Maisha Yenye Usalama wa Kudumu
UKIWA na homa yaelekea utatafuta tembe ili kutuliza maumivu ya kichwa na labda barafu ili kukutuliza. Lakini ingawa tembe na barafu hukuwezesha kuvumilia dalili, hazitibu chanzo cha homa yako. Na ikiwa tatizo lako la kiafya ni baya sana, wahitaji matibabu kutoka kwa tabibu mwenye uzoefu.
Wanadamu wanasumbuliwa na homa isiyoisha ya ukosefu wa usalama. Kwa kufaa sisi huchukua hatua za kupunguza dalili kwa muda mfupi, lakini tiba yaweza kutokana na mtu fulani awezaye kuchunguza kwa umakini hali yetu. Na hakuna mtu ajuaye wanadamu vizuri zaidi kuliko Muumba wetu, Yehova Mungu. Yeye ajua kwamba maisha si salama kwa sababu ya matatizo yaliyoletwa juu yetu.
Mwanzo Wenye Usalama Waharibiwa
Neno la Mungu laeleza kwamba Yehova aliumba wanadamu wawili wa kwanza wakiwa wakamilifu na kuwaweka katika mazingira yenye usalama. Hawakuwa na hangaiko. Kusudi la Mungu kwa wanadamu lilikuwa waishi milele katika paradiso, yenye usalama kamili. Mazingira ya kwanza ya jamii ya kibinadamu yalitia ndani “kila mti unaotamanika kwa macho na kufaa kwa kuliwa.” Ona kwamba mahitaji yao ya kimwili yalishughulikiwa, na ndivyo na mahitaji yao ya kihisia-moyo, kwa kuwa mazingira hayo yalifafanuliwa kuwa “yenye kutamanika kwa macho.” Bila shaka hili lilimaanisha kwamba wanadamu wawili wa kwanza waliwekwa katika mazingira yaliyowapa maisha imara, yasiyo na taabu.—Mwanzo 2:9.
Adamu na Hawa walikataa utawala wenye upendo wa enzi kuu ya Mungu, hivyo wakitokeza hisia za shaka, hofu, aibu, hatia, na ukosefu wa usalama katika maisha yao. Baada ya kumkataa Mungu, Adamu alikiri kwamba ‘aliogopa.’ Wanadamu wa kwanza walijifunika na kujificha kutoka kwa Muumba wao mwenye upendo, ambaye kufikia wakati huo walikuwa wamefurahia uhusiano wa karibu na wenye faida pamoja naye.—Mwanzo 3:1-5, 8-10.
Kusudi la Yehova la awali halijabadilika. Biblia yasema kwamba Muumba wetu ni Mungu mwenye upendo, ambaye karibuni atawezesha wanadamu watiifu warudishe dunia iwe katika hali ya paradiso na kuishi katika usalama milele. Kupitia nabii Isaya ahadi hii yatolewa: “Naumba mbingu mpya na nchi mpya, . . . furahini, mkashangilie daima.” (Isaya 65:17, 18) Kuhusu hizi mbingu mpya na dunia mpya, mtume Petro asema hivi: “Na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.
Jambo hili litawezekanaje? Kupitia kwa serikali iliyowekwa mahali pake na Yehova. Huu ndio Ufalme ambao Yesu Kristo aliwaambia wafuasi wake waombe juu yake: “Baba yetu uliye katika mbingu, jina lako na litakaswe. Acha ufalme wako uje. Mapenzi yako na yatendeke, kama ilivyo katika mbingu, pia juu ya dunia.”—Mathayo 6:9, 10.
Ufalme wa Mungu utaondoa serikali za kibinadamu na kutekeleza kusudi la Mungu ulimwenguni pote kwa njia ya upendo. (Danieli 2:44) Shaka, hofu, aibu, hatia na ukosefu wa usalama ambao umewasumbua wanadamu tangu siku za Adamu utatoweka. Kulingana na Biblia, Ufalme huo uko karibu sana. Hata sasa, katika ulimwengu wetu wenye msukosuko, kuna kiasi fulani cha usalama kinachopatikana kwa wale wanaotamani Ufalme wa Mungu.
