Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 2/8 kur. 18-21
  • Kupanda kwa Machozi, Kuvuna kwa Shangwe

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kupanda kwa Machozi, Kuvuna kwa Shangwe
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Wakati wa Shangwe
  • Wakati wa Machozi
  • Nguvu kwa Machozi
  • Shangwe Upya
  • Shangwe Zaidi Baada ya Machozi Mengi
  • Masomo Ambayo Nimejifunza
  • Mkaribie Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Katika Masikio ya Kitoto
    Amkeni!—1997
  • “Kwa Kuwa Tuna Huduma Hii . . . , Hatuachi”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1995
  • Jinsi Nilivyonufaika Kutokana na Utunzaji wa Mungu
    Amkeni!—1995
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 2/8 kur. 18-21

Kupanda kwa Machozi, Kuvuna kwa Shangwe

“FURAHIA kustaafu kwako katika Hispania yenye jua!” Mamilioni ya Wanaulaya wamekubali toleo hili lenye kuvutia na kuhamia huko. Nilipofika umri wa miaka 59, mimi pia niliamua kuuza kila kitu na kuhama Uingereza kwenda Hispania, lakini nilikuwa nikitafuta kitu kingine zaidi ya jua na raha.

Nilichagua kwenda Santiago de Compostela—moja ya majiji yenye mvua zaidi ya Hispania—kwa kuwa lengo langu lilikuwa kutumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote badala ya kupumzika juani. Miaka 22 mapema, hali zilikuwa zimenilazimisha kuacha utumishi wangu wa kueneza evanjeli katika Hispania, ambapo nilikuwa nimekwenda kutumikia kwa sababu uhitaji wa utumishi huo ulikuwa mwingi zaidi huko. Sikuzote ilikuwa nia yangu kurudi, na sasa hatimaye nilifaulu.

Lakini badiliko hilo halikuwa rahisi kama nilivyofikiri. Mwezi wa kwanza ulikuwa wenye kuogofya! Sikumbuki hata nikipata kuchoka sana maishani kama nilivyochoka wakati huo. Nilikuwa nikiishi katika nyumba iliyokuwa orofa ya tano, na hakukuwa na lifti. Kila siku nilikokoteza miguu kupanda na kushuka barabara zenye milima za Santiago, nikipanda ngazi nyingi katika jitihada yangu ya kuhubiri habari njema kwa watu wengi kadiri nilivyoweza. Baada ya mwezi huo wenye kuchosha, nilianza kushambuliwa na shaka. Je, nilikuwa nimefanya uchaguzi ufaao? Je, nilikuwa nimezeeka sana nisiweze utendaji wa aina hii?

Hata hivyo, katika mwezi wa pili, nilipata kwamba nguvu zangu zilikuwa zikinirudia. Ilikuwa karibu kama nguvu mpya za mkimbiaji wa mwendo mrefu. Kwa hakika, niliingia katika moja ya vipindi vyenye furaha sana katika maisha yangu. Nilianza kupata shangwe ya kuvuna, baada ya miaka ya kupanda kwa machozi. (Zaburi 126:5) Acheni nieleze.

Wakati wa Shangwe

Mke wangu Pat nami tulihamia Hispania katika 1961. Wakati huo, utendaji wa Mashahidi wa Yehova haukutambuliwa rasmi huko. Hata hivyo, mgawo wetu wa kuhubiri ulikuwa jiji lenye jua sana la Seville, ambapo ni 25 tu waliokuwa wakishiriki katika kazi ya kuhubiri.

Katika huduma yetu siku moja, nilizungumza na Mfaransa mmoja ambaye alikuwa akipaka nyumba rangi. Siku iliyofuata bibi mmoja akatujia mimi na mke wangu na kutuuliza ikiwa tulikuwa tumezungumza na mpaka-rangi siku iliyotangulia. Yeye alisema kwamba huyo alikuwa mume wake, Francisco. Alikuwa amempa ufafanuzi sahihi sana hivi kwamba aliweza kututambua mara moja. “Yeye yuko nyumbani sasa ikiwa mwataka kumtembelea,” akatuarifu.

Tulikubali mara hiyo mwaliko huo, na muda si muda familia yote ilikuwa ikijifunza Biblia pamoja nasi. Wakati fulani baadaye, Francisco alirudi Ufaransa kwa sababu za kiuchumi. Tulikuwa na wasiwasi. Je, angepoteza uwasiliano na Mashahidi? Hata hivyo, mara tu baada ya kuondoka kwake, tulipokea barua kutoka kwake ambayo ilituliza akili zetu. Alisema kwamba mkubwa wake mpya alikuwa amemwuliza ni dini ngapi ziko Hispania.

“Kuna mbili, Katoliki na ya Protestanti,” Francisco akaeleza kwa hadhari. Kwa kuwa kazi yetu haikuwa imetambuliwa kisheria, alifikiri halingekuwa jambo la hekima kusema zaidi.

“Una hakika?” mkubwa wake akamwuliza.

“Kwa hakika, kuna tatu,” Francisco akajibu, “nami niko katika ile ya tatu—Mashahidi wa Yehova.”

“Nafurahi kusikia hivyo,” akaitikia mkubwa wake. “Mimi ni mtumishi katika kutaniko lako!” Jioni hiyo hiyo Francisco alikuwa katika mkutano wa kutaniko wa Mashahidi wa Yehova.

Katika 1963 tulihamishwa kutoka Seville hadi Valencia, na muda mfupi baada ya hapo, hadi Barcelona. Huko nilizoezwa kutumikia nikiwa mhudumu asafiriye. Kisha, tukarudishwa Valencia kutumikia katika kazi ya kusafiri katika eneo hilo. Lakini baada ya miaka miwili katika eneo hili zuri la utendaji, Pat alianza kuwa na tatizo kudumisha usawaziko wake. Muda si muda, alishindwa kutembea. Hivyo ukaanza wakati ambapo ‘tulipanda kwa machozi.’—Zaburi 126:5.

Wakati wa Machozi

Kwa kusita, tuliondoka Hispania ili kupata matibabu Uingereza. Kisababishi cha dalili za maradhi ya Pat? Multiple sclerosis, maradhi yenye kudhoofisha ambayo pole kwa pole huendelea kumfanya mtu asijiweze. Baada ya muda fulani, kwa sababu ya athari za kando na matatizo yaliyohusiana nazo, tokeo laweza kuwa kifo.

Ilikuwa vigumu sana kwetu kurekebisha maisha zetu na kukubali uhalisi wa maradhi haya. Lakini kupitia yote hayo, tulijifunza ukweli wa maneno ya mtunga-zaburi: “BWANA atamtegemeza [amkumbukaye mnyonge] alipo mgonjwa kitandani.”—Zaburi 41:3.

Kwa miaka kumi hivi, tulihamia nyumba moja hadi nyingine. Pat hakupenda kelele, na tulikuwa tukijaribu kutafuta mahali pa kuishi pafaapo kwa ajili yake—ambapo hatimaye tulitambua haiwezekani kupapata. Pat alilazimika kuzoea kutumia kiti chenye magurudumu. Ingawa aliweza kupika na kufanya kazi nyinginezo nyingi, alishuka moyo kwa sababu ya kutoweza kutembea. Kwa kuwa alikuwa mtu mwenye utendaji mwingi mbeleni, alipata kwamba kutojiweza huku daima kulikuwa chanzo cha mkazo wa kihisia-moyo.

Nguvu kwa Machozi

Nilijifunza jinsi ya kumsaidia Pat kuinuka, kuketi, kuvaa, kujiosha, na kuingia na kutoka kitandani. Kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida kulikuwa tatizo kweli. Kulihitaji jitihada kubwa ya kujitayarisha. Lakini tulijua kwamba njia pekee ya kutusaidia kudumu tukiwa wenye nguvu kiroho ilikuwa kushirikiana na ndugu zetu Wakristo.

Kwa miaka 11 nilimtunza Pat nyumbani, huku nikifanya kazi nikiwa mwandishi wa ramani wakati wa mchana. Hatimaye, tulitambua kwamba kwa sababu ya kuzorota kwa afya yake, alihitaji utunzi wa pekee ambao singeweza kuuandaa. Kwa hiyo alikaa hospitalini katikati ya juma, nami nilikuwa nikimtunza nyumbani mwisho-juma.

