Je, Mwisho wa Dini Uko Karibu?
“Dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.”
ISAYA, NABII MWISRAELI WA KARNE YA 8 K.W.K.
HIVYO nabii Mwebrania Isaya akatabiri kwamba siku moja kila mtu duniani ataunganishwa katika ibada ya Mungu Mweza Yote. Hata hivyo, leo taraja kama hilo huenda likaonwa kuwa mbali sana kuliko wakati mwingineo wote.
Kwa kielelezo, mapema katika karne hii, wanamapinduzi wa Kikomunisti katika Urusi waliamini kwamba uharibifu wa dini ulikuwa hatua muhimu ya kuweka huru makabwela. Wao walidai kwamba Uatheisti ‘ungeweka huru makabwela kutokana na mzigo wa upendeleo na madanganyo ya wakati uliopita.’ Kufikia 1939, Stalin alikuwa amepunguza idadi ya makanisa ya Othodoksi yaliyokuwa yakitenda katika Muungano wa Sovieti hadi 100, ikilinganishwa na zaidi ya 40,000 kabla ya 1917.
Hitler pia aliona dini kuwa kizuizi katika njia yake kuelekea mamlaka kamili. “Mtu apaswa kuwa ama Mkristo ama Mjerumani. Huwezi kuwa wote wawili,” akatangaza wakati mmoja. Yeye alikusudia kuondosha hatua kwa hatua namna zote za ibada ambazo hakuweza kuzidhibiti. Wakiwa na hilo akilini, Wanazi walianzisha sala zao wenyewe zinazofanana na za kidini, misherehekeo, ubatizo, na hata ibada za maziko. Hitler alikuwa mesiya wao, nayo nchi ilikuwa mungu wao. Ukatili wowote ungeweza kutendwa ikiwa ulikuwa mapenzi ya Hitler.
Je, Ni Siku za Mwisho za Dini?
Wala Stalin wala Hitler hawakufaulu katika kampeni zao za kukandamiza dini. Lakini sasa, yaonekana ubaridi wachukua daraka la kukandamiza dini. Kwa wanafunzi wa Biblia badiliko hili la matukio halishangazi. Mtume Paulo alimwambia Timotheo kwamba katika “siku za mwisho” watu wangekuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:1-4.
Je, Biblia yafundisha kwamba katika hizi “siku za mwisho,” zilizo na hali ya kutojali ya kidini, zingekuwa mwanzo wa kukoma kwa dini zote? La. Badala ya kutabiri mwisho wa dini zote, Biblia hueleza kwamba dini isiyo ya kweli—ambayo imepewa jina la mfano Babiloni Mkubwa—itakoma.a Kitabu cha Ufunuo chasema hivi: “Na malaika mmoja mwenye nguvu akainua jiwe, kama jiwe kubwa la kusagia, akalitupa katika bahari, akisema, Kama hivi, kwa nguvu nyingi, utatupwa Babeli [“Babiloni,” New World Translation], mji ule mkuu, wala hautaonekana tena kabisa.”—Ufunuo 18:21.
Hata hivyo, kutoweka kwa dini bandia hakutatokeza ulimwengu usiomhofu Mungu. Kinyume na hilo, Zaburi 22:27 hutoa unabii hivi: “Miisho yote ya dunia itakumbuka, na watu watamrejea BWANA; jamaa zote za mataifa watamsujudia.” Ebu wazia tu wakati ambapo “jamaa zote za mataifa” zitakapounganishwa pamoja katika kumwabudu Mungu mmoja wa kweli! Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, ahadi hiyo nzuri ajabu itapata utimizo mtukufu. (Mathayo 6:10) Wakati huo ujapo, dini—dini ya kweli—itakuwa na umaana mkubwa. Lakini namna gani sasa?
Kujaza Utupu wa Kiroho
Utupu wa kiroho ulioenea sana katika Ulaya leo hufanana na hali katika Milki ya Roma ya karne ya kwanza. Mwanahistoria Will Durant afafanua jinsi Ukristo wa karne ya kwanza ulivyoshughulikia kwa mafanikio uhitaji wa kiroho wa wakati huo: “Katika utupu wa maadili wa upagani uliokuwa ukiisha, katika ubaridi wa Ustoiki na ufisadi wa Uepikureo, katika ulimwengu uliojaa ukali, ukatili, ukandamizaji, na mchafuko wa kingono, katika milki iliyowekwa chini ya utawala ambayo ilionekana kutohitaji tena uwezo wa kiume au miungu ya vita, [Ukristo] ulileta maadili mapya ya udugu, ufadhili, adabu, na amani.”
