Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Mataifa Tajiri Yatumia Vibaya Mataifa Maskini Nina umri wa miaka 14, nami nawashukuru sana kwa mfululizo “Je, Sikuzote Mataifa Tajiri Yatatumia Vibaya Mataifa Maskini?” (Novemba 22, 1995) Mwalimu wangu wa jiografia alitupatia mgawo wa kuandika juu ya kichwa “Taabu.” Nilitazama katika magazeti ya habari na magazeti lakini sikupata chochote ambacho kingefaa kutumiwa. Kisha, wakati nilipohitaji sana habari hiyo, gazeti hili lilifika ili kutumika likiwa msingi wa ripoti yangu. Nilipata maksi nyingi zaidi darasani, nami nashukuru sana kwa makala hizi.
A. O., Brazili
Mwenendo wa Kushurutisha Asanteni kwa makala yenye kujenga “Mwenendo wa Kushurutisha—Je, Huo Hudhibiti Maisha Yako?” (Februari 8, 1996) Ninaugua kutokana na mwenendo wa kushurutisha, na inatia moyo sana kujua kwamba siko peke yangu. Tatizo hilo limenisumbua sana tangu utotoni. Tangu nijifunze Biblia, nimejawa akilini na wazo kwamba nimetenda dhambi dhidi ya roho takatifu. Hatua kwa hatua, nimedhibiti matatizo yangu. Ni vyema kama nini kujua kwamba Yehova huwaelewa watumishi wake wasio wakamilifu!
A. B., Ujerumani
Nilithamini sana kwamba Muumba wetu hufahamu ugonjwa huu na kwamba yeye “ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote.” (1 Yohana 3:20) Tafadhalini endeleeni kutangaza makala za aina hii; ni zenye kututia moyo sana.
W. E., Uswisi
Hamwezi kuwazia jinsi makala hii ilivyonifariji. Nimekuwa na mawazo mabaya, yenye kukufuru, ambayo yamenifanya nishuke moyo na nyakati fulani kuwa na mawazo ya kujiua kimakusudi. Lakini sasa ni kama kwamba uzito mkubwa mno umeondolewa mabegani mwangu, kwa kuwa natambua kwamba Yehova hajanikataa bali anipenda sana.
I. B., Ufaransa
Tangu nilipokuwa mdogo, nimenawa mikono kwa kurudia-rudia. Natazama jiko mara tatu, hata ikiwa itanilazimu kurudi kutoka nje ili kufanya hivyo. Natazama kama vifuniko viko kwenye sufuria zangu, na kwamba nimefunga milango yote vizuri. Nakwenda kitandani nikiwa nimechoka kutokana na kung’ang’ana na mienendo yenye kushurutisha. Asanteni kwa makala yenu.
M. P., Venezuela
Robini Nilivutiwa na makala “Robini Mwenye Urafiki.” (Februari 8, 1996) Miaka michache iliyopita, nilipokuwa nikichimba mtaro shambani, nilisikia wimbo wenye kupendeza wa robini aliyekuwa amesimama kwenye bustani iliyo karibu akinitazama. Mara tu nilipojaribu kuiga sauti yake alikuwa amesimama kando yangu katika mtaro. Robini huyo alifurahia kuokota wadudu waliotoka kwa kila mkupuo wa sepeto. Tafadhalini endeleeni kutangaza ripoti kuhusu ulimwengu wa wanyama!
F. S., Ujerumani
Vilima-Barafu Asanteni kwa makala “Majumba Yenye Kumetameta ya Baharini.” (Desemba 8, 1995) Kusoma tu habari hiyo na kujiwazia nikiwa mbele ya moja la hayo mapande ya barafu, nilipendezwa na vitu vyenye kustaajabisha ambavyo Muumba wetu, Yehova Mungu, ameandaa kwa ajili ya raha yetu. Ni kama mtunga-zaburi alivyosema kuhusu Yehova kwenye Zaburi 104:24, “dunia imejaa mali [zake].”
A. I. B., Brazili
Insha ya Shule Hadithi ya insha ya shule ya Eric “Ikiwa Ningeweza Kubadili Hali Fulani ya Wakati” (Februari 22, 1996) ilinipendeza sana. Ilichochea ndani yangu hisi ya kuvutiwa na shukrani kwa wazazi wake. Ni lazima walitoa wakati mwingi na nishati kwa kumlea mwana wao ambaye ana ujasiri na upendo huo wenye kutazamisha kwa Yehova, licha ya umri wake mdogo.
C. N., Italia