Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Urafiki Nawashukuru kwa moyo mweupe kwa makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Siwezi Kudumisha Marafiki?” (Mei 22, 1996) Hamjui jinsi makala hii ilivyonisaidia. Ilinionyesha kwamba japo vizuizi, inawezekana kuwa na urafiki wenye kudumu. Nyakati nyingine, sisi hupoteza marafiki kwa sababu sisi huahirisha kusuluhisha kutokuelewana. Makala hii ilinisaidia kupigana na udhaifu wangu kwa habari hii.
A. M. P., Brazili
Makala hiyo ilifika kwa wakati barabara. Miezi mitatu iliyopita urafiki wangu wenye thamani sana na msichana mwingine ulianza kupoa; tukafikia hatua ya kutozungumziana. Makala hiyo ilipofika, rafiki yangu nami tuliisoma na kutambua kwamba sote wawili tulikuwa tukitenda kipumbavu. Tulizungumza na kuelewesha wazi kutokuelewana kwingi kulikotokea. Sasa urafiki wetu una nguvu mpya.
N. T., Italia
Msiba wa Volkeno Nakumbuka ripoti za habari za mlipuko wa Mlima Pinatubo nyuma katika 1991. Lakini nilizisahau mpaka niliposoma makala “Lahari—Matokeo ya Baadaye ya Mlima Pinatubo.” (Mei 22, 1996) Sikuwa nimepata kamwe kusikia juu ya lahari na niliona makala hiyo kuwa yenye kupendeza sana. Moyo mkuu na msaada ulioonyeshwa na familia ya akina Garcia, ingawa walikuwa katika njia ya lahari, ulikuwa wenye kutokeza sana.
S. F., Kanada
Makala hiyo ilinigusa moyo sana. Ilisikitisha sana kusoma mambo waliyoyaona ndugu Wakristo ambao walidumisha bidii yao kwa mambo ya kiroho, hata ingawa walijikuta katika hali zisizopendeza. Hilo limenitia moyo nisiache mambo madogo-madogo yanifanye nikose mikutano ya Kikristo au kunizuia kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Asanteni kwa makala hiyo!
S. D., Italia
Mume wangu nami hatujapata kusikia juu ya lahari, lakini sasa tunatambua jinsi zilivyo mbaya na hatari. Tungependa ndugu zetu wa Filipino wajue kwamba tunasali kwa niaba yao na kwa wale ambao waliweza kuwasaidia.
C. A. B., Guatemala
Mmweko wa Kijani Nimetoka tu kusoma ile makala “Je, Umepata Kuona Mmweko wa Kijani?” (Mei 22, 1996) Miaka michache ambayo imepita, nilipokuwa nikipita kwa ndege juu ya vichaka vya Alaska, nilishangaa kuona mmweko wa buluu na kijani ambao ulionekana kwa kipindi kifupi sana. Sikuwa nimepata makala inayoelezea tukio hilo mpaka sasa. Nyakati nyingine nilidhani kwamba niliwazia tu kitu hicho!
G. C., Alaska
Mishiko ya Hofu Nataka kushukuru sana kwa makala “Kukabiliana na Mishiko ya Hofu ya Ghafula.” (Juni 8, 1996) Nimepatwa na mishiko kama hiyo kwa miaka sita. Baada ya kutumikia nikiwa painia (mweneza-evanjeli wa wakati wote) kwa mwaka mmoja, nililazimika kuacha kwa sababu sikuwa na nguvu za kukabiliana na hiyo mishiko. Jambo hilo lilinitia huzuni sana kwa sababu nilipoonekana kuwa mwenye afya nzuri, marafiki wangu wa karibu hawakuelewa tatizo hilo. Ni vigumu kusimulia jinsi nilivyofurahi niliposoma makala hii.
O. S., Ukrainia
Nimetumikia nikiwa mhudumu wa wakati wote kwa miaka minane. Lakini kwa miaka kadhaa, nilikuwa na hisia ya kutofaa kitu nami nimekuwa na hangaiko sana. Niliposoma makala hii inayofafanua dalili zinazofanana na zangu, mara moja nilianza kutumia shauri layo. Hisia zangu zimeanza kuboreka, na moyo wangu umetulia zaidi.
K. M., Thailand
Nimetibiwa kwa ajili ya mishiko ya hofu za ghafula nami nimesaidiwa. Lakini, nimeteseka kisiri kwa swali hili, ‘Je, mimi ni dhaifu au mvivu kiroho?’ Kusoma makala hii kuliniondolea mzigo wenye kulemea sana.
P. P., Finland