Utupu wa maadili na kiroho katika maisha ya watu katika wakati wetu waweza kujazwa kwa ujumbe uleule wenye nguvu uliohubiriwa kotekote katika Milki ya Roma na Wakristo wa mapema. Na kuna watu wanaosikia. Watu wengi wa Ulaya, ingawa kwa nje hawaonekani kuwa wa kidini, bado huhisi kwamba Mungu ana fungu muhimu katika maisha zao. Huenda hawahudhurii tena ibada za kidesturi za kanisa, hata hivyo wengine wamejaza utupu wao wa kiroho kwingineko.
Juan José, mwanamume kijana kutoka Palma de Mallorca, Hispania, alielimishwa katika shule ya Kikatoliki na kutumikia akiwa mvulana wa altare hadi alipokuwa na umri wa miaka 13. Yeye alihudhuria Misa kila Jumapili pamoja na familia yake, lakini akaacha kwenda kanisani alipokuwa tineja. Kwa nini? “Kwanza kwenda kwenye Misa kulinichosha,” aeleza Juan José. “Nilikariri sala ya dini. Kila kitu kilionekana kuwa rudio la kile nilichokuwa nimesikia mbeleni. Isitoshe, kasisi wa parishi yetu mara nyingi alitutendea sisi wavulana wa altare kwa ukali. Nami nilifikiria kuwa kosa kwamba watu maskini walipaswa kulipa kasisi ili awafanyie ibada ya maziko.
“Bado nilimwamini Mungu, lakini nilifikiri ningeweza kumtumikia katika njia yangu mwenyewe, nje ya mpango wa kanisa. Pamoja na kikundi cha marafiki, nilijaribu kufurahia maisha kwa njia bora kadiri nilivyoweza. Nafikiri ungesema kwamba kitumbuizo kikawa jambo la kwanza maishani mwangu.
“Lakini nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Walikuwa na nini cha kunipa ambacho sikuwa nimepata kanisani? Imani hakika inayotegemea Biblia badala ya desturi na ‘mafumbo’ ambayo sikuweza kuyafahamu. Hata hivyo, itikadi zangu mpya zilimaanisha mabadiliko makubwa kwangu. Badala ya kutumia mwisho-juma nikipanga karamu kwenye majumba ya disko, nilianza kwenda nyumba kwa nyumba ili kushiriki pamoja na majirani wangu imani yangu niliyopata karibuni. Kujihusisha kwa utendaji wa kusaidia wengine kulipatia maisha yangu maana. Kwa miaka saba iliyopita, nimekuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova.”
Si vijana tu ambao hutafuta kujaza utupu wao wa kidini. Antonia, mwanamke mzee-mzee kutoka Extremadura, Hispania, alitumia sehemu kubwa ya maisha yake “akimtafuta Mungu,” kama asemavyo. Katika miaka yake ya utineja, alienda kwenye Misa kila siku na hatimaye akaingia makao ya watawa ya Wakatoliki, kwa kuwa aliamini “kwamba ikiwa Mungu hawezi kupatikana katika makao ya watawa, hawezi kupatikana mahali penginepo pote.” Lakini miaka mitatu baadaye aliondoka kwenye hayo makao ya watawa, akihisi akiwa amevurugika hata zaidi na kukosa maana kuliko mbeleni.
Hatimaye, alipokuwa katika miaka yake ya 50, akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. “Nilifurahi sana wakati Mashahidi waliponitembelea na kujibu maswali yangu kutoka kwa Biblia yangu mwenyewe,” yeye aeleza. “Tangu niwe mmoja wa Mashahidi wa Yehova, maisha yangu yamekuwa na kusudi. Nina matatizo, lakini naweza kuyakabili kwa sababu sasa nimemjua Mungu wa kweli.”
Hayo si ndiyo mambo yaliyoonwa pekee. Wakikinza mwelekeo wa kidini, idadi zinazoongezeka za watu wanashirikiana na Mashahidi wa Yehova na wamepata kwamba kwa kuishi kupatana na imani yao na kuhubiria wengine kuihusu kunapatia maisha zao maana na kusudi.
Dini ya Kweli Ina Umaana Zaidi ya Wakati Mwingineo Wote
Ingawa twaishi katika wakati ambapo wengi wanakataa dini, halingekuwa jambo la hekima kuhukumu dini zote kuwa zisizofaa. Ni kweli, katika karne ya 20, watu wanaacha desturi zisizo na maana na kanuni za kale na zisizo za kimaandiko, nao hudhihaki kwenda kanisani ambako ni kwa ajili tu ya kuonekana kwa nje. Biblia hasa hupendekeza kwamba tuepuke dini yenye unafiki. Mtume Paulo alitabiri kwamba katika “siku za mwisho,” watu wengine ‘wangekuwa wenye mfano wa ujitoaji kimungu, lakini wakikana nguvu zao.’ Watu kama hao hudumisha wonyesho wa kijuu-juu wa dini, lakini mwenendo wao unakataa uhalali wao. Twapaswa kuitikiaje unafiki huo wa kidini? “Hao nao ujiepushe nao,” akashauri Paulo.—2 Timotheo 3:1, 5, NW.
Lakini Paulo alisema pia kwamba “dini hutokeza faida za juu.” (1 Timotheo 6:6, New English Bible) Paulo hakuwa akizungumza juu ya namna yoyote tu ya dini. Neno la Kigiriki lililotafsiriwa hapa kuwa “dini” lilikuwa eu·seʹbei·a, ambalo lamaanisha “ujitoaji au staha kwa Mungu.” Dini ya kweli, ujitoaji halisi wa kimungu, “unayo ahadi ya uzima wa sasa, na ya ule utakaokuwapo baadaye.”—1 Timotheo 4:8.
Kama vielelezo vilivyotajwa hapo juu vionyeshavyo, dini ya kweli yaweza kupatia maisha zetu maana na kutusaidia kukabili matatizo kwa uvumilivu. Zaidi ya hilo, dini ya kweli, huhakikisha wakati ujao wa milele. Namna hiyo ya ibada yastahili kufuatiwa, kwa kuwa twahakikishiwa ‘itaijaza dunia’ hatimaye.b (Isaya 11:9; 1 Timotheo 6:11) Hakuna shaka kwamba sasa ndio wakati ambapo dini ya kweli ina umaana kuliko wakati mwingineo wote.
[Maelezo ya Chini]
a Biblia hutumia jiji la kale la Babiloni kuwa mfano wa milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli, kwa kuwa ni katika jiji hili ambapo mawazo mengi ya kidini yasiyo ya kimaandiko yalianzia. Kwa kipindi cha karne nyingi mawazo haya ya Kibabiloni yalikuja kuenea katika dini kuu za ulimwengu.
b Kwa mazungumzo ya jinsi ya kutambua dini ya kweli, ona sura ya 5, “Ni Ibada ya Nani Anayoikubali Mungu?” ya kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichotangazwa katika 1995 na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Hadithi ya Majengo Mawili
Hispania imejaa majengo ya kidini, lakini bidii ambayo wakati mmoja ilitegemeza ujenzi wa makanisa yenye gharama kubwa yaonekana imetoweka. Kwa kielelezo, katika Mejorada del Campo, kwenye viunga vya Madrid, kanisa lenye kuvutia sana la Katoliki linajengwa. Justo Gallego Martínez, aliyekuwa mbeleni mtawa wa Kibenedikti, alianza huo mradi yapata miaka 20 iliyopita. Lakini bado jengo hilo halijamalizika ndani. Martínez, ambaye ndiye mjenzi pekee, sasa yuko katika miaka ya 60, kwa hiyo yaonekana haielekei kwamba kanisa hilo litamalizwa kamwe. Hata hivyo, kilometa 300 kusini, tukio tofauti liliendelea kusitawi.
“Imani Yahamisha Milima” ndivyo gazeti la mahali hapo lilivyofafanua ujenzi wa siku mbili wa Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova katika Martos, Jaén, Hispania. “Inawezekanaje,” likauliza gazeti la huko, “kwamba katika ulimwengu huu wa sasa unaotegemea ubinafsi, wajitoleaji kutoka maeneo tofauti [ya Hispania] wasafiri bila ubinafsi hadi Martos ili kujenga jengo ambalo limevunja rekodi kwa mwendo, ukamilifu, na utaratibu?” Katika kujibu swali hili, makala hiyo ilinukuu maneno ya mmoja wa hao wajitoleaji: “Hilo lawezekana tu kwa sababu ya uhakika wa kwamba sisi ni watu wanaofundishwa na Yehova.”
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mejorada del Campo
Jumba la Ufalme katika Martos