Kila Jumapili baada ya chakula cha mchana, nilimpeleka Pat kwenye Mkutano wa Watu Wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi, ambayo kwa wakati huu ndiyo ilikuwa mikutano aliyoweza kuihudhuria. Baadaye, nilimrudisha hospitalini. Kawaida hiyo ilikuwa yenye kunichosha sana, lakini ilistahili, kwa kuwa ilimfanya Pat aendelee kuwa mwenye nguvu kiroho. Nyakati fulani nilijiuliza ningeendelea kuvumilia hadi lini, lakini Yehova alinipa nguvu ya kuendelea. Kila Jumamosi asubuhi nilikuwa nikiongoza kikundi kwenda katika kazi ya kuhubiri kabla ya kumchukua Pat kutoka hospitali. Nilipata kwamba katika wakati huo wenye kufadhaisha, kawaida yangu ya Kikristo ilinisaidia kuendelea.

Wakati uleule, Pat alikuwa akifanya alichoweza ili kuhubiri habari njema. Hospitalini aliweza kuanzisha mafunzo mawili ya Biblia pamoja na wauguzi waliokuwa wakimtunza. Mmoja, aliyeitwa Hazel, alifanya maendeleo kufikia hatua ya kujiweka wakfu kwa Yehova. Kwa kuhuzunisha, Pat hakuweza kuhudhuria ubatizo wa Hazel kwa sababu alikufa muda mfupi kabla ya hapo, Julai 8, 1987.

Kifo cha Pat kilikuwa wakati wa kutuliza na vilevile wakati wa huzuni. Kilikuwa kitulizo kuona mwisho wa kuteseka kwake, lakini nilihisi huzuni nyingi kwa kumpoteza mwandamani wangu. Kifo chake kiliacha utupu mkubwa.

Shangwe Upya

Ingawa laweza kuonekana kuwa jambo la kushangaza, Pat nami tulikuwa tayari tumeamua kile ambacho ningefanya baadaye. Kwa kuwa sote tulijua kwamba uhai wake ulikuwa unakaribia mwisho, tulizungumza kuhusu jinsi ambavyo ningeweza kumtumikia Yehova vyema zaidi baada ya kifo chake. Uamuzi wetu sote wawili ulikuwa kwamba nirudi Hispania, mgawo tuliolazimika kuacha.

Miezi mitatu baada ya kifo cha Pat, nilisafiri hadi kwenye ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Hispania ili kujua ni wapi ningetumikia vyema zaidi. Nilipokea mgawo nikiwa mhudumu painia wa pekee na kupewa eneo la jiji la kale, lenye mvua nyingi la Santiago de Compostela.

Muda mrefu haukupita, nikapata barua kutoka ofisi ya tawi, ikinipa anwani ya mtu mwenye kupendezwa aliyeitwa Maximino. Baada ya kujaribu kumtafuta nyumbani kwa majuma matatu, hatimaye nikakutana naye. Maximino, ambaye alikuwa msafishaji katika hospitali moja ya hapo, alikuwa amepata trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani na alikuwa ameomba kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani.a Nilipomtembelea, tayari alikuwa amekisoma kitabu hicho mara tatu. Aliomba radhi kwa kutosoma Biblia sana—‘sehemu ya kale’ mara moja tu na ‘sehemu mpya’ mara mbili. Alifanya usomaji wote huo alipokuwa akingoja mtu amtembelee.

Aliniambia pia kwamba alikuwa amekwenda kwenye Jumba la Ufalme akiwa na nia ya kuhudhuria mmoja wa mikutano yetu. Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa mwenye haya sana, hakuwa ameingia katika mahali pa kukutania. Nilianza kujifunza Biblia naye, naye akahudhuria mikutano juma lilo hilo. Alikubali kweli kwa hamu, lakini alikuwa na tatizo kweli kupigana na uraibu wake wa tumbaku. Kwa msaada wa Yehova, aliweza hatimaye kuacha zoea la kuvuta tumbaku, na sasa ni Shahidi aliyebatizwa.

Shangwe Zaidi Baada ya Machozi Mengi

Mwaka mmoja tu baada ya kurudi Hispania, nilialikwa nitumikie nikiwa mwangalizi asafiriye tena. Lakini kabla ya kuchukua mgawo huo, maisha yangu yalipata badiliko lisilotazamiwa. Nilikutana na painia aliyeitwa Paquita, ambaye alikuwa akitumikia karibu na Santiago. Alikuwa mjane ambaye alikuwa amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka mingi. Muda si muda tukagundua kwamba tulipatana katika mambo mengi. Katika 1990, miezi sita tu baada ya kuanza kazi ya kusafiri, tulioana—shangwe tena.

