Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 2/8 kur. 8-12
  • Kukabiliana na Matokeo Yake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukabiliana na Matokeo Yake
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tegemezo la Familia na Marafiki
  • Kujifunza Kutoa Tegemezo
  • Kukabiliana na Hali, kwa Tegemezo Lenye Upendo la Yehova
  • Watunzaji Wapata Tegemezo
  • Kukabili Vizuizi Vikali
  • Mshtuko wa Akili—Kisababishi Chake
    Amkeni!—1998
  • Mshtuko wa Akili!
    Amkeni!—1998
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1998
  • Kuutazama Ulimwengu
    Amkeni!—1999
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 2/8 kur. 8-12

Kukabiliana na Matokeo Yake

AKIWA amelala katika kitanda cha hospitali mguu na mkono ikiwa imepooza, Gilbert alimwuliza daktari wake: “Je, nitapata kutumia tena mkono na mguu wangu?” Gilbert alisikia jibu hili lenye kuvutia: “Kadiri ufanyavyo bidii, ndivyo utakavyoweza kutumia tena mkono na mguu wako, na ndivyo utakavyotimiza hilo haraka zaidi.” Yeye alijibu: “Niko tayari!” Tibamaungo pamoja na mtazamo chanya ulimsaidia, akiwa na umri wa miaka 65, aache kutumia kiti chenye magurudumu, kisha kitembezi, kisha bakora na hatimaye aliweza kurudi kazini.

Mingi ya misaada ya kuwezesha kuishi maisha ya kawaida baada ya kupatwa na mshtuko wa akili leo, huunga mkono ile dhana kuwa ikiwa sehemu moja ya ubongo imeharibika, maeneo mengine ya ubongo yaweza kuchukua fungu la tishu zilizojeruhiwa. Kusudi moja la tiba hiyo ni kutokeza uwezekano wa maeneo hayo yasiyohusika na kuyachochea ili kuruhusu ubongo upange upya na kubadilikana,” wasema watafiti Weiner, Lee, na Bell. Hata hivyo, kupona kwategemea mambo mengine pia, kama vile mahali katika ubongo ambapo mshtuko wa akili ulitokea na ukubwa wa mshtuko huo, hali ya jumla ya afya ya mtu huyo, ubora wa utunzaji wa kitiba, na tegemezo la wengine.

Tegemezo la Familia na Marafiki

Erikka alishiriki katika mazoezi ya kumsaidia aweze kuishi maisha ya kawaida kwa muda wa miaka mitatu, akijifunza kutembea na kutumia mkono wake wa kulia kufidia mkono wa kushoto uliopooza. Aeleza kilichomsaidia kukabiliana na hali: “Jambo lililokuwa la maana zaidi lilikuwa kwamba mume wangu na marafiki wangu walibaki wakiwa waaminifu-washikamanifu kwangu. Kujua kwamba walinipenda kulinipa nguvu, na waliponitia moyo nisikate tamaa, hilo lilinichochea.”

Washiriki wa familia hupata kuwa wenzi katika hatua za kupona za mpendwa wao. Wanahitaji kuwauliza maswali watumishi wa kitiba na kuchunguza kwa makini tiba ambazo huenda zikahitaji kuendelezwa nyumbani ili kwamba asipoteze maendeleo ambayo tayari yamefanywa. Subira, fadhili, uelewevu, na shauku zionyeshwazo na washiriki wa familia na marafiki huandaa mazingira ya kihisia-moyo yaliyo salama ya kujifunzia upya usemi, kusoma, na kazi nyingine za maisha ya kila siku.

Akijaribu kuwa mwenye usawaziko kati ya kulazimisha na kubembeleza, John alifanya bidii kumsaidia mke wake Ellen na mazoezi na tiba. Aelezea jitihada za familia yake: “Hatungemruhusu Ellen ajisikitikie kupita kiasi. Nyakati nyingine tulikuwa wasimamizi wakali, lakini sikuzote tuliangalia vizuizi vyake na kutoa usaidizi. Yeye ni mwenye hisia nyepesi, kwa hiyo huwa najitahidi nisimsababishie mkazo.”

Kadiri Ellen alivyoendelea kujifunza tena kuzungumza kwa msaada wa mtaalamu wa matibabu ya usemi, John alimsaidia. “Kufanya mambo pamoja kulikuwa kitia-moyo, kwa hiyo tulisoma Biblia pamoja kwa sauti, jambo ambalo lilisaidia kuboresha usemi wake. Pia, pole kwa pole mwanzoni, tulishiriki katika huduma, kwani sisi tu Mashahidi wa Yehova. Kwa njia hii Ellen angeweza kushiriki na wengine tumaini tulilo nalo la wakati ujao. Kufanya hivyo kwenyewe kulikuwa tiba kwa Ellen.” Kufikia mwishoni mwa miaka mitatu, Ellen alikuwa amefanya maendeleo sana.

Kitia-moyo na nguvu ambazo marafiki waweza kutoa hazipasi kudharauliwa kamwe, kwa sababu zaweza kuwa na athari kubwa kuelekea kupona kwa mtu aliyepatwa na mshtuko wa akili. Jarida la kitiba Stroke liliripoti kwamba “Utegemezo mwingi wa kijamii ulipatikana kuwa unaashiria kupona kwa haraka zaidi na maendeleo makubwa zaidi katika kuweza kufanya mambo, hata miongoni mwa wagonjwa waliokuwa na mshtuko wa akili mbaya sana.”

Bernie alithamini sana tegemezo ambalo marafiki wake walimpa. Yeye atukumbusha: “Ziara za marafiki husaidia kukabiliana na hali. Sauti yenye kusikitikia na mwelekeo wenye kujali huuchangamsha moyo. Ingawa mtu hapaswi kufikiria sana kutojiweza kwake, kutambua maendeleo yoyote kwatia moyo sana.” Sisi sote twaweza kufanya nini ili kutoa tegemezo kwa wale wanaokabiliana na matokeo ya baadaye ya mshtuko wa akili? “Wapelekee maua,” apendekeza Bernie, “au shiriki nao wazo la Kimaandiko au jambo lililoonwa. Hayo yalikuwa yenye msaada sana kwangu.”

Melva, mzee-mzee aliyepatwa na mshtuko wa akili aliona kuwa jambo la msaada kwa mmoja wa ndugu zake wa kiroho kusali pamoja naye. Gilbert pia apendekeza hili, akieleza: “Yaonyesha kuwa kwa kweli wajali unaposali pamoja na mtu.” Peter, ambaye mshtuko wa akili ulimwacha akiwa haoni vizuri, huthamini sana wakati ambapo watu wengine wanafahamu kizuizi chake na kuchukua wakati kumsomea.

Pia kumsaidia mtu kwenda na kutoka mahali pa kumsaidia kuweza kuishi maisha ya kawaida ni ishara ya upendo. Kuhakikisha kwamba nyumba ya mhasiriwa wa mshtuko wa akili ni mahali salama ni muhimu pia. Kuanguka ni tisho la daima wakati usawaziko wa mwili unapokuwa tatizo. Kwa kielelezo, Gilbert, alithamini msaada wenye fadhili wa marafiki ambao, kati ya mambo mengine, walimwekea pao la kujishikilia kwenye bafu yake kwa ajili ya usalama.

Kujifunza Kutoa Tegemezo

Mabadiliko ya hali ya moyo na mwelekeo mkubwa wa kulia waweza kuwa wenye kuaibisha mhasiriwa wa mshtuko wa akili, na pia kutatanishwa kwa watu walio kando ambao huenda wasijue jinsi ya kutenda. Hata hivyo, kwa kujifunza kuwa mwenye kutegemeza, marafiki waweza kumwokoa mhasiriwa wa mshtuko wa akili ambaye aweza kujitenga na wengine. Kwa kawaida vipindi vya kulia hupunguka. Lakini machozi yajapo, baki ukiwa mtulivu na ukae na mtu huyo, ukimwambia yale ungependa kusikia ikiwa ungekuwa katika hali yake.

Zaidi ya yote, kuza upendo wa kimungu kwa wale ambao udhaifu wao huenda ukawa umebadili utu ambao uliujua hapo awali. Wao hutambua unavyohisi, na hilo, nalo, huathiri itikio lao kukuelekea. Erikka aeleza: “Huenda nisipate kuwa mtu yuleyule tena. Lakini hakuna yeyote anayepaswa kudai hilo kutoka kwa mhasiriwa wa mshtuko wa akili. Jamaa na marafiki wapaswa kujifunza kumpenda mtu huyo jinsi alivyo. Wakichunguza kwa uangalifu utu wake, watagundua kuwa sifa nyingi zenye kupendeza za wakati uliopita zingali zipo.”

