Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 2/22 kur. 7-10
  • Kulikabili Hilo Tatizo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kulikabili Hilo Tatizo
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuandaa Utegemezo
  • “Kaa Tuli na Ukaze Fikira!”
    Amkeni!—1997
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1995
  • Kulea Mtoto Aliye Mgumu
    Amkeni!—1994
  • Wakati Mengi Yahitajiwa
    Amkeni!—1994
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 2/22 kur. 7-10

Kulikabili Hilo Tatizo

KWA miaka ambayo imepita matibabu kadhaa yametokezwa kwa ajili ya ADHD. Baadhi yayo yamekazia ulaji. Hata hivyo, uchunguzi fulani unadokeza kwamba viongezwaji vya chakula kwa kawaida havisababishi utendaji wa kupita kiasi na kwamba masuluhisho ya lishe mara nyingi hayana matokeo. Njia nyinginezo za kutibu ADHD ni dawa, kurekebisha mwenendo, na uzoezaji wa kufahamu tatizo hilo.a

Dawa. Kwa kuwa ADHD kwa wazi huhusisha kasoro ya ubongo, dawa za kurudisha usawaziko ufaao wa kemikali zimethibitika kuwa za msaada kwa wengi.b Hata hivyo, dawa hazichukui mahali pa kujifunza. Hizo zasaidia tu mtoto akaze fikira, zikimpa msingi ambao juu yao aweza kujifunza stadi mpya.

Watu wazima wengi wenye ADHD wamesaidiwa na dawa pia. Hata hivyo, tahadhari yafaa—kwa vijana na watu wazima—kwa kuwa dawa chochezi zitumiwazo kutibu ADHD zaweza kuraibisha.

Kurekebisha mwenendo. ADHD ya mtoto haiondolei wazazi wajibu wa kutoa nidhamu. Ingawa huenda mtoto akawa na mahitaji ya kipekee kwa habari hii, Biblia huonya wazazi hivi: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Katika kitabu chake Your Hyperactive Child, Barbara Ingersoll ataja: “Mzazi ambaye hujiacha ashindwe na kumwacha mtoto wake mwenye utendaji wa kupita kiasi atende bila kuzuiwa hamsaidii mtoto wake. Kama tu vile mtoto yeyote, mtoto mwenye utendaji wa kupita kiasi ahitaji nidhamu yenye kuendelea yenye staha kwa mtoto akiwa mtu. Hilo lamaanisha mipaka iliyowekwa wazi na thawabu na adhabu zifaazo.”

Kwa hiyo ni jambo la muhimu kwamba wazazi waandae kanuni thabiti. Zaidi ya hayo, kwapasa kuwa na kawaida yenye kufuatwa sana ya utendaji wa kila siku. Huenda wazazi wakataka kumpa mtoto uhuru wa kutengeneza ratiba hii, kutia ndani wakati wa mgawo wa masomo ya nyumbani, kujifunza, kuoga, na kadhalika. Kisha dumu katika kufuatia ratiba hiyo. Hakikisha kwamba kawaida ya kila siku inafuatwa. Phi Delta Kappan lataja hivi: “Madaktari, wanasaikolojia, maofisa wa shule, na walimu wana wajibu kwa mtoto na kwa wazazi wa mtoto kueleza kwamba kuainishwa ADD au ADHD hakumaanishi kwamba mtoto aweza kufanya chochote bila kutiwa nidhamu, bali badala ya hivyo kuainishwa huko ni elezo liwezalo kuongoza kwenye msaada ufaao kwa mtoto aliye na kasoro hiyo.”

Uzoezaji wa kufahamu tatizo hilo. Hii yatia ndani kumsaidia mtoto kubadili maoni yake kujihusu na kuhusu tatizo lake. “Watu walio na kasoro ya upungufu wa makini huhisi kwamba ni ‘wasiovutia, wapumbavu, na wasiofaa kitu’ hata ingawa ni wenye kuvutia, wenye akili, na wenye moyo mzuri,” aonelea Dakt. Ronald Goldberg. Kwa hivyo, mtoto aliye na ADD au ADHD ahitaji kuwa na maoni yafaayo ya thamani yake, na ahitaji kujua kwamba matatizo yake ya kukosa makini yaweza kushughulikiwa. Hili ni muhimu hasa wakati wa ubalehe. Kufikia wakati mtoto mwenye ADHD yuko katika umri wa utineja, huenda tayari akawa amepatwa na kejeli nyingi kutoka kwa marika wake, walimu, ndugu zake, na labda hata kutoka kwa wazazi wake. Sasa yeye ahitaji kuweka miradi ya kihalisi na kujichanganua istahilivyo badala ya kujiona kuwa mbaya.

