Mambo Halisi Yamezidi Mataraja Yangu
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA WILLEM VAN SEIJL
Ilikuwa mwaka wa 1942, nchi yetu ilipokuwa ikishiriki katika Vita ya Ulimwengu ya Pili. Nilikuwa mmojawapo wa vijana watano waliokuwa wakijificha Wanazi huko Groningen, Uholanzi. Tukiwa tumeketi katika chumba kidogo, tulianza kuzungumza juu ya uwezekano wa kuokoka.
KWA WAZI kulikuwa na uwezekano mdogo sana kwamba tungeokoka. Ikatukia kwamba, vijana watatu kati yetu walichinjwa kinyama. Kwa kweli, mimi peke yangu ndiye niliyesalia hadi kufikia umri wa uzee. Hili ni mojawapo tu ya mambo halisi yanayozidi mataraja yangu.
Kisa kilichotajwa mwanzoni kilipotukia, nilikuwa na umri wa miaka 19 tu, na sikujua mengi kuhusu Biblia au dini. Kwa kweli, Baba alikataa dini zote. Juhudi ya Mama ya kutafuta dini ilimwongoza kwa uwasiliani-roho. Mimi sikuwa na tumaini lolote. Niliona kwamba hata kama ningekufa kwenye shambulio la bomu au kwa njia nyingineyo yote, Mungu hangekuwa na sababu ya kunikumbuka. Hata sikuwa nimejaribu kujifunza juu yake.
Jitihada ya Kutafuta Yathawabishwa
Upesi baada ya yale mazungumzo pamoja na wale vijana wanne, nilikamatwa na Wanazi na kupelekwa katika kambi ya wafungwa huko Ujerumani, karibu na Emmerich. Kazi yetu ilitia ndani kufagia vifusi na kurekebisha uharibifu uliosababishwa na mashambulizi ya mabomu ya majeshi ya Muungano. Ijapokuwa vita ilikuwa imepamba moto, nilitoroka na kurudi Uholanzi mwishoni mwa 1943.
Kwa njia fulani nilipokea kijitabu chenye maswali na maandiko mengi ya Biblia. Kilitumiwa katika funzo la kitabu Salvation, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Kwa kusoma maswali na kutafuta maandiko, nilipendezwa sana na utimizo wa unabii wa Biblia.
Nilizungumza na mchumba wangu, Gré, juu ya mambo niliyokuwa nikisoma, lakini mwanzoni hakupendezwa sana. Kwa upande mwingine, Mama alisoma kwa makini kijitabu hicho. “Hii ndiyo kweli ambayo nimekuwa nikiitafuta katika maisha yangu yote!” akasema kwa mshangao. Niliwaeleza pia marafiki, na baadhi yao walitaka kujua zaidi. Kwa hakika, mmoja wao, akawa Shahidi, na tuliwasiliana naye kwa ukawaida kupitia kwa barua na kutembeleana hadi alipokufa mnamo 1996.
Wakati huohuo, Gré alianza kujifunza Biblia, tukabatizwa sote mnamo Februari 1945. Miezi michache baadaye vita ikakoma. Baada ya kufunga ndoa, tulitaka kuwa mapainia, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Lakini tulikabili vizuizi—magonjwa na matatizo ya kifedha. Fursa za kuweza kuchuma fedha nyingi zaidi zilijitokeza pia. Je, tungefanya kazi ili tupate ulinzi wa kifedha kwanza halafu tuanze kupainia, au tungeanza mara moja?
Huduma Yetu Huko Uholanzi
Tuliamua kuanza kazi ya upainia mara moja, tuliyoianza Septemba 1, 1945. Siku iyo hiyo, nilipokuwa nikirejea nyumbani usiku sana, niliingia kwenye mkahawa kupata kinywaji. Nilimpa mhudumu wa mkahawa kile nilichodhani kuwa noti moja ya gulden nikamwambia: “Chukua fedha zitakazosalia.” Nilipofika nyumbani, niligundua kwamba nilikuwa nimempa noti ya gulden 100! Tulibaki na gulden moja tu tulipoanza upainia!
Nilipoanza kutoa hotuba za Biblia za watu wote mnamo 1946, nilikuwa na koti moja la ngozi. Rafiki mwenye umbo sawa na langu, alikuwa mwenyekiti. Angenikaribisha kutoa hotuba na mara moja angerudi nyuma ya jukwaa na kunipa koti lake. Kisha ningetoa hotuba. Mwishoni mwa hotuba tulifanya vivyo hivyo!
Katika Machi 1949, mimi na Gré tulipokea mwaliko wa kushiriki kazi ya mzunguko, kuzuru makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ili kuyaimarisha kiroho. Fritz Hartstang, ambaye amekuwa mhudumu mwaminifu kabla na baada ya vita, alinizoeza kazi ya mzunguko. Alinipa shauri zuri: “Wim, fuata maagizo unayopokea kupitia kwa tengenezo la Yehova hata ikiwa mwanzoni unaona kwamba hayafai. Hutajuta kamwe.” Alisema kweli.
Mnamo 1951, Nathan H. Knorr, msimamizi wa Watch Tower Bible and Tract Society, alizuru Uholanzi. Wakati huo, mimi na Gré tulijaza ombi la mazoezi ya umishonari katika Marekani. Muda mfupi baadaye, tulipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 21 la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower. Tulipoanza kupainia mwaka wa 1945, kulikuwa na Mashahidi wapatao 2,000 huko Uholanzi, lakini kufikia 1953, walikuwa zaidi ya 7,000, jambo halisi lililozidi kwa mbali mataraja yetu!
Huduma Katika Makao Yetu Mapya
Tulipata mgawo wa kwenda Dutch New Guinea, ambao sasa ni mkoa wa Indonesia, lakini tuliponyimwa kibali, tulipata mgawo mwingine huko Suriname, nchi yenye joto ya Amerika Kusini. Tuliwasili Desemba 1955. Wakati huo Suriname ilikuwa na Mashahidi wapatao mia moja tu, lakini walitusaidia sana. Punde si punde tukazoea makao hayo.
Ni kweli kwamba, tulihitaji kujipatanisha na hali mbalimbali, na nyakati nyingine kufanya hivyo kulihitaji jitihada kubwa. Kwa mfano, Gré alihofu sana mdudu wa aina yeyote. Huko Uholanzi, alipoona buibui mdogo katika chumba chetu cha kulala, alishindwa kulala hadi nilipomwondoa buibui huyo. Lakini Suriname ina buibui ambao ni wakubwa kuliko hao wa Uholanzi kwa mara kumi, na baadhi yao ni wenye sumu! Makao yetu ya mishonari yalikuwa pia na mende, panya, chungu, mbu, na panzi. Hata nyoka waliingia nyumbani pia. Gré amezoea viumbe hao hivi kwamba ni kawaida yake kuwaondoa nyumbani.
Baada ya zaidi ya miaka 43, tumepata kuijua nchi hii vizuri zaidi ya wenyeji wengi. Tumependezwa na mito yake, misitu ya mvua, na vinamasi vyake karibu na pwani. Tumejua pia wanyama wengi wa nchi hii—nungunungu, sloth, chui wa Amerika ya Kati, naam, hata aina mbalimbali za nyoka, ambao kwa kawaida ni wenye rangi maridadi sana. Lakini hasa tumekuja kuthamini jamii mbalimbali za watu wa huku. Wazazi wa kale wa baadhi yao walitoka Afrika na hata India, Indonesia, China, na nchi nyinginezo. Baadhi yao ni Wahindi wa Amerika wazao wa wakazi wa kale kabisa.
Katika huduma yetu ya Kikristo, tunakutana na watu wa aina mbalimbali tunapozuru nyumbani kwao. Katika Majumba yetu ya Ufalme, sisi hufurahia pia kuwa na ndugu na dada Wakristo wa aina mbalimbali wenye kuvutia. Tumeona ukuzi kutoka kwa Jumba la Ufalme moja lililochakaa mwaka wa 1953 hadi Majumba ya Ufalme zaidi ya 30 yenye kuvutia, Jumba la Kusanyiko zuri, na ofisi nzuri ya tawi, iliyowekwa wakfu katika Februari 1995.
Masomo Niliyojifunza
Ndani kabisa ya Suriname, kuna makutaniko kadhaa ya watu wanaoitwa eti Wabush Negroe, wazao wa watumwa Waafrika waliotoroka kutoka kwa mashamba na kuelekea karibu na vyanzo vya mito kadiri walivyoweza. Sikuzote nimestaajabishwa na uhodari wao—kwa mfano, jinsi wanavyoweza kusafiri mtoni na kuishi katika misitu ya mvua. Wao hukata miti, hujenga mashua, na kuendesha mashua hizo kupitia maporomoko ya maji na mikondo yenye nguvu. Wao hupata chakula kwa kuwinda na kuvua samaki, hupika chakula pasipo kifaa chochote cha kisasa, na kutekeleza kazi nyingine nyingi ambazo hutulemea.
Baada ya miaka mingi, tumekuja kujua watu wengine wanaoishi hapa Suriname, desturi zao, njia zao za kufikiri, na njia zao za maisha. Nakumbuka ziara yangu katika kijiji cha Wahindi wa Amerika huko nyuma katika miaka ya 1950. Katikati ya usiku niliwasili katika kambi iliyoachwa ukiwa katika msitu wa mvua, ambapo mimi na Mhindi wa Amerika aliyeniongoza tulikusudia kusafiri kwa mashua. Alikoka moto, akapika chakula, akafunga kitanda cha bembea. Ilikuwa kawaida kwake kunifanyia kila kitu kwa sababu alifahamu kwamba sikujua jinsi ya kufanya mambo hayo.
Nilipoporomoka kutoka kwenye kitanda changu cha bembea wakati wa usiku, hakunicheka. Badala yake, alizikung’uta mavumbi nguo zangu na kukifunga tena kitanda hicho. Tulipoabiri kwenye mto mwembamba, kulikuwa na giza tititi hivi kwamba sikuweza hata kuona mikono yangu, lakini kiongozi wangu aliweza kuendesha mashua hiyo kupitia kona nyingi na vizuizi. Nilipomwuliza kilichomwezesha afaulu, alisema: “Wewe unatazama upande usiofaa. Tazama juu na uone tofauti iliyopo baina ya vilele vya miti na anga. Itakuonyesha mto unapojipinda. Tazama chini ili uone viwimbi. Vitakusaidia kujua endapo kuna miamba au vizuizi vingine mbele. Sikiliza. Mvumo huonyesha pia kilicho mbele.”
Kusafiri kwa mitumbwi, kuvuka mikondo yenye nguvu, na kupita penye maporomoko ya maji kwaweza kuwa hatari na kwenye kuchosha. Lakini mwishoni mwa safari, tunapokutana na ndugu na dada zetu Wakristo wanaosubiri kutulaki kwa ukaribishaji-wageni mchangamfu, sisi hujihisi tumeburudika. Sikuzote kuna chakula cha wageni, labda bakuli la mchuzi. Sikuzote maisha ya umishonari yamekuwa yenye kujaribu na magumu lakini si yenye kukatisha tamaa kamwe.
Kilichotusaidia Kuendelea
Hatujabarikiwa kuwa na afya bora sana. Wala hatujatiwa moyo na washiriki wa familia, kwa kuwa mama yangu ndiye mtu pekee wa ukoo wetu aliye Shahidi. Lakini, bado tunaendelea kupokea kitia-moyo na msaada kutoka kwa marafiki wapendwa, wakitusaidia kuendelea katika mgawo wetu. Mama hasa alitutia moyo sana.
Baada ya kutumika kwa miaka sita hivi katika mgawo wetu, Mama akawa mgonjwa sana. Marafiki walituomba turudi kumwona mara ya mwisho, lakini Mama aliandika hivi: “Tafadhali, endeleeni katika mgawo wenu. Nikumbukeni jinsi nilivyokuwa kabla ya kuugua. Ninatumaini kuwaona wakati wa ufufuo.” Alikuwa mwanamke mwenye imani yenye nguvu.
Hatukuweza kurudi Uholanzi kwa ajili ya likizo hadi mwaka wa 1966. Tulifurahi sana kukutana na marafiki wa zamani, lakini tulihisi kwamba Suriname ilikuwa nyumbani kwetu sasa. Hivyo tunaona hekima ya shauri la tengenezo la kwamba wamishonari wasirejee makwao likizoni hadi wanapotumika angalau kwa miaka mitatu katika mgawo wao.
Jambo jingine ambalo limetusaidia kuonea shangwe mgawo wetu ni kuwa wacheshi—kuweza kucheka, hata kujichekelea. Hata Yehova alitia ucheshi katika baadhi ya viumbe vya asili. Utazamapo vituko vya sokwe na fisi maji, na hasa vitoto vya wanyama wengi, hukufanya utabasamu. Ni muhimu pia kuangalia upande unaofaa wa mambo na kutojiona kuwa wa maana sana—jambo ambalo tumejifunza kwa miaka mingi.
Kazi yetu yenye kuthawabisha katika huduma imetusaidia hasa kuendelea na mgawo wetu. Gré alianza kujifunza Biblia na wanaume tisa katika makao ya watu wazee-wazee huko Paramaribo. Wote walikuwa na umri wa zaidi ya miaka 80. Kila mmoja wao ama alikuwa balatableeder (mgemaji wa mpira) ama mchimba dhahabu. Kila mmoja wao alipendezwa na mambo aliyojifunza, akabatizwa, na akashiriki kwa uaminifu katika kazi ya kuhubiri hadi alipokufa.
Mhubiri mzee aliyeitwa Rivers, kutoka kanisa la New Church of Swedenborg, alisikiliza kwa makini wakati wa funzo na kutoa maelezo ya kukejeli. Lakini kila juma angejongea karibu zaidi, na dhihaka yake ikaanza kupungua. Hatimaye aliketi pamoja na wengine na kushiriki. Alikuwa na umri wa miaka 92 na hangeweza kuona wala kusikia, lakini aliweza kunukuu maandiko kana kwamba alikuwa akiyasoma. Hatimaye alianza kushiriki pamoja nasi katika huduma na alimhubiria kila mtu aliyesikiliza. Kabla tu hajafa, tulipokea ujumbe akituomba twende. Tulipowasili alikuwa ameshakufa tayari, lakini chini ya mto wake tulipata ripoti yake ya saa alizotumia katika huduma mwezi huo.
Mnamo 1970, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi ya Suriname baada ya kuhubiri kwa wakati wote kwa zaidi ya miaka 25. Haikuwa rahisi kufanya kazi ofisini na nilitamani kuwa kama Gré, ambaye alikuwa bado anashiriki huduma ya shambani kila siku. Sasa Gré anafanya kazi katika ofisi ya tawi pia, na sote tuna kazi yenye kusudi ya kutekeleza hapa tunapozeeka.
Kwa kweli, ninapolinganisha wapiga-mbiu watendaji wa Ufalme wanaopungua 160,000 waliokuwepo ulimwenguni pote huko nyuma mwaka wa 1945 na wapiga-mbiu 6,000,000 waliopo leo, naona kwamba mambo halisi yamezidi kwa mbali mataraja yangu. Na katika Suriname idadi ya wale wanaoshiriki katika huduma imeongezeka mara zaidi ya 19 tangu tulipofika huko mnamo 1955—kutoka wastani wa 100 wakati ule hadi zaidi ya 1,900 leo!
Nina hakika kwamba tutaona maendeleo makubwa zaidi katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova wakati ujao endapo tutabaki tu waaminifu kwa Mungu wetu. Na hiyo ndiyo nia yetu.
[Picha katika ukurasa wa 13]
Mnamo 1955, tulipofika Suriname
[Picha katika ukurasa wa 15]
Kusafiri kwa mitumbwi katika huduma yetu
[Picha katika ukurasa wa 15]
Nikiwa na mke wangu