Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Ukosefu wa Kazi ya Kuajiriwa Asanteni sana kwa mfululizo “Ukosefu wa Kazi ya Kuajiriwa—Kuna Suluhisho.” (Machi 8, 1996) Habari hiyo ilifika wakati nilipokuwa nikitafuta kazi, lakini sikupata. Nilijaribu kubuni kazi nyumbani, kama mlivyotaja katika ukurasa 11, na hili limekuwa na mafanikio. Nashukuru Yehova kwa ajili yenu!
J. M., French Guiana
Makala hizo zilielezea hali nilizokuwa nazo hivi karibuni. Kwa miezi michache, nililazimika kubadilika kufanya “aina zote za kazi,” jinsi tu makala moja ilivyosema. Lakini sikuvunjika moyo. Nilijaribu kuwa na mtazamo unaofaa, na hatimaye nilipata kazi ya kudumu. Katika kipindi hicho, nilisaidiwa na mke wangu, ambaye alikuwa mwangalifu sana katika ununuaji wa bidhaa. Asanteni tena kwa habari ambazo hutusaidia kutumia kanuni za Biblia katika hali ngumu.
U. C., Italia
Nilipenda hasa kisanduku “Kubuni Kazi Nyumbani.” Mimi ni painia wa kawaida, mweneza-evanjeli wa wakati wote, na kwa miaka miwili niliendesha kituo cha nyumbani cha utunzaji wa mchana chenye kibali. Niliwaangalia watoto kabla ya na baada ya shule na nimepata mapato mazuri. Imenipa wakati wa kuhubiri saa za adhuhuri, na nilifanya kazi kwa muda wa saa nne tu kwa siku. Wazazi wengi walikuwa wenye uthamini kwa sababu ni vigumu kupata utunzaji bora. Natumaini wengine pia watapata kazi ya kuajiriwa ambayo itawasaidia kumtumikia Yehova.
T. K. L., Marekani
Mlishauri kwamba watu wasio na kazi ya kuajiriwa wanaweza kujiajiri wenyewe kwa kufanya kazi kama upambaji nyumba, unyoaji nywele, ubawabu na kadhalika. Pia mlisema kwamba katika hali fulani wanaweza kutangaza huduma zao bila malipo au kwa gharama ndogo. Je, jambo hili si uvunjaji wa sheria katika Ujerumani?
R. T., Ujerumani
Seria hutofautiana kati ya nchi na nchi, na pengine madokezo haya yangeweza kuwa uvunjaji wa sheria katika mabara fulani. Hiyo ndiyo sababu katika ukurasa 9 tulitaja umuhimu wa kujua na kuheshimu sheria za ushuru na kodi kabla ya kuanza shughuli kama hiyo. Wakristo wana wajibu wa kufuata sheria za mabara ambayo wanaishi. (Warumi 13:1)—Mhariri.
Hifadhi ya Wanyama Nilifurahia kwelikweli makala “Kujifunza Biblia—Katika Hifadhi ya Wanyama!” (Machi 8, 1996) Nilipenda habari zihusuzo wanyama wanaotajwa katika Biblia. Kamwe sikujua kwamba punda-milia walitajwa katika Biblia. Pia nilifurahia fungu lililoelezea chungu. Makala hiyo ilinitia moyo kufanya utafiti wa mnyama tofauti kila mwezi.
M. F., Marekani
Rafiki Yangu Mpendwa Ninataka kueleza uthamini wangu mkubwa kwa ajili ya makala yenye kufurahisha, “Rafiki Yangu Mpendwa.” (Februari 22, 1996) Ilipendeza kusoma kwamba urafiki wenye kupendeza namna hiyo upo ingawa kuna tofauti kubwa ya umri namna hiyo. Inaonyesha kwamba siyo lazima marafiki wa karibu sana wa vijana wawe tu walio katika umri wao. Kuna wengi waliozeeka ambao wana mengi ya kutoa katika njia ya ujuzi, hekima, na ucheshi.
S. T., Uingereza
Makala hiyo ilithibitisha kwamba vijana na wazee waweza kupatana na kwamba vijana waweza kunufaika kutokana na ujuzi wa hicho kizazi chenye umri mkubwa zaidi. Mimi mwenyewe nimetumia saa nyingi za kupendeza na kufurahisha pamoja na rafiki mzee. Amefanya mengi kunisaidia kukabiliana na matatizo kama msongo wa marika.
W. S., Austria
Hadi kufikia sasa sijajaribu kamwe kujifunza kutoka kwa walio na umri mkubwa. Asante kwa makala hiyo, sasa ninaelewa ni mambo gani ninayoweza kujifunza kutoka kwa watu kama hao. Ninataka sana kuwa rafiki wa karibu wa baadhi ya walio na umri mkubwa ambao wana hekima nyingi.
R. K., Japani