Kama mimi, Paquita alikuwa ‘amepanda kwa machozi.’ Mgawo wake wa kwanza akiwa painia wa pekee uliharibiwa na msiba. Walipokuwa wakihamisha fanicha kuelekea Orense, makao yao mapya, mume wake alikufa katika aksidenti ya gari—lori lililokuwa likija lilivuka kuingia upande wake. Paquita na binti yake mwenye umri wa miaka kumi tayari walikuwa Orense walipopata habari ya kifo chake. Japo potezo hilo baya, siku mbili baada ya maziko, Paquita alianza mgawo wake kama ilivyopangwa.

Kwa miaka hiyo yote, Paquita aliendelea katika utumishi wa wakati wote. Kisha, msiba ukapiga tena. Aksidenti nyingine ya gari ikamwua binti yake, ambaye wakati huo alikuwa na umri wa miaka 23. Maumivu yalikuwa mengi, na kipindi cha kuomboleza kikawa kirefu. Kama wakati uliopita, kawaida yake ya Kikristo na utegemezo aliopata kutoka kwa Wakristo wenzake ulimsaidia sana kupata nafuu. Nilijuana na Paquita katika 1989, miaka miwili tu baada ya kifo cha binti yake.

Tangu tufunge ndoa katika 1990, tumetumikia katika kazi ya kusafiri katika Hispania. Ingawa miaka hii michache iliyopita imekuwa mojawapo vipindi vyenye kuridhisha sana vya maisha zetu, hatuna majuto kwamba tulipitia majaribu. Tuna hakika kwamba yametufinyanga katika njia chanya.—Yakobo 1:2-4.

Masomo Ambayo Nimejifunza

Naamini kwamba hata majaribu makali sana yana sehemu zifaazo, kwa sababu hayo hutufunza masomo. Juu ya yote, majaribu yamenifunza umuhimu wa hisia-mwenzi, sifa muhimu sana kwa mwangalizi Mkristo. Kwa kielelezo, muda mrefu haujapita tangu nilipoongea na ndugu Mkristo ambaye ana mwana asiyejiweza. Nilifahamu kikamili jitihada kuu aliyokuwa akifanya kila juma kwa kumpeleka mwana wake katika mikutano yote. Baada ya mazungumzo yetu, alinishukuru na kusema ilikuwa mara ya kwanza kwamba mtu alifahamu kikweli magumu waliyokuwa wakikabili yeye na mke wake.

Somo jingine muhimu nililojifunza ni kumtegemea Yehova. Mambo yote yanapokwenda shwari, twaweza kuelekea kutegemea nguvu na uwezo wetu wenyewe. Lakini jaribu kali liendeleapo mwaka baada ya mwaka na huwezi kukabiliana nalo kwa nguvu zako mwenyewe, unajifunza kumtegemea Yehova. (Zaburi 55:22) Mkono wa Mungu wenye kusaidia uliniwezesha kuendelea.

Bila shaka, hilo halimaanishi kwamba mambo yalikuwa shwari sikuzote. Ni lazima nikiri kwamba wakati wa ugonjwa wa mke wangu wa kwanza, nyakati fulani nilikasirikia na kufadhaikia hali yangu, hasa nilipokuwa mchovu. Baadaye, nilihisi nikiwa na hatia kuhusu hisia zangu. Nilizungumza na mzee mwenye huruma ambaye alikuwa na uzoefu wa kitaaluma katika kutibu wagonjwa wenye ugonjwa wa muda mrefu. Alinihakikishia kwamba nilikuwa nikifanya vyema katika hali zangu na kwamba ni jambo la kawaida sana kwa wanadamu wasiokamilika kukosea kwa njia hiyo wanapokabili mkazo wa muda mrefu wa kihisia-moyo.

Ingawa Paquita nami sasa twafurahia sana utumishi wetu wa wakati wote, sifikiri tutapata kamwe kuona baraka zetu kivivi-hivi. Yehova ametuthawabisha katika njia nyingi na ametupa kazi yenye kuridhisha kufanya, ile ambayo twaweza kuifanya pamoja. Kwa miaka ambayo imepita sote tulipanda kwa machozi, lakini sasa, kwa sababu ya Yehova, tunavuna kwa kilio cha shangwe.—Kama ilivyosimuliwa na Raymond Kirkup.

[Maelezo ya Chini]

a Vilivyochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Paquita nami twafurahia huduma yetu pamoja

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki