Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g99 4/22 kur. 3-5
  • Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye Kuhuzunisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye Kuhuzunisha
  • Amkeni!—1999
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hisia Nyingi Kwelikweli
  • Hasira na Hangaiko
  • Hatia na Mshuko-Moyo
  • Udanganyifu Maradufu
  • Je, Kupatana Kwawezekana?
    Amkeni!—1999
  • Kuchagua Talaka
    Amkeni!—1999
  • Talaka Biblia Inasema Nini Hasa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Ndoa-Sababu Inayofanya Wengi Waivunje
    Amkeni!—1993
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1999
g99 4/22 kur. 3-5

Kukosa Uaminifu—matokeo Yenye Kuhuzunisha

“Nimeondoka,” ikasema sauti kwenye simu—labda hayo ndiyo maneno yaliyokuwa yenye kuvunja moyo zaidi ambayo Pata aliwahi kuambiwa na mume wake. “Singeweza kuamini usaliti huo,” asema. “Jambo ambalo nilikuwa nimehofu zaidi—kwamba mume wangu angeniacha na kuchukua mwingine—likawa ukweli mchungu.”

PAT mwenye umri wa miaka 33 alitaka kufanikisha ndoa yao; mume wake alikuwa amemhakikishia kwamba hangemwacha kamwe. “Tulikuwa tumeahidi kukaa pamoja, hata kuwe na matatizo gani,” akumbuka Pat. “Nilisadiki kwamba alikuwa mnyoofu. Kisha . . . aliniacha. Sasa nimeachwa peke yangu—sina hata paka kipenzi nimebaki mpweke kabisa!”

Hiroshi hatasahau kamwe siku ambayo mama yake aligunduliwa kuwa na uhusiano wa kingono nje ya ndoa. “Nilikuwa na umri wa miaka 11 tu,” akumbuka. “Mama aliingia ndani ya nyumba mbiombio akiwa na hasira. Baba alikuwa nyuma yake, akisema, ‘Usifanye haraka. Acha tuzungumzie jambo hili.’ Ningeweza kuhisi kwamba jambo baya sana lilikuwa limetukia. Baba alivunjika moyo kabisa. Hajapata kurudia tena hali yake ya kawaida. Kwa kuongezea, hakuwa na mtu wa kumtumaini. Hivyo alikuja kwangu. Ebu wazia: mtu mwenye umri wa miaka 40 hivi akimwendea mwanaye mwenye umri wa miaka 11 ili afarijiwe na kuonyeshwa hisia-mwenzi!”

Hata ziwe ni kashfa za kimapenzi ambazo zimevuruga familia za kifalme, wanasiasa, mashujaa wa sinema, na viongozi wa kidini au uwe ni usaliti na machozi katika familia zetu wenyewe, kukosa uaminifu katika ndoa kwaendelea kusababisha majonzi mengi. Kichapo The New Encyclopædia Britannica, chasema, “inaonekana kwamba uzinzi ni jambo linalokubalika ulimwenguni pote, na katika visa fulani ni wa kawaida kama ndoa.” Watafiti fulani wanakadiria kwamba kati ya watu wapatao asilimia 50 hadi 75 wakati fulani walikosa uaminifu. Mtafiti wa mambo ya ndoa Zelda West-Meads asema kwamba ingawa mara nyingi kukosa uaminifu hakugunduliwi, “uthibitisho mwingi waonyesha kwamba kuna ongezeko la kukosa uaminifu.”

Hisia Nyingi Kwelikweli

Ingawa takwimu za kukosa uaminifu na talaka zinashtua, hazifunui madhara kamili yanayowapata watu katika maisha yao ya kila siku. Mbali na hasara kubwa za kifedha, fikiria hisia nyingi sana zinazohusika katika takwimu hizo—machozi mengi sana, na mvurugo unaopita kiasi, kihoro, hangaiko, na maumivu makali sana, na vilevile siku nyingi kupindukia ambazo washiriki wa familia hukosa usingizi. Huenda watu wanaopatwa na masaibu haya wakaendelea kuishi, lakini inaelekea watabaki na maumivu ya kihisia-moyo kwa muda mrefu. Maumivu na madhara hayo hayaishi kwa urahisi.

“Kwa kawaida mvunjiko wa ndoa hutokeza hisia-moyo nyingi sana,” chaeleza kitabu How to Survive Divorce, “zinakuwa nyingi sana hivi kwamba nyakati fulani hutisha kukuvuruga usijiendeshe kwa busara. Unapaswa kufanya nini? Unapaswa kutenda namna gani? Utakabilianaje na tatizo hilo? Huenda ukayumbayumba kati ya kuwa na uhakika na kuwa na shaka, kati ya kukasirika na kuhisi ukiwa na hatia au kati ya kuwa na itibari na kushuku.”

Hivyo ndivyo Pedro alivyohisi baada ya kupata habari kwamba mke wake alikosa uaminifu. “Kukosa uaminifu kunapotokea,” aungama hivi, “ndipo hisia-moyo nyingi sana zenye kutatanisha humlemea mtu.” Huwa vigumu sana kwa wahasiriwa kuelewa ile hali ya kuvunjika moyo—sembuse watu wasiohusika, wasioelewa vema hali hiyo. Pat adai kwamba “hakuna mtu yeyote anayeelewa kikweli jinsi ninavyohisi. Ninapofikiri juu ya mume wangu akiwa na mwanamke mwingine, mimi huhisi maumivu halisi ya kimwili, kuumwa ambako ni vigumu kuelezea mtu yeyote.” Aongezea hivi: “Kuna nyakati fulani ambapo mimi huhisi kana kwamba ninashikwa na kichaa. Siku moja ninahisi kana kwamba ninaweza kudhibiti hali; siku inayofuata nahisi siwezi. Siku moja mimi humkosa; siku inayofuata hukumbuka njama zote, udanganyi wote na kutwezwa kote alikofanya.”

Hasira na Hangaiko

“Nyakati fulani,” akiri mtu mmoja ambaye mwenzi wake alikosa uaminifu, “hisia-moyo inayokukumba ni hasira tu.” Si ghadhabu tu kuhusu kosa lililofanywa na madhara yaliyosababishwa. Badala ya hivyo, kama alivyoeleza mwandishi mmoja wa habari, ni “uchungu wa moyo kuhusu ndoa ambayo ingekuwa nzuri, lakini ikaharibiwa.”

Pia hisia za kutojistahi na kutofaa huwa jambo la kawaida. Pedro akiri hivi: “Unakuwa na hisia hizi: ‘Je, sivutii vya kutosha? Je, nina kasoro kwa njia fulani?’ Unaanza kujichanganua ili upate kosa.” Katika kitabu chake To Love, Honour and Betray, Zelda West-Meads, wa Baraza la Kitaifa la Mashauri ya Ndoa la Uingereza, atoa uthibitisho huu: “Mojawapo ya mambo magumu zaidi kukabiliana nayo . . . ni kutojistahi.”

Hatia na Mshuko-Moyo

Kwa kawaida hisia-moyo hizi hufuatiwa kwa haraka na hisia nyingi za hatia. Mke mmoja aliyekata tamaa asema: “Nafikiri wanawake husumbuliwa sana na hatia. Unajilaumu mwenyewe na kujiuliza: ‘Ni jambo gani baya nililofanya?’”

Mwanamume mmoja aliyesalitiwa afunua jambo jingine analoliita hisia-moyo zinazobadilika kwa ghafula. Aeleza hivi: “Mshuko-moyo unakuwa jambo jipya ambalo hutokea kama halihewa mbaya.” Mwanamke mmoja anakumbuka kwamba baada ya kuachwa na mume wake, hakuna siku hata moja ambayo hakulia. “Naweza kukumbuka waziwazi siku ya kwanza ambayo sikulia majuma kadhaa baada ya kuachwa,” asimulia. “Miezi kadhaa ilipita kabla sijamaliza juma moja bila kulia. Siku na majuma ambayo sikulia yakawa matukio muhimu yaliyoashiria kurudia hali yangu ya kawaida.”

Udanganyifu Maradufu

Jambo wasilotambua watu wengi ni kwamba mara nyingi mzinzi anakuwa amemwumiza sana mwenzi wake maradufu. Katika njia gani? Pat atupatia dokezo: “Ilikuwa vigumu kwa upande wangu. Hakuwa tu mume wangu bali pia rafiki yangu—rafiki bora zaidi—kwa miaka mingi.” Ndiyo, katika visa vingi mke humwendea mume wake ili kupata utegemezo matatizo yanapotokea. Sasa, hajawa tu chanzo cha matatizo yenye kufadhaisha bali pia ameacha kuwa chanzo cha msaada kinachohitajiwa sana. Katika tendo moja, amesababisha maumivu makali na kumnyang’anya mke wake mtu wa kutumaini.

Tokeo ni kwamba, mojawapo ya mambo yanayowalemea wenzi wasio na hatia ni hisi ya kina kirefu ya kusalitiwa na kuvunjwavunjwa kwa imani. Mshauri mmoja wa ndoa aeleza sababu kwa nini usaliti wa ndoa waweza kusababisha madhara makubwa sana ya kihisia-moyo: “Tunajitoa sana sisi wenyewe, matumaini yetu, miradi na mataraja yetu, kwa ndoa . . . , tukitafuta mtu fulani tunayeweza kumwitibari kikweli, mtu tunayehisi tunaweza kumtegemea sikuzote. Itibari hiyo inapopotezwa kwa ghafula, inaweza kuwa kama nyumba iliyojengwa kwa karata inayoanguka ghafula.”

Kwa wazi, kama inavyosemwa katika kitabu How to Survive Divorce, wahasiriwa “wanahitaji msaada kuchanganua mabadiliko makubwa ya kihisia-moyo . . . Huenda wakahitaji msaada wa kuamua ni mambo gani watakayofanya na jinsi ya kuyafanya.” Lakini mambo hayo ni yapi?

Huenda ukajiuliza, ‘Je, kupatana ndilo suluhisho letu?’ ‘Au je, nitaliki?’ Hasa ndoa inapokuwa na mikazo, waweza kuchochewa kufikia mkataa wa haraka kwamba talaka ndiyo suluhisho kwa matatizo yenu. Huenda ukasababu kwamba ‘kwa vyovyote, Biblia huruhusu talaka kwa msingi wa kukosa uaminifu katika ndoa.’ (Mathayo 19:9) Kwa upande mwingine, huenda ukasababu kwamba Biblia haisisitizi juu ya talaka. Kwa hiyo, waweza kuhisi kwamba ingekuwa bora kutafuta upatanisho, kujenga upya ndoa na kuiimarisha.

Kumtaliki au kutomtaliki mwenzi asiye mwaminifu ni uamuzi wa kibinafsi. Lakini unaweza kujuaje jambo la kufanya? Kwanza, tafadhali chunguza baadhi ya mambo yanayoweza kukusaidia kuamua ikiwa kupatana kunawezekana.

[Maelezo ya Chini]

a Baadhi ya majina yamebadilishwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki