SOMO LA 36
Kufafanua Kichwa Kikuu
WASEMAJI wenye uzoefu wanajua kwamba ni muhimu kuwa na kichwa kikuu. Wanapotayarisha hotuba, kichwa kikuu huwasaidia kulenga habari fulani hususa na kuifikiria kwa undani. Matokeo yanakuwa kwamba badala ya kugusia mambo mengi kijuu-juu tu, wao hufafanua habari kwa njia inayofaidi wasikilizaji zaidi. Ikiwa kila jambo kuu linahusiana na kichwa kikuu na linasaidia kukifafanua, wasikilizaji huweza kukumbuka mambo hayo na kuona umuhimu wake.
Ingawa inasemekana kwamba kichwa kikuu ni habari unayozungumzia, hotuba zako zitaboreka sana ukiwa na maoni ya kwamba kichwa kikuu ni njia hususa unayotumia kuifafanua habari hiyo. Ufalme, Biblia, na ufufuo ni habari za ujumla. Unaweza kutokeza vichwa vikuu kutokana na habari hizo. Hapa pana mifano kadhaa: “Ufalme Ni Serikali Halisi,” “Ufalme wa Mungu Utafanya Dunia Iwe Paradiso,” “Biblia Imepuliziwa na Mungu,” “Biblia Ni Mwongozo Unaofaa Katika Siku Zetu,” “Ufufuo Huwapa Tumaini Waliofiwa,” na “Tumaini la Ufufuo Hutusaidia Kubaki Imara Tunapokabili Mnyanyaso.” Vichwa hivyo vyote vinahitaji kufafanuliwa kwa njia tofauti-tofauti kabisa.
Mahubiri ya Yesu Kristo wakati wa huduma yake duniani yanapatana na kichwa kikuu cha Biblia kwa sababu alikazia: “Ufalme wa mbingu umekaribia.” (Mt. 4:17) Kichwa hicho kikuu kilifafanuliwaje? Ufalme huo unatajwa zaidi ya mara 110 katika vitabu vinne vya Injili. Lakini Yesu hakutumia neno “ufalme” kwa kurudia-rudia tu. Kupitia mafundisho yake na miujiza yake, Yesu alionyesha wazi kwamba yeye aliyekuwa akiongea nao ndiye Mwana wa Mungu, Mesiya, ambaye Yehova angempa Ufalme. Pia Yesu alionyesha kwamba kupitia yeye njia ilikuwa inafunguliwa ili wengine washiriki katika Ufalme huo. Alitaja sifa ambazo wale ambao wangepewa pendeleo hilo wanapaswa kuonyesha. Kupitia mafundisho yake na miujiza yake, alionyesha wazi jinsi ambavyo Ufalme wa Mungu ungewasaidia watu na alisema kwamba uwezo wake wa kufukuza roho waovu kupitia roho ya Mungu ni uthibitisho wa kwamba ‘ufalme wa Mungu kwa kweli ulikuwa umewapata ghafula’ wasikilizaji wake. (Luka 11:20) Yesu aliagiza wafuasi wake watoe ushahidi kuhusu Ufalme uo huo.—Mt. 10:7; 24:14.
Kutumia Kichwa Kikuu Kinachofaa. Hutazamiwi kufafanua kichwa kikuu kwa kadiri ambavyo Biblia inakifafanua, lakini bado ni muhimu kuwa na kichwa kikuu kinachofaa.
Ikiwa ni juu yako kuchagua kichwa kikuu, kwanza fikiria kusudi la hotuba yako. Kisha unapochagua mambo makuu ya muhtasari, hakikisha kwamba mambo hayo yanategemeza kichwa kikuu ambacho umechagua.
Ikiwa umepewa kichwa kikuu, kichunguze kwa makini ili ujue jinsi utakavyokifafanua. Utahitaji kutia bidii ili kufahamu vizuri umuhimu wa kichwa hicho kikuu na jinsi unavyoweza kukifafanua. Ikiwa ni juu yako kuchagua habari ya kufafanua kichwa hicho, uwe mwangalifu ili habari unayochagua iambatane na kichwa kikuu. Lakini, kama umepewa habari ya kuzungumzia, bado utahitaji kuichunguza na kuona jinsi ya kuitumia kuhusiana na kichwa kikuu. Pia unahitaji kufikiria kusudi la habari hiyo na umuhimu wake kwa wasikilizaji. Hiyo itakusaidia kujua mambo ya kukazia unapohutubu.
Jinsi ya Kukazia Kichwa Kikuu. Ili ukazie vizuri kichwa kikuu, ni lazima uweke msingi unapochagua habari zako na kuzipanga. Ukitumia tu mambo yanayounga mkono kichwa kikuu na ukifuata kanuni zinazohusu kutayarisha muhtasari mzuri, itakuwa rahisi sana kukazia kichwa kikuu.
Kurudia mambo makuu kunaweza kusaidia kukazia kichwa kikuu. Ebu fikiria mfano wa muziki wa mapenzi. Kotekote katika wimbo huo, mwimbaji anataja tena na tena jinsi anavyompenda mpenzi wake. Anaweza kurudia-rudia neno “upendo” kwa njia mbalimbali. Pia anaweza kutumia maneno mengine yanayoonyesha upendo na kutumia semi, lugha ya kishairi, au mifano mingine. Na utaona kwamba wimbo huo unazingatia hasa kichwa kilekile cha upendo. Ndivyo ilivyo na kichwa kikuu cha hotuba. Jinsi wazo la upendo linavyotajwa tena na tena katika wimbo huo ndivyo wewe unavyopaswa kurudia-rudia maneno ya kichwa kikuu. Pia unaweza kutumia maneno tofauti-tofauti yanayorejelea hicho kichwa kikuu au kutaja kichwa kikuu kwa njia nyinginezo. Ukifanya hivyo wasikilizaji watakumbuka sana kichwa kikuu.
Mbali na hotuba, kanuni hizi pia zinahusu mazungumzo yetu katika huduma ya shambani. Mazungumzo mafupi tu yanaweza kukumbukwa ikiwa kichwa kikuu kinajitokeza wazi. Mafundisho katika funzo la Biblia yatakumbukwa kwa urahisi ukikazia kichwa kikuu. Jitihada unazofanya kuchagua na kufafanua vichwa vikuu vinavyofaa zitakusaidia kuwa msemaji na mwalimu bora wa Neno la Mungu.