Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kukosa Uaminifu Asanteni kwa mfululizo wa makala za Amkeni!, Aprili 22, 1999, “Mwenzi Anapokosa Uaminifu.” Mwenzi wangu alikosa uaminifu. Ijapokuwa nimetalikiwa kwa miaka mitatu sasa, bado nina uchungu mwingi. Makala hizo zilinisaidia kutambua kwamba nahitaji kuacha kufikiria hayo, nirudie hali ya kawaida, na kusonga mbele na maisha yangu.
V. B., Trinidad
Nimechunguza habari hiyo hapo awali, lakini haijapata kusimuliwa vizuri zaidi hivyo. Kuanzia wakati niliposikia ujumbe wa Biblia mara ya kwanza, nilielewa kwamba ulikuwa wa kweli. Sasa Yehova amenipa sababu nyingine ya kuuamini hivyo.
G. B., Italia
Talaka yangu ilinifanya nipatwe na mshuko wa moyo mbaya sana, kutojistahi, na matatizo ya afya yasiyokwisha. Ijapokuwa bado nateseka, ninafarijika sana kwa imani yangu katika ahadi za Yehova na upendo na tegemezo la kihisia-moyo kutoka kutaniko langu!
A. B., Kanada
Miezi tisa ikiwa imepita tangu nitengane na mume wangu, bado nakabiliana na uchungu wa kuishi peke yangu. Nitembeeje barabarani bila mtu wa kunishika mkono? Ni nani atakayeketi nami kwenye mikutano ya Kikristo? Ni nani atakayeandamana nami kwa daktari? Asanteni kwa kunikumbusha kwamba Yehova hawaachi wenzi wasio na hatia.
E. S., Brazili
Lile Sanduku “Ni Nani Mwenye Kulaumika?” lilinifariji sana. Niliamua kumtaliki mume wangu alipokosa uaminifu. Kama Yobu, nyakati nyingine nilitamani kufa. (Ayubu 17:11-13) Lakini tegemezo la washiriki wa familia na ndugu na dada Wakristo limenisaidia.
M. O., Argentina
Sikusoma tu mfululizo huo wa makala, bali niliusoma kwa shauku nyingi sana! Nimetalikiwa, na makala hizo zilizungumzia maswali na mahangaiko yote yaliyotokezwa. Asanteni kwa kutujali.
E. L., Ufaransa
Nilikuwa na umri wa miaka saba baba yangu alipoiacha familia yetu. Ulikuwa ukatili mbaya sana. Miaka kadhaa baadaye, Baba alituomba tumkubali arudi tena. Mimi na ndugu zangu hatukutaka, lakini Mama alikubali. Baada ya kusoma makala zenu, naanza kuelewa kwa nini alifanya uamuzi huo mgumu.
A. A., Brazili
Asanteni, asanteni, asanteni kwa mfululizo huo! Inafariji kujua kwamba hisia-moyo za mtu ni sawa na za watu wengine wanaopatwa na hali kama hiyo. Hata hivyo, mlisema: “Labda hukumwonyesha mwenzi wako upendo mwingi, shauku nyororo, pongezi na heshima aliyohitaji.” Maelezo hayo yanaumiza sana wale ambao kati yetu tumejaribu kufanya ndoa yenye matatizo ifaulu. Mtu anapofikiria kufanya uzinzi, anaweza kuwa mwenye makuruhu sana, na ni vigumu kumwonyesha mtu wa aina hiyo shauku.
L. W., Marekani
Twaomba radhi kama maelezo hayo yaliumiza yeyote kati ya wasomaji wetu. Lakini hatukunuia kumaanisha kwamba mzinzi anaweza kumlaumu mwenzi wake kwa sababu ya mwenendo wake usio mzuri. Katika sanduku “Ni Nani Mwenye Kulaumika?” tulikazia kwamba mzinzi anawajibika kwa kosa lake, bila kujali “kutokamilika kwa mwenzi asiye na hatia.” Maelezo hayo yalikuwa sehemu ya mazungumzo ya kupatana. Tulikuwa tukikazia tu uhitaji wa mawasiliano mazuri, tukitia moyo wenzi wenye kupatana watambue maeneo ya matatizo katika ndoa yao ambayo huenda yakahitaji kukaziwa fikira kwa uharaka. Huenda pia kukawa na chuki iliyojificha ambayo yahitaji kuzungumziwa waziwazi. Kwa kawaida, mazungumzo hayo hufanya wenzi wote wawili wakubali makosa fulani. Hata hivyo, “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Ingawa mazungumzo hayo mara nyingi huwa yenye kuhuzunisha sana, kama vile makala ilivyoeleza, huchangia “sehemu muhimu katika hatua ya kuaminiana tena.”—Mhariri.