Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Familia za Mzazi-Mmoja Nimetoka tu kupokea Amkeni! langu la Oktoba 8, 1995, na kusoma ule mfululizo “Familia za Mzazi Mmoja—Zaweza Kufanikiwa kwa Kadiri Gani?” Nawashukuru sana kwa makala hizi. Ni za wakati ufaao kabisa. Nimekuwa mzazi aliye peke yake kwa miaka saba na nusu, na mambo yamekuwa magumu sana. Nina binti mwenye umri wa miaka 15 ambaye yuko kwenye kipindi kigumu na chenye kuasi. Pia, hali ya kazi yangu si imara. Hata hivyo, nashukuru kuwa katika kutaniko la Mashahidi wa Yehova lenye kutegemeza na lenye upendo. Wakati wowote ambapo nimehitaji msaada kwa gari langu au mtu wa kuongea naye, sikuzote ndugu zangu wamenisaidia.
D. R., Marekani
Nimekuwa mzazi aliye peke yake tangu 1978. Kwa sababu ya kusumbuka na mshuko wa moyo wa aina mbili, sikuwa mzazi mzuri sikuzote. Hata hivyo, mimi sikuzote husikiliza magazeti kwenye ukanda. Tayari nimesikiliza makala hii mara mbili, na hata sasa naisikiliza kwenye kinanda changu. Maadamu magazeti yaendeleapo kuwa na habari nzuri ajabu hivyo, nahisi kwamba familia yangu itafanikiwa!
T. O., Marekani
Je, Ni Vigumu Kumpendeza Mungu? Mimi ni mzazi aliye peke yake, na nilipoona jalada la toleo la Oktoba 8, 1995, lenye makala zinazohusu wazazi walio peke yao, nililia. Lakini makala niliyosoma kwanza ilikuwa “Maoni ya Biblia: Je, Viwango vya Mungu Ni Vigumu Mno Kufikia?” Naam, nikiwa mama ambaye aonekana akishindwa, makala hii ilikuwa kitulizo kikubwa. Ilinionyesha kwamba sijashindwa. Ni fursa yangu tu ya kumthibitisha Shetani kuwa mwongo. Shukrani na zimwendee Yehova kwa makala hii nzuri ajabu!
R. N., Marekani
Ni makala iliyonigusa moyo sana. Inashangaza kufikiri kwamba hata ingawa Yehova ni mweza yote, yeye yuko tayari kutusamehe makosa yetu ambayo tumefanya. Makala hii ilinisaidia kung’amua kwamba twaweza kuwa na furaha kuishi kwa viwango vya Mungu, hata ingawa tutakosea nyakati nyingine.
D. C., Marekani
Upofu wa Mtoni Hivi majuzi, mwakilishi wa serikali aligawanya tembe za dawa za kuzuia upofu wa mtoni katika kijiji chetu. Upesi baada ya hapo nilipokea toleo la Oktoba 8, 1995, lenye makala “Upofu wa Mtoni—Kuishinda Tauni Mbaya Mno.” Nilitumia vizuri habari hiyo na jirani zangu. Mwakilishi wa serikali alipoona makala hiyo, alisema kwa mshangao: “Tengenezo lenu ni zaidi ya kuwa dini tu!” Zaidi ya hayo, daktari wa sehemu ya kwetu alijipatia andikisho la magazeti yote mawili Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wengi katika eneo letu wanaagiza magazeti hayo. Wanafurahi kuona kwamba yanataja yale yanayotokea katika Nigeria.
A. A., Nigeria
Ushindi wa Kisheria Niliisoma ile makala “Ushindi wa Wachache—Katika Bara la Usawa.” (Oktoba 8, 1995) Nilipokuwa katika shule ya sekondari, ilinibidi niepuke madarasa ya judo. Nilitiwa moyo kusoma kwamba akina ndugu katika Kobe wamekuwa wakipigania suala hili katika mahakama ili kulinda uhuru wao wa ibada na haki yao ya kupokea elimu. Kwa vile sasa shule imekata rufani kwenye Mahakama Kuu, nasali kwamba akina ndugu wapate hukumu yenye kufaa.
Y. K., Japani