Tanguliza Mambo ya Kiroho
Daudi alikuwa mtumishi wa Mungu aliyefahamu hali ya kuogopa na kuwa na msononeko. Na bado Daudi aliandika hivi, kama ilivyorekodiwa kwenye Zaburi 4:8: “Katika amani nitajilaza na kupata usingizi mara, maana Wewe, BWANA, peke yako, ndiwe unijaliaye kukaa salama.” (Italiki ni zetu.) Ingawa nyakati fulani Daudi alizungukwa na matatizo, Yehova alimpa usalama. Je, twaweza kujifunza jambo fulani kutokana na hili? Twaweza kupataje kiasi fulani cha usalama hata katika ulimwengu usio na usalama?
Fikiria simulizi la Mwanzo juu ya Adamu na Hawa. Ni lini walipopoteza usalama? Mara tu walipopoteza uhusiano wao wa kibinafsi pamoja na Muumba wao na kukataa kuishi kupatana na kusudi lake kwa wanadamu. Kwa sababu hiyo, tukirudisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova na kujaribu kuishi kupatana na mapenzi yake, hata sasa tunaweza kufurahia maisha yenye usalama kuliko iwezekanavyo kwa njia nyingineyo.
Kumjua Yehova kupitia kwa funzo la Biblia hutusaidia kuelewa kusudi la uhai. Ndipo tu tuwezapo kufahamu sisi ni akina nani na kwa nini tuko hapa. Maisha yenye usalama yawezekana tunapompenda Mungu, kujua kusudi lake kwa wanadamu, na kuelewa mahali panapotufaa. Mtu mmoja anayeitwa Paul aligundua jambo hilo miaka kadhaa iliyopita.
Paul alizaliwa na kukulia katika kimojawapo cha visiwa vilivyo katika pwani ya Ujerumani. Kwa sababu ya mambo ambayo wazazi wake walijionea katika Vita ya Ulimwengu ya Pili, familia yao haikupendezwa na dini. Paul asema hivi kujihusu alipokuwa kijana: “Sikuamini katika kitu chochote na sikustahi mtu yeyote. Nilizoea kutatua huzuni yangu kwa kunywa kileo, nikinywa kupita kiasi mara mbili au tatu kwa juma. Sikuwa na usalama maishani mwangu.”
Kisha Paul akawa na mazungumzo na mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Paul alibishana sana, lakini alifikiria jambo moja lililosemwa na Shahidi huyo. “Hakuna kitu kinachotokea chenyewe.” Yaani, kila kitu cha asili kinachotuzunguka kina Muumba.
“Nilifikiria jambo hilo mara kadhaa, nikakubali.” Kwa hiyo Paul alijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova akaja kumjua Yehova. Akiri hivi: “Mbali na wazazi wangu, Yehova ndiye mtu wa kwanza kupata kunifanyia jambo fulani maishani mwangu.” Paul alibatizwa akawa Shahidi katika mwaka wa 1977 na asema hivi: “Sasa nafahamu kikweli kusudi la uhai ni nini. Nafurahia kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova. Nahisi usalama, kwa kuwa hakuna jambo lolote liwezalo kunipata mimi au familia yangu asiloweza kurekebisha Yehova katika wakati ujao.”
Twaweza kujifunza nini kutokana na jambo hili? Paul alishinda ukosefu wake wa usalama—mzigo wa kihisia-moyo—kwa kutokazia mali za kimwili, bali mambo ya kiroho. Alisitawisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Muumba. Mamilioni ya Mashahidi wa Yehova wanafurahia uhusiano wa namna hiyo. Huu huwapa nguvu za ndani zinazowasaidia wajidhabihu wanaposhughulika na wengine. Kwa kuwatembelea watu nyumbani kwao, Mashahidi wa Yehova hutumia wakati wao kusaidia watu wengine wafanye maisha yao kuwa salama zaidi kwa kukazia mambo ya kiroho. Lakini Mashahidi hufanya mengi zaidi ya kuhubiri tu.
“Mwitieni Mungu Wenu, Yehova”
Mnamo Julai 1997 Mto Oder ulipogharikisha maeneo makubwa ya kaskazini mwa Ulaya, Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani walisikia habari za taabu iliyowapata watu katika nchi jirani ya Poland. Wangefanya nini? Mashahidi mmoja-mmoja katika Berlin na maeneo ya karibu walionyesha ukarimu wa ajabu kwa kutoa kwa hiari pesa zinazozidi dola 116,000 kwa siku chache.
Mashahidi waliokuwa na ujuzi wa kujenga walisafiri kwa gharama yao wenyewe, kwa muda wa saa sita kwa gari—kutoka Berlin hadi kwenye eneo linalokaribia Wroclaw, Poland. Katika mji mmoja mdogo, nyumba nyingi zilikuwa zimeharibiwa vibaya. Nyumba moja ya familia ya Mashahidi ilikuwa kwenye maji yaliyofikia kina cha meta 6. Binti kutoka familia hiyo alipanga kuolewa mwezi ambao ungefuata na kuishi katika nyumba hiyo pamoja na mume wake. Ni nini lingeweza kufanywa ili kurekebisha nyumba hiyo na kusaidia familia hiyo, iliyokuwa imepoteza karibu kila kitu?
Maji yalipopungua, jirani mmoja aliuliza hivi kwa kudhihaki: “Mbona msimwitie Mungu wenu Yehova, na kuona kama atawasaidia?” Jirani huyo alishangaa kama nini wakati siku iliyofuata magari kadhaa kutoka Ujerumani yalipokuja kwenye nyumba ya familia hiyo ya Mashahidi! Kikundi cha wageni kilitoka katika magari hayo na kuanza kurekebisha nyumba hiyo. “Hao ni akina nani? Ni nani anayegharimia vifaa?” akauliza jirani. Familia hiyo ya Mashahidi ilieleza kwamba hao walikuwa ndugu zao wa kiroho na kwamba wageni hao walilipia vifaa. Wakazi wa mji huo walitazama kwa mshangao nyumba ilipokuwa ikirekebishwa. Ikatukia kwamba ndoa hiyo ilifanyika katika tarehe iliyopangiwa.
Familia hii iligundua kwamba kuwa miongoni mwa udugu wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova hakuleti tu baraka za kiroho bali pia kiasi fulani cha usalama katika ulimwengu wenye msukosuko. Si wao peke yao waliopatwa na jambo hili. Katika eneo lote lililokumbwa na msiba huu, nyumba na Majumba ya Ufalme ya Mashahidi wa Yehova yalirekebishwa. Na majirani wasiokuwa Mashahidi hawakusahauliwa. Kazi nyingi ilifanywa pia katika nyumba zao, nao walithamini sana.
Uadilifu, Utulivu, na Usalama
Sisi humshukuru kama nini tabibu aliyetusaidia wakati homa kali iishapo na kurejelea afya nzuri! Jinsi tutakavyomshukuru Muumba wetu wakati homa ya ukosefu wa usalama inayowapata wanadamu itakapoondolewa milele kupitia kwa Ufalme wa Mungu! Ndiyo, ni yeye anayetuahidi uhai “uadilifu wa kweli, utulivu na usalama kwa wakati usio dhahiri.” Ni tazamio la ajabu kama nini!—Isaya 32:17, NW.
[Blabu katika ukurasa wa 10]
Twaweza kuondoa mzigo wa kihisia-moyo kwa kutokazia mali za kimwili bali mambo ya kiroho
[Picha katika ukurasa wa 8, 9]
Mungu aahidi ulimwengu mpya ambapo watu wote wataishi katika usalama wenye kudumu