Mtu awapo hawezi kuzungumza au kueleweka staha ya kibinafsi hushuka. Kwa kufanya jitihada ya kuzungumza nao, marafiki waweza kuwahakikishia wale ambao usemi wao umedhoofika. Takashi aeleza: “Ninachofikiria na kuhisi moyoni hakijabadilika. Hata hivyo, watu huelekea kuniepuka kwa sababu hawawezi kuwa na mazungumzo ya kawaida nami. Ni vigumu kwangu kuwafikia watu, lakini mtu ajapo kuzungumza nami, huwa ni kitia-moyo kikubwa sana kwangu na hilo hunifurahisha sana sana!”

Ifuatayo ni miongozo fulani iwezayo kutusaidia sote tuweze kuwategemeza na kuwatia moyo wale wenye udhaifu wa usemi.

Mishtuko mingi ya akili haiathiri uwezo wa kufikiri. Watu wengi ambao wamepatwa na mshtuko wa akili hubaki wakiwa chonjo kiakili, hata ingawa huenda usemi wao ukawa mgumu kuuelewa. Usiseme nao kwa njia yenye kushusha au kusema kana kwamba wasema na mtoto. Watendee kwa adhama.

Sikiliza kwa subira. Huenda wakahitaji wakati ili kupanga upya wazo au kumaliza neno, fungu la maneno, au sentensi. Kumbuka kwamba msikilizaji mwenye kujali zaidi hana haraka ya kusikia.

Usijifanye kuwa waelewa ikiwa huelewi. Kiri kwa ufadhili: “Samahani. Yaonekana sipati kukuelewa. Tujaribu tena baadaye.”

Sema polepole na waziwazi kwa sauti ya kawaida.

Tumia sentensi fupi na maneno yajulikanayo.

Tumia maswali ambayo yanahitaji jibu la ndiyo au la, na umtie moyo kujibu. Kumbuka kwamba huenda wasiweze kufahamu maneno yako.

Punguza kelele za kando-kando.

Kukabiliana na Hali, kwa Tegemezo Lenye Upendo la Yehova

Huku likiwa jambo muhimu kujua kisababishi cha mshtuko wako wa akili, kwani hilo hukuwezesha kuchukua hatua na kupunguza hatari ya kupatwa na mishtuko ya akili wakati ujao, kudhibiti hofu inayoandamana ni kwa muhimu pia. Ellen aeleza: “Maneno ya Mungu kwenye Isaya 41:10 hasa hunitia moyo. Hapo yeye husema: ‘Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe; usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia, naam, nitakushika kwa mkono wa kuume wa haki yangu.’ Yehova amekuwa wa halisi sana kwangu, akinifanya nisiogope.”

Biblia pia inamsaidia Anand akabiliane na kukata tumaini anakohisi: “Huniandalia tegemezo kubwa, kwa kuwa huniamsha na kuniburudisha.” Tatizo la Hiroyuki lilikuwa jinsi awezavyo kufaidika kutokana na Maandiko, kwa kuwa hakuweza kukaza fikira. Yeye asema: “Nilipata faraja kutokana na kusikiliza vitabu vya Biblia katika kaseti.”

Mtume Paulo alitaarifu: “Niwapo dhaifu, ndipo niwapo mwenye nguvu.” (2 Wakorintho 12:10) Ni roho ya Yehova iliyomsaidia Paulo kutimiza yale ambayo hangeweza kwa uwezo wake mwenyewe. Wale watu ambao wamepatwa na mshtuko wa akili pia wanaweza kumtegemea Yehova ili kupata nguvu za kiroho. Erikka aeleza: “Wakati tuna afya na twafanya kila jambo kwa nguvu zetu, huenda tusimpe Yehova fursa nyingi za kutusaidia. Lakini kutojiweza kwangu kumeniwezesha kufanya uhusiano wangu naye uwe wenye nguvu zaidi katika njia ya pekee sana.”

Watunzaji Wapata Tegemezo

Watunzaji wahitaji tegemezo katika fungu lao la maana. Wanaweza kugeukia wapi ili kupata tegemezo? Mahali pamoja ni katika familia. Kila mshiriki ahitaji kushiriki mzigo wa kutunza. Yoshiko aeleza jinsi wana wake walivyompa tegemezo la kihisia-moyo: “Walikuwa wakiyasikiliza matatizo yangu kana kwamba yalikuwa yao.” Washiriki wa familia wahitaji kupata habari yote iwezayo kupatikana ili wajifunze jinsi ya kumtunza mhasiriwa wa mshtuko wa akili na pia jinsi ya kukabiliana na mabadiliko ya utu wa mpendwa wao.

Nani wengine wawezao kutoa tegemezo kwa watunzaji? David na familia yake waliigeukia familia yao ya kiroho ndani ya kutaniko la Mashahidi wa Yehova ili kumtunza Victor: “Waliitikia uhitaji wetu. Wakipokezana zamu, nyakati fulani wao huja na kulala katika nyumba yetu ili kumtunza Victor usiku kucha kwa ajili yetu.”

