Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Sayari Iliyotishwa Naandika kuhusu mfululizo wa makala “Sayari Yetu Iliyotishwa—Je, Yaweza Kuokolewa?” (Januari 8, 1996) Ni vizuri kuweza kusoma jambo lenye kutia-moyo. Makala ya tatu katika mfululizo huo yatupatia tumaini la Paradiso, ambamo hatutahangaika juu ya mfumo wa ikolojia au matundu katika tabaka ya ozoni! Natumaini kuishi katika paradiso hiyo pamoja na familia yangu na marafiki.
A. C., Marekani
Tulipenda lile sanduku lenye kuarifu lililo kwenye kurasa 8 na 9 ambalo lilishughulikia matatizo kama kukatwa kwa miti, uhaba wa maji, na spishi zilizohatarishwa. Hizo makala zilifanya tuelewe hali mbaya sana inayokabili sayari yetu sasa. Twahisi salama tukijua kwamba ni Muumba wetu aliye na suluhisho la pekee kwa tatizo hili.
O. P. na F. J. O., Hispania
Ripoti ya Jessica Nimetoka tu kumaliza kusoma “Ripoti ya Jessica” katika toleo la Januari 8, 1996. Ilinitia moyo sana! Mimi hufurahi nionapo kijana mwenye kielelezo kizuri, akimtumikia Yehova kwa shangwe na kwa uaminifu. Masimulizi ya Jessica yanikumbusha juu ya uhitaji wa kutoa ushahidi kila pindi.
A. H., Marekani
Nilipata Kusudi Maishani Ile makala “Sikuwa na Lengo Lakini Nikapata Kusudi Maishani” (Januari 8, 1996) ilinigusa moyo sana. Nilipoisoma, niliona kana kwamba makala hiyo ilikuwa ikisema kunihusu. Mimi pia nilikuwa nikitangatanga bila kusudi nikiwa sina mtazamo mzuri wa wakati ujao. Lakini nilialikwa kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova na kuanza funzo la Biblia. Sasa nashiriki kwa furaha katika kazi ya huduma ya wakati wote, nikisaidia wengine kuona tumaini zuri ajabu ambalo Yehova amenionyesha.
C. R., Marekani
Tiba ya Utasa Ile Habari “Je, Ni Tumaini Jipya kwa Wenzi wa Ndoa Wasiozaa” ya “Kuutazama Ulimwengu” ilivuta uangalifu wangu. (Septemba 22, 1995) Nilimwonyesha mwanabiolojia mmoja habari hiyo akasema kwamba hajapata kamwe kusikia njia hiyo ya tiba inayofafanuliwa, ambayo shahawa moja ya mwanamume inaingizwa kwenye yai “ndani ya mwanamke.”
E. K., Ujerumani
Habari yetu ilitegemea ripoti ya shirika la habari la France-Presse iliyokuwa ikijadili hotuba iliyotolewa na tabibu Mdenmark Anders Nyboe Andersen. Kwa kusikitisha mambo fulani hayakuripotiwa kwa usahihi. Dakt. Andersen aliliambia “Amkeni!” kwamba kuingizwa kwa shahawa hasa kunafanywa nje ya mwili wa mwanamke. Kisha lile yai lililotungishwa huingizwa katika mwanamke. Tulisema kwa usahihi kwamba utaratibu huo waweza kutumia “shahawa ya mume badala ya ile ya mtoaji shahawa asiyejulikana—hivyo ikiepusha maswali ya kimaadili na kidini.” Kwa sababu hiyo, wenzi wa ndoa Wakristo ni lazima wafanye maamuzi ya kibinafsi kuhusu njia hiyo ya tiba. (Ona “Mnara wa Mlinzi” la Julai 15, 1983, ukurasa 23.)—Mhariri.
Rafiki Mpotovu Ninaandika kuhusu makala “Vijana Huuliza . . . Nifanye Nini Rafiki Akitumbukia Katika Matatizo?” (Januari 22, 1996) Mmoja wa marafiki wangu wa karibu zaidi alitengwa na ushirika mwaka mmoja uliopita. Nilishtuka sana. Nilihisi kama sikuwa nimemsaidia vya kutosha, sikutumia wakati wa kutosha pamoja naye, na sikuwa rafiki mzuri sana kwake. Niliposoma kwamba si kosa langu lililofanya aache kweli, nilihisi kana kwamba mzigo mzito umeniondokea!
L. T., Marekani
Katika kisa changu mtu aliye karibu na mimi aliyeanza “kufuata mtindo-maisha wenye kutilika shaka” alikuwa si rafiki wa karibu tu bali mama yangu mpole ambaye hakuna mtu aliyekuwa kama yeye. Hatimaye niliwaendea wazee wa kutaniko kuhusu hali yake, akatengwa. Nilijishutumu kwa kuwaambia wazee. Sasa nataka kujaribu kushinda hisia zangu zisizofaa za hatia kwa kutumia madokezo yaliyo katika hiyo makala.
I. Y., Japani