Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 12/22 kur. 25-27
  • Naweza Kuishije Bila Wazazi?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuishije Bila Wazazi?
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Ni Nani Atakayenitunza?’
  • Madaraka ya Familia
  • Kujiandalia Mwenyewe
  • Kukabili Mwito wa Ushindani
  • Nawezaje Kuwa Kiolezo kwa Ndugu na Dada Zangu Wachanga?
    Amkeni!—1992
  • Kuzoea Bidii ya Kujitolea Mungu Kuhusiana na Wazazi Wazee-Wazee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1987
  • Kwa Nini Niishi Bila Wazazi?
    Amkeni!—1998
  • Kwa Nini Mimi Niwe Ndiye Kitindamimba?
    Amkeni!—1992
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 12/22 kur. 25-27

Vijana Huuliza . . .

Naweza Kuishije Bila Wazazi?

“Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu na dada yangu minne, wazazi wangu walitaliki. Waling’ang’ana juu ya malezi yetu mahakamani, na mwishowe tukajipata na mama yetu. Hata hivyo, nilipokuwa na umri wa miaka saba, dada yangu nami, tuliamua kwenda kuishi na baba yetu.”—Horacio.

MIAKA kadhaa baadaye, baba ya Horacio alikufa na msichana aliyeishi naye bila kufunga ndoa akatoroka akiwaacha Horacio na dada yake. Horacio akumbuka: “Hivyo ndivyo nikiwa na umri wa miaka 18, nilivyokuja kusimamia nyumba iliyohusisha dada yangu mwenye umri wa miaka 19, dada yangu wa kambo mwenye umri wa miaka 12—aliyeamua kuishi nasi—na mimi.”

Kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, mamilioni ya vijana duniani kote hujipata bila wazazi.a Kama Horacio, vijana fulani wameachwa. Hali, wazazi wa wengine wamekufa au wakatenganishwa na vita au misiba ya asili. Hata hali iweje, kuishi bila wazazi si rahisi na kwaweza kufadhaisha. Kwaweza kukutwika madaraka yanayokuzidi nguvu.

‘Ni Nani Atakayenitunza?’

Kufanikiwa kwako katika kukabiliana na hili kwategemea sana umri na hali zako. Kwa wazi, hali ni ngumu hata zaidi iwapo ungali mchanga au katika miaka ya mapema ya utineja. Hata wakati huo, huenda ukawa hujaachwa peke yako kabisa. Labda mjomba, shangazi, kaka, au dada ataka kuishi nawe.

Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, kutunza mayatima na wajane ni sehemu ya ibada yao. (Yakobo 1:27; 2:15-17) Na mara nyingi, watu mmoja-mmoja kutanikoni watasaidia. Kwa mfano, Horacio na ndugu zake, walikuwa wamejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na walikuwa wakihudhuria mikutano yao. Huko walikutana na familia ya Kikristo iliyoanza kuwasaidia. “Jinsi ninavyomshukuru Yehova kwa mwongozo wake na utunzaji wenye upendo siku baada ya siku!” Asema Horacio. “Tulibarikiwa kusaidiwa na familia moja ya kiroho sana kutanikoni iliyokuwa na vijana wa umri wetu. Ni kama walituasilisha, na hivyo, sawa na isivyopata kutukia awali, tulijihisi kuwa sehemu ya familia ambayo tungetegemea itusaidie.”

Hata hivyo, si vijana wote wanaofanikiwa hivyo. Ripoti moja ya Hazina ya Watoto ya Umoja wa Mataifa husema hivi: “Nyakati nyingine watoto wasioandamana na mtu hupelekwa kwa familia ambazo huwatenda vibaya kimwili, zinazowalazimisha kufanya kazi bila malipo au fursa ya kufanya maendeleo, zinazowatumia katika umalaya au hata zinazowatumikisha.” Hivyo, iwapo una mtu anayekutunza vyema, uwe mwenye shukrani.

Ni kweli, kuishi bila wazazi wako ni msiba mkubwa. Na kwa kawaida, huenda ukachukizwa na wao kutokutunza. Kuamrishwa jambo la kufanya na mtu wa jamaa au ndugu au dada mwenye umri mkubwa zaidi kwaweza kuzidisha ghadhabu yako. Lakini usiwaghadhabikie wanaojaribu kukutunza. Biblia husema hivi: “Basi ujitunze, isije hasira ikakuvuta hata ukafanya mzaha . . . Jitunze, usiutazame uovu.” (Ayubu 36:18, 21) Mkumbuke mwanamke mchanga katika Biblia aliyeitwa Esta. Akiwa yatima, alilelewa na binamu yake mkubwa Mordekai. Ijapokuwa hakuwa mzazi wake wa asili, Mordekai ‘alimwagiza’ naye alitii, hata alipopata kuwa mtu mzima! (Esta 2:7, 15, 20) Jaribu kuwa mtiifu na mwenye kushirikiana. Itasaidia sana kuondoa migogoro na kufanya maisha yawe rahisi kwa kila anayehusika.

Madaraka ya Familia

Iwapo una kaka au dada mkubwa—au iwapo u mkubwa kiasi fulani—labda mwaweza kujitegemea. Huenda hata ukahitajika kuchukua daraka la kusimamia familia—daraka linaloelekea kuzidi nguvu zako! Hata hivyo, katika hali hizo wengi wamefanya kazi zenye kusifika za kulea ndugu na dada zao wachanga.

Kwa kueleweka, huenda ukalazimika kupambana na hisia fulani za uchungu wa moyo. Kukumbuka kwamba wawapenda ndugu na dada zako kwaweza kukusaidia kuchukua mambo kwa njia nzuri. Hata laweza kukusaidia iwapo waona kuwatunza kuwa wajibu uliogawiwa na Mungu. Kwa vyovyote, Wakristo wanaagizwa wawatunze walio wao wenyewe. (1 Timotheo 5:8) Lakini hata ujaribu kadiri gani kuwa baba au mama kwa ndugu na dada zako, kwa kweli huwezi kamwe kuwa mzazi wao.

Huwezi kuwatazamia ndugu na dada zako wakuchukulie sawa na vile walichukulia wazazi wenu. Kwa kweli, huenda ikawachukua muda kuukubali mwelekezo wako. Hivyo, kabla ya wakati huo kufika, usivunjike moyo. Epuka “uchungu wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi.” Kwa kielelezo chako, wafundishe ndugu na dada zako ‘wawe wenye fadhili wao kwa wao, wenye huruma kwa njia nyororo, wakisameheana kwa hiari mtu na mwenzake.’—Waefeso 4:31, 32.

Horacio akubali alifanya makosa: “Nyakati fulani nilikuwa mkali sana kwa ndugu zangu. Lakini kwa kiasi fulani, huo ulikuwa ulinzi, nasi tulidumisha mwenendo unaofaa machoni pa Yehova.”

Kujiandalia Mwenyewe

Bila shaka, kujiandalia kimwili ni hangaiko kubwa iwapo wazazi hawapo kukutunza. Labda watu wazima walio washiriki wa kutaniko la Kikristo waweza kusaidia kukufunza wewe na ndugu na dada zako, ikiwa unao, jinsi ya kupika, kusafisha, na kutunza kazi za kila siku za nyumbani ambazo ni lazima sasa uzishughulikie. Lakini utafanya nini ili kupata pesa? Labda huna namna ila kutafuta kazi.

Hata hivyo, kazi za kuajiriwa ni chache sana kwa vijana wasio na elimu ya kutosha, wala uzoefu, wala stadi za kazi. Hivyo, ikiwezekana umalize elimu yako ya msingi—au hata upate mafunzo zaidi ya kazi—usisite kufanya hivyo. Horacio akumbuka hivi: “Dada yangu mkubwa nami tulifanya kazi tukategemeza elimu yangu na ya dada yangu wa kambo.” Iwapo waishi katika nchi inayoendelea, huenda ukalazimika kutumia ubunifu wako kupata kazi.—Ona “Kubuni Kazi Katika Nchi Zinazositawi,” katika toleo la Amkeni! la Oktoba 22, 1994.

Katika nchi zilizoendelea kiuchumi, yawezekana hata kupata msaada wa kifedha kutoka kwa serikali. Mara nyingi, kuna mashirika ya kiserikali au ya kibinafsi yaliyojitoa kusaidia mayatima na watoto walioachwa. Kwa mfano, mashirika fulani, yaweza kukusaidia upate chakula au mahali pa kuishi. Bila shaka, msaada wowote upatao wapasa kutumiwa kwa njia ya hekima. ‘Fedha ni ulinzi,’ Biblia yasema. (Mhubiri 7:12) Na usipokuwa mwangalifu katika kupanga na kuzitumia kwa uangalifu, fedha zaweza ‘kujifanyia mabawa haraka na kuruka.’—Mithali 23:4, 5.

Kujiandalia kimwili kwaweza kuwa rahisi iwapo mtu mzima anakutunza. Hata hivyo, wakati ujao, kuna wakati utakapohitaji kujiandalia mwenyewe. Kwa kuwa sasa huna wazazi wa kukuhimiza kielimu, huenda ikahitaji jitihada ya pekee kumakinika katika masomo yako. Shauri la mtume Mkristo Paulo kwa Timotheo kuhusu maendeleo ya kiroho laweza kutumiwa kuhusu masomo yako ya shule: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.” (1 Timotheo 4:15) Kwa kufanya hivyo, utawawekea kielelezo kizuri watu walio karibu nawe na vilevile utajinufaisha.

La muhimu zaidi ya yote ni uhitaji wa kujiandalia kiroho. Jaribu kusitawisha kawaida iliyosawazika ya utendaji wa kiroho. (Wafilipi 3:16) Kwa mfano, miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, ni kawaida kwa familia kuzungumzia Andiko la siku la Biblia kila siku. Mbona usifanye hili kuwa kawaida yako? Kawaida ya funzo la Biblia na ukawaida wa kuwepo kwenye mikutano ya Kikristo itakusaidia pia uwe mwenye nguvu kiroho.—Waebrania 10:24, 25.

Kukabili Mwito wa Ushindani

Si rahisi kuishi bila wazazi, lakini haimaanishi kwamba ni lazima maisha yawe yasiyovutia na yasiyofurahisha. Mama ya Paola mwenye umri wa miaka 20 alikufa Paola alipokuwa na umri wa miaka sita tu. Baba yake alikufa Paola alipokuwa na umri wa miaka kumi. Mwanamke mwenye fadhili aliwapa yeye na dada zake wanne makao. Je, maisha yake yamekuwa yenye taabu kabisa? La. Paola asema hivi: “Huenda tusiwe kama familia ya kawaida, lakini twaishi maisha ya kawaida. Kwa kweli, upendo tulio nao miongoni mwetu ni wenye nguvu kushinda familia nyingi.”

Dada ya Paola aitwaye Irene aongezea hivi: “Tujapokuwa bila wazazi wetu, tuko tu kama vijana wengine.” Ni nini shauri lake kwa wengine walio katika hali hii? “Hilo lisikufanye uhisi hufai.” Vivyohivyo Horacio asema hivi: “Hali hii ilinifanya nikomae haraka sana.”

Kupoteza wazazi ni moja ya matukio yenye maumivu yawazikayo. Ingawa hivyo, uwe na uhakika kwamba kwa msaada wa Yehova, waweza kushinda na kupokea baraka yake.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Niishi Bila Wazazi?,” katika toleo la Amkeni! la Novemba 22, 1998.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wazee Wakristo waweza kukutegemeza

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki