Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Biashara ya Tumbaku Ule mfululizo “Kuua Mamilioni Ili Kufanya Mamilioni” (Mei 22, 1995) ulikuwa wenye kuarifu na uliandikwa kwa weledi. Ule mchoro kwenye jalada (“Skull With Cigarette”) uliochorwa na Vincent van Gogh ulitisha! Labda picha hii pekee itatosha kufanya watu wengine kuacha kuvuta sigareti ama angalau kuzuia wengine kuanza.
M. B., Marekani
Kwa kuwa nafanya kazi katika American Cancer Society, kihususa nilikuwa na hamu ya kusoma makala hizi. Nilipeleka nakala moja kwa mwanamke ambaye ni mwenyekiti wa tawi la hapa la muungano wa kupinga tumbaku. Alipendezwa na ubora wa uandishi na utafiti akaomba nakala 35 kwa ajili ya wenzake.
J. O., Marekani
Mume wangu pamoja nami tuliacha kuvuta sigareti kwa karibu miezi mitatu, lakini bado nilikuwa na uchu wa kuvuta sigareti. Kisha nilisoma makala hii, nayo ilinifanya kung’amua kwamba baadhi ya viungo katika sigareti ni vyenye sumu sana hivi kwamba ni kinyume cha sheria kuvitupa katika jaa! Hili lilinitia nguvu kuchukia kile ambacho ni kibaya.
L. T., Afrika Kusini
Mgonjwa wa Mapaku-Mekundu Nawashukuru sana kwa habari kuhusu ugonjwa wa mapaku-mekundu katika ile makala “Sasa Ni Mia Tu na Yehova.” (Februari 22, 1995) Nina umri wa miaka 18, na nimekuwa nikiugua ugonjwa huu kwa karibu miaka miwili. Inatia moyo kujua jinsi kuugua kunavyovumiliwa na ndugu na dada wengine katika sehemu mbalimbali za ulimwengu na kuona jinsi Muumba wetu sikuzote hututegemeza kwa upendo.
J. A. Y., Italia
Wazazi Wenye Tatizo Nilisali ili nipate makala kama “Vijana Huuliza . . . Namna Gani Ikiwa Mzazi Wangu Hatimizi Matakwa ya Kimungu?” (Mei 22, 1995) Jinsi nilivyohuzunika na kuumizwa wakati mama yangu alipotengwa kutoka kwa kutaniko la Kikristo! Nilikuwa karibu kuacha upainia, kueneza evanjeli kwa wakati wote. Hiyo makala ilinitia nguvu ‘kutimiza wokovu wangu mwenyewe kwa kuogopa na kutetemeka’ badala ya kuwa na hangaiko la kupita kiasi kuhusu msimamo wa mama pamoja na Yehova. (Wafilipi 2:12) Asanteni sana.
J. P., Filipino
Mimi ni Mkristo aliyebatizwa, nami nimeona ikiwa vigumu sana kuheshimu baba yangu ambaye huja nyumbani kila siku akiwa mlevi. Nilipokuwa nikisoma makala hii, sikuweza kuacha kulia. Sasa kwa sababu nimeisoma, hisia na kufikiri kwangu hasi kuelekea baba yangu zimepungua sana, nami nahisi nikiwa nimetulia sana kindani.
N. M., Japani
Sayansi ya Kikristo Ile makala “Seminari za Kuboresha Mahusiano Kati ya Madaktari na Mashahidi wa Yehova” (Machi 22, 1995) ina maelezo juu ya mfikio wa Sayansi ya Kikristo kwa ugonjwa. Katika upendezi wa kujenga uelewano baina ya imani zetu, ningependa kuwahakikishia wasomaji wenu ya kwamba, Wakristo Wanasayansi huthamini na hulinda uhai wa kibinadamu kama vile Kristo Yesu alivyotuonyesha tufanye tukitegemea uponyaji wa kiroho. Rekodi ya maponyo yaliyohakikishwa yachapishwayo katika majarida yetu kwa zaidi ya karne huonyesha kwamba ni ibada ya Mungu, si ufia-imani, ambayo ni madhumuni yetu. Hali-njema ya kiroho, kiadili, na kimwili kwa udumifu ndilo tokeo.
M. V. W., Meneja, Kamati za Uchapaji, The First Church of Christ, Scientist, Marekani
Asante kwa maelezo haya. Kusudi letu la kunukuu maneno ya daktari wa kitiba lilikuwa kutokeza uhakika wa kwamba Mashahidi wa Yehova hukubali matibabu ya kitiba. Huku tukistahi haki za wengine za kuamini kama watakavyo, Yesu Kristo kwa hakika alisema kwamba “wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi.” (Mathayo 9:12) Na Paulo alipozungumzia kuhusu ‘magonjwa yaliyompata [Timotheo] mara kwa mara,’ yeye hakupendekeza uponyaji wa kiroho bali alimtolea matibabu ya kawaida ya kitiba. (1 Timotheo 5:23) Basi maoni ya Biblia kuhusu matibabu ya kitiba hupingana na mafundisho ya Sayansi ya Kikristo.—Mhariri.