Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Tofauti Zinazogawanya Twataka kushukuru sana kwa makala “Je Ni Lazima Tofauti Zitugawanye?” (Julai 8, 1996) Tumekuwa tukifanya kazi tukiwa sehemu ya kikundi cha wajitoleaji wa kimataifa hapa katika Mexico kwa mwaka mmoja hivi. Hata baada ya miezi kadhaa, tuliendelea kupata magumu ya kubadilikana, lakini hatukuelewa ni kwa nini. Makala hizo zilitusaidia kutambua tatizo kuwa mshtuko wa kitamaduni. Tumetii taarifa kwamba “kufahamu tamaduni nyinginezo kwaweza kuboresha maisha yetu” na tayari twapata shangwe zaidi katika mgawo wetu.
C. H. na J. H., Mexico
Niliguswa moyo na jinsi habari hii yenye kuvuta uangalifu ilivyotolewa na kukuzwa. Tofauti kwa kweli zimechochea chuki nyingi sana katika historia ya binadamu. Mfululizo huu kuanzia sasa utanisaidia kuona tamaduni nyinginezo kwa ufahamu mwingi zaidi. Laiti kila mtu ulimwenguni angesoma makala hizi na kubadili maoni yasiyofaa kuhusu wengine!
G. O., Nigeria
Makala hizo zilinifanya nilie. Nina rafiki ambaye wakati mwingi tuna mahusiano mazuri pamoja naye. Lakini sikuzote nimehisi kwamba kumekuwa na kizuizi kisichoonekana kati yetu. Sasa natambua kwamba tunatoka katika tamaduni tofauti sana. Habari hii itafanyiza tofauti kubwa sana katika njia ambayo nitashughulika naye wakati ujao.
A. F., Marekani
Nilipokuwa nikifanya utafiti wa tasnifu yangu juu ya sayansi ya binadamu, nilikaa majuma kadhaa katika nchi moja ya Afrika. Nilipata kujua Mashahidi wa Yehova wengi wenyeji na kuhudhuria mikutano yao. Lilikuwa ono lenye kusisimua sana! Kama makala hiyo ilivyosema, kuwa karibu na watu wa tamaduni nyingine huthawabisha. Niliweza kutengeneza urafiki mpya ulio wa maana.
S. B., Italia
Habu Nilipendezwa sana na makala “Habu—Nyoka wa Kuepukwa.” (Julai 8, 1996) Iliandikwa kwa namna yenye kupendeza sana, na picha zilikuwa nzuri ajabu!
E. P., Ukrainia
Makala hiyo ilikuwa yenye kuarifu na yenye ucheshi. Lakini hoja moja hupingana na kile ambacho nimefundishwa. Mlinukuu kitabu ambacho kilipendekeza kunyonya sumu mahali ambapo kuna alama za muumo. Je, ni salama kufanya hivyo kweli?
C. D., Nigeria
Yaonekana kwamba wataalamu wengi wa kitiba hawakubaliani na chanzo tulichonukuu katika makala yetu. Kwa kweli, madaktari fulani huhisi kwamba kujaribu kunyonya sumu kwaweza kuwa hatari kwa anayetoa msaada na hakumsaidii sana yule aliyeumwa na nyoka. Madaktari wanakubali kwamba huduma ya kwanza ya maana kabisa ni kumfikisha mhasiriwa hospitalini haraka iwezekanavyo.—Mhariri.
UFO Asanteni kwa makala “Maoni ya Biblia: UFO—Je, Ni Wajumbe Kutoka kwa Mungu?” (Julai 8, 1996) Katika eneo letu watu fulani huamini ripoti kuhusu viumbe kutoka anga za nje. Wakifikiri kwamba Biblia haizungumzii jambo hili, wana shaka kuhusu Biblia. Makala hiyo ilitusaidia kuona kwamba Shetani na mashetani wanajaribu kuongoza watu vibaya na kwamba halingekuwa jambo la hekima kuamini ripoti zisizo na msingi kuhusu viumbe kutoka anga za nje.
A. W., Taiwan
Tulipu Asanteni kwa makala nzuri ajabu iliyokuwa na kichwa “Tulipu—Ua Lenye Historia ya Fujo.” (Julai 8, 1996) Nilipata habari kuhusu mwanzo walo na vilevile madokezo ya kukuza tulipu kuwa yenye kupendeza zaidi.
D. G., Marekani