Maoni ya Biblia
Thamani ya Faragha
KATIKA pindi moja Yesu “a[li]panda kwenda katika mlima akiwa peke yake mwenyewe ili kusali. Ingawa ilikuwa jioni-jioni, alikuwa huko peke yake.” (Mathayo 14:23) Katika pindi nyingine, “kulipokuwa mchana, akatoka kwenda na kuendelea mbele hadi mahali pa upweke.” (Luka 4:42) Maandiko haya yashuhudia kwamba Yesu Kristo alitafuta na kuthamini vipindi vya mara kwa mara vya faragha.
Biblia huandaa vielelezo vingine vya wanaume ambao, kama vile Yesu, walithamini pindi za faragha. Mtunga-zaburi alitafakari juu ya ukuu wa Muumba wake Mtukufu wakati wa faragha ya ulinzi wa usiku. Na katika hali ya Yesu Kristo, baada tu ya kusikia habari za kifo cha Yohana Mbatizaji, alikwenda “katika mahali pa upweke.”—Mathayo 14:13; Zaburi 63:6.
Leo, kukiwa na ghasia na vurugu ya maisha ya kisasa, faragha, iwe ni kwa hali au kwa kujichagulia, si jambo ambalo huonwa kuwa la maana sana. Je, wakumbuka ni lini ulipochukua muda kuwa peke yako? Mwanamke mmoja mchanga aliyeolewa alisema hivi: “Sijapata kamwe kuwa peke yangu maishani.”
Lakini je, kweli faragha yahitajiwa? Ikiwa ndivyo, nyakati za unyamavu zaweza kutumiwaje kwa manufaa na kwa kuthawabisha? Na usawaziko watimiza fungu gani katika kutafuta faragha?
Faragha—Kwa Nini Ni Yenye Thamani?
Biblia hutuambia kwamba mwanamume wa kale wa Mungu, Isaka, alitafuta kuwa na faragha “wakati wa jioni.” Kwa nini? Yasema, “ili kutafakari.” (Mwanzo 24:63) Kulingana na kamusi moja, kutafakari ni “kufikiri kwa njia ya kuzingatia au taratibu.” “Hudokeza kipindi cha bidii na kilicho kirefu cha kukaza fikira.” Kuhusu Isaka, ambaye alikuwa akikaribia kutwaa madaraka mazito, kutafakari huko kusikoingiliwa kungemwezesha kufikiri waziwazi, kupanga mawazo yake, na kukadiria mambo ya kutangulizwa.
Mtaalamu wa afya ya kiakili asema kwamba mradi tu ‘upweke una mipaka yake, wengine wasipokuwapo hufanya iwezekane kupanga mawazo yetu, tukaze fikira vema.’ Wengi wangeweza kushuhudia kwamba hilo laweza kuburudisha, kuimarisha, na kuleta afya.
Miongoni mwa matokeo yenye kupendeza ya kutafakari ni ukamili na kujizuia, sifa zinazoelekea kuleta usemi na matendo yenye busara ambayo mwishowe, huleta upatano katika mahusiano ya kibinadamu. Kwa mfano, mtu ajuaye kutafakari pia aweza kujua wakati wa kunyamaza. Badala ya kuongea kwa haraka, yeye hufikiria mapema uwezekano wa matokeo ya maneno yake. “Je! umemwona mtu mwenye kuhamaki katika maneno?” auliza mwandikaji wa Biblia aliyepuliziwa. Yeye aendelea kusema hivi: “Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye.” (Mithali 29:20) Dawa ya matumizi hayo ya ulimi yasiyo ya kufikiri ni nini? Biblia husema: “Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu.”—Mithali 15:28; Linganisha Zaburi 49:3.
Kwa Mkristo, kutafakari kwa unyamavu pamoja na faragha ni jambo muhimu kwa ukuzi wa ukomavu wa kiroho. Maneno haya ya Paulo ni ya kufaa: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.”—1 Timotheo 4:15.
Tumia Faragha ili Kumkaribia Mungu
Mwandishi mmoja Mwingereza alisema: “Faragha ni chumba cha mapokezi cha Mungu.” Nyakati nyingine, Yesu alihisi uhitaji wa kuwa mbali na wanadamu wenzake ili kuingia mbele za Mungu akiwa faraghani. Kielelezo kimoja chafafanuliwa katika Biblia hivi: “Mapema asubuhi, kulipokuwa bado kuna giza, akaondoka akatoka nje akaenda mahali pa upweke, na huko akaanza kusali.”—Marko 1:35.
Katika Zaburi, kutafakari kwa kimungu kwatajwa kwa kurudiwa-rudiwa. Akiongea na Yehova, Mfalme Daudi alisema hivi: “Nakutafakari Wewe.” Ndivyo yalivyo maneno ya Asafu: “Nitaitafakari kazi yako yote; nitaziwaza habari za matendo yako.” (Zaburi 63:6; 77:12, italiki ni zetu.) Hivyo, kuzifikiria sifa za Mungu na shughuli zake huleta thawabu nyingi sana. Huongeza uthamini wetu kwa Mungu, kukimfanya mtu amkaribie zaidi.—Yakobo 4:8.
Kiasi Chahitajiwa
Bila shaka, faragha yapaswa kufuatiwa kwa kiasi. Faragha yaweza kufafanuliwa kuwa mahali penye kuthawabisha ambapo mtu aweza kupatembelea lakini ambapo ni hatari kubakia. Kujitenga mwenyewe sana hupingana na uhitaji wa msingi wa kibinadamu wa kushirikiana, kuwasiliana, na kupendana. Zaidi ya hilo, kujitenga kwaweza kuwa msingi ambamo kitu kama magugu ya upumbavu na ubinafsi hukua. Mithali ya Biblia huonya hivi: “Ajitengaye na wenzake hutafuta matakwa yake mwenyewe; hushindana na kila shauri jema.” (Mithali 18:1) Ili tusawazike kutafuta faragha, lazima tutambue hatari za kujitenga.
Kama Yesu na wanaume wengine wa kiroho wa nyakati za Biblia, Wakristo leo huthamini vipindi vyao vya faragha. Ni kweli, kukiwa na madaraka mengi sana na mambo ya kuhangaikia, kupata wakati na fursa ya kutafakari faraghani kwaweza kuwa jambo gumu. Hata hivyo, kama ilivyo katika kisa cha mambo yote ya thamani ya kweli, lazima ‘tujinunulie wakati unaofaa.’ (Waefeso 5:15, 16) Ndipo, kama mtunga-zaburi, twaweza kusema: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA.”—Zaburi 19:14.