Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 1/8 kur. 6-9
  • Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Pupa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Pupa
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Fanya Uwezayo Chini ya Hali Zilizoko
  • Epuka Kuambukizwa na Pupa
  • Usikate Tumaini Kamwe la Kuokolewa
  • Endeleeni Kuepuka Mtego wa Pupa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Fanikiwa Katika Kuepuka Mtego wa Pupa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Wazia Ulimwengu Usio na Pupa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Enzi ya Pupa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 1/8 kur. 6-9

Kuishi Katika Ulimwengu Wenye Pupa

“NAWEZA kuendeleaje kuishi?” James Scott alikabili swali hilo alipopotea kabisa katika Milima ya Himalaya. Alikuwa katika hatari kubwa ya kuganda au kufa njaa. Alikumbuka kuona watu katika mashindano ya karate “wakipoteza nguvu polepole, kila pigo likiwadhoofisha, mpaka . . . wakawa wasioweza kujikinga kabisa.” Akasema: “Ndivyo nilivyohisi nilipokuwa nikifunga mfuko wangu wa kulala na kula theluji kwa udhaifu. Roho yangu ya kuendelea kuishi ilikuwa imekwisha na tamaa yangu ya kuishi kutokomea. Sikuwa nimepata kuhisi hoi hivyo kamwe.”—Lost in the Himalayas.

Leo, kwa maana fulani, wengi wako kama yeye—wamenaswa katika ulimwengu ambao umedhibitiwa na pupa. Unaweza kuhisi kwamba unadhoofika polepole na kushindwa. Ni watu wachache wawezao kuepa kabisa athari za moja kwa moja za pupa. Ikitegemea mahali uishipo duniani, matatizo unayokabili hutofautiana kabisa—pupa huathiri watu katika nchi zinazoendelea kwa njia tofauti kabisa na wale wanaoishi katika mataifa matajiri. Hata hivyo, hata magumu yawe yapi, labda unaweza kujifunza jinsi ya kuishi bila kudhoofika kimwili, kihisia-moyo, na kiroho mpaka upate kuokolewa. Kwa njia gani? Kwa kufuata shauri la msingi la wataalamu wa kuishi kwa magumu.

Mambo mawili yanajitokeza katika shauri lao. Jambo la kwanza ni kuepuka kuzidisha hali ambayo tayari ni mbaya. “Mbinu yako,” chasema The Urban Survival Handbook, “ni lazima iwe kuepuka hatari zisizo za lazima . . . na kupunguza madhara yasababishwayo na hatari hizo ambazo huwezi kuepuka.” Jambo la pili—na labda lililo muhimu zaidi—linahusu mtazamo. “Kuendelea kuishi,” chasema The SAS Survival Handbook, “kunahusu mtazamo wa akili kama ulivyo uvumilivu wa kimwili na ujuzi.”

Fanya Uwezayo Chini ya Hali Zilizoko

“Mtu fulani huuawa kimakusudi Marekani kila dakika 22, hunyang’anywa kitu kimabavu kila sekunde 47 na kushambuliwa vibaya kila sekunde 28,” chasema Staying Alive—Your Crime Prevention Guide. Katika hali kama hizo, unaweza kufanya nini? Angalau, unaweza kujaribu kuepuka kuwa katika hali iliyo rahisi kushambuliwa. Uwe macho na mwenye busara. Fanya uwezalo ili kupunguza hatari.a

Kwa mfano, usifanye hali kuwa mbaya zaidi kwa kuwa zuzu. Gazeti The New York Times laripoti kwamba asilimia 18 ya Wamarekani hukiri kudanganywa—wakihadaiwa maelfu ya dola na watu wasio wanyoofu ambao huwawinda watu walio rahisi kudanganywa. Mara nyingi wahasiriwa ni wale wenye umri mkubwa kama mjane mmoja mwenye umri wa miaka 68 ambaye alinyang’anywa dola 40,000. Jambo alilojionea lilitokeza kichwa hiki kikuu: “Ukiwa na Mvi, Walaghai Waona Noti.”

Lakini si lazima uwe mhasiriwa mwingine asiye na hatia anayengoja tu kutumiwa vibaya. Kitabu Staying Alive chatuonya: “Jihadhari na mbwa-mwitu mwenye ngozi ya kondoo.” Nyanya mmoja mwenye umri wa miaka 70 alitii shauri hilo. Alipata toleo la bima la kulipia gharama zake za tiba, kwa gharama ya dola kumi kila mwezi. “Jambo tu ambalo nyanya huyo alihitaji kufanya,” yasema ripoti hiyo, “lilikuwa ni kumpa huyo mwuzaji wa bima dola 2,500 kwanza.” Hakufanya hivyo. Kwa kupigia simu kampuni hiyo ya bima, aligundua kwamba mtu yule alikuwa laghai. “Alipokuwa akimtilia huyo mwuzaji wa bima kikombe cha pili cha chai, polisi walifika na kumkamata.”

Kufanya yote uwezayo ili kujilinda ni shauri sahili litolewalo katika Biblia. “Mjinga huamini kila neno; bali mwenye busara huangalia sana aendavyo.” (Mithali 14:15; 27:12) Wengi hupuuza Biblia kuwa ya kale na isiyotumika. Lakini shauri layo lenye kutumika laweza kukusaidia uendelee kuishi. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika: “Hekima [kama ile ipatikanayo katika Biblia] ni ulinzi, kama vile fedha ilivyo ulinzi; na ubora wa maarifa ni ya kwamba hekima humhifadhi yeye aliye nayo.”—Mhubiri 7:12.

Wasomaji wengi wa Amkeni! wameona ukweli huo. Kwa mfano, wengine wamepata ulinzi kwa kadiri fulani kwa kupiga mayowe wanapotishwa kubakwa au na ujeuri mwingine, kwa kupatana na yale yanayotajwa kwenye Kumbukumbu la Torati 22:23, 24. Wengine wametii shauri la Biblia la kuepuka kabisa chochote “ambacho kinachafua ama mwili ama roho.” (2 Wakorintho 7:1, The Twentieth Century New Testament) Kwa kufanya hivyo wamejilinda dhidi ya wachuuzi wa tumbaku na dawa za kulevya, ambao hujitajirisha kwa madhara ya afya ya watu. Wasomaji wengi pia wameepuka mitego ya wahubiri wa televisheni wenye kuchuma pesa na wanasiasa wenye pupa ya kutaka mamlaka. (Ona sanduku, ukurasa 7.) Soma Biblia. Unaweza kushangaa kuona kiasi cha msaada wenye kutumika ambacho Biblia hutoa.

Epuka Kuambukizwa na Pupa

Bila shaka, kuna hatari nyingine ya pupa—wewe mwenyewe waweza kuwa na pupa. Hiyo itakunyang’anya sifa zako nzuri za maadili ambazo hutofautisha mwanadamu na hayawani. Akifafanua hali ya biashara ya jinyakulie uwezavyo ambayo katika hiyo wafanyabiashara walikuwa wakinyakua chochote wawezacho, mchunguzi mmoja alinukuliwa akiwa akisema: “Nguruwe hao walikuwa wakila kwelikweli. Kiwango cha pupa . . . hakikudhibitiwa.” Yaelekea hilo ni tukano kwa nguruwe kuliko kwa mabwanyenye wa kibiashara! Hakika wao walionekana kupuuza shauri zuri lililotolewa na Yesu Kristo: “Fulizeni kufungua macho yenu na mlinde dhidi ya kila namna ya tamaa.”—Luka 12:15.

Yesu Kristo aliwapa shauri hilo kwa sababu alijua jinsi unavyoweza kujidhuru ukiwa mwenye pupa. Tamaa ya kuwa na vitu vya kimwili—na pia, bila shaka, tamaa ya mamlaka au ngono—yaweza kuwa ndiyo hamu yako kuu, ikikunyang’anya wakati wowote au mtazamo wowote ambao huenda ukawa nao wa kushughulika na watu au kushughulikia maadili ya kiroho. “Pesa,” asema Anthony Sampson katika kitabu chake The Midas Touch, “imepata sifa nyingi za dini.” Kwa njia gani? Pesa imekuwa mungu. Kila kitu kinadhabihiwa kwenye madhabahu ya pupa na mapato. Jambo kubwa ni faida. Faida kubwa ndiyo nzuri zaidi. Hata hivyo, jambo la hakika ni kwamba hata utumie muda gani, pupa ya vitu vya kimwili hairidhishwi kamwe. Mhubiri 5:10 lasema hivi: “Apendaye fedha hatashiba fedha, wala apendaye wingi hatashiba nyongeza.” Vivyo hivyo, “apendaye” mamlaka, mali, au ngono hatashiba, hata apate kiasi kingi kadiri gani.

