Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Bustani ya Duniani Pote Ninawashukuru sana kwa ajili ya ule mfululizo mzuri “Bustani ya Duniani Pote—Je, Ni Ndoto au Ni Uhalisi wa Wakati Ujao?” (Aprili 8, 1997) Ndiyo, bustani na rangi zaweza kuathiri afya yetu na kutufanya tuhisi shangwe. Nilipenda sehemu iliyokuwa na kichwa “Njia ya Kurudia Paradiso.” Maneno hayo machache yalikuwa yenye kutia moyo sana—kama mwaliko wenye kusema, “Njia ni hii.” Itafurahisha kama nini siku moja kufanya kazi kuanzia machweo ya jua hadi mshuko-jua katika kusaidia kugeuza dunia kuwa paradiso! Kama nioneavyo shangwe kupaka rangi, kuchora, na kazi za mkono, pia mimi hupendezwa na kazi yote ya sanaa katika magazeti.
V. R., Australia
Nataka kuwapongeza kwa sababu ya hizo makala. Nilizifurahia kikamili. Ninakaribia umri wa miaka 80 na ningali napenda kufanya kazi katika ua wangu. Maua na mboga zangu hazingechukua nafasi ya kwanza katika mashindano, lakini mimi hufurahia kuwa nje na kutunza mimea hii. Tangu niliposoma hizi makala, naelewa vizuri kwa nini wanadamu hupenda kufanya kazi katika bustani.
R. R., Marekani
Kuokoa Ndoa? Wakati niliposoma ile makala “Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa Baada ya Ukosefu wa Uaminifu?” (Aprili 8, 1997), nilikuwa na wazo la kwamba Yehova alikuwa akinitumia barua. Ilionyesha sawasawa lile lililokuwa likinipata na jinsi nilivyohisi. Mume wangu alikosa uaminifu, lakini alitubu kwa unyoofu wa moyo. Kama ilivyoeleza hiyo makala, nilihisi kama nilikuwa ndani ya kimbunga. Nilichagua kumsamehe, lakini nyakati nyingine niliaibishwa na mawazo yangu. Hiyo makala ilinisaidia kuelewa kwamba maitikio yangu yalikuwa ya kawaida na halali kabisa. Yehova amebariki sana jitihada zetu, na ndoa yetu imeokolewa.
L. P., Ufaransa
Ingawa ndoa yangu haingeweza kuokolewa, makala hii ilikuwa baraka halisi kwa sababu ilifafanua sawasawa jinsi nilivyohisi. Kwa kweli ningeweza kuhusisha hali yangu yenyewe na kila jambo lililofafanuliwa katika makala hii. Mimi pia nawajua wengine ambao hali kadhalika wamenufaika kutokana nayo. Wengi huona kuwa vigumu kuelewa jinsi mtu aliye katika hali yangu huhisi, kwa hiyo makala hii itakuwa msaada mkubwa, ikiwaandalia ufahamu wenye kina.
M. C., Ireland
Mimi nimeolewa kwa miaka tisa na asiyeamini ambaye amekuwa mwenzi asiye mwaminifu. Lakini niliposoma mafungu chini ya kichwa kidogo “Je, Ndoa Yaweza Kuokolewa?” Nilihisi vizuri zaidi. Mume wangu angependa kutunza ndoa yetu lakini akiendeleza uhusiano pamoja na mwanamke yule mwingine. Kwa hiyo, nafurahi kwamba ninaikomesha ndoa yetu. Sasa nalazimika kuanza tena na kuwa mama aliye mzazi pekee.
M. S. B., Trinidad
Asanteni kwa ajili ya makala nzuri na yenye kuchochea hisia. Shauri lilikuwa bora kabisa kutumia katika kuhakikisha ikiwa upatanisho utakuwa na mafanikio. Sikuzote nilikuwa nikidhania kwamba ikiwa mume wangu angekosa uaminifu, singeweza kumsamehe kamwe. Sasa nang’amua kwamba hilo si jibu lililo sawa sikuzote. Ni aibu kwamba ukosefu wa uaminifu katika ndoa kwa wazi ni tatizo linaloendelea kukua, lakini asanteni kwa ufahamu wenye kina wa Kimaandiko unaoonyesha jinsi tunavyoweza kujisaidia. Tegemeo langu katika Yehova limenisaidia kupitia mshuko-moyo wenye kina kirefu na kunisaidia kupata nguvu za kusamehe, kwa kuwa mume wangu alikuwa (na bado) ametubu kikweli.
S. N., Marekani