Njia za matibabu zilizo juu zaweza pia kufuatiwa na watu wazima walio na ADHD. “Marekebisho ni ya muhimu yakitegemea umri,” aandika Dakt. Goldberg, “lakini misingi ya matibabu—dawa mahali pafaapo, kurekebisha mwenendo, na [mazoezi ya] kufahamu tatizo hilo—hubaki ikiwa njia zifaazo kwa muda wote wa maisha.”

Kuandaa Utegemezo

John, baba ya balehe aliye na ADHD, awaambia wazazi walio katika hali kama hiyo: “Jifunze yote uwezayo kuhusu tatizo hili. Fanya maamuzi yategemeayo ujuzi. Juu ya yote, mpende mtoto wako, msaidie akuze kujiheshimu. Kutojiheshimu kutaangamiza mtazamo wake.”

Ili mtoto aliye na ADHD apate utegemezo wa kutosha, ni lazima wazazi wote wawili washirikiane. Dakt. Gordon Serfontein aandika kwamba mtoto aliye na ADHD ahitaji “kujua kwamba anapendwa nyumbani na kwamba upendo huo hutoka kwa upendo uliopo kati ya wazazi.” (Italiki ni zetu.) Kwa kuhuzunisha, upendo huo haudhihirishwi sikuzote. Dakt. Serfontein aendelea: “Imehakikishwa kwamba katika familia ambapo kuna [mtoto mwenye ADHD], kuna karibu asilimia 33 ya tukio la mgawanyiko na mvunjiko wa ndoa kuliko katika familia ya kawaida.” Ili kuzuia mgawanyiko huo, baba apaswa kuchangia sana katika kumlea mtoto aliye na ADHD. Daraka halipasi kuwekewa mama tu.—Waefeso 6:4; 1 Petro 3:7.

Marafiki wa karibu, ingawa si sehemu ya familia, waweza kutoa utegemezo mkubwa sana. Jinsi gani? “Uwe mwenye fadhili,” asema John, aliyenukuliwa mapema. “Usitazame tu mambo ya nje-nje. Pata kumjua mtoto huyo. Zungumza pamoja na wazazi wake pia. Wanaendeleaje? Wanakabiliana na nini kila siku?”—Mithali 17:17.

Washiriki wa kutaniko la Kikristo waweza kufanya mengi ili kutegemeza mtoto aliye na ADHD na vilevile wazazi. Jinsi gani? Kwa kuwa wenye mtazamo ufaao kwa matarajio yao. (Wafilipi 4:5) Nyakati fulani, mtoto aliye na ADHD huenda akawa mwenye kusumbua. Badala ya kusema bila kuwa na hisia, “Kwa nini huwezi kumdhibiti mtoto wako?” au “Kwa nini humtii nidhamu?” mwamini mwenzi mwenye kufikiri atatambua kwamba huenda tayari wazazi wamelemezwa na kazi ngumu ya kila siku ya kumlea mtoto aliye na ADHD. Bila shaka, wazazi wapaswa kufanya kila wawezalo ili kuwekea mipaka mwenendo wenye kusumbua wa mtoto huyo. Hata hivyo, badala ya kushambulia kwa maneno ya hasira, wale wenye uhusiano katika imani wapaswa kujaribu kuonyesha “hisia-mwenzi” na ‘kutoa baraka.’ (1 Petro 3:8, 9) Kwa hakika, mara nyingi Mungu “hufariji wale walioshushwa chini,” kupitia waamini wenzi.—2 Wakorintho 7:5-7.

Wanafunzi wa Biblia wanatambua kwamba kutokamilika kote kwa kibinadamu, kutia ndani matatizo ya kutoweza kujifunza na ADHD, kumerithiwa kutoka kwa mwanadamu wa kwanza, Adamu. (Waroma 5:12) Wanajua pia kwamba Muumba, Yehova, atatimiza ahadi yake ya kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu ambapo magonjwa yenye kuhuzunisha hayatakuwapo tena. (Isaya 33:24; Ufunuo 21:1-4) Hakikisho hilo ni nanga ya utegemezo kwa wale wenye matatizo kama vile ADHD. “Umri, mazoezi, na yaliyoonwa yanamsaidia mtoto wetu kufahamu na kushughulikia tatizo lake,” asema John. “Lakini hatatibiwa kikamili kamwe katika mfumo huu wa mambo. Faraja yetu ya kila siku ni kwamba katika ulimwengu mpya, Yehova atarekebisha tatizo la mwana wetu na kumsaidia kufurahia maisha kikamili.”

[Maelezo ya Chini]

a Amkeni! halipendekezi matibabu yoyote hususa. Wakristo wapaswa kuwa waangalifu kwamba matibabu yoyote wanayotafuta hayapingani na kanuni za Biblia.

b Wengine hupatwa na athari za kando kutokana na dawa, kutia ndani wasiwasi na matatizo mengineyo ya kihisia-moyo. Zaidi ya hayo, dawa chochezi zaweza kuchochea mivuto katika wagonjwa walio na matatizo ya mitetemo kama vile ugonjwa wa Tourette. Kwa hiyo dawa zapasa kutumiwa chini ya usimamizi wa daktari.

[Sanduku katika ukurasa wa 8]

Neno la Hadhari kwa Wazazi

KARIBU watoto wote nyakati fulani hawakazi fikira, ni wenye kutenda kwa msukumo wa ghafula, na wenye kutenda kupita kiasi. Kuwapo kwa vitabia hivi hakuashirii sikuzote kwamba mtoto ana ADHD. Katika kitabu chake Before It’s Too Late, Dakt. Stanton E. Samenow asema: “Nimeona visa vingi mno ambapo mtoto ambaye hataki kufanya jambo fulani anaachwa kwa sababu anafikiriwa kwamba ana ulemavu fulani au hali fulani ambayo si kosa lake.”

Dakt. Richard Bromfield pia aona uhitaji wa kuwa na hadhari. “Kwa hakika, watu fulani walio na ADHD wana tatizo katika mfumo wa neva na wanahitaji dawa,” yeye aandika. “Lakini tatizo hilo huonwa kimakosa kuwa kisababishi cha namna zote za kutenda vibaya, unafiki, upuuzaji na matatizo mengine ya jamii ambayo katika visa vingi hayahusiani hata kidogo na ADHD. Kwa hakika, ukosefu wa kanuni katika maisha ya kisasa—jeuri ya kila mahali, utumizi mbaya wa dawa za kulevya na, mambo ambayo hayatishi sana, kama vile nyumba ambamo hakuna nidhamu na zenye fujo—waweza kusitawisha ukosefu wa utulivu kama ule wa ADHD kuliko upungufu wowote ule wa kiakili.”

Kwa hiyo ni kwa sababu nzuri kwamba Dakt. Ronald Goldberg aonya dhidi ya “kuona dalili tofauti-tofauti kuwa uthibitisho wa kuwapo kwa ADHD.” Yeye atoa shauri kwamba “kila udodosaji uwezekanao ufanywe ili kufikia mkataa sahihi.” Dalili zinazofanana na ADHD huenda zikaonyesha lolote la matatizo mengi ya kimwili au kihisia-moyo. Kwa hiyo usaidizi wa daktari mwenye uzoefu ni wa muhimu katika kufanya udodosaji sahihi.

Hata ikiwa udodosaji unafanywa, wazazi wafanya vyema kupima mazuri na mabaya ya dawa zitakazotumiwa. Ritalin yaweza kuondosha dalili zisizotakwa, lakini yaweza pia kuwa na athari za kando zisizofurahisha, kama vile kukosa kupata usingizi, hangaiko lililoongezeka, na wasiwasi. Hivyo, Dakt. Richard Bromfield atahadharisha dhidi ya kumpa mtoto dawa haraka sana ili tu kumwondoshea dalili zake. “Watoto wengi sana, na watu wazima wengi zaidi, wanapewa Ritalin isivyofaa,” yeye asema. “Kutokana na uzoefu wangu, utumizi wa Ritalin hutegemea hasa uwezo wa wazazi na walimu wa kuvumilia mwenendo wa watoto. Najua kuhusu watoto ambao wamepewa ili kuwatuliza badala ya kushughulikia mahitaji yao.”

Kwa hiyo wazazi hawapaswi kufanya haraka sana kuamua kwamba watoto wao wana ADHD au tatizo la kutoweza kujifunza. Badala ya hivyo, wanapaswa kupima uthibitisho kwa uangalifu, kwa msaada wa mtaalamu mwenye ustadi. Ikiwa yaamuliwa kwamba mtoto ana tatizo la kasoro ya kujifunza au ADHD, wazazi wapaswa kuchukua wakati kujua vyema tatizo hilo ili kwamba waweze kutenda kwa matokeo mema ya watoto wao.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mtoto aliye na ADHD ahitaji nidhamu yenye fadhili lakini yenye kuendelea

[Picha katika ukurasa wa 10]

Pongezi ya kimzazi hutimiza mengi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki