Kulinda Uhuru—Jinsi Gani?
KATIKA mji mdogo wa Rengasdengklok, Indonesia, vikundi vya kikabila viliishi pamoja kwa amani kwa miaka kadhaa. Hata hivyo, inaonekana uvumiliano ulifikia kikomo mnamo Januari 30, 1997. Jeuri ilizuka kabla tu ya saa tisa za usiku katika siku ya karamu ya kidini, wakati muumini alipoanza kupiga ngoma. Mtu mmoja wa dini tofauti alishawishika kumtupia matusi jirani yake kwa sababu ya kelele hiyo. Walianza kupaaziana sauti, na mawe yakaanza kutupwa. Kulipambazuka, na ghasia zikaendelea huku watu wengine wakijiunga na ugomvi huo. Mwishoni mwa siku, mahekalu mawili ya Wabudha na makanisa manne ya Jumuiya ya Wakristo yalikuwa yameharibiwa. Gazeti la habari la International Herald Tribune liliripoti kisa hiki chini ya kichwa “Moto wa Ghasia za Kikabila Wachochewa na Kutovumiliana.”
Katika nchi nyingi, vikundi vidogo vya kikabila ambavyo haki zao zinalindwa na sheria, mara nyingi hujipata vikikosa kuvumiliwa. Kutoa uhakikisho wa uhuru kupitia sheria hakumalizi visababishi vya msingi vya kutovumiliana. Uhakika wa kwamba kutovumiliana hakuonekani waziwazi haumaanishi kwamba hali hiyo haiko. Ikiwa hali zabadilika wakati fulani ujao na labda kuongoza kwenye hali zenye ubaguzi, hali ya kutovumiliana iliyojificha yaweza kujitokeza kwa urahisi. Hata ikiwa watu hawanyanyaswi moja kwa moja, waweza kuonyeshwa uhasama au mawazo yao yaweza kukandamizwa. Hali hii yaweza kuzuiwa jinsi gani?
Kufahamu Visababishi vya Kutovumiliana
Kiasili sisi huelekea kukataa au kushuku kitu ambacho ni tofauti au kisicho cha kawaida, hasa maoni ambayo hutofautiana na yetu. Je, hii yamaanisha kwamba uvumiliano ni jambo lisilowezekana? Kichapo cha UM Elimination of All Forms of Intolerance and Discrimination Based on Religion or Belief chaorodhesha kukosa ujuzi na uelewevu kuwa “miongoni mwa visababishi vya maana sana vya kutovumiliana na kubaguana kuhusiana na mambo ya kidini na itikadi.” Hata hivyo, kukosa ujuzi, ambacho ni kisababishi cha kutovumiliana, chaweza kushindwa. Jinsi gani? Kupitia elimu yenye usawaziko. “Elimu yaweza kuwa njia kuu ya kupambana na ubaguzi na kutovumiliana,” yasema ripoti moja ya Tume ya UM ya Haki za Kibinadamu.
Elimu hiyo yapasa iwe na lengo gani? Gazeti UNESCO Courier lapendekeza kwamba badala ya kuendeleza kukataliwa kwa harakati za kidini, “elimu kwa ajili ya uvumiliano yapaswa kuwa na lengo la kukinza mavutano yanayoongoza kwenye hofu na kuwatenga wengine, na yapaswa kusaidia vijana wasitawishe uwezo wa kujiamulia mambo, kufikiri kwa makini na kusababu kiadili.”
Bila shaka, vyombo vya habari vyaweza kuchangia sehemu ya maana katika kuendeleza “kufikiri kwa makini na kusababu kiadili.” Mashirika mengi ya kimataifa yanatambua uwezo wa vyombo vya habari wa kuelekeza maoni ya watu na kuendeleza maafikiano. Ingawa hivyo, ikiwa vyombo vya habari vitaendeleza kuvumiliana badala ya kutovumiliana kama vile vingine hufanya, uandishi wa habari usiopendelea wahitajiwa. Pindi kwa pindi, waandishi wa habari wanapaswa kupuuza maoni yanayokubalika na wengi. Wanapaswa kutokeza mchanganuo na maoni yasiyopendelea. Lakini je, hilo latosha?
Njia Bora ya Kupigana na Kutovumiliana
Uvumiliano haumaanishi kwamba kila mtu apaswa kuwa na mawazo yaleyale. Watu wanaweza kukosa kuafikiana. Huenda wengine wakahisi kwa dhati kwamba itikadi za mtu yule mwingine ni zenye makosa sana. Huenda hata wakaongea hadharani juu ya kukosa kuafikiana kwao. Hata hivyo, maadamu hawaenezi uwongo ili kuchochea upendeleo, huku si kutovumiliana. Hali ya kutovumiliana yaonekana wakati kikundi fulani kinaponyanyaswa, sheria mahususi zinapoelekezwa kwake, kinapotengwa, kinapopigwa marufuku, au kinapozuiwa kufuata itikadi zake katika njia fulani. Katika kutovumiliana kunakopita kiasi, wengine huua na wengine hulazimika kufa kwa ajili ya itikadi zao.
Hali ya kutovumiliana yaweza kushindwa namna gani? Yaweza kufunuliwa hadharani, kama vile mtume Paulo alivyofunua hali ya kutovumiliana ya viongozi wa kidini wa siku yake. (Matendo 24:10-13) Ingawa hivyo, inapowezekana, njia bora ya kupigana na kutovumiliana ni kufanya kazi pamoja—kuendeleza uvumiliano, yaani, kuelimisha watu wawaelewe wengine vizuri zaidi. Ile ripoti ya UM kuhusu kuondolewa kwa kutovumiliana iliyorejezewa mapema yasema: “Kwa kuwa chanzo cha namna zote za kutovumiliana na ubaguzi unaotegemea dini au itikadi kiko katika akili ya mwanadamu, kwa hiyo ni katika akili za mwanadamu ambapo hatua ya kwanza yapasa kuelekezwa.” Elimu ya namna hiyo yaweza hata kuongoza watu wachunguze itikadi zao wenyewe.
Federico Mayor, mkurugenzi mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi, na Utamaduni, aliandika hivi: “Uvumiliano ni wema wa mtu aliye na usadikisho.” Akiandika katika gazeti Réforme, kasisi wa Dominika Claude Geffré alisema: “Uvumiliano halisi hutegemea usadikisho imara.” Mtu anayeridhishwa na itikadi zake mwenyewe haelekei kutishwa na itikadi za wengine.
Mashahidi wa Yehova wamepata kwamba njia bora ya kuendeleza uvumiliano ni kuongea na watu wengine wenye itikadi tofauti. Mashahidi huchukua kwa uzito unabii wa Yesu kwamba “habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote,” na wanajulikana vizuri kwa huduma yao ya kueneza evanjeli peupe. (Mathayo 24:14) Katika kazi hii, wanapata fursa ya kuwasikiliza watu wa dini nyingi tofauti—vilevile waatheisti—wakieleza itikadi zao. Na Mashahidi wanakuwa tayari kueleza itikadi zao kwa wale wanaotaka kusikiliza. Hivyo wanaendeleza ukuzi katika ujuzi na kuelewana. Ujuzi na uelewevu huo hufanya iwe rahisi zaidi uvumiliano usitawi.
Uvumiliano na Zaidi
Licha ya makusudio mazuri ya wengi na jitihada za pamoja za wengine, kwa wazi hali ya kutovumiliana ya kidini ingali tatizo leo. Ili kuwe na badiliko halisi, kitu fulani zaidi chahitajiwa. Gazeti la habari la Kifaransa Le Monde des débats lilikazia tatizo hilo: “Mara nyingi zaidi jamii ya kisasa husumbuka kwa kukosa mambo ya kihisia-moyo na ya kiroho. Sheria yaweza kulinda wale wanaotisha uhuru wa kidini. Sheria yaweza na inapaswa kuhakikisha kuna usawa mbele ya sheria, bila ubaguzi usio na msingi.” Kitabu Democracy and Tolerance chakiri hivi: “Tuna mengi sana ya kufanyia kazi ili kufikia mradi wa kuafikiana na kustahi kiwango cha mwenendo kwa wote.”
Biblia inaahidi kwamba karibuni wanadamu wote wataunganishwa katika ibada safi ya Mungu mmoja wa kweli. Muungano huo utatokeza udugu wa ulimwenguni pote, ambapo watu watastahiana. Wanadamu hawatakosa ujuzi tena, kwa kuwa Ufalme wa Mungu utawafundisha watu njia za Yehova, hivyo ukitosheleza mahitaji yao ya kiakili, ya kihisia-moyo na ya kiroho. (Isaya 11:9; 30:21; 54:13) Usawa na uhuru halisi utajaa duniani. (2 Wakorintho 3:17) Kwa kujipatia uelewevu sahihi juu ya makusudi ya Mungu kwa wanadamu, unaweza kushinda kukosa ujuzi na kutovumiliana.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
Dini Yatishwa
Katika miaka ya hivi majuzi wenye mamlaka wamejaribu kuwadhoofisha Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa kwa kukataa kuwapa mapendeleo kama dini nyinginezo. Hivi majuzi, michango inayopokewa ili kutegemeza utendaji wa kidini wa Mashahidi ilitozwa kodi nyingi sana. Wenye mamlaka nchini Ufaransa waliweka isivyo haki kodi ya dola milioni 50 (kodi na adhabu), wakiwa na kusudi dhahiri la kudhoofisha kikundi hiki cha Wakristo 200,000 na watetezi wao katika Ufaransa. Hili ni tendo dhahiri la ubaguzi wa kidini ambalo linapingana na kanuni zote za uhuru, udugu, na usawa.
[Picha katika ukurasa wa 10]
Mara nyingi kutovumiliana huongoza kwenye jeuri
[Picha katika ukurasa wa 12]
Licha ya utendaji wa kidini wa Mashahidi wa Yehova, maofisa fulani wa Ufaransa wanadai kwamba wao si dini!