Maoni ya Biblia
Mwaka wa 2000 Ni Wenye Maana Kadiri Gani?
WATU wengi hawaambatishi umaana wowote wa kidini na kile kitakachotukia katika nchi za Magharibi na nyinginezo kwenye mwaka wa 2000. Kwa kielelezo, Wayahudi, Waislamu, na Wahindu wote wana kalenda zao za kidini ambazo hazilingani na za Magharibi. Kuhusu tarehe za kidini na za kidesturi, Wachina hufuata kalenda ya mwezi. Hivyo, mabilioni ya watu leo, labda idadi kubwa ya watu ulimwenguni, hawauhesabii mwaka wa 2000 umaana wa kipekee.a
Hata hivyo, hasa katika nchi za Magharibi, wengi wanangojea kwa hamu kilele kinachokaribia cha milenia inayofuata kama ilivyoonyeshwa na kalenda ya Gregory. Kwa wengine si udadisi tu. Wanauona mwaka wa 2000 ukianzisha muhula mpya, ukiwa wakati wa badiliko la maana katika historia. Wengi wanaodai kuitikadi katika Biblia hushirikisha utimizo wa unabii na mwaka wa 2000. Wengine hutarajia udhihirisho wa kiroho ulio mkubwa. Wengine huhofia badiliko la ghafula—mwisho wa ulimwengu. Je, Biblia huandaa msingi wowote kwa mataraja haya?
Yehova, Yule Mtunza-Wakati
Mungu wa Biblia hufafanuliwa kuwa “mzee wa siku.” (Danieli 7:9) Yeye hudhibiti wakati kwa usahihi kamili, kama ishuhudiwavyo na utendaji mwingi wa uumbaji wake, kutoka kwenye mhimili wa sayari mpaka kwenye mwendo ndani ya atomi. Yeye ana ratiba yake ambayo hushikamana nayo kwa usahihi. “Naye aliagiza nyakati zilizowekwa na mipaka iliyowekwa ya makao ya watu,” yasema Biblia. (Matendo 17:26) Yehova ni Mtunza-Wakati barabara.
Kulingana na hayo, Biblia hutolea uangalifu mahususi kronolojia. Inaandaa rekodi yenye kuendelea ambayo huruhusu njia ya kuhesabia kurudi nyuma hadi mwanzo wa historia ya kibinadamu. Kikokotoo cha namna hiyo huelekeza kwenye mwaka wa 4026 K.W.K. kuwa mwaka ambao Mungu alimwumba Adamu. Karibu miaka 2,000 baadaye, Abrahamu alizaliwa. Miaka mingine 2,000 ilikuwa imepita kufikia wakati wa kuzaliwa kwa Yesu.
Watu fulani ambao hujifunza kronolojia ya Biblia wamebuni milinganyo isiyo na msingi ambayo huelekeza kwenye tarehe mahususi katika wakati ujao. Kwa kielelezo, wakitumia kama msingi vipindi vya mfululizo vinavyokaribia miaka 2,000 ambavyo vilitenganisha Adamu, Abrahamu, na Yesu, wengine hutabiri tukio lenye kutisha mwishoni mwa kipindi cha miaka 2,000 tangu kuzaliwa kwa Yesu. Hiki ni kielelezo kimoja tu cha njia kadhaa za kuhesabia ambazo hudaiwa kuwa zategemea kronolojia ya Biblia.
Kwa kweli, Biblia husema juu ya wakati ambapo Yehova Mungu ataingilia mambo ya binadamu kwa kuondoa uovu na kuleta ulimwengu mpya. Unabii wa Biblia husema juu ya “wakati wa mwisho,” “umalizio wa mfumo wa mambo,” “siku za mwisho,” na “siku ya Yehova.” (Danieli 8:17; Mathayo 24:3; 2 Timotheo 3:1; 2 Petro 3:12) Hata hivyo, “mwisho” unaotolewa unabii katika Biblia hauhusiani kwa vyovyote na mwaka wa 2000. Hakuna jambo lolote katika Maandiko linalohesabia umaana wa pekee mwisho wa milenia ya pili kama inavyohesabiwa na kalenda ya Gregory.
“Ni Wakati Gani Mambo Haya Yatakuwa?”
Mitume wa Yesu walidhihirisha upendezi mwingi katika ratiba ya Mungu wakati walipomwuliza Yesu: “Tuambie, Ni wakati gani mambo haya yatakuwa, nayo itakuwa ni nini ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Wengi leo hushiriki hamu inayofanana na hiyo kuhusu wakati ujao. Ni jambo la asili kupendezwa sana na unabii wa Biblia wenye maana kama huo na wakati wa kutimizwa kwao. Hata hivyo, ni jambo la hekima kukubali na kustahi msimamo wa Mungu katika jambo hilo.
Kupitia kwa Mwana wake, Yehova amefunua akili yake na ametoa jibu la moja kwa moja juu ya suala hili. Muda mfupi kabla ya Yesu kupaa mbinguni, mitume wake walimwuliza tena kuhusu mpangilio wa utimizo wa ahadi za Mungu. Yesu alijibu: “Si juu yenu kupata ujuzi wa nyakati au majira ambayo Baba ameweka katika mamlaka yake mwenyewe.” (Matendo 1:7) Kwenye pindi iliyotangulia, Yesu aliwaambia mitume wake: “Kuhusu siku hiyo na saa hiyo hakuna mtu ajuaye, wala hao malaika wa mbingu wala Mwana, ila Baba tu.”—Mathayo 24:36.
Kwa wazi, “ujuzi wa nyakati au majira,” hasa kwa habari ya utimizo wa wakati ujao wa unabii wa Biblia, hauko chini ya mamlaka ya binadamu. Mungu ameamua kutotufunulia habari kama hiyo. (Mathayo 24:22-44) Je, tungeweza kwa njia yoyote kuathiri kusudi la Mungu kwa kufumbua “siku hiyo na saa hiyo” kwa njia yetu wenyewe, kinyume cha matakwa yake? Bila shaka, jambo hili halingewezekana. (Hesabu 23:19; Waroma 11:33, 34) Biblia hutaarifu: “Shauri la BWANA lasimama milele.” (Zaburi 33:11) Akiwa Mungu mweza yote, yeye hufanikiwa sikuzote.—Isaya 55:8-11.
Licha ya uwezo wa Mungu wa kuweka “ujuzi wa nyakati au majira . . . chini ya mamlaka yake mwenyewe,” wengi bado hupenda kukisia. Wengine huwa manabii waliojiweka wenyewe wa maangamizi. Kwa sababu hii mtume Paulo alitoa maagizo hususa kwa Wathesalonike kuhusu hatari za kuwasikiliza wale wanaokisia tarehe. Aliandika: “Twawaomba nyinyi msiwe wenye kutikiswa upesi kutoka kwenye kufikiri kwenu wala kuwa wenye kusisimuliwa ama kupitia usemi uliopuliziwa au kupitia ujumbe wa maneno au kupitia barua kama kwamba ni kutoka kwetu, ya kuwa siku ya Yehova ipo hapa. Msiache mtu yeyote awashawishi nyinyi katika namna yoyote.”—2 Wathesalonike 2:1-3.
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwa uthabiti kwamba makusudi ya Mungu kwa wakati ujao yatatekelezwa kwa uhakika katika wakati alioamua kimbele, mpaka kwenye siku na saa barabara aliyochagua. (Habakuki 2:3; 2 Petro 3:9, 10) Na twaamini kwamba matukio haya yatatukia wakati ujao usio mbali sana. (2 Timotheo 3:1-5) Hata hivyo, hatukisii au kuunga mkono nadharia zinazoenea leo.b Kwa hakika, wala mwaka wa 2000, wala wa 2001, wala badiliko lolote la ghafula lililowekwa na wanadamu hauhusiani na ratiba ya Yehova.
[Maelezo ya Chini]
a Kutokana na maoni ya kistadi, inayosemekana kuwa milenia ya tatu itaanza Januari 1, 2001. Milenia ya kwanza ilianza kwa mwaka wa 1, badala ya mwaka wa sufuri. Hata hivyo, umma hushirikisha neno “milenia ya tatu” na mwaka wa 2000. Makala hii huelekeza kwenye mataraja yanayopendwa na wengi kuhusu mwaka wa 2000.
b Toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1997, ukurasa wa 21-22, lilitaarifu: “Mashahidi wa Yehova wamekuwa na hamu ya kujua wakati ambapo siku ya Yehova itatukia. Nyakati nyingine kwa sababu ya hamu yao wamejaribu kukadiria wakati ambao huenda siku hiyo ikaja. Lakini kwa kufanya hivyo, kama vile walivyofanya wanafunzi wa mapema wa Yesu, wameshindwa kutii onyo la Bwana-Mkubwa wao kwamba “sisi ha[tu]jui ni lini ulio wakati uliowekwa rasmi.” (Marko 13:32, 33) Wadhihaki wamewadhihaki Wakristo waaminifu kwa sababu ya mataraja yao ya kabla ya wakati. (2 Petro 3:3, 4) Hata hivyo, Petro athibitisha kwamba siku ya Yehova itakuja, kulingana na ratiba Yake.”