Hatimaye—Serikali Itakayomaliza Uhalifu
BIBLIA ilitabiri kwamba katika siku zetu watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema.” (2 Timotheo 3:2, 3) Watu wa namna hiyo hutenda uhalifu.
Kwa kuwa watu hutenda uhalifu, kwa kadiri wabadilikavyo na kuwa watu wema, ndivyo uhalifu unavyopunguka. Lakini haijapata kuwa rahisi kwa watu kubadilika na kuwa watu wazuri. Ni vigumu zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote, kwa kuwa tangu 1914, tarehe iliyotajwa katika kronolojia ya Biblia, tumekuwa tukiishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. Kama Biblia ilivyotabiri, kipindi hiki ni “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Hizi nyakati za hatari zimesababishwa na Shetani Ibilisi, mhalifu mkubwa kuliko wote, ambaye ana “ghadhabu nyingi, akijua ya kwamba ana wakati mchache tu.”—2 Timotheo 3:1, NW; Ufunuo 12:12.
Hilo laonyesha sababu ya ongezeko la uhalifu leo. Shetani ajua kwamba yeye na mfumo wake wataangamizwa karibuni. Katika huo muda mfupi unaobaki, yeye anatafuta kila njia iwezekanayo kuingiza katika wanadamu vitabia vibaya vinavyotajwa katika 2 Timotheo sura ya 3. Hivyo, ili serikali yoyote imalize uhalifu, ni lazima iondoe uvutano wa Shetani na pia isaidie kubadili watu ili wasitende kamwe kwa njia inayofafanuliwa hapo juu. Lakini je, kuna serikali iwezayo kutimiza jambo hili lililo gumu kupita uwezo wa wanadamu?
Hakuna serikali ya kibinadamu iwezayo kufaulu. J. Vaskovich, mwalimu wa sheria katika Ukrainia, adokeza uhitaji wa kuwa na “shirika moja lenye uwezo, ambalo laweza kuunganisha na kuratibu jitihada za mashirika yote ya serikali na ya umma.” Na Rais Fidel Ramos wa Filipino alisema hivi katika mkutano mmoja kuhusu uhalifu: “Kwa sababu maendeleo yamefanya ulimwengu wetu uonekane kuwa mdogo, uhalifu umeweza kuvuka mipaka ya mataifa nao umekuwa tatizo la kimataifa. Na hivyo masuluhisho yapaswa kuwa pia ya kimataifa.”
“Msiba wa Ulimwenguni Pote”
Umoja wa Mataifa ni shirika la kimataifa. Tangu lianzishwe, limejaribu kupambana na uhalifu. Lakini halina masuluhisho kuliko serikali za mataifa. Kitabu The United Nations and Crime Prevention chasema: “Uhalifu unaofanywa nchini umeshinda udhibiti wa mataifa moja-moja na uhalifu wa kimataifa umeongezeka sana kuliko uwezo wa jumuiya ya kimataifa. . . . Uhalifu uliofanywa na vikundi vya magenge ya uhalifu umeongezeka kwa kiasi cha kushangaza sana, ukiwa na matokeo mabaya sana kwa habari ya jeuri ya kimwili, matisho na ufisadi wa maofisa wa umma. Uharamia umeua makumi ya maelfu ya watu wasio na hatia. Ulanguzi wa dawa za kulevya wenye kudhuru umekuwa msiba wa ulimwenguni pote.”
Pindi moja, James Madison, rais wa nne wa Marekani, alisema hivi: “Katika kuanzisha serikali itakayoongozwa na watu wanaotawala watu, kuna tatizo hili kubwa: ni lazima kwanza uiwezeshe serikali idhibiti wenye kutawalwa; kisha uilazimishe ijidhibiti yenyewe.” (Linganisha Mhubiri 8:9.) Hivyo suluhisho lifaalo lingekuwa kubadili serikali ‘inayoongozwa na watu wanaotawala watu’ kwa mfumo ambao Mungu angetawala. Lakini, je, suluhisho hilo lawezekana?
Serikali Itakayomaliza Uhalifu
Wakristo wa kweli wanaamini kile ambacho Biblia husema kuhusu Ufalme wa Mungu.a Hiyo ni serikali halisi. Ingawa huo Ufalme hauonekani, matimizo yao duniani yanaonekana. (Mathayo 6:9, 10) Huo umefanyizwa na Kristo Yesu na watu 144,000 ambao walitolewa kutoka ‘kila kabila na lugha na jamaa na taifa watakaomiliki juu ya nchi.’ Serikali hii yenye nguvu itatawala “mkutano mkubwa” wa raia ambao, kama Biblia ilivyotabiri, ni “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha.” (Ufunuo 5:9, 10; 7:9, italiki ni zetu.) Hivyo, wote watawala na raia ni wa kimataifa, watu wa mataifa yote walioungana kwelikweli, ambao wamepata kibali cha kimungu.
Wakikubali utawala wa Mungu, Mashahidi wa Yehova wameshinda kwa kadiri kubwa tatizo la uhalifu miongoni mwao. Kwa njia gani? Kwa kujifunza kung’amua hekima ya kanuni za Biblia, kwa kuzitumia maishani mwao, na kwa kujiacha wachochewe na kani yenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote mzima, roho ya Mungu, na tunda layo—upendo. Neno la Mungu lataarifu hivi: “Jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.” (Wakolosai 3:14) Katika nchi zaidi ya 230, Mashahidi wa Yehova hufuata upendo huo na muungano huo, wakionyesha jinsi Ufalme wa Mungu tayari unachukua hatua za kumaliza uhalifu.
Jambo hilo laweza kutolewa kielezi na matokeo ya uchunguzi fulani wa 1994 ambamo Mashahidi wa Yehova 145,958 katika Ujerumani walihojiwa. Wengi wao walikiri kwamba ilikuwa lazima washinde kasoro kubwa ili wawe Mashahidi. Wao walichochewa wafanye hivyo kwa kujifunza Biblia. Kwa kielelezo, 30,060 walishinda uraibu wa tumbaku au wa dawa za kulevya; 1,437 waliacha kucheza kamari; 4,362 walirekebisha tabia zao zenye jeuri au za uhalifu; 11,149 walishinda vitabia kama wivu au chuki; na 12,820 walirudisha utulivu wa nyumbani katika maisha ya familia iliyovurugika.
Ingawa uchunguzi huo ulihusisha Mashahidi wa Yehova katika nchi moja tu, matokeo hayo ni ya kawaida miongoni mwa Mashahidi ulimwenguni pote. Chukua kielelezo cha Mwukrainia mchanga aitwaye Yuri. Wakati alipoanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, yeye alikuwa sinzia. Hata alikuwa amesafiri kwenda Moscow ambako alijua umati wa watu ungefanya “kazi” yake kuwa rahisi.
Katika 1993, Yuri alirudi Moscow, akiwa miongoni mwa umati wa watu. Lakini hakuna yeyote kati ya wale watu zaidi ya 23,000 waliokuwapo katika Stediamu ya Locomotive mnamo Ijumaa, Julai 23, aliyemwogopa, kwa kuwa sasa alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, Yuri alikuwa jukwaani akishiriki katika programu iliyotolewa mbele ya wasikilizaji wa kimataifa. Akiwa amebadilika kuwa mtu mzuri, yeye hutii agizo hili la Biblia: “Mwibaji asiibe tena.”—Waefeso 4:28.
Wengine wengi kama Yuri wameacha maisha ya uhalifu ili wastahili kupata uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. Hilo lakazia ukweli wa yale Sir Peter Imbert, aliyekuwa zamani ofisa wa polisi wa Uingereza, alisema: “Uhalifu waweza kudhibitiwa haraka sana kila mtu akiwa tayari kujitahidi.” Programu ya elimu ya Biblia inayoandaliwa na serikali ya Mungu huwapa watu wenye mioyo ya kufuatia haki kichocheo cha uhitaji wa “kujitahidi.”
Ulimwengu Usio na Uhalifu
Uhalifu katika njia yoyote ile huonyesha ukosefu wa upendo kwa wengine. Wakristo hufuata kielelezo cha Yesu, aliyesema hivi: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.” Na, “Mpende jirani yako kama nafsi yako.”—Mathayo 22:37-39.
Serikali ya pekee ambayo imejitoa katika kukomesha uhalifu kwa kufundisha watu watii amri hizo mbili ni Ufalme wa Mungu. Leo, zaidi ya Mashahidi wa Yehova milioni tano hunufaika na fundisho hilo. Wao wameazimia wasiache mielekeo yao ya uhalifu ikue mioyoni mwao, wakiwa tayari kufanya dhabihu yoyote ile ihitajikayo ili kuchangia ulimwengu usio na uhalifu. Kile ambacho Mungu ametimiza katika maisha zao chaonyesha kimbele kile ambacho atafanya katika ulimwengu mpya wake chini ya utawala wa serikali yake ya kimbingu. Ebu wazia ulimwengu usio na uhitaji wa polisi, mahakimu, mawakili, au magereza!
Kutimiza jambo hilo ulimwenguni pote kutahusisha badiliko kubwa zaidi la kiserikali katika historia, ambalo litaletwa na Mungu mwenyewe. Danieli 2:44 husema: “Katika siku za wafalme hao [waliopo leo] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [wa kimbingu] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” Mungu pia atamponda Shetani, akimaliza uvutano wake mwovu.—Warumi 16:20.
Wakati serikali ya kimbingu ya Mungu itakapokuwa imechukua mahali pa serikali za kibinadamu, wanadamu hawatatawalana tena. Wafalme wa kimbingu—wafalme ambao hata ni wa juu kuliko malaika—watafundisha wanadamu katika njia ya uadilifu. Kisha, hakutakuwapo tena mauaji, mashambulizi ya gesi za sumu, au mabomu ya maharamia! Ukosefu wa haki katika jamii ambao husababisha uhalifu hautakuwapo tena! Hakutakuwapo tena hali ya kwamba wengine ni matajiri na wengine ni masikini!
Profesa S. A. Aluko, wa Chuo Kikuu cha Obafemi Awolowo katika Nigeria, alisema hivi: “Maskini hawawezi kulala usingizi usiku kwa sababu wao ni wenye njaa; matajiri hawawezi kulala usingizi usiku kwa sababu maskini wako macho.” Lakini karibuni kila mtu ataweza kulala usingizi mnono akijua kwamba serikali—serikali ya Mungu—hatimaye imemaliza uhalifu!
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo zaidi juu ya kile ambacho Ufalme wa Mungu ulicho na jinsi utakavyonufaisha wanadamu wenye kuamini, tafadhali soma kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Aliyekuwa mwizi na mhasiriwa wake, sasa wakiwa wameungana wakiwa ndugu wa Kikristo