Kila mtunzaji apaswa kuhisi upendo wenye joto na tegemezo la familia yake ya kiroho. Lakini wengine waweza kuona vigumu kuomba msaada. Haruko aeleza: “Mara nyingi mimi huambiwa: ‘Ikiwa kuna msaada wowote unaohitaji, usisite kutujulisha.’ Lakini nikijua jinsi kila mtu ni mwenye shughuli nyingi, nasita kuomba msaada. Ningeshukuru sana ikiwa watu wangetoa msaada katika njia hususa: ‘Naweza kukusaidia kusafisha. Ni siku gani iliyo nzuri kwako?’ ‘Naweza kukununulia vitu unavyohitaji, je, ni sawa nikija sasa?’”

Mke wa Kenji alipatwa na mshtuko wa akili; hata hivyo, Kenji aliweza kuandaa utunzaji ambao mke wake alihitaji. Alipata kwamba kwa sala angeweza kumtwika Yehova mizigo yake yenye kulemea. Hatimaye, mke wake akapoteza uwezo wa kusema, na kwa hiyo, Kenji akampoteza mwenzi wa kuzungumza naye. Lakini yeye husoma Biblia kila siku. Asema: “Hunikumbusha kuhusu utunzaji mwororo wa Yehova kwa wale waliopondeka katika roho, na hilo limenizuia nisishuke moyo au kuwa mpweke.”

Kutegemea roho ya Yehova kwaweza kutusaidia wakati ionekanapo kana kwamba tunashindwa na hisia-moyo. Yoshiko, akikabiliana na mabadiliko ya utu wa mume wake na hamaki za mara kwa mara baada ya kupatwa na mshtuko wa akili, asimulia: “Nyakati fulani nimehisi nikichochewa na msukumo wa kutaka kupiga yowe kwa sauti kubwa. Katika nyakati hizo nilikuwa nikisali kwa Yehova sikuzote, na roho yake ilikuwa ikiniletea amani.” Akithamini uaminifu-mshikamanifu wa Yehova kumwelekea, haruhusu chochote kuingilia njia yake ya maisha ya Kikristo. Yeye huhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, hushiriki katika huduma, na hufanya funzo la kibinafsi la Biblia. “Kwa kufanya sehemu yangu,” Yoshiko asema, “Najua kwamba Yehova hataniacha kamwe.”

Mahangaiko yanaponyemelea, sikuzote Yehova yuko tayari kusikiliza. Midori, ambaye mume wake alipatwa na mshtuko wa akili, hupata faraja kutokana na uhakika wa kwamba, kitamathali, Yehova ameweka machozi yote ambayo amelia katika “chupa” yake. (Zaburi 56:8) Yeye hukumbuka maneno ya Yesu: “Msihangaike kamwe juu ya siku ifuatayo.” Yeye asema: “Nimeamua kuwa mwenye subira hadi ulimwengu mpya ujapo.”—Mathayo 6:31-34.

Kukabili Vizuizi Vikali

Ni kweli kwamba katika kujaribu kuishi maisha ya kawaida watu fulani hupata nafuu sana, lakini wengine hufaulu kidogo tu katika kupata tena uwezo mbalimbali waliokuwa nao kabla ya kupatwa na mshtuko wa akili. Ni nini kiwezacho kuwasaidia wenye kufaulu kidogo kukabili ugumu wa vizuizi vyao, ingawa huenda vikawa vikali na vyenye kudumu sana?

Bernie, ambaye alipoteza uwezo mkubwa wa kusonga kwa sababu ya mshtuko wa akili, ajibu: “Shangwe ya tumaini langu la uhai udumuo milele katika dunia iliyo paradiso na sala kwa Baba yangu wa kimbingu, Yehova, zilinisaidia kukubali vizuizi vyangu kwa utulivu.”

Tumaini hilo lilimsaidia Erikka na mume wake, Georg, wakubali vizuizi vyake na bado waendelee kuonea shangwe maisha. Georg aeleza: “Tuna ahadi ya Mungu ya kuponywa kabisa siku moja. Kwa hiyo hatukazii fikira kutojiweza huku. Bila shaka, tungali twafanya yote tuwezayo kwa ajili ya afya ya Erikka. Lakini waweza kujifunza kuishi na kutopatana kwa misuli na kukazia fikira mambo yaliyo chanya zaidi.”—Isaya 33:24; 35:5, 6; Ufunuo 21:4.

Katika visa ambapo kupona ni kwa kadiri ndogo, tegemezo la familia na marafiki ni muhimu hata zaidi. Wanaweza kumsaidia mhasiriwa kukabiliana hadi wakati wa Mungu ufikapo wa kurekebisha taabu zote za afya.

Kujua kwamba kuna wakati ujao mtukufu kwa ajili ya wahasiriwa wa mshtuko wa akili na familia zao wakati ambapo afya itarudishwa huwawezesha kukabiliana na maisha siku kwa siku. Kwa hiyo wanaweza kungojea kwa subira kitulizo bila kuteseka kote, katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja karibuni. (Yeremia 29:11; 2 Petro 3:13) Wakati huohuo, wote wanaomgeukia Yehova wanaweza kuwa na uhakika kwamba hata sasa atawasaidia na kuwategemeza katika kukabiliana na matokeo yenye kulemaza ya mshtuko wa akili.—Zaburi 33:22; 55:22.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Familia na marafiki wanaweza kumsaidia mhasiriwa kukabiliana hadi wakati wa Mungu ufikapo wa kurekebisha taabu zote za afya

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Kuzuia Mshtuko wa Akili

“NJIA bora zaidi ya kukabiliana na mshtuko wa akili ni kujaribu kuuzuia,” ataarifu Dakt. David Levine. Na jambo kuu zaidi lihusishwalo na mishtuko ya akili iliyo mingi ni msukumo mkubwa wa damu.

Kwa watu wengi, msukumo mkubwa wa damu waweza kudhibitiwa kwa ulaji wenye potasiamu nyingi na kiasi kidogo cha chumvi, mafuta kifu, na kolesteroli. Kupunguza unywaji wa alkoholi huenda kukawa kwa muhimu pia. Programu ya kawaida ya mazoezi yanayofaa kwa umri wa mtu na hali njema yake kwaweza kusaidia kupunguza uzito, ambao kwa upande ule mwingine huenda kukapunguza msukumo wa damu. Huenda ikawa lazima kutumia dawa—chini ya uangalizi wa daktari, kwani kuna madawa mengi yapatikanayo.

Ugonjwa wa ateri hufanya njia kubwa ya kupitishia damu kuelekea kwenye ubongo iwe nyembamba na ni kisababishi kikubwa cha mshtuko wa akili. Ikitegemea ateri imezibika kadiri gani, huenda upasuaji uitwao carotid endarterectomy ukapendekezwa ili kuifungua mishipa iliyoziba. Uchunguzi mbalimbali umeonyesha kwamba watu fulani ambao walikuwa wakionyesha dalili za kuzibika kwa ateri na ambao mishipa yao ilikuwa imefinyaa sana walinufaika na upasuaji pamoja na tiba ya madawa. Hata hivyo, kwaweza kuwa na matatizo yanayohusiana na upasuaji, kwa hiyo huo wapaswa kufikiriwa kwa uangalifu.

Maradhi ya moyo yaweza kuongezea hatari ya mshtuko wa akili. Atrial fibrillation (mpigo wa moyo usio wa kawaida), ambao waweza kusababisha vidonge vya damu na kuvipeleka kwenye ubongo, waweza kutibiwa kwa kutumia dawa za kuzuia kuganda. Matatizo mengine ya moyo yaweza kuhitaji upasuaji na matibabu ili kupunguza hatari ya mshtuko wa akili. Ugonjwa wa kisukari huhusika katika visa vingi vya mshtuko wa akili, kwa hiyo kuudhibiti husaidia kuzuia mshtuko wa akili.

Mashambulio ya ghafula ya upungufu wa damu kwenye tishu, TIA, ni maonyo ya wazi ya kuwa mshtuko wa akili waweza kutokea. Hakikisha kuwa hayapuuzwi. Mwone daktari wako, na ushughulike na kisababishi cha msingi, kwani TIA huongeza hatari ya mshtuko wa akili mara nyingi.

Mtindo-maisha mzuri, wa kiasi waweza kufanya mengi katika kuzuia mshtuko wa akili. Ulaji uliosawazika na kufanya mazoezi kwa ukawaida pamoja na kupunguza sana unywaji wa alkoholi na kuacha kuvuta sigareti kwaweza kusaidia kuwa na mishipa iliyo na afya na huenda hata kukaletea afya mishipa ambayo tayari imeharibika. Kuongeza ulaji wa matunda mabichi na mboga na nafaka, kulingana na chunguzi mbalimbali, kumesaidia kupunguza hatari ya mshtuko wa akili.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki