 130:3) Wanajua kwamba wao ni watenda dhambi na nyakati nyingine wanafanya mambo mabaya, kama vile mtume Paulo mwenyewe alivyosema:

“Basi nimeona sheria hii, ya kuwa kwangu mini nitakaye kutenda lililo jema, lipo lililo baya. Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu. Ole wangu, maskini mimi! ni nani atakayeniokoa na mwili huu wa mauti? Namshukuru Mungu, kwa Yesu Kristo Bwana wetu. Basi, kama ni hivyo, mimi mwenyewe kwa akili zangu naitumikia sheria ya Mungu, bali kwa mwili wangu sheria ya dhambi.”​—⁠Rum. 7:21-25.

12, 13. (a) Wakristo wanaepukaje kuwa wenye “haki kiasi” au wenye “hekima mno”? (b) Wakati shahidi Mkristo anapoghafilika katika dhambi, yeye anafanya nini? (c) Kwa sababu gani Mashahidi wanapelekea wengine “habari njema”?

12 Basi, mtu anayeifuata “ile Njia” kweli kweli anajaribu kuepuka kuwa na “haki kupita kiasi” au kuwa na “hekima mno,” yaani, hajioni mwenye hekima wala mwenye haki akitafuta aone makosa au maamuzi mabaya ya wengine. (Mhu. 7:16) Bali yeye anakuwa mnyofu na kuwa na lengo la kutafuta haki. Hajilegezi aongozwe na tamaa mbaya wala mikazo inayoweza kumtendesha makosa mazito hata avunje ukamilifu wake kwa Mungu. Hata hivyo, nyakati nyingine kutokamilika kunaweza kumtendesha makosa na dhambi. Akitenda dhambi, anakubali ameifanya na kutubu, kisha anamwomba Yehova msamaha kwa jina la Kristo. (Matendo 10:43) Anaitegemea dhabihu kamilifu ya Kristo kama msingi wa kusamehewa dhambi. (1 Tim. 2:5, 6) Halafu anajitahidi iwezekanavyo asiirudie dhambi hiyo. Anajua kwamba akifuata mwendo wenye dhambi atapoteza upendeleo wa Mungu. Kwa sababu ya kuwapenda wengine, anawaeleza “habari njema” ambazo amepata. Anakuwa mtangazaji mwenye juhudi wa “habari njema” na kujaribu kuonyesha watu uhitaji wa kuwa na imani na ubora wa kupatanisha maisha yao na kanuni za Biblia. Anawaonyesha kwamba Yesu Kristo na watu wengine waliokuwa na imani maishani mwao, wanaosimuliwa katika Biblia, ni mifano myema inayopasa kufuatwa. ​—⁠Ebr. 11:1–12:3.

13 Kwa kuwa kuzitii “habari njema” kunahusu mwenendo wa Mkristo katika mambo yote, hapa tunazungumza baadhi ya kanuni za msingi ambazo Mungu anawekea wote wanaotaka kuwa Wakristo.

JINSI KUSEMA KWELI KUNAVYOHUSIKA KATIKA MAISHA YA MKRISTO

14, 15. (a) Kwa sababu gani lazima Yehova aabudiwe ‘kwa kweli’? (b) Kusema “kweli” katika jamaa kuna maana gani?

14 Kwa kuwa Yehova Mungu ndiye aliyemfanya mwanadamu na anayajua mahitaji yake, mwanadamu anahitajiwa sana aishi kulingana na kanuni za adili ambazo Mungu ameonyesha katika Biblia, na hapo ndipo atakapoweza kuwa na hali njema. Kwanza, Yehova ndiye “Mungu wa kweli.” (Zab. 31:5) Lazima aabudiwe “kwa roho na kweli.” (Yohana 4:24) Kusema kweli kunahitajiwa sana, si kwa kusudi la kuwa na amani na Mungu tu, bali ili kuishi kwa amani na wengine pia. Mtume Paulo alishauri Wakristo hivi: “Basi uvueni uongo, mkaseme kweli kila mtu na jirani yake.” ​—⁠Efe. 4:25.

15 Ufikirie ubora wa kusema “kweli” katika jamaa. “Kweli” ikisemwa nyakati zote, washiriki wa jamaa wanatumainiana. Mume na mke wanaheshimiana na kuwa na urafiki mwingi. Hawakai bila kusemezana. Watoto nao wanataka sana kujulisha wazazi wao mambo yanayoendelea maishani mwao, kwa maana wana hakika kwamba watasikilizwa na kupewa uongozi wa kutatua matatizo yao. Wanajua pia kwamba wazazi wao hawawaagizi wafanye hivi kisha wao wenyewe wanafanya vingine. Wanaweza kutegemea wazazi wao wawasaidie katika hali yo yote.

16. Maneno ya Yesu katika Yohana 14:6 yanakaziaje uhitaji wa Mkristo wa kusema kweli?

16 Yesu Kristo alisema: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima.” (Yohana 14:6) Kwa Mkristo, “njia” ni kuwaza, kuwa na maoni na matendo kama ya Yesu. Basi anatakiwa aifuate “kweli” katika pande zake zote, sawa na vile Yesu alivyoyatimiza mambo yote ambayo Mungu alikuwa amemwekea ayafanye. Makala inayofuata inazungumza matakwa mengine ya “njia” hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alimpendeza Mungu, akahurumia wengine lakini hakujinyima mambo kupita kiasi . . .

Wala hakuonyesha kiburi wala kujiona mno kuwa mtawa kama Mafarisayo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki