Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kuutazama Ulimwengu Magazeti yenu yanakuwa yenye kupendeza zaidi na zaidi. Yanashughulika na habari za aina zote—matukio ya sasa, michezo, sayansi, na nyinginezo. “Kuutazama Ulimwengu” yapendeza sana. Nafikiri kwamba ikiwa habari za televisheni zingetegemea sehemu hii, zingekuwa zenye kupendeza hata zaidi.
R. S., Italia
Nathamini sana vichwa vinavyoshughulikiwa katika “Kuutazama Ulimwengu.” Kimoja kilichonifaa kabisa kilikuwa katika toleo la Aprili 22, 1995. Kichwa hicho kilikuwa “Ni Nini Huwafanya Walimu Wawe Maarufu?” Makala hiyo ilisema kwamba wanafunzi si lazima wawapende walimu wanaopeana kazi chache za kufanyia nyumbani, lakini wanawapenda walimu ambao ni wenye fadhili, wenye kujali, na wenye haki. Huo ndio ukweli! Nimeona hali nyingi za walimu wanaowapendelea wanafunzi walio maarufu ili wawe maarufu. Lakini hatimaye walimu wa aina hiyo hawaendelei kuwa maarufu. Asanteni tena kwa habari hii yenye thamani.
L. K., Marekani
Matabiri Bandia Asanteni kwa ule mfululizo “Matabiri Bandia au Unabii wa Kweli—Waweza Kutofautishaje?” (Juni 22, 1995) Ingawa nimejifunza Biblia kila siku kwa miaka 42 na nimejaribu kufyonza ile habari kuhusu ishara ya siku za mwisho, naweza kusema kwamba muhtasari ulio wazi mliotoa wa maandiko yote juu ya habari hii ulinisaidia sana. Mmeifanya habari hii iwe rahisi kukumbukwa. Kilikuwa chakula cha kiroho cha ajabu!
M. B., Marekani
Kuiba Nina umri wa miaka 13, na nilikuwa na tatizo la kuiba. Nilikuwa nikiiba pesa, au nilikuwa nikienda kwenye duka na kuiba peremende ya kutafuna. Nilitaka kuacha kuiba, lakini hakuna lililosaidia mpaka nilipopata Amkeni! ya Juni 22, 1995, na kufungua ile makala “Vijana Huuliza . . . “Kwa Nini Nisiibe?” Ilinigusa sana. Ilinisaidia kutoa sala kwa Yehova na kujua kwamba angeweza kunisamehe kwa njia kubwa. Nataka kuwa katika Ufalme wa Mungu, nami najua kuwa watu wanaoiba hawatakuwako. Shukrani kwa kuchapisha makala hii.
J. A., Kanada
Nina umri wa miaka 23 na nimefungwa kwa sababu ya kuiba. Yote haya yalianza kwa sababu ya msongo wa marika. Walitaka nimfanyie mtu mzaha, na toka hapo mambo yakawa mabaya. Makala hiyo ni ya kweli kabisa. Natumaini kwamba vijana watatii shauri hilo kabla ya kuchelewa mno. Kwa njia hiyo, wanaweza kuepuka kuishia nilipo mimi—gerezani.
M. S., Marekani
Simulizi la Maisha Nimemaliza tu kusoma ile makala “Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu.” (Juni 22, 1995) Kusoma juu ya jinsi Celeste Jones alivyotendwa vibaya na washiriki wa familia—na bado akadumisha imani yake na kuvumilia—kulinifanya niahidi kwamba ningejaribu sana kutolalamika tena kamwe juu ya matatizo ya afya yangu mwenyewe.
J. P., Marekani
Nikiwa na vizuizi kidogo kuliko vya Celeste Jones, nafahamu kijuujuu tu ujasiri uliohitajiwa ili abaki mshikamanifu. Shukrani za pekee ziwaendee wote waliomsaidia Celeste na kumpa utunzaji uliohitajiwa kwa ajili ya huduma yake.
W. R., Kanada
Niliguswa sana na hii makala. Hiyo imeimarisha imani yangu na kunisaidia kutambua kwamba njia yenye matokeo zaidi ya kuwasaidia jirani zetu ni kutumia njia zozote ziwezekanazo kuwahubiria.
P. H. P., Nigeria
Nilichochewa sana na kutiwa moyo na maono ya Celeste. Ninazeeka na ninapata maumivu na uchungu wote unaoambatana na kuzeeka, lakini maono yake yananipa nguvu ya kukabili hiyo.
M. R., Jamaika