Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Tumaini Nilikuwa nahisi nimeshuka moyo kwa sababu ya kusalitiwa na marafiki fulani na watu wa ukoo. Nikaanza kutilia shaka ustahilifu wa kila mtu karibu nami. Lakini ule mfululizo “Ni Nani Uwezaye Kumtumaini?” (Februari 8, 1996) ulinipa maoni yenye usawaziko zaidi kuhusu tumaini. Asanteni kwa habari hiyo ya wakati ufaao.
E. I., Korea
Katika miaka ambayo imepita nimesalitiwa na baba yangu, aliyenitenda vibaya, na waume wawili, na pia ndugu Mkristo. Nikafikia hatua ambapo niliamua sitatumaini mtu yeyote. Nilijisadikisha kwamba sihitaji watu. Lakini makala hiyo ilinisaidia kuwa mwenye usawaziko zaidi. Ingawa ni vigumu sana kwangu kutumaini, nitaendelea kujaribu. Wakati huu nitakuwa mwenye uangalifu zaidi kwa yule ninayemtumaini.
C. H., Marekani
Matterhorn Nilisoma ile makala “Matterhorn wa Kipekee.” (Februari 8, 1996) Picha ya huu mlima maridadi ilinivutia sana! Makala hiyo ilinifanya nithamini uumbaji wa Mungu hata zaidi.
J. W., Marekani
Matofaa Asanteni sana kwa makala “Tofaa Moja Kila Siku, Huleta Afya.” (Februari 8, 1996) Iliamsha upendezi wangu kwa kuwa tuna mitofaa 100 katika shamba letu dogo. Sisi hufurahia kupogoa na kutunza mitofaa hiyo ili itokeze mazao vizuri. Twathamini usahihi wa makala zenu zote. Hizo huandaa habari zenye kuburudisha na kutumainika.
P. B., Marekani
Mwenendo wa Kushurutisha Asanteni kwa makala nzuri sana “Mwenendo wa Kushurutisha—Je, Huo Hudhibiti Maisha Yako?” (Februari 8, 1996) Mimi nina umri wa miaka 20 pekee, na nina tatizo la mwenendo wa kushurutisha. Mara kwa mara nimemwomba Yehova katika sala aniletee habari juu ya yale yaliyokuwa yakinipata.
M. A. C., Hispania
Nilianza kusumbuliwa na mawazo yaliyokuja yenyewe yasiyo na staha kuhusu Mungu karibu na wakati ambapo nilianza kufanya upainia, kutumikia nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote. Nilifikiri nimetenda dhambi isiyoweza kusameheka, na nililia mara nyingi. Hamwezi kuwazia jinsi ninavyohisi sasa, nikiona hisia zangu zikifafanuliwa waziwazi. Sijapata kufikiria kamwe kwamba kuna mtu yeyote anayepatwa na mambo hayo. Asanteni sana, enyi ndugu, kwa kututegemeza sikuzote.
C. B., Nigeria
Nilisoma makala hiyo tena na tena huku nikitokwa machozi. Ilinifafanua kwa undani kabisa! Nilikuwa nimejiuliza ikiwa ninarukwa akili au ikiwa roho waovu walikuwa wanatwaa akili yangu. Nilipata kitulizo kujua kwamba wengine miongoni mwa akina ndugu wanapatwa na tatizo lilo hilo.
K. T., Japani
Mara nyingi nilimwendea Yehova anipe msaada kwa tatizo hili. Lakini niliamua kuacha kwa sababu niliona ni kazi bure na hakuna kitu ambacho kingeweza kunisaidia. Sasa najielewa, na nahisi kitulizo. Naona wazi kwamba makala hiyo iliandikwa kwa njia yenye upendo zaidi. Nina hakika kwamba kwa kweli Yehova anatujali.
J. F., Jamhuri ya Cheki
Nimeteswa kiakili na mawazo ya kushurutisha kwa miaka saba sasa. Yamenifanya nihisi nimechoka sana na kushuka moyo. Nimehisi aibu mno na mwenye hatia sana nisiweze kuzungumza jambo hilo na mtu mwingine. Hakika nilifikiri nimerukwa akili. Niliposoma makala hii, sikuamini. Kulikuwa na mtu mwingine mbali na mimi ambaye alikuwa amepatwa na yale yaliyokuwa yakinipata! Machozi yakanidondoka. Sikuwa peke yangu tena. Sikuwa nimefanya dhambi isiyoweza kusameheka, na Yehova hakuwa amekasirika nami.
S. B., Afrika Kusini