Vifaa vya Mnyanyaso Mkatili
JE, MANENO “pingu,” “mateso,” na “kufisha” yakushtua? Kwa maelfu ya watu walioteswa na Baraza la Kuhukumu Wazushi na wale walioteswa kwa kushukiwa kuwa wachawi katika Ulaya (kati ya karne ya 13 na ya 19), hayo yalikuwa mambo halisi yenye kusononesha. Vifaa ambavyo vimepigwa picha hapa, ambavyo ni mali ya jumba la makumbusho katika mji wa Rüdesheim kwenye Rhine, Ujerumani, vilitumiwa wakati huo. Vinatudokezea kuteseka kwa wale walioteswa.
Mhasiriwa huyo wa kusikitikiwa alipata maumivu makali sana alipoketishwa kwenye Kiti cha mateso, chenye kujaa miiba mikali akiwa uchi wa mnyama ili ahojiwe. Mikono, miguu, au viungo vya mhasiriwa viling’olewa-ng’olewa au kuharibiwa kabisa na parafujo za goti. Makucha ya paka yalitumiwa kurarua nyama yake vipande-vipande; hakuna sehemu ya mwili iliyoachwa. Kola yenye miiba ilifanya shingo, mabega, na utaya wa mwenye kuteswa kushikwa na ugonjwa wa kuoza, ambao ulitokeza kifo cha haraka kwa sababu ya damu kuingiwa na sumu.
Watesaji walioagizwa na Kanisa Katoliki la Kiroma walitumia vifaa vinavyofanana na hivyo ili kuwatesa wazushi—ambao wengi wao walikuwa watu wa kawaida ambao walikuwa wameshutumiwa na ambao walilazimishwa “kuungama” kwa njia ya kuteswa. Kwa kweli, wakati wa Baraza la Kuhukumu lililowahusisha Wawaldo, vifaa vya mateso hata vilinyunyiziwa maji matakatifu.
Jumuiya ya Wakristo ina hatia nzito kwa sababu ya matendo ya Baraza la Kuhukumu Wazushi. Mwanahistoria Walter Nigg aeleza: “Jumuiya ya Wakristo haitapata baraka tena mpaka hatimaye iungame—kwa wazi na kwa uzito—dhambi zilizofanywa wakati wa Baraza la Kuhukumu Wazushi, kwa moyo mweupe na bila masharti yoyote kukana kila aina ya ujeuri kuhusiana na dini.”
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kiti cha mateso
Parafujo za goti
Kola yenye miiba
Makucha ya paka
[Hisani]
Picha zote: Mittelalterliches Foltermuseum Rüdesheim/Rhein