Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kutozwa Hesabu Asanteni kwa mfululizo wenu wenye kutokeza “Je, Twapaswa Kutoa Hesabu kwa Matendo Yetu?” (Septemba 22, 1996) Nimepata makala hizi kuwa zenye matokeo sana katika kuchochea mazungumzo mazuri pamoja na mawakili, wawakilishi wa bima, maofisa wakuu wa biashara, wachapishaji, maofisa wa serikali, na wengine ambao nimezungumza nao katika maeneo ya kibiashara ya jiji letu. Nilimwonyesha ofisa wa uegeshaji wa jiji makala “Si Kosa Langu.” Alinyakua jarida hilo kutoka mkononi mwangu, akisema kwamba ni “watu wachache wanaokiri makosa yao siku hizi.” Alisema kwamba alitaka kila mfanyakazi aisome.
B. S., Marekani
Nyakati Zenye Kufurahisha Asanteni kwa makala “Vijana Huuliza . . . Naweza Kuwaje na Wakati Wenye Kufurahisha?” (Septemba 22, 1996) Nina umri wa miaka 15, na kuna vijana wengi katika kutaniko letu. Mara nyingi sisi hufanya mambo pamoja. Kwa mfano, twaweza kuhubiri asubuhi kisha twende kuogelea alasiri. Hufurahisha sana! Nyakati nyingine wengine kutoka kutaniko letu hujiunga nasi. Na inafariji kwa wazazi wetu kujua kwamba tuna ushirika wa aina ifaayo.
I. W., Ujerumani
Anemia ya Sickle-Cell Nimesoma na kusoma tena makala “Anemia ya Sickle-Cell—Ujuzi Ndio Kinga Bora Zaidi.” (Oktoba 8, 1996) Hiyo yafafanua hali yangu! Nimekuwa nikiishi na ugonjwa huu kwa miaka 18 sasa. Machozi yalikuja machoni pangu nilipokuwa nikiisoma. Nilifurahi kuona kwamba mliwafikiria wale wanaougua ugonjwa huu.
R. S., Italia
Nina anemia ya sickle-cell. Sikujua kwamba wengine wengi sana walikuwa nayo pia. Makala hiyo ilinisaidia kuelewa kwa nini nina maumivu na jinsi ilivyo muhimu kunywa viowevu vingi. Mama yangu aliwapa walimu wangu nakala za makala hiyo ili waelewe maradhi yangu.
A. H., Marekani
Ndugu yangu mchanga alikufa kutokana na anemia ya sickle-cell. Katika Nigeria, watu 60,000 hufa kila mwaka kutokana nayo. Kwa hiyo makala hiyo ilishughulikia tatizo halisi. Kila familia ya Nigeria yapaswa kusoma makala hii. Ilikuwa yenye kuarifu na ilielezwa kwa njia mpya.
F. A., Nigeria
Siwezi kujizuia kueleza jinsi ninavyohisi kuhusu makala juu ya anemia ya sickle-cell. Nimevumilia maradhi hayo kwa miaka 26 sasa bila habari hii. Asanteni sana kwa habari hiyo.
D. C., Zambia
Upendo Unaoshikamanisha Nataka kuwashukuru, ndugu wapendwa, kwa kuchapa makala “Maoni ya Biblia: Upendo Unaoshikamanisha.” (Oktoba 8, 1996) Nimekabili majaribu mengi sana ya imani yangu kwa miaka ambayo imepita, kutia ndani vifo vya ghafula vya wazazi wangu. Lakini jaribu baya zaidi limetoka kwa mtu fulani kutanikoni. Makala hii ilinipa nguvu na faraja, kwa kuwa naona kwamba Yehova hujua na huelewa machozi yangu na umizo na maumivu ambayo nimehisi moyoni mwangu. Nilijifunza kwamba hata mtume Paulo alipatwa na maumivu kama hayo. Naitibari kwamba kwa kupita kwa wakati Yehova ataponya majeraha yangu.
S. B., Kanada
Katika mfumo huu mwovu, ni rahisi mtu kukosa kukazia uangalifu wake mambo ya kiroho. Makala hiyo ilikuwa yenye kutia moyo na yenye kunichochea sana. Hivi majuzi, nimepatwa na mkazo sana kwa sababu ya mahangaiko ya kila siku ya maisha. Makala hiyo ilinisaidia kuthamini umuhimu wa kutegemea upendo wa Yesu, badala ya hisia zetu wenyewe zisizokamilika.
A. M., Marekani
Mimi nina tatizo la kushuka moyo linalosababishwa na ukosefu wa usawaziko wa kikemikali mwilini. Makala hiyo imenisaidia kufanya maendeleo katika kushughulikia mshuko-moyo wangu.
B. U., Marekani