Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Talaka Naandika ili niwashukuru sana kwa ajili ya mfululizo wa makala “Malezi ya Mtoto—Ni Maoni Gani Yaliyosawazika?” (Desemba 8, 1997) Baada ya talaka yangu kulikuwa na matatizo ya kuamua ni muda gani aliyekuwa mume wangu alipaswa kutumia pamoja na binti yangu. Mume wangu wa pili alihisi kwamba uhuru huo wa kumwona binti yangu ulipaswa kukatishwa kwa kadiri iwezekanavyo. Lakini gazeti la Amkeni! lilisuluhisha suala hili kwa kutanguliza hali njema ya mtoto na siyo hisia za wazazi au wazazi wa kambo.
L. C., Wales
Nilikuwa na binti, mtoto wangu pekee ambaye alichukuliwa mahakama ilipoamua kwamba alipaswa kuishi na baba yake. Kwa hiyo makala hiyo ilionekana kama iliandikwa kwa ajili yangu. Ni baraka kujua kwamba Yehova anatupatia ‘chakula kwa wakati unaofaa.’—Mathayo 24:45.
D. B., Uswisi
Nilimshukuru Yehova nikilia machozi nilipoona jalada la Amkeni!, kwa kuwa nilikuwa katika pigano la malezi ya mtoto kwa miaka miwili. Limekuwa lenye kugusa hisia sana. Kwa kweli nathamini jinsi habari hii ilivyoandikwa kwa njia yenye kuarifu na kwa ufikirio mzuri.
A. F., Marekani
Nilipokuwa mtoto tu, wazazi wangu walitalikiana. Nilihisi nimegawanyika katikati yao wawili. Basi waweza kuwazia jinsi nilivyovutiwa na makala kuhusu habari hii. Nathamini sana kwamba mlishughulikia tatizo hili kwa kufikiria maoni ya watoto.
K. D., Yugoslavia
Mbuga za Milimani Ningependa kuwashukuru sana kwa makala “Umaridadi wa Mbuga za Taifa za Milimani.” (Novemba 22, 1997) Kwa kusema wazi, nilikuwa nimepuuza kimakusudi makala za hapo awali kuhusu maumbile. Lakini niliona picha zenye kupendeza zilizoandamana na makala na kuamua kuisoma. Nilipomaliza, niling’amua jinsi ambavyo nimepoteza fursa nzuri ya kusoma makala nyingine nyingi zenye kupendeza kuhusu maumbile.
T. M., Ukrainia
Ugoni-Jinsia-Moja Nilisisimuka kupokea Amkeni! la Desemba 8, 1997, lililokuwa na makala “Maoni ya Biblia: Je, Wakristo Wachukie Wagoni-Jinsia-Moja?” Iliandikwa vizuri na ilishughulikia kwa njia yenye usawaziko habari yenye kuhitaji busara.
L. W., Marekani
Uchoshi Nilimpa msimamizi wangu nakala ya ile makala “Je, Wachoshwa na Kazi Yako?” (Desemba 22, 1997) Asubuhi iliyofuata tulipokuwa kazini, aliniambia kwamba makala hiyo ilikuwa bora kabisa. Aliwapa baadhi ya wafanyakazi wenzangu na kuacha nakala ya gazeti hilo katika ukumbi wetu wa kupumzikia. Makala yenu ilikuja kwa wakati unaofaa!
V. L., Marekani
Asanteni kwa habari yenye kupendeza. Nina umri wa miaka 17 na ninafanya kazi ya wakati wote. Makala hiyo ilitoa shauri bora kabisa la jinsi ambavyo ninaweza kufanya kazi yangu ipendeze zaidi. Asanteni!
E. A., Italia
Asanteni sana kwa makala hiyo. Kwa wakati huu niko katika mwaka wa pili wa kujifunza ufundi na nilikuwa nikipatwa na msononeko, bila kufurahia kazi yangu tena kamwe. Makala hiyo ilinisaidia kufurahia tena kazi yangu.
I. F., Ujerumani
Rave Nina umri wa miaka 19 na nimefurahia kikweli kusikiliza muziki wa techno. Lakini nilipendezwa sana na makala “Vijana Huuliza . . . Je, Rave Ni Burudani Zisizo na Madhara?” (Desemba 22, 1997) Hii ndiyo makala ya kwanza kuona ambayo hufafanua kwa usahihi aina hii ya muziki. Ninashukuru hasa kwa ile sehemu “Je, kwa Kweli Rave Inakufaa?” Kwa njia ya maswali na maandiko, nilisaidiwa kufikia mkataa sahili na wa kiakili.
A. P., Slovenia