Niliimarishwa Kukabili Majaribu Yaliyokuwa Mbele
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA EDWARD MICHALEC
Mkubwa wa polisi wa Wharton, Texas, Marekani, alikuwa mwenye ghadhabu sana. Akinipeleka jela kwa mara ya nne, alisema kwa sauti kubwa: “Kwa nini hutii amri?”
“Nina haki kabisa ya kufanya jambo hili,” nikajibu mara moja. Kusema hivyo kulimghadhabisha mkuu huyo hata zaidi, akaanza kunipiga kwa fimbo. Polisi wengine wakajiunga naye, wakinipiga kwa sehemu za nyuma za bastola zao.
HILO lilitokea karibu miaka 60 iliyopita. Ninapokumbuka, naweza kuona kwamba Yehova Mungu alitumia pindi kama hizo kunizoeza kukabili ugumu wa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova wawili pekee katika Bolivia, ambayo ni nchi ya Amerika Kusini iliyo kubwa kama Ufaransa. Yale niliyojionea yaweza kukusaidia uone jinsi Yehova awezavyo kukuimarisha unapokabili majaribu mbalimbali.
Zamani katika 1936, nilipokuwa nikifanya kazi katika duka la kurekebisha redio katika Boling, Texas, nilisikia kwenye redio hotuba ya Joseph F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society. Hotuba yake ilisimulia juu ya baraka ambazo Ufalme wa Mungu utaletea wanadamu watiifu. Hotuba hiyo ilinivutia sana. (Mathayo 6:9, 10; Ufunuo 21:3, 4) Baadaye nilipata vitabu fulani vya Rutherford katika maktaba yetu ya kibinafsi nikaanza kuvisoma.
Mama yangu wa kambo akawa mwenye hofu kwa kuona kupendezwa kwangu kwa kile alichokiita “hivyo vitabu vyote vya kale vya kidini.” Akavificha na kutisha kuvichoma. Nilipoandikia Watch Tower Society ili nipate maandikisho ya Mnara wa Mlinzi na Golden Age, ambalo ni jina la awali la Amkeni!, Sosaiti ilimwomba William Harper, wa Kutaniko la Wharton lililotoka tu kufanyizwa, anitembelee. Muda si muda, mama yangu wa kambo, ndugu yangu, ndugu-nusu yangu, nami sote tulikuwa tukijifunza Biblia pamoja na Ndugu Harper. Muda si muda, sote tukaonyesha wakfu wetu kwa Yehova kwa ubatizo wa maji.
Katika 1938, Shield Toutjian, mwakilishi asafiriye wa Sosaiti, alizuru nyumbani kwetu katika Boling na kutoa hotuba ya Biblia. Sebule yetu ilijaa pomoni—watu walikuwa wamesimama hata kwenye milango ya kuingia katika vyumba vingine. Ndugu Toutjian alisema kuhusu uvumilivu wa nabii Yeremia katika kuhubiria watu wa wakati wake ajapopingwa na hao. (Yeremia 1:19; 6:10; 15:15, 20; 20:8) Kupitia hotuba kama hizo, Yehova alikuwa anatuimarisha kukabili majaribu ambayo tungepata.
Uamuzi na Matokeo Yao
Muda si muda nikatambua kwamba nilihitaji kufanya uamuzi. Mapema, nilikuwa nimejifunza somo la biashara na nilikuwa ninataka kupata umashuhuri katika ulimwengu wa biashara. Nilikuwa na biashara ya kuuza na kurekebisha redio na pia nilifanya kazi katika kampuni moja ya simu, nikiwekea watu laini za simu. Lakini sasa nilianza kutambua kwamba ufanisi wa kweli maishani unatia ndani kumpendeza Muumba wetu, Yehova Mungu. Hivyo, nikafunga biashara yangu na kutengeneza gari la nyumba. Kufikia Januari 1, 1939, nilikuwa nimejiunga na kikundi cha mapainia, wahudumu wa wakati wote, karibu na mji wa Three Rivers, katika Wilaya ya Karnes, Texas.
Mnamo Septemba 1939, Vita ya Ulimwengu 2 ilizuka Ulaya. Wapinzani wakatwaa fursa hiyo kuchongea Mashahidi wa Yehova. Walidai kwamba sisi tulikuwa majasusi wa muungano wa Ujerumani, Italia, na Japani. Wengi waliamini mashtaka hayo ya uwongo na kuanza kutuletea matatizo. Katika miaka ya mapema ya 1940, nilifungwa jela mara tisa au kumi, kutia ndani wakati uliotajwa hapo juu ambapo yule mkubwa wa polisi na polisi wengine waliponipiga kwelikweli. Ilibidi nitibiwe baada ya kupigwa huko.
Ikatukia kwamba mkubwa huyo huyo wa polisi baadaye alijitolea kumwachilia huru mtu mmoja aliyekuwa ameshtakiwa kucheza kamari isiyo halali iwapo tu mtu huyo angemfanyia jambo fulani—mtu huyo mwenye nguvu, afanyaye kazi ya machimbo ya mafuta, alipaswa kunipiga. Tokeo likawa kwamba siku moja nilipokuwa nikiangusha magazeti barabarani, mtu huyo alinishambulia kwa mnyororo! Polisi fulani walitokea, lakini badala ya kumshika, wakanifunga jela! Baadaye, mtu yule aliyenipiga aliniambia sababu ya kunishambulia na kuomba msamaha.
Masomo Niliyojifunza kwa Majaribu
Kukabili majaribu kama hayo hasa kuliimarisha imani yangu katika Mungu. Kwanza, sikumbuki nikihisi uchungu nilipokuwa nikipigwa, lakini nakumbuka utulivu na amani niliyohisi baadaye. (Matendo 5:40-42) Hivyo, nilijifunza kufanya jinsi mtume Paulo alivyohimiza: “Na tufurahi katika dhiki pia; tukijua ya kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi.” (Warumi 5:3) Baadaye, nilipokumbuka mapigo niliyopokea, niliazimia kwamba kwa msaada wa Yehova sitaruhusu mawakili wa Shetani wanizuie kuhubiri.
Isitoshe, nilijifunza somo jingine muhimu. Maneno yangu yasiyo na busara, “Nina haki kabisa ya kufanya jambo hili,” yalimghadhabisha mkuu wa polisi. Baadaye alinikabili tena, wakati huu akiwa amekasirika kwa sababu Mashahidi hawajihusishi na vita. (Isaya 2:4) Akijaribu kunichokoza, aliuliza: “Kama ungaliitwa kuitumikia nchi yako, je, ungalikubali?”
Kwa vile sasa nilikuwa nimejifunza somo la kutumia busara, nikajibu: “Ikiwa nina hakika ni mapenzi ya Yehova, bila shaka nitaenda.” Jibu hilo liliondosha hasira yake, na hakuna kitu kilichotendeka baada ya hapo.
Napata Mazoezi kwa Ajili ya Kazi Yangu ya Maisha
Jambo kuu maishani mwangu lilikuwa kuhudhuria darasa la tatu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower, katika 1944. Shule hii hutoa mtaala wa miezi mitano wa mazoezi ya kazi ya umishonari. Kabla ya kuhudhuria shule hii, nilikuwa na woga wa kusema mbele ya watu. Lakini kwa kulazimika kutoa hotuba kwa ukawaida mbele ya wanafunzi karibu mia moja, mara nyingi katika ukumbi wa nje, kulinisaidia sana. Mfunzi wetu wa usemaji wa hadharani, Maxwell Friend, angenikatiza na kusema kwa sauti: “Ndugu Michalec, sikusikii!” Na hivyo nikaja kung’amua kwamba kumbe nilikuwa na sauti yenye nguvu.
Baada ya Nathan H. Knorr, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa shule hiyo, kutangaza kwamba mgawo wangu wa umishonari ulikuwa Bolivia, nakumbuka akinishauri kwa upole: “Utapata watu wengi wanyenyekevu huko. Uwe mwenye upendo, subira, na mwenye ufikirio kwao.” Kwa sababu Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa ingali ikiendelea, tulilazimika kungoja kwa muda fulani kabla ya kwenda kwenye migawo yetu. Hatimaye, mnamo Oktoba 25, 1945, Harold Morris—mwanadarasa mwenzangu—na mimi tukafika Uwanja wa Ndege wa El Alto, nje tu ya La Paz, jiji kuu la Bolivia. Basi tukawa Mashahidi wawili pekee katika nchi ya tatu kwa ukubwa katika Amerika Kusini.
Basi lilitusafirisha kutoka uwanja wa ndege, ambao ulikuwa meta 4,100 juu ya usawa wa bahari, hadi jiji kuu, La Paz, ambalo limeenea kotekote katika sakafu na pande za bonde moja kubwa. Ilikuwa vigumu kujipatanisha na kuishi kwenye kimo cha kilometa tatu juu ya usawa wa bahari.
Mianzo Midogo Yenye Fujo
Mara hiyo tukaanza kuzuru watu nyumba hadi nyumba. Wao walikuwa wenye fadhili na wenye saburi kwetu tulipokuwa tuking’ang’ana na Kihispania kidogo tulichojua. Punde tu kila mmoja wetu alikuwa akiongoza kati ya mafunzo 18 hadi 20 ya Biblia ya nyumbani kila juma. Miezi sita baadaye, mnamo Aprili 16, 1946, kikundi kidogo chenye furaha kilikutana na sisi kwa ajili ya mwadhimisho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo. Muda mfupi baadaye, wahitimu wengine wa Gileadi wakafika, kutia ndani Elizabeth Hollins, ambaye baadaye akawa mke wangu.
Muda si muda mimi na Ndugu Morris tukaanza kuzuru majiji mengine, kutia ndani Cochabamba na Oruro, wakati huo yakiwa ya pili na ya tatu kwa ukubwa katika Bolivia. Nilipotoa ripoti kwa Ndugu Knorr kuhusu upendezi tuliopata na fasihi ya Biblia tuliyotolea watu, yeye alipendekeza kwamba tuzuru majiji hayo kila miezi mitatu hivi ili kusaidia wale waliopendezwa. Wengi wa watu hawa wakaribishaji na wenye urafiki baadaye walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova.
Kwa kuwa Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa imekwisha mwaka uliotangulia tu, Bolivia sasa ilikuwa ikipatwa na msukosuko wa kisiasa. Upinzani wa kisiasa na hofu ya kuzuka tena kwa Nazi katika Amerika Kusini zilitokeza maandamano makali barabarani na mauaji. Katika kiangazi cha 1946, rais wa nchi hiyo aliuawa, mwili wake ukaning’inizwa kwenye nguzo ya taa mbele ya makao ya rais. Nyakati nyingine ujeuri ulifanya isiwezekane kwa watu kuondoka nyumbani kwao.
Siku moja Elizabeth alipokuwa akipita baraza kuu la mji kwa basi, aliona vijana watatu ambao walining’inizwa kwenye miti. Kwa ogofyo akatoa sauti ndogo ya kilio. Abiria mwenzake akasema: “Kama hupendi kile unachoona, basi tazama upande mwingine.” Matukio kama hayo yalitukazia uhitaji wa kumtegemea Yehova sana.
Hata hivyo, katikati ya mchafuko huo, kweli ya Biblia ilikuwa imeanza kusitawi katika mioyo yenye unyenyekevu. Katika Septemba 1946, ofisi ya tawi ilifunguliwa katika La Paz, nami nikawekwa kuwa mwangalizi wa tawi. Nyumba tuliyokodi kuwa ofisi ilitumika pia kuwa makao ya mishonari. Miezi michache baadaye, kutaniko la kwanza la Bolivia lilipoanzishwa, nyumba iyo hiyo pia ikatumika ikiwa mahali petu pa kukutania.
Katika 1946 tulianza pia kuwa na hotuba za watu wote. Tulipata jumba la Maktaba ya Manispaa mjini La Paz kwa hotuba ya kwanza. Mtu mmoja kutoka Yugoslavia mwenye urafiki alilipia tangazo katika gazeti ili kutangaza hiyo hotuba. Jumba hilo lilijaa sana. Kwa kuwa bado nilikuwa niking’ang’ana na Kihispania, nilikuwa na wasiwasi mwingi sana kuhusu kutoa hotuba hiyo. Lakini kwa msaada wa Yehova, mkutano huo ulifanikiwa. Ikawa kwamba hiyo ilikuwa hotuba ya kwanza kati ya nne zilizotolewa katika jumba hilo.
Katika 1947 tulipokea mishonari wengine sita kutoka Gileadi, na wengine wanne katika 1948. Nyumba ambazo tuliweza kukodi hazikuwa na vifaa vya kisasa. Mbali na kudumisha ratiba yetu ya mishonari yenye shughuli nyingi, sisi mishonari wa mapema hatimaye tulilazimika kufanya kazi ya nusu wakati ili kupata fedha za kununua nguo za kubadili na zetu zilizokuwa zimechakaa. Kusafiri jiji hadi jiji kulikuwa kugumu pia. Mara nyingi, nilisafiri kupitia vipito vya milima yenye baridi nikiwa nimebebwa nyuma ya lori. Lakini Yehova aliendelea kutupa kitia moyo chenye kuimarisha kupitia tengenezo lake.
Katika Machi 1949, Ndugu Knorr na mwandishi wake, Milton Henschel, walikuja kutoka New York na kuzuru makao yetu matatu ya mishonari, katika La Paz, Cochabamba, na Oruro. Lilikuwa jambo la kutia moyo kama nini kusikia juu ya maongezeko makubwa katika nchi nyingi na juu ya Makao ya Betheli na majengo ya kuchapa yaliyokuwa yakijengwa kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn! Ndugu Knorr akapendekeza kwamba tuwe na makao na Jumba la Ufalme sehemu iliyo katikati zaidi katika La Paz. Akatuambia pia kwamba bado kuna mishonari wengine watakaoletwa.
Baadaye katika 1949, tulifanya kusanyiko letu la kwanza la mzunguko, katika jiji la Oruro. Ilitia moyo kwa wengi wa ndugu na dada zetu wapya wa Kikristo kukutana kwa mara ya kwanza. Kufikia wakati huo Bolivia ilikuwa na kilele kipya cha watangazaji wa Ufalme 48 nayo ilikuwa na makutaniko matatu.
Mwenzi Wangu Mwaminifu
Kwa sababu ya kushiriki miaka mingi ya utumishi wa mishonari tukiwa pamoja, Elizabeth nami tukaja kujuana na kupendana. Hatimaye, tukafunga ndoa katika 1953. Alikuwa ameanza huduma ya upainia katika Januari 1939, sawa tu na mimi. Miaka hiyo ya mapema ya upainia ilikuwa migumu kwake vilevile. Kwa sababu ya kuhubiri kwake kwa moyo mkuu, yeye pia alifungwa gerezani, akitembezwa barabarani kama mhalifu wa kawaida.
Elizabeth akiri kwamba aliogopa aliposhiriki katika maandamano ya kubeba mabango ambayo yaliandikwa: “Dini Ni Mtego na Hila.” Lakini alifanya jambo ambalo tengenezo la Yehova lilikuwa limetuagiza kufanya wakati huo. Kama alivyosema, alifanya hivyo kwa Yehova. Mambo hayo aliyojionea yalimwimarisha kwa ajili ya majaribu ambayo alivumilia katika miaka hiyo ya mapema katika Bolivia.
Migawo Mbalimbali
Kwa miaka kadhaa baada ya kufunga ndoa, tulitumia muda wetu mwingi katika kazi ya kusafiri. Hatukuzuru yale makutaniko manne tu katika Bolivia bali pia tulizuru vikundi vya mbali vya watu wenye kupendezwa na vilevile kila mji wenye watu zaidi ya 4,000. Kusudi letu lilikuwa kupata na kukuza upendezi wowote katika kweli ya Biblia miongoni mwa watu walioishi katika sehemu hizo. Lilikuwa jambo la kusisimua kuona kwamba kufikia katikati ya miaka ya 1960, makutaniko yalikuwapo katika karibu miji yote midogo ambayo tulikuwa tumezuru miaka kumi hivi iliyopita.
Kwa wakati huo, nilikuwa na matatizo ya afya ambayo yalizidishwa na mwinuko wa juu wa La Paz. Hivyo, katika 1957 ndugu mwingine akachukua daraka la kusimamia tawi, na Elizabeth nami tukapewa mgawo wa kwenda katika makao ya mishonari katika Cochabamba, jiji lililo katika bonde na ambalo lilikuwa chini zaidi. Katika mkutano wetu wa kwanza, ni mishonari wachache tu waliokuwapo bila Mbolivia mwenyeji hata mmoja. Kufikia wakati tulipoondoka Cochabamba miaka 15 baadaye, katika 1972, kulikuwa na makutaniko mawili. Sasa kuna makutaniko 35 yenye watangazaji wa Ufalme 2,600 katika bonde la Cochabamba!
Katika 1972 tulihamia Santa Cruz katika nyanda za chini za kitropiki. Tungali tunaishi hapa katika vyumba kadhaa vilivyoko juu ya Jumba la Ufalme. Tulipofika, Santa Cruz pia lilikuwa na makutaniko mawili, lakini sasa kuna zaidi ya 45, kukiwa na watangazaji zaidi ya 3,600 wanaoshiriki katika huduma ya Kikristo.
Tulifurahi kama nini kwamba tulibaki kwenye mgawo wetu wa mishonari katika miaka hii izidiyo 50 na kuona kukusanywa kwa watu wa Yehova wapatao 12,300 katika nchi hii! Kwa kweli tumefurahi sana kutumikia wapendwa hao.
Maisha Yenye Furaha ya Kutumikia Wengine
Kabla ya kwenda kwenye mgawo wangu wa mishonari, mshauri wa mambo ya kisheria wa Watch Tower Society, Hayden C. Covington, anayetoka Texas kama mimi, alisema: “Ed, katika Texas tulikuwa na nafasi nyingi. Lakini katika makao ya mishonari, mtasongamana. Itamaanisha kufanya mabadiliko.” Alisema kweli. Ni vigumu kuishi na wengine kwa ukaribu, na ni mojawapo tu ya magumu mengi ambayo mishonari wa Kikristo hupata.
Basi, ukifikiria kwenda mbali na nyumbani ili kumtumikia Yehova katika eneo jingine, kumbuka kwamba maisha ya mfuasi wa kweli wa Kristo ni yale ya kutumikia wengine. (Mathayo 20:28) Basi, mishonari anapaswa kujitayarisha kiakili ili kuishi maisha ya kujinyima. Wengine waweza kuwazia kwamba wao watapata umashuhuri. Labda watapata—wanapowaaga marafiki na watu wa ukoo nyumbani. Lakini hayo hupotea mtu afikapo katika mji mdogo au katika sehemu ya jiji yenye umaskini ambayo itakuwa mgawo wake. Natoa shauri gani?
Unapokabili magumu, kama vile matatizo ya afya, hisi za kuwa mbali na familia yako, au labda magumu ya kupatana na ndugu zako wa Kikristo katika mgawo, kubali hayo yote kuwa sehemu ya mazoezi yako. Ukifanya hivyo, baadaye utathawabishwa, kama mtume Petro alivyoandika: “Mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu.”—1 Petro 5:10.
Edward Michalec alikufa Julai 7, 1996, wakati wa matayarisho ya mwisho ya kuchapisha gazeti hili.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Katika Bolivia 1947
[Picha katika ukurasa wa 20, 21]
Masomo ya usemaji wa hadharani yalifanywa nje mara nyingi, kama ionyeshwavyo katika picha hii ya baadaye ya ukumbi wa nje wa Gileadi
[Picha katika ukurasa wa 23]
Nikiwa na mke wangu