Usikate Tumaini Kamwe la Kuokolewa

Jambo moja muhimu la kuokoka ni kudumisha mtazamo mzuri wenye matumaini. Nyakati nyingine huwezi kufanya chochote kuepuka athari ya watu wenye pupa. Kwa mfano, mara nyingi watu wenye njaa hawawezi kuepuka hali inayowapata wakati huo. Lakini usife moyo; usikubali kushindwa. “Ni rahisi kujiachilia ushindwe, uporomoke na kushindwa na hali ya kujisikitikia” unapokabiliwa na mazingira makali yaliyo hatari, chasema The SAS Survival Handbook. Usishindwe na mawazo na hisia moyo zisizofaa. Unaweza kushangaa kwa jinsi unavyoweza kuvumilia. “Wanaume kwa wanawake wameonyesha kwamba wao wanaweza kuishi katika hali mbaya zaidi,” chasema kitabu hichohicho. Walifauluje? Wao waliendelea kuishi, kitabu hicho chasema, “kwa sababu ya azimio lao la kuendelea kuishi.” Azimia kutoshindwa na mfumo huu wenye pupa.

James Scott, aliyetajwa mapema, hatimaye aliokolewa kutoka kile ambacho kingekuwa kaburi lake la Himalaya. Alisema kwamba jitihada yake ya kuendelea kuishi ilimfundisha angalau somo moja muhimu. Somo gani? “Hakuna ugumu wowote maishani ambao hauwezi kukabiliwa,” akasema. Tim Macartney-Snape, mpanda mlima mwenye uzoefu aliyeshangaa kwamba James Scott aliweza kuendelea kuishi muda mrefu hivyo hata akapatikana akiwa angali hai, pia alipata somo. Yeye alisema: “Maadamu kuna dalili yoyote ya tumaini, usife moyo kamwe.” Kwa hiyo, hata hali ionekane mbaya jinsi gani, utafanya mambo yawe mabaya zaidi ukipoteza tumaini. Usipoteze tumaini la kuokolewa.

Lakini je, kuna “dalili [yoyote] ya tumaini,” uwezekano wowote halisi wa kuokolewa kutoka kwa ulimwengu uliokolea pupa? Je, kweli watu wenye pupa ambao wanaharibu dunia hii na kuangamiza mabilioni ya uhai watapata kuondolewa? Kwa kweli, kuna tazamio hakika la kuokolewa. Fikiria jibu la Biblia katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Jeuri—Wewe Waweza Kujikinga,” katika toleo la Amkeni! la Januari 8, 1990, kurasa 7-10.

[Sanduku katika ukurasa wa 7]

Maonyo ya Biblia ya Wakati Ufaao

Mithali 20:23 “Vipimo mbalimbali ni chukizo kwa BWANA; tena mizani ya hila si njema.”

Yeremia 5:26, 28 “Katika watu wangu wameonekana watu waovu; huotea kama vile watu wategao mitego; hutega mtego, na kunasa watu. Wamewanda sana, wang’aa; naam, wamepita kiasi kwa matendo maovu; hawatetei madai ya yatima, ili wapate kufanikiwa; wala hawaamui haki ya mhitaji.”

Waefeso 4:17-19 “Kwa hiyo, nasema hili na kutoa ushahidi katika Bwana, kwamba nyinyi msiendelee tena kutembea kama vile mataifa watembeavyo pia katika ukosefu wa faida wa akili zao, huku wao wakiwa katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu, kwa sababu ya kule kutokuwa na ujuzi ambako kumo ndani yao, kwa sababu ya ukosefu wa hisi wa mioyo yao. Wakiisha kuishiwa na hisia zote za adili, walijikabidhi wenyewe kwenye mwenendo mlegevu ili wafanye ukosefu wa usafi wa kila namna pamoja na pupa.”

Wakolosai 3:5 “Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili wenu vilivyo juu ya dunia kwa habari ya uasherati, ukosefu wa usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya sanamu.”

2 Timotheo 3:1-5 “Lakini jua hili, kwamba katika siku za mwisho nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo zitakuwa hapa. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wapenda-fedha, wenye kujitanguliza, wenye kiburi, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio waaminifu-washikamanifu, wasio na shauku ya kiasili, wasiotaka upatano wowote, wachongezi, wasio na hali ya kujidhibiti, wakali, wasio na upendo wa wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kututumuka kwa kiburi, wenye kuzipenda raha badala ya kuwa wapenda-Mungu, wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakithibitika kuwa si kweli kwa nguvu ya hiyo; na geukia mbali kutoka kwa hawa.”

2 Petro 2:3 “Pia, kwa tamaa watawatumia nyinyi kujifaidi kwa maneno bandia. Lakini kuwahusu wao, hukumu ya tangu zamani za kale haiendi polepole, na uangamizo wao hausinzii.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki